Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwalinda Wale Wanaomtumainia

Yehova Huwalinda Wale Wanaomtumainia

Yehova Huwalinda Wale Wanaomtumainia

“Fadhili zako zenye upendo na ukweli wako zinilinde daima.”—ZABURI 40:11.

1. Mfalme Daudi alimwomba Yehova nini, na ombi hilo linatimizwaje hata sasa?

MFALME DAUDI wa Israeli la kale ‘alimtumainia Yehova kwa bidii’ naye alichochewa kusema kwamba Yehova ‘alimtegea sikio lake na kusikia kilio chake cha kuomba msaada.’ (Zaburi 40:1) Daudi alijionea mara nyingi jinsi Yehova alivyowalinda wale waliompenda. Kwa hiyo, Daudi angeweza kumwomba Yehova amlinde daima. (Zaburi 40:11) Daudi ni kati ya wanaume na wanawake waaminifu ambao wameahidiwa “ufufuo ulio bora.” Sasa yeye yuko katika kumbukumbu ya Yehova na atapokea thawabu hiyo. (Waebrania 11:32-35) Hivyo, hapana shaka yoyote kwamba ataishi wakati ujao. Jina lake limeandikwa katika “kitabu cha kumbukumbu” cha Yehova.—Malaki 3:16.

2. Maandiko hutusaidiaje kuelewa maana ya kulindwa na Yehova?

2 Ingawa watu waaminifu wanaotajwa kwenye Waebrania sura ya 11 waliishi kabla ya Yesu Kristo kuishi duniani, wao waliishi kupatana na jambo ambalo Yesu alifundisha aliposema: “Yule anayeipenda sana nafsi yake huiangamiza, lakini yule anayeichukia nafsi yake katika ulimwengu huu atailinda kwa ajili ya uzima wa milele.” (Yohana 12:25) Hivyo, ni wazi kwamba kulindwa na Yehova hakumaanishi kuwa hatutapatwa na mateso. Kunamaanisha kulindwa kiroho ili tuweze kudumisha msimamo mzuri mbele za Mungu.

3. Tuna uthibitisho gani kwamba Yehova alimlinda Kristo Yesu, na matokeo yakawa nini?

3 Yesu mwenyewe aliteswa kikatili na kushutumiwa, na hatimaye adui zake wakafaulu kumuua kwa njia yenye aibu na yenye kuumiza sana. Lakini hiyo haimaanishi kwamba Mungu alivunja ahadi yake ya kumlinda Masihi. (Isaya 42:1-6) Kufufuliwa kwa Yesu siku ya tatu baada ya kifo chake cha aibu kunathibitisha kwamba Yehova alisikia kilio chake cha kuomba msaada, kama vile alivyosikia kilio cha Daudi. Yehova aliitikia kwa kumpa Yesu nguvu za kudumisha utimilifu. (Mathayo 26:39) Kwa sababu ya ulinzi huo, Yesu alipewa uhai usioweza kufa mbinguni, nao mamilioni ya watu ambao wameonyesha imani katika fidia wana tazamio la kuishi milele.

4. Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wamehakikishiwa nini?

4 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova yuko tayari na anaweza kuwalinda watumishi wake sasa kama alivyofanya siku za Daudi na za Yesu. (Yakobo 1:17) Ndugu za Yesu watiwa-mafuta ambao wamebaki duniani wanaweza kutegemea ahadi hii ya Yehova: “Urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia . . . umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu, mnaolindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati.” (1 Petro 1:4, 5) “Kondoo wengine” wenye tumaini la kuishi duniani, wanaweza pia kumtegemea Mungu na ahadi hii aliyotoa kupitia mtunga-zaburi: “Enyi washikamanifu wake wote, mpendeni Yehova. Yehova anawalinda waaminifu.”—Yohana 10:16; Zaburi 31:23.

Wamelindwa Kiroho

5, 6. (a) Watu wa Mungu wamelindwaje siku hizi? (b) Watiwa-mafuta wana uhusiano gani pamoja na Yehova, na vipi wale walio na tumaini la kuishi duniani?

5 Siku hizi, Yehova ameandaa mipango ya kuwalinda watu wake kiroho. Ingawa yeye hawakingi wasipatwe na mateso, magumu, na misiba ambayo ni ya kawaida maishani, sikuzote amewapa msaada wanaohitaji na kuwatia moyo ili walinde uhusiano wao wa karibu pamoja naye. Wamejenga uhusiano huo juu ya msingi wa imani yao katika fidia ambayo Mungu aliandaa kwa upendo. Baadhi ya Wakristo hao waaminifu wametiwa mafuta kwa roho ya Mungu ili wawe watawala pamoja na Kristo mbinguni. Wametangazwa kuwa waadilifu wakiwa wana wa roho wa Mungu, na maneno haya yanawahusu: “Yeye alitukomboa kutoka katika mamlaka ya giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa upendo wake, ambaye kwa njia yake tunaachiliwa huru kupitia fidia, kusamehewa dhambi zetu.”—Wakolosai 1:13, 14.

6 Mamilioni ya Wakristo wengine waaminifu wamehakikishiwa kwamba wao pia wanaweza kunufaika na maandalizi ya Mungu ya fidia. Tunasoma hivi: “Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake iwe fidia badala ya wengi.” (Marko 10:45) Katika wakati unaofaa, Wakristo hao wanatazamia kufurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Kwa sasa wanathamini urafiki wao na Mungu, nao hujitahidi kikweli kuimarisha uhusiano huo.

7. Leo Yehova hulindaje hali ya kiroho ya watu wake?

7 Njia moja ambayo Yehova huwalinda watu wake kiroho ni kwa kuandaa mpango wa kuwazoeza hatua kwa hatua. Mpango huo huwawezesha kuijua kweli kwa usahihi zaidi. Yehova pia huendelea kuwaongoza kupitia Neno lake, tengenezo lake, na roho yake takatifu. Chini ya mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” watu wa Mungu ulimwenguni pote ni kama familia ya kimataifa. Jamii ya mtumwa hushughulikia mahitaji ya kiroho na inapohitajika inashughulikia pia mahitaji ya kimwili ya familia ya watumishi wa Yehova, hata wawe wa taifa au tabaka gani.—Mathayo 24:45.

8. Yehova ana uhakika gani kuhusu washikamanifu wake, naye anawahakikishia nini?

8 Yehova hakumlinda Yesu asishambuliwe na adui zake. Vivyo hivyo, leo yeye hawalindi Wakristo wasishambuliwe na adui zao. Lakini hilo halimaanishi hata kidogo kwamba Mungu hapendezwi na Wakristo! Bali, linaonyesha kwamba ana uhakika wataunga mkono upande wake kuhusiana na suala kuu linalohusu ulimwengu wote. (Ayubu 1:8-12; Methali 27:11) Yehova hatawaacha kamwe walio washikamanifu kwake, “kwa maana Yehova ni mpenda-haki, naye hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 37:28.

Fadhili Zenye Upendo na Ukweli Huwalinda

9, 10. (a) Ukweli wa Yehova huwalindaje watu wake? (b) Biblia huonyeshaje kwamba Yehova huwalinda washikamanifu wake kupitia fadhili zake zenye upendo?

9 Katika sala yake kwenye Zaburi 40, Daudi aliomba fadhili zenye upendo za Yehova na ukweli wake zimlinde. Kwa kuwa Yehova ni Mungu wa ukweli na anapenda uadilifu, yeye hueleza viwango vyake waziwazi. Wale wanaofuata viwango hivyo maishani huepuka matatizo mengi, hofu, na taabu zinazowapata wale wanaovipuuza. Kwa mfano, tukiepuka dawa za kulevya, ulevi, uasherati, na maisha yenye jeuri, tunaweza kujikinga na kuwakinga wapendwa wetu wasipatwe na matatizo yenye kuhuzunisha. Hata wale wanaoiacha njia ya Yehova ya ukweli, kama vile Daudi alivyofanya nyakati nyingine, wanahakikishiwa kwamba Mungu bado ni ‘mahali pa kujificha’ kwa wakosaji wenye kutubu. Watu hao wanaweza kupaaza sauti hivi kwa shangwe: “Utanilinda kutokana na taabu.” (Zaburi 32:7) Huo ni wonyesho ulioje wa fadhili zenye upendo za Mungu!

10 Mungu pia huonyesha fadhili zake zenye upendo kwa kuwaonya watumishi wake wajitenge na ulimwengu mwovu, ambao utaharibiwa hivi karibuni. Tunasoma hivi: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” Kwa kutii onyo hilo, tunaweza kulinda maisha yetu kihalisi kwa umilele wote, kwa kuwa andiko hilo linaendelea kusema: “Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:15-17.

Uwezo wa Kufikiri, Utambuzi, na Hekima Huwalinda

11, 12. Eleza jinsi uwezo wa kufikiri, utambuzi, na hekima hutulinda.

11 Sulemani mwana wa Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi kuhusu wale wanaotumainia kukubaliwa na Mungu: “Uwezo wa kufikiri utakutunza, utambuzi utakulinda.” Pia alihimiza: “Jipatie hekima . . . Usiiache, nayo itakutunza. Ipende, nayo itakulinda.”—Methali 2:11; 4:5, 6.

12 Tunatumia uwezo wa kufikiri tunapotafakari juu ya mambo tunayojifunza katika Neno la Mungu. Kufanya hivyo hutuwezesha kuwa na utambuzi mwingi zaidi na hivyo kuweza kutanguliza mambo yanayofaa. Hilo ni muhimu, kwa kuwa wengi wetu tunajua, labda kupitia mambo yaliyotupata, kwamba matatizo hutokea wakati watu wanapotanguliza mambo yasiyofaa, iwe wanajua au hawajui. Ulimwengu wa Shetani huweka mbele yetu miradi ya kuwa matajiri, mashuhuri, au kuwa na uwezo, bali Yehova hukazia miradi ya kiroho iliyo muhimu zaidi. Kutanguliza miradi ya kimwili badala ya ile ya kiroho kunaweza kusambaratisha familia, kuvunja urafiki, na kufanya tupuuze mambo ya kiroho. Kwa hiyo, hali ya mtu inaweza kuwa kama ile inayoonyeshwa na maneno haya ya Yesu: “Mtu anapata faida gani ikiwa ataupata ulimwengu wote na kuipoteza nafsi yake?” (Marko 8:36) Ikiwa tuna hekima tutatii maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:33.

Hatari ya Kuwa na Ubinafsi

13, 14. Inamaanisha nini kuwa mwenye ubinafsi, na kwa nini si jambo la hekima kuwa hivyo?

13 Ni kawaida kwa wanadamu kujifikiria wenyewe. Hata hivyo, tatizo hutokea wakati tamaa na mapendezi ya mtu yanapotawala maisha yake. Kwa hiyo, Yehova hutuagiza tuepuke ubinafsi ili kulinda urafiki wetu pamoja naye. Neno ubinafsi humaanisha “hali ya mtu kujifikiria na kujipenda yeye mwenyewe.” Leo watu wengi hujifikiria wenyewe tu. Biblia ilitabiri kwamba “katika siku za mwisho” za mfumo mwovu wa Shetani, “watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe,” au wenye ubinafsi.—2 Timotheo 3:1, 2.

14 Wakristo wanaelewa kwamba ni jambo la hekima kutii amri ya Biblia ya kuwafikiria wengine, na kuwapenda jinsi mtu anavyojipenda mwenyewe. (Luka 10:27; Wafilipi 2:4) Huenda watu kwa ujumla wakaona hilo haliwezekani. Lakini ni muhimu kufanya hivyo ili tuwe na ndoa zenye mafanikio, mahusiano ya familia yenye furaha, na urafiki wenye kuridhisha. Hivyo, mtumishi wa kweli wa Yehova hapaswi kamwe kuruhusu maisha yake yatawaliwe na tamaa ya asili ya kujifikiria mwenyewe tu, huku akipuuza mambo yaliyo muhimu zaidi. Kutanguliza mapenzi ya Mungu wake, Yehova, ndilo jambo muhimu kabisa.

15, 16. (a) Mtazamo wa ubinafsi unaweza kutokeza nini, kama inavyoonyeshwa na nani? (b) Kwa kweli, kuwa mwepesi kuwahukumu wengine ni sawa na kufanya nini?

15 Ubinafsi unaweza kufanya mtu ajione kuwa mwadilifu. Hilo linaweza kufanya awe kimbelembele na asikubali maoni ya wengine. Kwa kufaa, Biblia inasema: “Wewe huna sababu ya kujitetea, Ee mwanadamu, hata uwe nani, ukihukumu; kwa maana katika jambo lile ambalo unamhukumu mwingine, unajihukumu mwenyewe kuwa una hatia, kwa sababu wewe unayehukumu una mazoea ya kufanya mambo hayo hayo.” (Waroma 2:1; 14:4, 10) Viongozi wa dini katika siku za Yesu walijiona kuwa waadilifu sana hivi kwamba walihisi wanastahili kumshutumu Yesu na mitume wake. Kwa kutenda hivyo, walijifanya kuwa waamuzi. Kwa kweli, walijiletea hukumu kwa kushindwa kutambua kasoro zao.

16 Yuda, mfuasi wa Yesu aliyemsaliti, alianza kuwahukumu wengine. Pindi moja huko Bethania, Yuda alipinga vikali wakati Maria, dada ya Lazaro, alipomtia Yesu mafuta yenye marashi. Alionyesha ghadhabu yake kwa kusema: “Kwa nini mafuta haya yenye marashi hayakuuzwa kwa dinari mia tatu na kupewa maskini?” Lakini Biblia inaendelea kusema hivi: “Ingawa hivyo, alisema hilo si kwa sababu aliwahangaikia maskini, bali kwa sababu yeye alikuwa mwizi na alikuwa na sanduku la pesa na alikuwa akichukua pesa zilizowekwa ndani yake.” (Yohana 12:1-6) Tusiwe kama Yuda au wale viongozi wa dini, waliokuwa wepesi kuwahukumu wengine, na hivyo kujihukumu wenyewe.

17. Eleza hatari ya kujidai au kujitumaini kupita kiasi.

17 Inasikitisha kwamba Wakristo fulani wa mapema walikuwa wenye kiburi na wenye kujidai, ingawa hawakuwa wezi kama Yuda. Yakobo aliandika hivi kuwahusu: “Mnajivunia kujigamba kwenu kwa kujidai.” Kisha akaongeza: “Majivuno yote ya namna hiyo ni maovu.” (Yakobo 4:16) Tunajidhuru wenyewe tunapojisifu kwa mambo tuliyotimiza au mapendeleo yetu katika utumishi wa Yehova. (Methali 14:16) Tunakumbuka yaliyompata mtume Petro ambaye pindi moja alijitumaini kupita kiasi na kujisifu hivi: “Ijapokuwa wengine wote wakwazike kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe! . . . Hata nikilazimika kufa pamoja nawe, mimi sitakukana kamwe.” Kwa kweli, sisi hatuna sababu ya kujisifu. Vitu vyote tulivyo navyo vimetokana na fadhili zenye upendo za Yehova. Kukumbuka jambo hilo kutatusaidia tuepuke kujidai.—Mathayo 26:33-35, 69-75.

18. Yehova huhisije kuhusu kiburi?

18 Tunaambiwa kwamba “kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” Kwa nini? Yehova anajibu: “Nimechukia kujiinua na kiburi.” (Methali 8:13; 16:18) Haishangazi kwamba Yehova alighadhabishwa na “dharau la moyo wa mfalme wa Ashuru na kwa ajili ya kujihesabia makuu kwa majivuno ya macho yake”! (Isaya 10:12) Yehova alimwadhibu mfalme huyo. Hivi karibuni Mungu ataadhibu ulimwengu wote wa Shetani pia, kutia ndani viongozi wake wenye kiburi ambao hujiona kuwa wa maana, wawe wenye kuonekana au wasioonekana. Tusiige kamwe mtazamo huo wa ushupavu wa adui za Yehova!

19. Watu wa Mungu wanawezaje kujivunia kumtumikia Yehova na wakati huohuo kuwa wanyenyekevu?

19 Wakristo wa kweli wana kila sababu ya kujivunia kuwa watumishi wa Yehova. (Yeremia 9:24) Wakati huohuo, wana kila sababu ya kuwa wanyenyekevu. Kwa nini? Kwa sababu “wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa hiyo, ili kulinda msimamo wetu tukiwa watumishi wa Yehova, lazima tuwe na mtazamo kama wa mtume Paulo aliyesema kwamba “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-dhambi.” Kisha akaongeza: “Kati ya hao mimi ni wa kwanza kabisa.”—1 Timotheo 1:15.

20. Yehova huwalindaje watu wake leo, naye atawalindaje wakati ujao?

20 Kwa kuwa watu wa Yehova hutanguliza mapenzi yake badala ya mapendezi yao wenyewe, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwalinda kiroho. Pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba dhiki kuu itakapotokea, Yehova atawalinda kiroho na kimwili. Watakapoingia katika ulimwengu mpya wa Mungu, wataweza kupaaza sauti hivi: “Tazama! Huyu ndiye Mungu wetu. Tumemtumaini yeye, naye atatuokoa. Huyu ndiye Yehova. Tumemtumaini yeye. Na tuwe na shangwe na kushangilia katika wokovu wake.”—Isaya 25:9.

Je, Unakumbuka?

• Mfalme Daudi na Yesu Kristo walilindwaje?

• Watu wa Yehova hulindwaje leo?

• Kwa nini tuepuke kujifikiria kupita kiasi?

• Kwa nini tunaweza kujivunia kumtumikia Yehova na wakati huohuo kuwa wanyenyekevu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yehova aliwalindaje Daudi na Yesu?

[Picha katika ukurasa wa 10, 11]

Ni katika njia zipi watu wa Mungu hulindwa kiroho leo?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ingawa tunajivunia kumtumikia Yehova, lazima sikuzote tuwe wanyenyekevu