Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu alimaanisha nini alipomwambia Nikodemo: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni ila yule aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu”?Yohana 3:13.

Wakati huo Yesu alikuwa duniani, na hakuwa amepanda kuingia au kurudi mbinguni. Hata hivyo, yale tunayojua kuhusu Yesu na muktadha wa maneno yake yanaweza kutusaidia kuelewa alichomaanisha.

Yesu ‘alishuka kutoka mbinguni’ katika maana ya kwamba hapo awali aliishi katika makao ya roho pamoja na Baba yake, lakini kwa wakati uliowekwa, uhai wa Mwana huyo ulihamishwa hadi ndani ya tumbo la Maria, na hivyo Yesu akazaliwa akiwa mwanadamu. (Luka 1:30-35; Wagalatia 4:4; Waebrania 2:9, 14, 17) Baada ya kifo chake, Yesu angefufuliwa akiwa kiumbe wa roho na kurudi awe pamoja na Yehova. Hivyo, muda mfupi kabla ya kuuawa Yesu alisali hivi: “Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.”—Yohana 17:5; Waroma 6:4, 9; Waebrania 9:24; 1 Petro 3:18.

Yesu alipozungumza na Nikodemo, ambaye alikuwa Farisayo na mwalimu katika Israeli, Yeye hakuwa amerudi mbinguni. Ni wazi kwamba hakuna mwanadamu mwingine aliyekuwa amekufa na kupanda kwenda kwenye makao ya roho, mbinguni. Yesu mwenyewe alisema kwamba Yohana Mbatizaji alikuwa nabii mkuu zaidi wa Mungu, lakini “mtu aliye mdogo zaidi katika ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.” (Mathayo 11:11) Na mtume Petro alieleza kwamba hata Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu alikufa na bado alikuwa kaburini; Daudi hakupanda mbinguni. (Matendo 2:29, 34) Kuna sababu inayoonyesha kwa nini watu waliokufa kabla ya Yesu kama vile Daudi, Yohana Mbatizaji, na wanaume wengine wenye imani hawakwenda mbinguni. Walikufa kabla ya Yesu kuzindua njia au uwezekano wa wanadamu kufufuliwa ili waishi mbinguni. Mtume Paulo aliandika kwamba Yesu akiwa mtangulizi ‘alizindua njia mpya na yenye uzima’ ya kuingia mbinguni.—Waebrania 6:19, 20; 9:24; 10:19, 20.

Kwa kuwa Yesu hakuwa amekufa na kufufuliwa, alimaanisha nini alipomwambia Nikodemo: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni ila yule aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu”? (Yohana 3:13) Fikiria muktadha, au mazungumzo ya Yesu na Nikodemo.

Mtawala huyo Myahudi alipomjia Yesu wakati wa usiku, Yesu alimwambia hivi: “Kwa kweli kabisa ninakuambia, Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Nikodemo akauliza: ‘Inawezekanaje? Mtu anaweza kuzaliwaje tena?’ Hakuelewa fundisho hilo la kimungu kuhusu kuwa katika Ufalme wa Mungu. Angepataje kujua jambo hilo? Hangeweza kulijua kwa kutegemea maoni ya wanadamu. Hakuna mwanadamu ambaye angeweza kumfundisha kuhusu Ufalme huo kwa sababu hakuna mwanadamu aliyewahi kuishi mbinguni na hivyo aweze kumweleza kuhusu kuingia katika Ufalme huo. Yesu tu ndiye angeweza kumfundisha jambo hilo. Angeweza kumfundisha Nikodemo na wengine kwa sababu Alikuwa ameshuka kutoka mbinguni, naye alistahili kuwafundisha watu kuhusu mambo kama hayo.

Hivyo, swali lililoulizwa kuhusu andiko hilo linatufundisha jambo fulani muhimu kuhusu kujifunza Neno la Mungu. Haifai kukwazwa na andiko fulani kwa sababu tu linaonekana kuwa halieleweki. Yale ambayo Biblia husema katika sehemu moja yanapaswa kueleweka kulingana na mambo ambayo yanasemwa katika Maandiko mengine, na yanapaswa kupatana nayo. Isitoshe, mara nyingi muktadha, yaani, hali au mambo yanayozungumziwa yanaweza kutusaidia kuelewa maana kamili ya andiko fulani linalotatanisha.