Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini Tukufu la Ufufuo

Tumaini Tukufu la Ufufuo

Tumaini Tukufu la Ufufuo

WATU wengi wanaamini ufufuo. Kitabu kitakatifu cha Waislamu, Kurani, kina sura nzima inayozungumzia ufufuo. Sehemu fulani ya Sura ya 75 inasema: “Naapa kwa siku ya Kiama . . . Anadhani mtu ya kuwa sisi hatutaikusanya mifupa yake? . . . Anauliza: ‘Itakuwa lini hiyo siku ya Kiama?’ . . . Je! Hakuwa Huyo ni Muweza wa kuhuisha wafu?”—Sura 75:1-6, 40.

Kulingana na kitabu The New Encyclopædia Britannica, dini ya Zoroaster “hufundisha kwamba Uovu utashindwa kabisa, kutakuwa na ufufuo wa watu kwa ujumla, Hukumu ya Mwisho, na kusafishwa kwa ulimwengu kwa ajili ya waadilifu.”

Kitabu Encyclopaedia Judaica hufafanua ufufuo kuwa “imani kwamba hatimaye wafu watafufuliwa na kuishi tena duniani.” Kitabu hichohicho kinasema pia kwamba fundisho lililokubaliwa rasmi katika Dini ya Kiyahudi kuwa mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa linatatanisha. Kinakiri hivi: “Imani katika ufufuo inapingana na imani katika nafsi isiyoweza kufa.”

Wahindu hufundisha kwamba mwanadamu huzaliwa upya katika mwili mwingine tena na tena. Kwa hiyo, lazima mwanadamu awe na nafsi inayoendelea kuishi baada ya kifo ili aweze kuzaliwa upya. Kitabu kitakatifu cha Wahindu, Bhagavad Gita, kinasema: “Nafsi iliyo katika kila sehemu ya mwili haiwezi kuharibiwa. Hakuna anayeweza kuharibu nafsi isiyoweza kuharibiwa.”

Wabudha hutofautiana na Wahindu kwa kufundisha kwamba nafsi inaweza kufa. Hata hivyo, leo Wabudha wengi katika Mashariki ya Mbali wanaamini kwamba nafsi haifi bali huhama na kuingia katika mwili mwingine. *

Wachanganyikiwa Kuhusu Fundisho la Ufufuo

Mara nyingi dini zinazojidai kuwa za Kikristo hutaja ufufuo na pia nafsi inayoendelea kuishi baada ya kifo katika ibada zao za mazishi. Kwa mfano, ni kawaida kwa kasisi Mwanglikana kukariri maneno haya: ‘Kwa kuwa imempendeza Mungu Mweza-Yote katika rehema zake nyingi kuichukua nafsi ya ndugu yetu mpendwa ambaye ametuacha, basi tunaurudisha mwili wake kwenye ardhi; udongo urudi kwenye udongo, majivu yarudi kwenye majivu, na mavumbi yarudi kwenye mavumbi; tukitumaini kabisa kwamba Bwana wetu Yesu Kristo atamfufua aishi milele.’—The Book of Common Prayer.

Maneno hayo yanaweza kumtatanisha mtu asijue kama Biblia hufundisha kuhusu ufufuo au nafsi isiyoweza kufa. Hata hivyo, ona maneno yaliyoandikwa na Oscar Cullmann, ambaye ni Profesa Mprotestanti nchini Ufaransa. Anaandika hivi katika kitabu chake, Immortality of the Soul or Resurrection of the Dead?: “Kuna tofauti kubwa kati ya imani ya Wakristo katika ufufuo wa wafu na imani ya Wagiriki katika nafsi isiyoweza kufa. . . . Ingawa baadaye Ukristo ulionyesha kwamba imani hizi mbili zinahusiana, na leo Mkristo wa kawaida amechanganyikiwa kuhusu imani hizo, sioni sababu ya kuficha kile ambacho mimi na wasomi wengi hukiona kuwa kweli. . . . Imani katika ufufuo ndilo fundisho muhimu katika Agano Jipya. . . . Mwanadamu aliyekufa kabisa hufufuliwa kupitia tendo jipya la uumbaji.”

Haishangazi kwamba watu kwa ujumla wamechanganyikiwa kuhusu kifo na ufufuo. Ili kutatua tatizo hilo, tunahitaji kuitegemea Biblia ambayo ina kweli zilizofunuliwa na Muumba wa mwanadamu, Yehova Mungu. Biblia imetaja visa kadhaa vya ufufuo. Acheni tuchunguze visa vinne na tuone mambo ambayo vinafunua kuhusu ufufuo.

“Wanawake Waliwapokea Wafu Wao kwa Ufufuo”

Katika barua yake kwa Wayahudi waliokuwa Wakristo, mtume Paulo alisema kwamba wanawake wenye imani “waliwapokea wafu wao kwa ufufuo.” (Waebrania 11:35) Mmoja wao aliishi Sarefathi, mji wa Foinike uliokuwa karibu na Sidoni kwenye Pwani ya Mediterania. Mwanamke huyo alikuwa mjane, naye alimkaribisha Eliya nabii wa Mungu na hata kumpa chakula wakati wa njaa kali. Kwa kusikitisha, mwana wa mwanamke huyo alishikwa na ugonjwa na kufa. Eliya alimpeleka mvulana huyo moja kwa moja kwenye chumba cha darini, ambako nabii huyo alikuwa akikaa, kisha akamwomba Yehova amfufue. Muujiza ulitokea, na kijana huyo “akawa hai.” Eliya alimrudisha kwa mama yake na kusema: “Tazama, mwana wako yuko hai.” Mwanamke huyo alifanyaje? Alisema hivi kwa furaha: “Kwa kweli sasa najua kwamba wewe ni mtu wa Mungu na kwamba neno la Yehova kinywani mwako ni la kweli.”—1 Wafalme 17:22-24.

Elisha aliyekuwa nabii baada ya Eliya, alitunzwa na mtu mmoja na mkewe ambao waliishi umbali wa kilometa 100 hivi kusini ya Sarefathi. Mke wa mtu huyo alikuwa mashuhuri katika kijiji cha kwao cha Shunemu. Yeye na mumewe walikubali Elisha akae katika chumba cha darini nyumbani kwao. Walikuwa na huzuni kwa sababu hawakuwa na watoto, lakini walifurahi mwanamke huyo alipozaa mtoto wa kiume. Mvulana huyo alipoendelea kukua, mara nyingi alikuwa akienda shambani kujiunga na wavunaji na babake. Siku moja, msiba ulitokea. Mvulana huyo alisema kwamba anaumwa na kichwa. Mtumishi mmoja alimpeleka nyumbani haraka ambako mamake alimweka kwenye mapaja yake. Lakini mtoto huyo akafa. Mama huyo mwenye huzuni aliamua kumwita Elisha amsaidie. Huku akiandamana na mtumishi fulani, mama huyo alisafiri kuelekea Mlima Karmeli, upande wa kaskazini-magharibi, ambako Elisha alikuwa akikaa.

Nabii huyo alimtuma Gehazi, mtumishi wake, atangulie, naye akakuta kwamba kwa hakika mvulana huyo alikuwa amekufa. Elisha na mwanamke huyo walikuja baadaye, lakini ni nini kilichotukia walipofika Shunemu? Andiko la 2 Wafalme 4:32-37 linasema: “Mwishowe Elisha akaingia katika hiyo nyumba, na, tazama, huyo mvulana alikuwa amekufa, amelazwa juu ya kitanda chake. Ndipo akaingia ndani, akafunga mlango nyuma yao wawili, akaanza kusali kwa Yehova. Mwishowe akaenda juu, akajilaza juu ya yule mtoto, akakitia kinywa chake juu ya kinywa chake, na macho yake juu ya macho yake, na mikono yake juu ya mikono yake, akaendelea kuinama juu yake, na hatua kwa hatua mwili wa mtoto ukawa na joto. Kisha akaanza kutembea tena ndani ya nyumba, mara moja huku mara moja kule, halafu akaenda juu, akainama juu yake. Na yule mvulana akaanza kupiga chafya mara saba, kisha mvulana huyo akafungua macho yake. Sasa akamwita Gehazi na kusema: ‘Mwite huyo mwanamke Mshunamu.’ Basi akamwita, naye akaingia kwake. Kisha akasema: ‘Mchukue mwana wako.’ Naye akaingia, akaanguka miguuni pake, akamwinamia mpaka chini, kisha akamchukua mwana wake, akatoka nje.”

Kama yule mjane wa Sarefathi, mwanamke huyo wa Shunemu alijua kwamba mtoto wake alifufuliwa kwa nguvu za Mungu. Wanawake hao wawili walipata shangwe kubwa Mungu alipowafufua watoto wao wapendwa.

Ufufuo Wakati wa Huduma ya Yesu

Miaka 900 hivi baadaye, ufufuo ulitokea kaskazini ya Shunemu, nje ya kijiji cha Naini ambacho hakikuwa mbali na Shunemu. Yesu Kristo na wanafunzi wake waliposafiri kutoka Kapernaumu na kukaribia lango la Naini, walikutana na msafara wa mazishi, na Yesu akamwona mjane aliyekuwa amefiwa na mwanawe wa pekee. Yesu alimwambia aache kulia. Luka, ambaye alikuwa daktari, anaeleza kilichotukia: “Ndipo [Yesu] akakaribia na kuligusa sanduku, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Kijana, ninakuambia, Inuka!’ Na huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake.” (Luka 7:14, 15) Wale walioona muujiza huo walimtukuza Mungu. Habari kuhusu ufufuo huo zilienea upande wa kusini hadi Yudea na wilaya ya karibu. Wanafunzi wa Yohana Mbatizaji walisikia habari hizo, nao wakamweleza Yohana kuhusu muujiza huo. Yohana naye akawatuma kumtafuta Yesu na kumuuliza kama Yeye ndiye Masihi anayetarajiwa. Yesu aliwaambia: “Nendeni, mkamwambie Yohana yale mliyoona na kusikia: vipofu wanaona, vilema wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa na viziwi wanasikia, na wafu wanafufuliwa, maskini wanaambiwa ile habari njema.”—Luka 7:22.

Muujiza ambao Yesu alifanya alipomfufua rafiki yake Lazaro ndio maarufu zaidi kati ya miujiza yake ya ufufuo. Katika kisa hiki kuhusu kifo cha Lazaro, Yesu hakwenda nyumbani kwa akina Lazaro moja kwa moja. Hatimaye, Yesu alipofika Bethania, Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne. Yesu alipoagiza kwamba jiwe lililokuwa kwenye mlango wa kaburi liondolewe, Martha alikataa na kusema hivi: “Bwana, kufikia sasa lazima awe ananuka, kwa maana ni siku nne.” (Yohana 11:39) Hata hivyo, Lazaro alifufuliwa licha ya kuharibika kwa mwili wake. Kwa amri ya Yesu, “huyo mtu aliyekuwa mfu akatoka miguu na mikono yake ikiwa imefungwa vitambaa, na uso wake ulikuwa umefungwa-fungwa kwa kitambaa.” Matendo ya adui za Yesu baadaye yanathibitisha pasipo shaka kwamba Lazaro alifufuliwa.—Yohana 11:43, 44; 12:1, 9-11.

Tunafikia mkataa gani kutokana na visa hivyo vinne vya ufufuo? Kila aliyefufuliwa alikuwa mtu yuleyule aliyekufa. Wote walitambuliwa na watu, kutia ndani jamaa zao wa karibu. Hakuna yeyote kati yao aliyeeleza kilichotukia katika kipindi kifupi alipokuwa mfu. Hakuna yeyote aliyetaja kwamba alisafiri kwenda katika ulimwengu mwingine. Yaonekana wote walifufuliwa wakiwa na afya nzuri. Kama Yesu alivyodokeza, ni kana kwamba walikuwa wamelala usingizi kwa muda mfupi, kisha wakaamka. (Yohana 11:11) Hata hivyo, wote walikufa baadaye.

Tazamio Tukufu la Kuwaona Tena Wapendwa Wetu

Muda mfupi baada ya kifo chenye kuhuzunisha cha Owen, aliyetajwa katika makala inayotangulia, babake alimtembelea jirani. Akiwa huko, aliona juu ya meza kikaratasi cha kuwakaribisha watu kwenye hotuba ya watu wote iliyopangwa na Mashahidi wa Yehova. Kichwa cha hotuba hiyo, “Wafu Wako Wapi?,” kilimvutia. Alikuwa anajiuliza swali hilohilo. Alienda kusikiliza hotuba hiyo naye akapata faraja ya kweli kutoka katika Biblia. Alijifunza kwamba wafu hawateseki. Badala ya kuteseka motoni au kuchukuliwa na Mungu ili wawe malaika mbinguni, wafu, kutia ndani Owen, wanangojea kaburini hadi watakapoamshwa katika ufufuo.—Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4.

Je, familia yako imepatwa na msiba? Je, kama vile babake Owen, wewe unataka kujua mahali walipo wapendwa wako waliokufa na kama inawezekana kuwaona tena? Basi tunakualika uchunguze mafundisho zaidi ya Biblia kuhusu ufufuo. Labda unajiuliza: ‘Ufufuo utakuwa lini? Ni nani hasa watakaofufuliwa?’ Tafadhali soma makala zinazofuata ambazo zitazungumzia maswali hayo na mengineyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, ukurasa wa 150-154, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Eliya alimwomba Yehova amfufue mvulana fulani

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yehova alimtumia Elisha kumfufua mwana wa mwanamke Mshunamu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yesu alimfufua mwana wa mjane wa Naini

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ufufuo utawaunganisha jamaa na wapendwa wao tena