Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Ujuzi wa Kweli

Kupata Ujuzi wa Kweli

Kupata Ujuzi wa Kweli

ILIKUWA Desemba 18, mwaka wa 1810. Giza lilikuwa linaingia. Meli ya Jeshi la Wanamaji la Uingereza, iliyoitwa HMS Pallas ilikuwa imepoteza mwelekeo katika bahari yenye msukosuko mbali na pwani ya kusini-mashariki mwa Scotland. Giza pamoja na theluji zilifanya iwe vigumu kwa nahodha kuona ishara zilizokuwa kwenye mnara wa taa zilizohitajiwa ili kuongoza meli yao mahali salama. Wazia jinsi walivyofurahi hatimaye walipoona taa na kuelekeza meli yao kuzielekea! Hata hivyo, inasikitisha kwamba hizo hazikuwa taa walizohitaji. Ulikuwa moto uliowashwa na watu waliofanya kazi karibu na pwani. Meli hiyo iligonga miamba na kuvunjika kabisa. Mabaharia 11 walizama. Huo ulikuwa msiba mbaya sana!

Katika kisa cha meli hiyo, kosa moja tu lilisababisha msiba. Hata hivyo, wakati mwingine mabaharia walikabili hatari kubwa hata zaidi, yaani, taa za kuongoza za bandia. Kulingana na kitabu kimoja (Wrecks, Wreckers and Rescuers), taa hizo ziliwekwa kimakusudi kuongoza meli kwenye bandari zenye miamba ili kuzipora.

‘Maandishi Matakatifu Yanayoweza Kukusaidia Ili Upate Wokovu’

Unapoendelea kutafuta ujuzi, unakabili hatari kama wale mabaharia. Huenda ukafuata habari zenye kupotosha au huenda ukadanganywa kimakusudi. Njia zote hizo zinaweza kusababisha msiba. Unaweza kujilindaje? Hakikisha kwamba unapata ujuzi katika chanzo cha kweli na kinachotegemeka. Kwa zaidi ya miaka 125, gazeti hili limetetea Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho, kuwa chanzo pekee kinachotegemeka cha ujuzi kwa sababu ina “maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.”—2 Timotheo 3:15-17.

Bila shaka, ili uwe na uhakika kwamba Biblia ndiyo mwongozo unaotegemeka, ni jambo la busara kuchunguza mambo yanayothibitisha kwamba ni ya kweli. (Zaburi 119:105; Methali 14:15) Kwa habari zaidi, waandikie wachapishaji wa gazeti hili, ambalo limewasadikishia mamilioni ya watu kwamba kwa kweli Biblia imeongozwa kwa roho ya Mungu. Kwa mfano, soma broshua yenye kichwa Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote. * Broshua hiyo ina habari nyingi zinazoonyesha kwamba Biblia ni sahihi, na imeongozwa kwa roho ya Mungu.

Kweli za Msingi

Ni baadhi ya kweli gani za msingi zinazopatikana katika ‘maandishi hayo matakatifu’? Fikiria mifano ifuatayo.

Kuna Mungu mmoja Mweza-Yote aliye Muumba wa vitu vyote. (Mwanzo 1:1) Tunaishi ‘kwa sababu Mungu aliumba vitu vyote’ na akatupa uhai. (Ufunuo 4:11) Hiyo ndiyo sababu ni yeye tu anayestahili ibada yetu. Muumba ndiye Chanzo pekee cha ujuzi. (Zaburi 36:9; Isaya 30:20, 21; 48:17, 18) Ana jina ambalo anataka tulitumie. (Kutoka 3:15) Jina hilo lililoandikwa kwa herufi za Kiebrania na kutafsiriwa YHWH, linapatikana katika Biblia mara 7,000 hivi. Kwa miaka mingi jina “Yehova” limetumiwa katika Kiswahili.—Zaburi 83:18.

Yehova aliwaumba wanaume na wanawake waishi milele wakiwa na hali nzuri katika Paradiso hapa duniani. Aliwapa wanadamu sifa za kiroho zinazofanana na zake. Aliwapa vipawa ambavyo vingewawezesha kufurahia uzima wa milele wenye kuridhisha duniani. (Mwanzo 1:26-28) Mungu hakukusudia dunia iwe mahali pa kuwajaribia wanadamu ili kuona kama wanastahili kuwa viumbe wa roho huko mbinguni, kana kwamba huko tu ndiko wangeweza kufurahia uhusiano pamoja na Mungu.

Mungu hakumuumba mwanadamu akiwa na uovu wowote. Uovu ulianza tu wakati baadhi ya viumbe wa Mungu, yaani, wanadamu na malaika, walipotumia vibaya uhuru wao wa kuchagua na kumwasi Mungu. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Wazazi wetu wa kwanza waliamua kujiamulia wenyewe yaliyo mema na yaliyo mabaya. (Mwanzo 2:17; 3:1-5) Hilo likasababisha kifo kwa wanadamu. (Mwanzo 3:19; Waroma 5:12) Ili kusuluhisha masuala yaliyotokezwa na uasi huo, Yehova aliamua kuruhusu uovu uwepo kwa muda. Lakini kusudi lake kuelekea dunia na wanadamu halijabadilika. (Isaya 45:18) Bado wanaume na wanawake wataishi milele katika Paradiso juu ya dunia iliyosafishwa.—Mathayo 6:10; Ufunuo 21:1-5.

Yesu Kristo si Mungu Mweza-Yote bali ni Mwana wa Mungu. Yesu Kristo mwenyewe aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Hakudai kuwa sawa na Mungu. Badala yake alisema: “Baba ni mkuu kuliko mimi.”—Yohana 14:28.

Yesu ana sehemu muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Mungu alimtuma akiwa “nuru ulimwenguni, ili kila mtu anaye[mwa]mini asipate kukaa katika giza.” (Yohana 12:46) Kulingana na mtume Petro, “hakuna wokovu katika mwingine yeyote.” (Matendo 4:12) Maneno hayo ni ya kweli kwa sababu wokovu wetu unategemea damu yenye thamani ya Kristo. (1 Petro 1:18, 19) Yesu Kristo alitoa uhai wake kuwa dhabihu ya fidia ili kuwakomboa wanadamu kutokana na dhambi ambayo tulirithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Mathayo 20:28; 1 Timotheo 2:6) Pia, Mungu alimtumia Yesu kufunua mapenzi Yake na kusudi Lake.—Yohana 8:12, 32, 46, 47; 14:6; Matendo 26:23.

Mungu amesimamisha Ufalme au serikali ya mbinguni inayofanyizwa na Yesu Kristo pamoja na wanadamu waliochaguliwa kutoka duniani. Ujumbe huo kuhusu Ufalme wa Mungu unarudiwa-rudiwa katika Biblia. Mungu amekabidhi serikali hiyo jukumu la kuhakikisha kwamba mapenzi yake yanatendeka duniani kama vile mbinguni. (Mathayo 6:10) Halikuwa kusudi la Mungu hapo mwanzoni kwamba wanadamu fulani waende mbinguni. Walipaswa kuishi duniani. Lakini kwa sababu ya dhambi ya mwanadamu, Mungu alifanya mpango mpya. Aliamua kuchagua watu ‘kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa ili watawale wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo katika Ufalme wa mbinguni. (Ufunuo 5:9, 10) Karibuni Ufalme huo ‘utavunja na kukomesha’ kila aina ya utawala wa wanadamu ambao umesababisha matatizo na maumivu mengi.—Danieli 2:44.

Nafsi hufa. Fundisho hilo la msingi la Biblia linaeleza wazi kuhusu wanadamu na matarajio yao maishani. Pia, linaonyesha ukweli kuhusu hali ya wafu, jambo ambalo limewatatanisha watu wengi.

Kitabu cha kwanza cha Biblia kinasema hivi: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Je, unaelewa maana ya maneno hayo? Nafsi si kitu kisichoonekana ambacho huwa ndani ya mwanadamu. Mwanadamu hana nafsi. Yeye ni nafsi, yaani, mchanganyiko wa vitu vilivyo katika “mavumbi ya nchi” na nguvu za uhai kutoka kwa Mungu. Nafsi hufa. Mtu anapokufa, nafsi inakufa.—Mwanzo 3:19; Mhubiri 9:5, 10.

Wale ambao wamekufa wanaweza kufufuliwa. Wakati ambao Mungu ameruhusu uovu uendelee kwa muda utakapokwisha, “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Ufufuo utawawezesha watu kuishi katika paradiso duniani, kama Mungu alivyokusudia mwanzoni kwa ajili ya wanadamu.

Chunguza Maandiko kwa Makini Kila Siku

Je, unaona jinsi kujua ukweli huo wa msingi kunavyoweza kukusaidia? Ujuzi huo unaweza kukulinda kutokana na “ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi’” unaoenezwa na Shetani Ibilisi katika siku hizi za hatari na zenye misukosuko. Yeye hujifanya kuwa “malaika wa nuru” na wawakilishi wake hujifanya kuwa “wahudumu wa uadilifu.” (1 Timotheo 6:20; 2 Wakorintho 11:13-15) Ujuzi sahihi wa Biblia unaweza kukulinda kutokana na ule unaoitwa ujuzi unaotegemea falsafa za ulimwengu za “wenye hekima na wenye akili” ambao “wamelikataa neno la Yehova.”—Mathayo 11:25; Yeremia 8:9.

Kwa sababu kulikuwa na mafundisho mengi na falsafa nyingi za uwongo katika siku zake, mtume Yohana aliwaonya hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Msiamini kila neno lililoongozwa na roho.” Kisha akasema: “Yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) Fikiria mfano huu. Ikiwa ungepokea ujumbe ambao ungeathiri sana maisha yako, je, ungeukubali tu eti kwa sababu unaonekana kuwa unatokana na chanzo chenye kutegemeka? Hapana. Utahitaji kuwa na uhakika kuhusu chanzo chake kisha uuchunguze kabla ya kutenda.

Kwa kuandaa maandishi yaliyoongozwa kwa roho yake ambayo yana kweli za msingi, Mungu amekuwezesha ‘kuhakikisha’ kwamba taa zinazokuongoza ni za kweli. (1 Wathesalonike 5:21) Watu wasikivu wa karne ya kwanza walipongezwa kwa ‘kuyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku’ ili kuhakikisha kwamba mambo waliyojifunza yalikuwa ya kweli. (Matendo 17:11) Unaweza kufanya hivyo pia. Iache Biblia ikuongoze kwenye usalama kama vile “taa inayoangaza mahali penye giza.” (2 Petro 1:19-21) Ukiiacha ikuongoze, “utapata kumjua Mungu,” na hiyo ndiyo njia ya kupata ujuzi wa kweli.—Methali 2:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Neno la Mungu ni kama taa

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mungu anaitwa nani?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wakati ujao wa wanadamu utakuwaje?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, Yesu ni Mungu Mweza-Yote?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Wafu wako wapi?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ufufuo ni mojawapo ya kweli za msingi za Biblia