Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujitahidi Kuonyesha Fadhili Katika Ulimwengu Wenye Uadui

Kujitahidi Kuonyesha Fadhili Katika Ulimwengu Wenye Uadui

Kujitahidi Kuonyesha Fadhili Katika Ulimwengu Wenye Uadui

“Kinachotamanika katika mtu wa udongo ni fadhili zake zenye upendo.”—METHALI 19:22.

1. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kuonyesha fadhili?

JE, WEWE hujiona kuwa mtu mwenye fadhili? Ikiwa ndivyo, inaweza kuwa vigumu kuishi katika ulimwengu wa sasa. Kwa kweli, katika Biblia sifa ya fadhili inatajwa kuwa sehemu ya “matunda ya roho,” lakini kwa nini ni vigumu sana kuonyesha fadhili hata katika nchi zinazoitwa za Kikristo? (Wagalatia 5:22) Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, jibu hilo linaweza kupatikana kwa sehemu katika maneno ambayo mtume Yohana aliandika, yaani, ulimwengu mzima unatawaliwa na mtu fulani wa roho asiye na fadhili, Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Yesu Kristo alimtambulisha Shetani kuwa “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Hivyo, ulimwengu huu una mwelekeo kama wa mtawala wake mwasi na mkatili.—Waefeso 2:2.

2. Ni magumu gani yanayoweza kufanya tusionyeshe fadhili?

2 Maisha yetu huathiriwa sana wengine wanapotutendea kwa njia isiyo ya fadhili. Ukosefu huo wa fadhili unaweza kuonyeshwa na majirani wenye chuki, watu wenye ubaridi tusiowajua, na hata marafiki na watu wa familia ambao nyakati nyingine wanaweza kutenda bila kufikiri. Mara nyingi sisi huumizwa sana na mkazo wa kushughulika na watu wenye jeuri, ambao hupigiana kelele na kutukanana. Wengine wanapokosa kuonyesha fadhili, jambo hilo linaweza kutufanya tuwe na chuki, na huenda tukataka kulipiza kisasi kwa kuwatendea wengine bila fadhili. Huenda mtazamo huo hata ukasababisha matatizo ya afya ya kimwili au ya kiroho.—Waroma 12:17.

3. Watu hukabili matatizo gani makubwa ambayo hufanya iwe vigumu kwao kuonyesha fadhili?

3 Pia hali za ulimwengu zenye mkazo zinaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuonyesha fadhili. Kwa mfano, wanadamu kwa ujumla hupatwa na mkazo kwa sababu ya vitisho na vitendo vya kigaidi, na pia uwezekano wa kutumiwa kwa silaha za kibiolojia au za nyuklia na vikundi mbalimbali vya mataifa. Isitoshe, mamilioni ya watu ni maskini, nao hupata chakula, makao, mavazi, na matibabu ya kuwawezesha tu kuendelea kuishi. Inakuwa vigumu kufuatia fadhili hali zinapoonekana kuwa zenye kukatisha tamaa.—Mhubiri 7:7.

4. Watu fulani wanaweza kufikia mkataa gani wenye makosa wanapofikiria kuwaonyesha wengine fadhili?

4 Mtu anaweza kufikia mkataa kwa urahisi kwamba si jambo muhimu sana kuonyesha fadhili na huenda hata akaona kufanya hivyo kuwa ishara ya udhaifu. Huenda akahisi ametendewa isivyo haki hasa wengine wanapomtendea bila kujali hisia zake. (Zaburi 73:2-9) Hata hivyo, Biblia inatutolea mwongozo ufaao inaposema: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Methali 15:1) Upole na fadhili ni sehemu mbili za matunda ya roho yanayohusiana sana, na hizo ni sifa muhimu sana mtu anapokabili hali ngumu.

5. Tunahitaji kuonyesha fadhili katika sehemu zipi za maisha?

5 Kwa kuwa ni muhimu sana kuonyesha matunda ya roho takatifu ya Mungu tukiwa Wakristo, tunapaswa kufikiria jinsi tunavyoweza kuonyesha mojawapo ya sifa hizo, yaani, fadhili. Je, inawezekana kufuatia fadhili katika ulimwengu wenye uadui? Ikiwa ndivyo, ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba haturuhusu uvutano wa Shetani utuzuie kuonyesha fadhili, hasa tunapokabili mikazo? Na tuone jinsi tunavyoweza kufuatia fadhili katika familia, katika huduma, kazini, shuleni, na pamoja na majirani na waamini wenzetu.

Fadhili Katika Familia

6. Kwa nini sifa ya fadhili ni muhimu sana katika familia, nayo inaweza kuonyeshwaje?

6 Ili kupata baraka na mwongozo wa Yehova, matunda ya roho ni muhimu, nayo yanahitaji kusitawishwa kikamili. (Waefeso 4:32) Na tuzungumzie uhitaji wa washiriki wa familia wa kuonyeshana fadhili. Katika shughuli zao za kila siku, mume na mke wanapaswa kuonyesha roho ya fadhili na ya kujali kati yao na kwa watoto wao. (Waefeso 5:28-33; 6:1, 2) Sifa hiyo ya fadhili inahitaji kuwa wazi katika njia ambayo washiriki wa familia huzungumziana, huku watoto wakiwaheshimu wazazi, nao wazazi wakiwatendea watoto wao ifaavyo. Usiwe mwepesi kushutumu, bali uwe mwepesi kupongeza.

7, 8. (a) Tunapaswa kuepuka mwenendo gani ili kuonyesha fadhili za kweli katika familia? (b) Mawasiliano mazuri husaidiaje kuwa na familia thabiti? (c) Unawezaje kuonyesha fadhili katika familia yako?

7 Ili tuwe wenye fadhili kwa washiriki wa familia yetu tunahitaji kufuata shauri hili la mtume Paulo: “Kwa kweli, yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.” Familia za Wakristo zinapaswa kuwasiliana kila siku kwa heshima. Kwa nini? Kwa sababu mawasiliano mazuri ni muhimu ili familia ziwe thabiti. Ili kutuliza hali wakati kutoelewana kunapotokea, jaribu kutatua tatizo badala ya kujaribu kushinda mabishano. Washiriki wa familia wenye furaha hujitahidi sana kukuza fadhili na huruma kati yao.—Wakolosai 3:8, 12-14.

8 Fadhili ni sifa nzuri ambayo hutuchochea kuwatendea wengine mema. Hivyo, sisi hujitahidi kuwasaidia na kuwaonyesha ufikirio washiriki wengine wa familia katika njia yenye kupendeza. Jitihada ya kila mmoja na wote kwa ujumla inahitajiwa ili kuonyesha fadhili ambayo huiletea familia sifa. Kwa kufanya hivyo, watapata baraka za Mungu, nao watamheshimu Yehova, Mungu wa fadhili, kutanikoni na mahali wanapoishi.—1 Petro 2:12.

Fadhili Kazini

9, 10. Taja baadhi ya matatizo yanayoweza kutokea kazini, na eleza jinsi yanavyoweza kutatuliwa kwa fadhili.

9 Huenda ikawa vigumu kwa Mkristo kuwaonyesha fadhili wafanyakazi wenzake katika shughuli za kila siku kazini. Huenda mashindano kati ya wafanyakazi yakahatarisha kazi ya mtu pale mfanyakazi mwenzake anapotumia udanganyifu au hila ili amharibie sifa kwa mkubwa wa kazi. (Mhubiri 4:4) Si rahisi kuonyesha fadhili nyakati kama hizo. Hata hivyo, kwa kukumbuka kwamba kuonyesha fadhili ndilo jambo linalofaa, mtumishi wa Yehova anapaswa kujitahidi kadiri awezavyo ili awavute wale ambao ni vigumu kupatana nao. Kuonyesha kwamba tunawajali kunaweza kutusaidia kuwavuta. Labda unaweza kuonyesha kwamba unajali ikiwa mfanyakazi mwenzako ni mgonjwa au washiriki fulani wa familia yake ni wagonjwa. Hata kumjulia hali kunaweza kufanya awe na maoni yanayofaa. Naam, Wakristo wanapaswa kujitahidi kukuza upatano na amani kwa kadiri inavyowategemea. Nyakati nyingine neno la fadhili linaloonyesha kwamba unajali linaweza kuboresha hali hiyo.

10 Pindi nyingine, huenda mkubwa wa kazi akalazimisha wafanyakazi wake wakubali maoni yake ama akataka kila mtu ashiriki katika sherehe fulani za kutukuza taifa au sherehe nyingine isiyopatana na Maandiko. Huenda hali ya kutoelewana ikatokea iwapo dhamiri ya Mkristo haitamruhusu kushiriki katika sherehe hizo. Wakati huo huenda lisiwe jambo la hekima kumweleza kindani mkubwa wa kazi ubaya wa kukubaliana na mapendezi yake. Hiyo ni kwa sababu huenda watu wasioamini wasione ubaya wowote wa kushiriki katika sherehe hiyo. (1 Petro 2:21-23) Labda unaweza kueleza kwa fadhili sababu zako za kutoshiriki. Usilipize kisasi kwa kumdhihaki mtu anayekudhihaki. Inafaa Mkristo kufuata shauri hili zuri la Waroma 12:18: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”

Fadhili Shuleni

11. Vijana hukabili magumu gani wanapoonyesha fadhili kwa wanafunzi wenzao?

11 Inaweza kuwa vigumu sana kwa vijana kuwaonyesha wanafunzi wenzao fadhili. Mara nyingi vijana hutamani kukubaliwa na wanafunzi wenzao. Ili kuwavutia wanafunzi wengine, wavulana fulani hutenda kijeuri na hata huwadhulumu wengine shuleni. (Mathayo 20:25) Vijana wengine hupenda kujionyesha wao ni bora katika masomo, michezo, au katika mambo mengine. Ili kuonyesha ustadi wao, mara nyingi wao huwatendea wanadarasa na wanafunzi wengine kwa njia isiyo ya fadhili, wakifikiri kimakosa kwamba kufanya hivyo kutawafanya wawe bora kwa njia moja au nyingine. Kijana Mkristo anapaswa kujihadhari asiwaige vijana hao. (Mathayo 20:26, 27) Mtume Paulo alisema kwamba “upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili” na kwamba ‘haujigambi wala haujivuni.’ Hivyo, Mkristo anapaswa kufuata shauri la Kimaandiko anaposhughulika na wanafunzi wenzake badala ya kufuata kielelezo kibaya cha wale wanaotenda bila fadhili.—1 Wakorintho 13:4.

12. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwa vijana kuwaonyesha walimu wao fadhili? (b) Vijana wanaweza kutafuta msaada wa nani wanapokazwa wasionyeshe fadhili?

12 Vijana wanapaswa pia kuwatendea walimu wao kwa fadhili. Wanafunzi wengi hufurahia kuwakasirisha walimu wao. Wao hujiona kwamba ni werevu wanapokosa kuwaheshimu walimu wao kwa vitendo vinavyovunja sheria za shule. Huenda wakawatisha wengine ili wawaunge mkono. Kijana Mkristo anapokataa kuwaunga mkono, huenda wakamdhihaki au kumtukana. Azimio la Mkristo la kuonyesha fadhili linaweza kujaribiwa anapokabili hali kama hizo kila mwaka shuleni. Hata hivyo, kumbuka kwamba ni muhimu kuwa mtumishi mshikamanifu wa Yehova. Uwe na hakika kwamba atakutegemeza kwa roho yake nyakati hizo ngumu maishani.—Zaburi 37:28.

Fadhili kwa Majirani

13-15. Ni nini kinachoweza kutuzuia tusiwaonyeshe majirani wetu fadhili, na tunawezaje kukabiliana na magumu hayo?

13 Uwe unaishi katika nyumba ya orofa, nyumba ya kawaida, au mahali pengine, unaweza kufikiria njia za kuonyesha kwamba una fadhili na unawajali majirani. Jambo hilo pia si rahisi.

14 Namna gani ikiwa unabaguliwa na majirani wako wa karibu kwa sababu ya rangi, taifa, au dini? Namna gani ikiwa nyakati nyingine ni wajeuri au wanakupuuza kabisa? Ukiwa mtumishi wa Yehova, utanufaika kwa kuonyesha fadhili kadiri uwezavyo. Utakuwa tofauti kwa njia yenye kuburudisha, na jambo hilo linamtukuza Yehova ambaye ni kielelezo bora cha fadhili. Huwezi kujua wakati ambapo jirani yako anaweza kubadili maoni yake kwa sababu ya fadhili zako. Huenda hata akawa msifaji wa Yehova.—1 Petro 2:12.

15 Fadhili zinaweza kuonyeshwaje? Njia moja ni kupitia mwenendo mzuri katika familia, huku wote wakionyesha matunda ya roho. Huenda majirani wakatambua jambo hilo. Nyakati nyingine unaweza kumtendea jirani yako kwa fadhili. Kumbuka kwamba fadhili humaanisha kupendezwa na wengine.—1 Petro 3:8-12.

Fadhili Katika Huduma Yetu

16, 17. (a) Kwa nini fadhili ni muhimu katika huduma yetu ya hadharani? (b) Tunawezaje kuonyesha fadhili tunaposhiriki sehemu mbalimbali za huduma yetu?

16 Tunapaswa kuonyesha fadhili katika huduma yetu ya Kikristo tunapojitahidi kuwatembelea watu makwao, kazini, na katika sehemu za umma. Tunapaswa kukumbuka kwamba tunamwakilisha Yehova, ambaye huonyesha fadhili sikuzote.—Kutoka 34:6.

17 Ni nini kinachohusika katika jitihada zako za kuonyesha fadhili katika huduma? Kwa mfano, unapohubiri barabarani, unaweza kuonyesha watu fadhili kwa kuwafikiria na kuongea nao kwa ufupi unapowafikia. Kwa kawaida njia za wanaotembea kwa miguu huwa na watu wengi, kwa hiyo uwe mwangalifu usifunge njia. Pia, unapohubiri katika eneo la biashara, onyesha fadhili kwa kuongea kwa ufupi, huku ukikumbuka kwamba wenye maduka wanahitaji kuwahudumia wateja.

18. Utambuzi hutimiza fungu gani katika kuonyesha fadhili katika huduma yetu?

18 Tumia busara katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Usikae sana katika nyumba moja, hasa ikiwa hali ya hewa si nzuri. Je, unaweza kutambua mtu anapoanza kukosa subira au hata kuudhiwa na ziara yako? Labda katika sehemu unayoishi ulimwenguni, Mashahidi wa Yehova hutembelea watu mara nyingi sana. Ikiwa ndivyo ilivyo, onyesha unafikiria hali za watu kwa njia ya pekee, sikuzote ukiwa mwenye fadhili na mchangamfu. (Methali 17:14) Jaribu kuonyesha kwamba unaelewa ni kwa nini mwenye nyumba hataki kusikiliza siku hiyo. Kumbuka kwamba huenda mmoja wa ndugu au dada zako Wakristo akatembelea nyumba hiyo karibuni. Ukikutana na mtu mjeuri, jitahidi sana kumwonyesha fadhili. Usizungumze kwa sauti kubwa au kukunja uso, bali zungumza kwa utulivu. Mkristo mwenye fadhili hangependa kuanzisha mabishano na mwenye nyumba. (Mathayo 10:11-14) Labda siku moja mtu huyo atasikiliza habari njema.

Fadhili Katika Mikutano ya Kutaniko

19, 20. Kwa nini fadhili zinahitajiwa kutanikoni, nazo zinaweza kuonyeshwaje?

19 Ni muhimu pia kuwaonyesha waamini wenzetu fadhili. (Waebrania 13:1) Kwa kuwa sisi ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote, fadhili ni sifa muhimu tunaposhughulika na mmoja na mwenzake.

20 Ikiwa kutaniko linatumia Jumba la Ufalme pamoja na makutaniko mengine, ni muhimu kushughulika kwa fadhili na akina ndugu wa makutaniko hayo mengine, na kuwaonyesha heshima. Mashindano huharibu roho ya ushirikiano katika kupanga saa za mikutano, na mambo ya lazima kama vile usafi au urekebishaji. Uwe mwenye fadhili na mwenye kufikiria wengine hata ingawa huenda maoni yakatofautiana. Katika njia hiyo, fadhili zitashinda, naye Yehova atakubariki sana kwa kuonyesha kwamba unawajali wengine.

Endeleeni Kuonyesha Fadhili

21, 22. Kupatana na Wakolosai 3:12, azimio letu linapaswa kuwa nini?

21 Sifa ya fadhili inatia ndani mambo mengi sana hivi kwamba inagusa kila sehemu ya maisha yetu. Kwa hiyo, tunapaswa kuifanya iwe sehemu muhimu ya utu wetu wa Kikristo. Kuwaonyesha wengine fadhili kwapaswa kuwa zoea.

22 Sote na tuwaonyeshe wengine fadhili kila siku na hivyo kufuata maneno haya ya mtume Paulo: “Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.”—Wakolosai 3:12.

Je, Unakumbuka?

• Ni nini hufanya iwe vigumu kwa Mkristo kuonyesha fadhili?

• Kwa nini ni muhimu mtu kuonyesha fadhili katika familia yake?

• Ni nini kinachoweza kufanya iwe vigumu kuonyesha fadhili shuleni, kazini, na kwa majirani?

• Eleza jinsi Wakristo wanavyoweza kuonyesha fadhili katika huduma yao ya hadharani.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Familia zinakuwa na umoja na ushirikiano wote wanapoonyesha fadhili

[Picha katika ukurasa wa 19]

Unaweza kuonyesha fadhili mfanyakazi mwenzako au washiriki fulani wa familia yake wanapokuwa wagonjwa

[Picha katika ukurasa wa 20]

Yehova huwategemeza wale wanaoonyesha fadhili kwa ushikamanifu wajapodhihakiwa

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kumsaidia jirani mwenye uhitaji ni tendo la fadhili