Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jinsi Kazi Zako Zilivyo Nyingi, Ee Yehova!”

“Jinsi Kazi Zako Zilivyo Nyingi, Ee Yehova!”

Fahari ya Uumbaji wa Yehova

“Jinsi Kazi Zako Zilivyo Nyingi, Ee Yehova!”

MAHALI popote tulipo, iwe ni katika sehemu za mashambani au mijini, juu milimani au pwani, tumezungukwa na uumbaji wenye fahari na wenye kuvutia. Kwa kufaa, Kalenda ya Mwaka wa 2004 ya Mashahidi wa Yehova ina mandhari ya kazi zenye kustaajabisha za Yehova Mungu.

Wanadamu wenye shukrani wamependezwa sikuzote na kazi za Mungu. Kwa mfano, mfikirie Sulemani ambaye alikuwa na hekima “pana zaidi kuliko hekima ya watu wengine wote wa Mashariki.” Biblia inasema: “Alikuwa akisema kuhusu miti, kuanzia mwerezi ulio katika Lebanoni mpaka mhisopo unaomea juu ya ukuta; na alikuwa akisema kuhusu wanyama na kuhusu viumbe vinavyoruka na kuhusu vitu vyenye kutambaa na kuhusu samaki.” (1 Wafalme 4:30, 33) Mara kwa mara, Mfalme Daudi, aliyekuwa baba ya Sulemani alitafakari kazi bora za Mungu. Alichochewa kumwambia hivi Mtengenezaji wake kwa shauku: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyotokeza.”—Zaburi 104:24. *

Sisi pia tunapaswa kuchunguza na kutafakari uumbaji. Kwa mfano, tunaweza ‘kuinua macho yetu juu’ na kuuliza: “Ni nani ameviumba vitu hivi?” Ni Yehova Mungu, ambaye ana “wingi wa nguvu zenye msukumo” na ambaye kwa kweli ni “hodari katika nguvu”!—Isaya 40:26.

Kutafakari kazi za uumbaji za Yehova kunapaswa kuwe na matokeo gani kwetu? Kutatufaidi katika angalau njia tatu. Kunaweza (1) kutukumbusha tuthamini uhai wetu, (2) kutusukuma tuwasaidie wengine wajifunze kutokana na uumbaji, na (3) kutuchochea tumjue na kumthamini Muumba wetu hata zaidi.

Uhai wetu tukiwa wanadamu ni wa hali ya juu sana kuliko ule wa “wanyama wasiofikiri,” kwa hiyo tunaweza kuchunguza na kuthamini maajabu ya uumbaji. (2 Petro 2:12) Macho yetu yanaweza kuona mandhari yenye kupendeza. Masikio yetu yanaweza kusikia nyimbo tamu za ndege. Nao uwezo wetu wa kutambua wakati na mahali hufanya tukumbuke mandhari yenye kupendeza. Hata ingawa maisha yetu ya sasa si makamilifu, bila shaka tunafurahia kuwa hai!

Wazazi wanaweza kufurahia watoto wao wanapovutiwa sana na uumbaji. Watoto hufurahia sana kuokota makombe kwenye ufuo wa bahari, kumpapasa-pasa mnyama, na kupanda miti. Wazazi watataka kuwasaidia watoto wao waone kwamba Muumba ndiye aliyeviumba vitu vyote. Kwa kufanya hivyo, watoto wao watapendezwa na kuheshimu uumbaji wa Yehova katika maisha yao yote.—Zaburi 111:2, 10.

Tungekuwa watu wasio na busara hata kidogo ikiwa tungevutiwa na uumbaji na tukose kumsifu Muumba. Unabii wa Isaya unatusaidia kutafakari jambo hilo unaposema: “Je, hujajua au, je, hujasikia? Yehova, Muumba wa miisho ya dunia, ni Mungu mpaka wakati usio na kipimo. Yeye hachoki wala hazimii. Haiwezekani kuchunguza kikamilifu uelewaji wake.”—Isaya 40:28.

Naam, kazi za Yehova huthibitisha hekima yake isiyo na kifani, nguvu zake zisizo na mipaka, na upendo wake mwingi kutuelekea. Tunapotazama uzuri wote unaotuzunguka na kutambua sifa za Yule aliyevifanya vitu hivyo vyote, tunachochewa kusema kama alivyosema Daudi: “Hakuna yeyote aliye kama wewe.  . . , Ee Yehova, wala hakuna kazi zozote kama zako.”—Zaburi 86:8.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba wanadamu watiifu wataendelea kustaajabishwa na kazi za uumbaji za Yehova. Tutakuwa na nafasi ya kujifunza mengi kumhusu Yehova milele. (Mhubiri 3:11) Na kadiri tunavyojifunza kumhusu, ndivyo tutakavyozidi kumpenda Muumba wetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona Kalenda ya Mwaka wa 2004 ya Mashahidi wa Yehova, Novemba/Desemba.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Sifa kwa Muumba

Wanasayansi wengi wenye uthamini hukubali kwamba Mungu alihusika katika uumbaji. Ifuatayo ni mifano michache:

“Jambo kuu na furaha yangu katika nyanja ya sayansi ninayoshughulikia huwa ninapovumbua kitu kipya na kujiambia, ‘Kumbe! hivi ndivyo Mungu alivyofanya.’ Lengo langu ni kuelewa angalau sehemu ndogo ya mpango wa Mungu.” —Henry Schaefer, profesa wa kemia.

“Kila mtu hufikia mkataa wake mwenyewe kuhusu kwa nini Ulimwengu unapanuka, lakini hatuwezi kufikia mkataa sahihi pasipo Mungu.” —Edward Milne, mtaalamu wa anga, Mwingereza.

“Vitu vyote hufuata utaratibu sahihi kabisa wa hisabati ya hali ya juu kwa sababu viliumbwa na Mungu.”—Alexander Polyakov, mwanahisabati Mrusi.

“Tunapojifunza kuhusu vitu vya asili, tunachunguza maoni ya Muumba, tunaelewa mawazo yake, na kufafanua mfumo Wake bali si wetu.”—Louis Agassiz, mwanabiolojia Mmarekani.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Pengwini aina ya Gentoo katika Rasi ya Antaktika

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mbuga ya Kitaifa ya Wanyama ya Grand Teton, Wyoming, Marekani

[Hisani]

Jack Hoehn/Index Stock Photography