Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uradhi wa Kimungu Umenitegemeza

Uradhi wa Kimungu Umenitegemeza

Simulizi la Maisha

Uradhi wa Kimungu Umenitegemeza

LIMESIMULIWA NA BENJAMIN IKECHUKWU OSUEKE

Baada tu ya kuanza utumishi wa wakati wote, niliwatembelea wazazi wangu nyumbani. Baba aliponiona, alinishika shati na kuanza kupiga kelele, “Mwizi!” Alichukua upanga wake na kunipiga kwa upande ulio bapa. Waliposikia kelele hiyo, wanakijiji walikusanyika nyumbani kwetu. Nilikuwa nimeiba nini? Acheni niwaeleze.

NILIZALIWA mwaka wa 1930, katika kijiji cha Umuariam, kilicho kusini-mashariki mwa Nigeria, nami ni mzaliwa wa kwanza kati ya watoto saba. Dada yangu aliyekuwa mkubwa kati ya dada zangu wengine alikufa akiwa na umri wa miaka 13. Wazazi wangu walikuwa Waanglikana. Baba alikuwa mkulima, naye Mama alikuwa akifanya biashara ndogo-ndogo. Alikuwa akisafiri kwenda kwenye masoko yaliyokuwa umbali wa kilometa 30 hivi kutoka kwenye kijiji chetu ili kununua debe la mafuta ya mawese na kurudi jioni hiyohiyo. Kisha, asubuhi iliyofuata angesafiri kwenda kwenye mji wenye kituo cha gari-moshi uliokuwa kilometa 40 hivi ili kuuza mafuta hayo. Kwa kawaida, alipopata faida ambayo haikuzidi senti 15 za Marekani, aliinunulia familia chakula na kurudi siku hiyohiyo. Alifanya hivyo kwa ukawaida kwa miaka 15 hivi hadi alipokufa mwaka wa 1950.

Nilianza masomo yangu kijijini mwetu katika shule iliyosimamiwa na Kanisa la Anglikana, lakini ilinibidi kuishi katika nyumba ya kukodi iliyokuwa umbali wa kilometa 35 hivi ili kumaliza shule ya msingi. Kwa kuwa wazazi wangu hawakuwa na pesa za kunilipia ili niendelee na masomo yangu, nilianza kutafuta kazi. Mwanzoni nilifanya kazi ya nyumbani kwa mlinzi wa kituo cha gari-moshi huko Lagos, magharibi mwa Nigeria, kisha nikafanya kazi hiyohiyo kwa mfanyakazi wa serikali huko Kaduna, kaskazini mwa Nigeria. Halafu nikaajiriwa kazi kama karani wa mwanasheria fulani huko Benin City, katikati-magharibi mwa Nigeria, na baadaye nikafanya kazi kwenye kiwanda cha mbao. Kutoka hapo nilisafiri hadi Kamerun mwaka wa 1953 kuishi na binamu yangu ambaye alinisaidia kupata kazi kwenye shamba la miti ya mpira. Mshahara wangu wa kila mwezi ulikuwa dola tisa hivi za Marekani. Nilifanya kazi za hali ya chini tu, lakini niliridhika maadamu nilipata chakula cha kutosha.

Napata Utajiri wa Kiroho Kutoka kwa Mtu Fukara

Mfanyakazi mwenzangu, Silvanus Okemiri, alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alitumia kila nafasi kunieleza mambo aliyojua katika Biblia tulipokuwa tukikata nyasi na kuweka matandazo ya majani kwenye mashina ya miti ya mpira. Ingawa nilimsikiliza, sikuchukua hatua yoyote wakati huo. Hata hivyo, binamu yangu alipojua kwamba nilikuwa nikizungumza na Mashahidi, alifanya yote awezayo kunivunja moyo. Alinionya: “Benji, usimtembelee Bw. Okemiri. Yeye ni mtu wa Yehova na fukara. Yeyote anayeshirikiana naye atakuwa fukara kama yeye.”

Katika mwaka wa 1954, nilirudi nyumbani niliposhindwa kuvumilia hali ngumu katika kampuni ambapo nilifanya kazi. Siku hizo, hali ya maadili katika Kanisa la Anglikana ilikuwa afadhali. Tangu utotoni, nilichukia ukosefu wa maadili. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, nilichukizwa na unafiki kati ya waenda-kanisani. Ingawa walidai kwa nguvu kwamba walifuata viwango vya Biblia, maisha yao yalikuwa tofauti na walivyodai. (Mathayo 15:8) Niligombana na baba yangu mara nyingi, jambo ambalo lilifanya uhusiano wetu uharibike zaidi. Usiku mmoja niliondoka nyumbani.

Nilihamia Omoba, mji mdogo kwenye kituo cha gari-moshi. Huko nilikutana tena na Mashahidi wa Yehova. Priscilla Isiocha, ambaye nilijuana naye katika kijiji chetu, alinipa vijitabu “Habari Njema Hizi za Ufalme” na After Armageddon—God’s New World. * Nilivisoma kwa hamu, nikisadiki kwamba nimepata ukweli. Katika kanisa letu hatukujifunza Biblia bali tulikazia mapokeo ya wanadamu. Lakini, vichapo vya Mashahidi wa Yehova viliinukuu Biblia sana.

Muda unaopungua mwezi mmoja baadaye, niliwauliza Ndugu na Dada Isiocha siku ambayo wao huenda kanisani. Nilipohudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza sikuelewa chochote. Makala ya Mnara wa Mlinzi ilizungumzia shambulio la ‘Gogu wa Magogu,’ anayetajwa katika kitabu cha unabii cha Ezekieli. (Ezekieli 38:1, 2) Sikufahamu maneno mengi yaliyotumiwa, lakini nilivutiwa sana na jinsi nilivyokaribishwa kwa uchangamfu, na hivyo nikaamua kurudi Jumapili iliyofuata. Nilipohudhuria mikutano mara ya pili, nilisikia kuhusu mahubiri. Hivyo nikamwuliza Priscilla wao huenda kuhubiri siku gani. Jumapili ya tatu, niliandamana nao nikiwa nimebeba Biblia ndogo. Sikuwa na mfuko wa mahubiri wala vichapo vyovyote vya Biblia. Hata hivyo, nikawa mhubiri wa Ufalme na kutoa ripoti ya utumishi mwisho wa mwezi huo!

Hakuna mtu aliyejifunza Biblia pamoja nami, lakini kila mara nilipoitembelea familia ya Isiocha, nilijifunza mambo fulani yenye kuimarisha imani na yenye kutia moyo kutoka katika Maandiko na pia nilipata vichapo kadhaa vinavyozungumzia Biblia. Kwenye kusanyiko moja la wilaya huko Aba, nilionyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji Desemba 11, 1954. Binamu yangu niliyeishi naye ili anizoeze kazi, aliacha kunipa chakula na kunizoeza kazi, na hakunilipa hata senti moja kwa kazi niliyomfanyia. Hata hivyo, sikuwa na kinyongo kumwelekea; nilifurahi tu kwamba nilikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Jambo hilo lilinifariji na kunipa amani ya akili. Mashahidi wenyeji walinisaidia. Familia ya Isiocha ilinipa chakula, na wengine wakanikopesha pesa za kuanzisha biashara ndogo. Katikati ya mwaka wa 1955, nilinunua baiskeli iliyotumika, na nikaanza upainia wa kawaida Machi 1956. Muda mfupi baadaye, nililipa madeni yangu. Nilipata faida ndogo sana kutokana na biashara hiyo, lakini ningeweza kutosheleza mahitaji yangu. Maandalizi ya Yehova yalinitosha.

“Kuwaiba” Ndugu na Dada Zangu

Punde tu nilipoanza kuishi peke yangu, hangaiko langu la kwanza lilikuwa kuwasaidia kiroho ndugu na dada zangu. Baba alipinga uamuzi wangu wa kuwa Shahidi kwa sababu alikuwa mwenye chuki na shaka nyingi. Hivyo basi, ningewezaje kuwasaidia ndugu na dada zangu wajifunze kweli ya Biblia? Nilijitolea kumsaidia Ernest, ndugu yangu mdogo, kwa hiyo Baba akamruhusu aje kuishi nami. Ernest alikubali kweli upesi na akabatizwa mwaka wa 1956. Badiliko ambalo Ernest alifanya lilizidisha upinzani wa baba. Hata hivyo, dada yangu ambaye tayari alikuwa ameolewa, alijifunza ukweli akiwa pamoja na mume wake. Nilipofanya mipango ili dada yangu wa pili, Felicia, aje kukaa nami wakati wa mapumziko ya shule, Baba alikubali shingo upande. Muda si muda, Felicia pia akabatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Katika mwaka wa 1959, nilienda nyumbani kumchukua Bernice, dada yangu wa tatu, ili akaishi na Ernest. Wakati huo ndipo Baba aliponishambulia na kunishutumu kwamba ninaiba watoto wake. Hakuelewa kwamba walikuwa wameamua wenyewe kumtumikia Yehova. Baba aliapa kwamba hatamruhusu Bernice kwenda pamoja nami. Lakini mkono wa Yehova haukuwa mfupi, kwa kuwa mwaka uliofuata, Bernice alienda kuishi na Ernest wakati wa mapumziko ya shule. Sawa na dada zake, alikubali kweli na kubatizwa.

‘Kujifunza Siri’

Nilianza kutumikia nikiwa painia wa pekee Septemba 1957, na nilihubiri muda wa saa 150 kila mwezi. Mimi na painia mwenzangu, Sunday Irogbelachi, tulitumika katika eneo kubwa la Akpu-na-abuo, Etche. Kwenye kusanyiko la kwanza la mzunguko tulilohudhuria tukiwa huko, watu 13 kutoka kikundi chetu walibatizwa. Tunafurahi kama nini leo kuona makutaniko 20 katika eneo hilo!

Katika mwaka wa 1958, nilijuana na Christiana Azuike, aliyekuwa painia wa kawaida katika kutaniko la Aba East. Nilivutiwa na bidii yake, na mnamo Desemba mwaka huo, tukaoana. Mapema mwaka wa 1959, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi asafiriye na niliyatembelea na kuyatia nguvu makutaniko ya ndugu zetu wa kiroho. Tangu wakati huo hadi mwaka wa 1972, mimi na mke wangu tulitembelea karibu makutaniko yote ya watu wa Yehova huko mashariki na katikati-magharibi mwa Nigeria.

Makutaniko yalikuwa mbali, nasi tulisafiri hasa kwa baiskeli. Tulipotembelea makutaniko katika miji mikubwa, ndugu zetu walikodisha teksi ili itupeleke kwenye kutaniko lililofuata. Katika maeneo fulani tulikaa katika nyumba zilizokuwa na sakafu ya udongo na ambazo hazikuwa na dari. Tulilalia vitanda vilivyotengenezwa kwa fito za mkindu. Baadhi ya vitanda hivyo vilikuwa na godoro la nyasi lililofunikwa kwa mkeka, navyo vingine hata havikuwa na godoro. Hatukuwa na tatizo kuhusiana na kiasi na ubora wa chakula. Kwa kuwa tulikuwa tumejifunza kutosheka na vitu vya lazima tu, tulifurahia chakula chochote tulichoandaliwa, nao waliotukaribisha walifurahia jambo hilo. Majiji fulani hayakuwa na umeme siku hizo, kwa hiyo sikuzote tulibeba taa yetu ya utambi. Hata hivyo, ingawa hali zilikuwa ngumu, tulikuwa na vipindi vingi vyenye furaha pamoja na makutaniko.

Miaka hiyo, tulitambua umuhimu wa himizo hili la mtume Paulo: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:8) Kupitia magumu, Paulo alijifunza siri iliyomsaidia kuridhika. Siri hiyo ilikuwa nini? Alieleza: “Kwa kweli najua jinsi ya kupungukiwa na vyakula, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi. Katika mambo yote na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji.” Tulijifunza siri hiyohiyo. Pia Paulo alisema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:12, 13) Tuliona maneno hayo kuwa ya kweli! Tulipata uradhi, tukafanya kazi nyingi za Kikristo zenye kujenga, na kupata amani ya akili.

Kutumikia Makutaniko Tukiwa Familia

Mwishoni-mwishoni mwa mwaka wa 1959, mwana wetu wa kwanza Joel alizaliwa, naye Samuel, mwana wetu wa pili, akazaliwa mwaka wa 1962. Mimi na Christiana tuliendelea na kazi ya mzunguko, tukitembelea makutaniko tukiwa pamoja na wana wetu. Mwaka wa 1967, vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria vilianza kwa ghafula. Shule zilifungwa kwa sababu ya mashambulizi ya ndege yasiyokoma. Mke wangu alikuwa mwalimu wa shule kabla ya kujiunga nami katika kazi ya mzunguko, kwa hiyo wakati wa vita, aliwafundisha watoto nyumbani. Samuel alipofikisha umri wa miaka sita, angeweza kusoma na kuandika. Alipoingia shule baada ya vita, alikuwa madarasa mawili mbele ya wanafunzi wenye umri sawa naye.

Wakati huo, hatukutambua kikamili magumu ya kulea watoto tukiwa katika kazi ya mzunguko. Hata hivyo, tulinufaika tulipopewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee mwaka wa 1972. Mgawo huo ulituwezesha kukaa mahali pamoja ili kutoa uangalifu wa kutosha wa kiroho kwa familia yetu. Wana wetu walipokuwa wachanga, tuliwafundisha umuhimu wa kuwa na uradhi wa Kimungu. Samuel alibatizwa mwaka wa 1973, naye Joel akaanza upainia wa kawaida mwaka huohuo. Wana wetu wawili walioa dada Wakristo wazuri, na sasa wanawalea watoto wao katika kweli.

Magumu ya Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe

Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipotokea, nilikuwa nikitembelea kutaniko moja huko Onitsha nikiwa mwangalizi wa mzunguko huku nikiandamana na familia yangu. Vita hivyo vilitusaidia kuelewa kwamba ni ubatili kurundika vitu vya kimwili au kuvitumaini. Niliona watu wakikimbia ili kuokoa maisha yao, huku wakitupa vitu vyao vyenye thamani barabarani.

Vita vilipozidi, wanaume wenye nguvu waliandikishwa jeshini. Ndugu wengi waliteswa kwa sababu ya kukataa kujiandikisha. Hatukuwa na uhuru wa kutembea. Ukosefu wa chakula ulisababisha mvurugo mkubwa nchini. Bei ya nusu kilo ya muhogo ilipanda kutoka senti 7 hadi dola 14 za Marekani, nacho kikombe cha chumvi kikapanda kutoka dola 8 hadi dola 42 za Marekani. Maziwa, siagi na sukari havikupatikana. Ili kuendelea kuishi, tulisaga papai mbichi na kulichanganya na unga kidogo wa muhogo. Pia tulikula panzi, maganda ya muhogo, majani ya habiskasi, nyasi, na majani yoyote tuliyopata. Nyama haikupatikana kwa urahisi, kwa hiyo nilikamata mijusi ili watoto wapate nyama ya kula. Lakini, ingawa hali ilikuwa ngumu, sikuzote Yehova alitutegemeza.

Hata hivyo, jambo lililokuwa hatari hata zaidi ni ukosefu wa chakula cha kiroho uliosababishwa na vita. Ndugu walio wengi walikimbia sehemu zenye vita na kuingia msituni au kukimbilia vijiji vingine. Walipokuwa wakikimbia walipoteza karibu vichapo vyao vyote vinavyozungumzia Biblia. Isitoshe, haingewezekana kuingiza vichapo katika eneo la Biafra kwa sababu vikosi vya serikali vilizingira eneo hilo. Ingawa makutaniko mengi yalijaribu kufanya mikutano, hali ya kiroho ya akina ndugu iliathirika kwa sababu hawangeweza kupata mwongozo kutoka katika ofisi ya tawi.

Kupambana na Njaa ya Kiroho

Waangalizi wasafirio walifanya yote wawezayo kuendelea na mpango wa kutembelea kila kutaniko. Kwa kuwa ndugu wengi walikuwa wamekimbia kutoka mijini, niliwatafuta mahali popote ambapo wangeweza kupatikana. Pindi moja, niliacha mke wangu na watoto mahali salama na kusafiri peke yangu kwa majuma sita, na kutembelea vijiji na sehemu mbalimbali za msitu nikitafuta akina ndugu.

Nilipokuwa nikitembelea kutaniko moja huko Ogbunka, nilisikia kwamba kulikuwa na Mashahidi wengi katika eneo la Isuochi, wilayani Okigwe. Kwa hiyo, nikaomba ujumbe upelekewe akina ndugu waliokuwa katika eneo hilo ili wakutane katika shamba la mikorosho katika kijiji cha Umuaku. Mimi na ndugu mmoja mzee tulisafiri kwa baiskeli umbali wa kilometa 15 hadi kwenye shamba hilo ambako Mashahidi 200 hivi, waliotia ndani wanawake na watoto, walikuwa wamekusanyika. Dada mmoja painia alinisaidia kuwapata Mashahidi wengine wapatao mia moja, ambao walikuwa wamekimbilia pori la Lomara.

Lawrence Ugwuegbu alikuwa mmojawapo wa akina ndugu wajasiri waliokuwa wakiishi katika mji ulioharibiwa na vita wa Owerri. Aliniambia kwamba kulikuwa na ndugu wengi katika eneo la Ohaji. Ndugu hao hawangeweza kutembea kwa uhuru kwa kuwa askari walikuwa wamevamia eneo hilo. Sote wawili tulisafiri kwa baiskeli usiku na kukutana na Mashahidi 120 hivi katika makao ya ndugu fulani. Pia tulitumia nafasi hiyo kutembelea Mashahidi wengine katika maficho yao.

Ndugu Isaac Nwagwu alihatarisha maisha yake ili kunisaidia kutafuta ndugu wengine waliokuwa wamehama. Alinivusha Mto Otamiri katika mtumbwi ili kukutana na Mashahidi zaidi ya 150 waliokuwa wamekusanyika huko Egbu-Etche. Ndugu mmoja huko alisema hivi: “Hii ndiyo siku nzuri kabisa katika maisha yangu! Sikuwazia kamwe ningepata kumwona tena mwangalizi wa mzunguko. Ikiwa nitakufa sasa katika vita hivi, nimeridhika.”

Nilikabili hatari ya kuandikishwa jeshini, lakini mara nyingi nilihisi kwamba Yehova alikuwa akinilinda. Alasiri moja, kikundi cha wanajeshi kilinisimamisha kwenye kizuizi cha barabarani nilipokuwa nikirudi mahali nilipokaa baada ya kuwatembelea ndugu wapatao 250 hivi. “Kwa nini hujajiunga na jeshi?” wakaniuliza. Niliwaeleza kwamba nilikuwa mishonari aliyehubiri Ufalme wa Mungu. Nilitambua kwamba walikuwa wanataka kunikamata. Baada ya sala fupi ya kimya-kimya, nilimwambia kapteni wao, “Tafadhali niachilie.” Nilishangaa aliponiuliza, “Ati! unasema tukuachilie uende zako?” “Ndiyo, niachilieni,” nikajibu. Kisha akasema, “Uko huru kwenda zako.” Hakuna yeyote kati ya askari hao aliyesema lolote.—Zaburi 65:1, 2.

Uradhi Waleta Baraka Zaidi

Vita vilipoisha mwaka wa 1970, niliendelea kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Lilikuwa pendeleo kusaidia kupanga mambo upya makutanikoni. Baada ya hapo, mimi na Christiana tulitumikia tukiwa mapainia wa pekee hadi mwaka wa 1976, nilipowekwa tena rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Kuelekea katikati ya mwaka huo, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa wilaya. Miaka saba baadaye, mimi na mke wangu tulialikwa kwenda kutumika kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Nigeria, ambako ndiko tunakaa sasa. Hapa ofisini, tunafurahi sana kuona ndugu na dada tuliokutana nao wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe na nyakati nyingine pia, ambao bado wanatumikia Yehova kwa uaminifu.

Katika miaka ambayo imepita, Christiana amekuwa mwandamani mwaminifu na mwenye kunitegemeza sana. Ingawa Christiana amekuwa na matatizo ya kiafya ambayo amevumilia tangu mwaka wa 1978, mtazamo wake mzuri na roho yake ya bidii imenisaidia kutimiza madaraka yangu. Tumeona ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi: “Yehova mwenyewe atamtegemeza katika kitanda cha ugonjwa.”—Zaburi 41:3.

Ninapokumbuka miaka hiyo ya utendaji wa kiroho, sina budi kumshukuru Yehova na baraka zake za ajabu. Kwa kweli, ninaweza kusema kwamba nimepata furaha nyingi kwa kuridhika na maandalizi yake. Ninafurahi kuona ndugu na dada zangu, watoto wangu, na familia zao wakimtumikia Yehova pamoja nasi, na hiyo ni baraka isiyo na kifani. Yehova ameniwezesha kuwa na maisha yenye uradhi na kusudi. Tamaa zangu zote zimetimizwa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Sasa havichapishwi tena.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Mpango wa Wakati Unaofaa Unasaidia Kutegemeza Akina Ndugu

Katikati ya miaka ya 1960, uadui kati ya makabila ya kaskazini na mashariki mwa Nigeria ulisababisha misukosuko, vurugu, uasi-sheria, na vita vya kikabila. Mambo hayo yaliwaletea mkazo mkubwa Mashahidi wa Yehova, ambao waliazimia kutojiingiza kabisa katika mizozo hiyo. Mashahidi wapatao 20 waliuawa na wengi wao wakapoteza mali zao zote.

Majimbo ya mashariki yalijitenga na serikali ya shirikisho ya Nigeria, na kuunda Jamhuri ya Biafra, Mei 30, 1967. Jeshi la serikali lilipelekwa na kuzingira kabisa Biafra. Kisha vita vikatili vya wenyewe kwa wenyewe na vyenye umwagikaji mwingi wa damu vikaanza.

Mashahidi wa Yehova katika eneo la Biafra walishambuliwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo. Magazeti yalichapisha habari zenye chuki, na kuchochea umma dhidi ya Mashahidi. Hata hivyo, Yehova alihakikisha kwamba watumishi wake walipokea chakula cha kiroho. Jinsi gani?

Mapema mwaka wa 1968, mtumishi mmoja wa serikali alipelekwa kufanya kazi katika ofisi fulani huko Ulaya na mwingine kwenye uwanja mdogo wa ndege wa Biafra. Wote wawili walikuwa Mashahidi. Kazi zao zilifanya iwezekane kuwa na mawasiliano kati ya Biafra na nchi za nje. Mashahidi hao wawili walijitolea kufanya kazi hatari ya kuingiza chakula cha kiroho Biafra. Pia walisaidia kupeleka misaada kwa ndugu zetu wenye shida. Ndugu hao wawili walifaulu kufanya kazi hiyo muhimu kipindi chote cha vita, ambavyo viliisha mwaka wa 1970. Baadaye, mmoja wao alisema, “Wanadamu hawangeweza kufanya mpango kama huo.”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mwaka wa 1956

[Picha katika ukurasa wa 25]

Tukiwa pamoja na wana wetu, Joel na Samuel, mwaka wa 1965

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ni baraka iliyoje kumtumikia Yehova tukiwa familia!

[Picha katika ukurasa wa 27]

Leo, mimi na Christiana tunatumika katika ofisi ya tawi ya Nigeria