Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Faida za Kuwa Mshikamanifu

Kuna Faida za Kuwa Mshikamanifu

Kuna Faida za Kuwa Mshikamanifu

KATIKA nchi fulani, watoto hufurahia kuwatania wenzao kwa kuwatupia mbegu zinazonata kwenye nguo. Mbegu hizo hushikamana sana na nguo na haziwezi kutoka hata watoto hao watembee, wakimbie, wajitikise, au waruke. Zinaweza tu kuondolewa zinapong’olewa mojamoja. Watoto hufurahia mchezo huo.

Bila shaka, si kila mtu anayefurahia mbegu hizo kwenye nguo zake, lakini kila mtu hushangazwa na uwezo wake wa kunata. Mtu aliye mshikamanifu ana sifa kama hiyo. Mtu mshikamanifu hudumisha uhusiano na wengine. Yeye hutimiza kwa uaminifu wajibu na matakwa ya uhusiano huo hata hali inapokuwa ngumu. Neno “ushikamanifu” hutukumbusha sifa kama vile, ukweli, utii, na ujitoaji. Hata hivyo, ingawa huenda unathamini watu walio washikamanifu, je, wewe hujitahidi kuwa mshikamanifu kwa wengine? Ikiwa ndivyo, unapaswa kuwa mshikamanifu kwa nani?

Ushikamanifu Katika Ndoa Ni Uhitaji wa Msingi

Ushikamanifu unapaswa kuonyeshwa katika ndoa, lakini inasikitisha kwamba mara nyingi hauonyeshwi. Mume na mke walio waaminifu kwa nadhiri zao za ndoa, yaani, wanaoishi pamoja huku kila mmoja akijitahidi kumfaidi mwenzake, wamechukua hatua muhimu ya kupata furaha na usalama. Kwa nini? Kwa sababu wanadamu waliumbwa wakiwa na uhitaji wa kuwa washikamanifu na kuonyeshwa ushikamanifu. Ndoa ya Adamu na Hawa ilipoanzishwa katika bustani ya Edeni, Mungu alisema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” Ilipaswa kuwa hivyo kwa mke pia; alipaswa kushikamana na mume wake. Mume na mke walipaswa kuwa waaminifu na kushirikiana.—Mwanzo 2:24; Mathayo 19:3-9.

Bila shaka hilo lilitukia maelfu ya miaka iliyopita. Lakini je, hilo linamaanisha kwamba kuwa mshikamanifu katika ndoa ni jambo lililopitwa na wakati? Wengi watasema hapana. Watafiti fulani huko Ujerumani waligundua kwamba asilimia 80 ya watu waliona uaminifu katika ndoa kuwa sifa muhimu sana. Uchunguzi wa pili ulifanywa ili kutafuta sifa zenye kuvutia zaidi za wanaume na wanawake. Kikundi cha wanaume kiliombwa kiorodheshe sifa tano za wanawake ambazo ziliwavutia zaidi, na kikundi cha wanawake kikaorodhesha sifa tano za wanaume zilizowavutia zaidi. Vikundi vyote viwili vilivutiwa zaidi na sifa ya uaminifu.

Naam, ushikamanifu ni sehemu ya msingi imara wa ndoa yenye mafanikio. Hata hivyo, kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, ushikamanifu ni sifa inayothaminiwa sana lakini mara nyingi haionyeshwi. Kwa mfano, kuongezeka kwa talaka katika nchi nyingi kunaonyesha kwamba watu wengi si washikamanifu. Wenzi wa ndoa wanawezaje kushinda mwelekeo huo na kuendelea kuwa washikamanifu?

Ushikamanifu Hudumisha Ndoa

Ushikamanifu huonyeshwa wakati wenzi wa ndoa wanapotafuta nafasi ya kuonyeshana upendo. Kwa mfano, ni vizuri kusema “yetu” badala ya “yangu”—“rafiki zetu,” “watoto wetu,” “makao yetu,” “mambo ambayo yametupata maishani,” na kadhalika. Mume au mke anapaswa kufikiria hisia na maoni ya mwenzake anapofanya mipango na maamuzi kuhusu makao, kazi ya kuajiriwa, kulea mtoto, burudani, likizo, au utendaji wa kidini.—Methali 11:14; 15:22.

Mtu huonyesha ushikamanifu anapomfanya mwenzi wake ahisi anahitajika na anapendwa. Mtu aliyefunga ndoa huwa na wasiwasi anapoona mwenzi wake akipendezwa kupita kiasi na mtu wa jinsia tofauti. Biblia inamshauri mume ashikamane na “mke wa ujana [wake].” Mwanamume hapaswi kuvutiwa na mwanamke mwingine ila mke wake. Anapaswa kuepuka kujihusisha katika mwenendo mchafu kingono na mwanamke mwingine. Biblia inaonya hivi: “Yeyote anayefanya uzinzi na mwanamke amepungukiwa moyoni; yule anayefanya hivyo anaiangamiza nafsi yake mwenyewe.” Mke pia anatazamiwa kushika viwango hivyohivyo vya uaminifu.—Methali 5:18; 6:32.

Je, kuna faida ya kujitahidi kuwa mwaminifu katika ndoa? Bila shaka. Kunafanya ndoa iwe imara na yenye kudumu, na wenzi wote wawili wanafaidika. Kwa mfano, mume anapokuwa mwaminifu kabisa kwa mahitaji ya mke wake, mke anajihisi salama na hivyo anaonyesha sifa zake nzuri. Ndivyo na mume pia. Azimio lake la kuwa mshikamanifu kwa mke wake humsaidia kushikamana na kanuni za uadilifu katika maisha yake yote.

Ikiwa mume na mke watakabili hali ngumu maishani, ushikamanifu utawafanya wajihisi salama. Kwa upande mwingine, ikiwa mume na mke si washikamanifu, mara nyingi matatizo yanapotokea wao hutengana au kutalikiana. Badala ya kusuluhisha matatizo, hatua hiyo huongoza kwenye matatizo mengine. Katika miaka ya 1980, mshauri fulani mashuhuri wa mitindo alitengana na mke wake na familia yake. Je, alikuwa na furaha akiwa peke yake? Miaka 20 baadaye alikubali kwamba kutengana na familia yake kulimfanya ajihisi ‘mpweke na akose usingizi usiku akitamani kuzungumza na watoto wake kabla ya kulala.’

Ushikamanifu Kati ya Wazazi na Watoto

Wazazi wanapoonyeshana ushikamanifu, kuna uwezekano mkubwa kwamba watoto wao wataiga sifa hiyo. Baadaye maishani, itakuwa rahisi kwa watoto ambao wamelelewa katika familia yenye ushikamanifu na upendo kuwajali wenzi wao wa ndoa na wazazi wao hasa wanapopata matatizo ya uzee.—1 Timotheo 5:4, 8.

Ni kweli kwamba nyakati nyingine si wazazi wanaohitaji kutunzwa. Huenda mtoto akahitaji kutunzwa kwa uaminifu. Herbert na Gertrud, wamekuwa Mashahidi wa Yehova kwa zaidi ya miaka 40. Mwana wao, Dietmar, alikuwa na kasoro za misuli muda wote wa maisha yake. Kwa miaka saba kabla ya kifo chake mnamo Novemba 2002, Dietmar alihitaji kutunzwa usiku na mchana. Kwa upendo, wazazi wake walishughulikia mahitaji yake. Hata waliweka vyombo vya tiba katika nyumba yao na wakapata mafunzo ya tiba. Huo ni mfano bora wa familia yenye ushikamanifu!

Ushikamanifu Ni Muhimu Kati ya Marafiki

“Mtu anaweza kuwa na furaha akiwa mseja, lakini ni vigumu kuwa na furaha bila rafiki,” anasema Birgit. Huenda unakubaliana naye. Uwe umefunga ndoa au la, ushikamanifu wa rafiki mzuri utakuchangamsha moyo na kuboresha maisha yako. Ikiwa umefunga ndoa, mwenzi wako wa ndoa anapaswa kuwa rafiki yako wa karibu zaidi.

Rafiki si mtu mnayefahamiana tu. Huenda tunawafahamu watu wengi, kama vile majirani, watu tunaofanya kazi nao, na watu tunaokutana nao mara kwa mara. Urafiki wa kweli unahitaji wakati, nguvu, na uhusiano wa karibu. Kuwa rafiki ya mtu fulani ni jambo lenye thamani. Urafiki una faida, lakini pia unatia ndani majukumu.

Tunapaswa kuwa na mawasiliano mazuri na marafiki wetu. Huenda mawasiliano hayo yakategemea hali. Birgit anasema: “Mmoja wetu anapokuwa na tatizo, mimi na rafiki yangu hupigiana simu mara moja au mbili kwa juma. Inatia moyo kujua kwamba yuko tayari kunisikiliza.” Umbali haupaswi kuwa kizuizi cha urafiki. Gerda na Helga wametenganishwa kwa maelfu ya kilometa, lakini urafiki wao umedumu kwa zaidi ya miaka 35. Gerda anaeleza: “Tunaandikiana barua kwa ukawaida, tukisimulia mambo ambayo yametupata maishani, yawe mazuri au mabaya, na pia tunaeleza hisia zetu. Ninafurahi sana ninapopata barua kutoka kwa Helga. Ni wazi kwamba tunafikiri kwa njia ileile.”

Ushikamanifu ni muhimu kati ya marafiki. Tendo moja la kutokuwa mshikamanifu linaweza kuharibu urafiki wa muda mrefu. Ni kawaida marafiki kushauriana hata kuhusu mambo yao ya siri. Marafiki huzungumza kutoka moyoni bila kuogopa kudharauliwa au siri zao kufichuliwa. Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Kwa kuwa marafiki wetu huchochea jinsi tunavyofikiri, tunavyohisi, na tunavyotenda, ni muhimu tufanye urafiki na watu ambao wanafuata njia ya maisha iliyo sawa na yetu. Kwa mfano, fanya urafiki na watu ambao wana imani kama yako, maoni kama yako kuhusu maadili, na viwango kama vyako kuhusu yaliyo sawa na yasiyo sawa. Marafiki kama hao watakusaidia kutimiza miradi yako. Isitoshe, kwa nini uwe na urafiki pamoja na mtu ambaye viwango na maadili yake hayapatani na yako? Biblia inaonyesha umuhimu wa kuchagua marafiki wazuri inaposema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

Unaweza Kujifunza Kuwa Mshikamanifu

Mtoto anapojua kwamba mbegu zinazonata zinaweza kushikamana na nguo ya mwingine, huenda akataka kucheza na mbegu hizo tena na tena. Ndivyo ilivyo na mtu mshikamanifu. Kwa nini? Kwa sababu tukizoea kuonyesha ushikamanifu inakuwa rahisi kuwa washikamanifu. Ikiwa tangu utotoni mtu anajifunza kuwa mshikamanifu katika familia, baadaye maishani itakuwa rahisi kwake kuwa na urafiki unaotegemea sifa hiyo. Hatimaye, urafiki huo imara na wenye kudumu unaweza kuchangia ushikamanifu katika ndoa. Hilo litamsaidia pia kuwa mshikamanifu katika urafiki ulio muhimu zaidi ya wote.

Yesu alisema kwamba amri iliyo kuu zaidi ni kumpenda Yehova Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili yetu yote, na kwa nguvu zetu zote. (Marko 12:30) Hilo linamaanisha tuna wajibu wa kuwa washikamanifu kabisa kwa Mungu. Kuwa mshikamanifu kwa Yehova Mungu huleta thawabu nyingi. Yehova hatatuvunja moyo kamwe kwani anasema hivi kujihusu: “Mimi ni mshikamanifu.” (Yeremia 3:12) Bila shaka, ushikamanifu au uaminifu kwa Mungu huleta thawabu za milele.—1 Yohana 2:17.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Ushikamanifu wa rafiki mzuri utakuchangamsha moyo

[Picha katika ukurasa wa 5]

Familia yenye ushikamanifu hujali mahitaji ya mmoja na mwenzake