Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Haki ya Binadamu ya Kuheshimiwa Hukandamizwa

Haki ya Binadamu ya Kuheshimiwa Hukandamizwa

Haki ya Binadamu ya Kuheshimiwa Hukandamizwa

“Kila jambo lililotendeka kambini lilitufanya tuhisi kwamba tumedharauliwa na kukandamizwa.”—MAGDALENA KUSSEROW REUTER, ALIYEOKOKA KAMBI YA MATESO YA NAZI.

INGAWA kulikuwa na ukatili mwingi katika kambi za mateso za utawala wa Nazi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, huo haukuwa mwanzo wala mwisho wa ukandamizaji wa heshima ya binadamu. Iwe tunachunguza mambo ya kale au ya sasa, jambo hili linaonekana wazi: Kwa muda mrefu, watu wengi ‘wamedharauliwa na kukandamizwa.’

Hata hivyo, kukandamizwa kwa heshima ya binadamu hakuhusishi tu matendo ya kinyama ambayo yamewahi kufanywa. Mara nyingi matendo hayo hufanywa kwa njia zisizo wazi. Fikiria mtoto anayedhihakiwa kwa sababu ana kasoro fulani za mwili. Au mhamiaji anayedhihakiwa kwa sababu ya desturi fulani za “kigeni.” Au mtu fulani anayebaguliwa kwa sababu ya rangi au taifa lake. Huenda wale wanaowadhihaki wakachukulia mambo hayo kuwa mzaha, lakini wale wanaodhihakiwa hawayaoni kuwa mambo ya kuchekesha kwa kuwa yanawaumiza na kuwaaibisha.—Methali 26:18, 19.

Maana ya Heshima ya Binadamu

Kamusi moja inafafanua heshima kuwa ‘sifa au hali ya kuwa mwenye thamani, kustahiwa, au kuthaminiwa.’ Kwa hiyo, heshima ya binadamu inatia ndani jinsi tunavyojiona na jinsi wengine wanavyotuona. Ingawa kuna mambo ambayo yanaweza kuathiri jinsi tunavyojiona, jinsi wengine wanavyotuona au kututendea hutufanya tuhisi kwamba tunathaminiwa maishani.

Katika kila jamii kuna maskini, kuna watu wasio na uwezo, na wanyonge. Hata hivyo, kuwa katika hali hiyo hakumpunguzii mtu heshima. Mtazamo na matendo ya wengine ndiyo yanayoweza kumvunjia mtu heshima. Inasikitisha kwamba mara nyingi watu wa hali ya chini ndio wanaodharauliwa. Mara nyingi sana tunasikia maneno kama vile “wewe ni bure kabisa” au “hufai kitu” yakitumiwa kuwatukana wazee, maskini, au watu wenye ugonjwa wa akili au walemavu!

Kwa nini watu hawaheshimiani? Je, haki ya msingi ya kuheshimiwa itatimizwa? Makala inayofuata itatoa jibu lenye kuridhisha kutoka kwa Neno la Mungu, Biblia.