Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukuu wa Yehova Hauchunguziki

Ukuu wa Yehova Hauchunguziki

Ukuu wa Yehova Hauchunguziki

“Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana, na ukuu wake hauchunguziki.”—ZABURI 145:3.

1, 2. Daudi alikuwa mtu wa aina gani, naye alijionaje akijilinganisha na Mungu?

MTUNGAJI wa Zaburi ya 145 ni mmoja wa watu wa zamani wanaojulikana sana. Akiwa mvulana, alikabiliana na jitu lenye silaha na kuliua. Na akiwa mfalme shujaa, mtunga-zaburi huyo alishinda adui wengi. Aliitwa Daudi, naye alikuwa mfalme wa pili wa Israeli la kale. Sifa zake zilidumu hata baada ya kifo chake, na hata sasa watu wengi sana wanajua jambo fulani kumhusu.

2 Ingawa Daudi alitimiza mambo mengi, alikuwa mnyenyekevu. Aliimba hivi kumhusu Yehova: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?” (Zaburi 8:3, 4) Badala ya kufikiria kwamba yeye mwenyewe alikuwa mkuu, Daudi alimsifu Yehova kuwa alimkomboa kutoka kwa adui zake wote na kusema hivi kumhusu: “Utanipa ngao yako ya wokovu, na unyenyekevu wako ndio hunifanya niwe mkuu.” (2 Samweli 22:1, 2, 36) Yehova hudhihirisha unyenyekevu anapowaonyesha wakosaji rehema, naye Daudi alithamini fadhili za Mungu zisizostahiliwa.

‘Nitamtukuza Mungu Mfalme’

3. (a) Daudi alikuwa na maoni gani kuhusu ufalme wa Israeli? (b) Daudi alitamani kumsifu Yehova kadiri gani?

3 Ingawa Daudi alikuwa mfalme aliyewekwa na Mungu, alimwona Yehova kuwa Mfalme halisi wa Israeli. Daudi alisema: “Ufalme ni wako, Ee Yehova, wewe unayejiinua kuwa kichwa juu ya wote.” (1 Mambo ya Nyakati 29:11) Daudi alimthamini sana Mungu kuwa Mtawala! Aliimba, “Nitakutukuza, Ee Mungu wangu Mfalme, nami nitalibariki jina lako mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele. Mchana kutwa nitakubariki, nami nitalisifu jina lako mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Zaburi 145:1, 2) Daudi alitamani kumsifu Yehova Mungu mchana kutwa na kwa umilele.

4. Zaburi ya 145 hufunua madai gani ya uwongo?

4 Zaburi ya 145 inajibu kwa njia yenye kusadikisha dai la Shetani kwamba Mungu ni mtawala mwenye ubinafsi anayewanyima viumbe wake uhuru. (Mwanzo 3:1-5) Zaburi hiyo pia hufunua uwongo wa Shetani kwamba wale ambao humtii Mungu hufanya hivyo ili wanufaike wala si kwa sababu wanampenda. (Ayubu 1:9-11; 2:4, 5) Kama Daudi, Wakristo wa kweli leo wanajibu madai ya uwongo ya Ibilisi. Wao huthamini tumaini lao la uzima wa milele chini ya utawala wa Ufalme kwa sababu wanatamani kumsifu Yehova kwa umilele. Tayari, mamilioni wameanza kufanya hivyo kwa kuonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu na kwa kumtumikia Yehova kwa utii kwa sababu wanampenda wakiwa waabudu wake waliojiweka wakfu na kubatizwa.—Waroma 5:8; 1 Yohana 5:3.

5, 6. Kuna nafasi gani za kumbariki na kumsifu Yehova?

5 Fikiria nafasi nyingi tulizo nazo za kumbariki na kumsifu Yehova tukiwa watumishi wake. Tunaweza kufanya hivyo katika sala tunapoguswa moyo sana na jambo fulani tunalosoma katika Neno lake, Biblia. Tunaweza kuonyesha uthamini na shukrani tunapoguswa moyo na jinsi Mungu anavyoshughulika na watu wake au tunapofurahishwa na jambo fulani kuhusu uumbaji wake wa ajabu. Tunambariki Yehova Mungu pia tunapozungumzia makusudi yake na waamini wenzetu kwenye mikutano ya Kikristo au katika mazungumzo ya kibinafsi. Kwa kweli, ‘matendo yote mazuri’ yanayofanywa kwa ajili ya Ufalme wa Mungu humletea sifa.—Mathayo 5:16.

6 Mifano ya karibuni ya matendo hayo mazuri inatia ndani kuwajengea watu wa Yehova majumba mengi ya ibada katika nchi maskini. Kiasi kikubwa cha kazi hiyo kimefanywa kwa msaada wa kifedha wa waamini wenzao katika nchi nyingine. Wakristo fulani wametoa msaada kwa kwenda katika maeneo hayo ili kushiriki kujenga Majumba ya Ufalme. Nayo matendo mazuri yaliyo muhimu zaidi ni kumsifu Yehova kwa kuhubiri habari njema kuhusu Ufalme wake. (Mathayo 24:14) Kama mistari inayofuata ya Zaburi 145 inavyoonyesha, Daudi alithamini utawala wa Mungu na kusifu ufalme Wake. (Zaburi 145:11, 12) Je, wewe pia unathamini njia ya Mungu ya kutawala yenye upendo? Na je, wewe huzungumza na wengine kwa ukawaida kuhusu Ufalme wake?

Mifano ya Ukuu wa Mungu

7. Toa sababu kuu ya kumsifu Yehova.

7 Zaburi 145:3 inatupatia sababu kuu ya kumsifu Yehova. Daudi anaimba: “Yehova ni mkuu na wa kusifiwa sana, na ukuu wake hauchunguziki.” Ukuu wa Yehova hauna kifani. Hauwezi kuchunguzwa kikamili, kueleweka, au kupimwa na wanadamu. Lakini bila shaka tutanufaika kwa kuchunguza sasa mifano ya ukuu wa Yehova usiochunguzika.

8. Ulimwengu hufunua nini kuhusu ukuu na uwezo wa Yehova?

8 Jaribu kukumbuka pindi ambapo ulitazama juu usiku kwenye anga lisilo na mawingu. Je, hukustaajabu kuona nyota nyingi sana? Je, hukuchochewa kumsifu Yehova kwa ukuu wake katika kuumba nyota hizo zote? Hata hivyo, nyota ulizoona ni chache sana zikilinganishwa na kikundi cha nyota ambacho dunia ni sehemu yake. Isitoshe, inakadiriwa kwamba kuna makundi ya nyota zaidi ya bilioni mia moja, na ni makundi matatu tu yanayoweza kuonekana bila darubini. Naam, nyota zisizoweza kuhesabika ambazo ni sehemu ya ulimwengu mkubwa ni ushuhuda kwamba Yehova ana uwezo wa kuumba na ukuu wake hauchunguziki.—Isaya 40:26.

9, 10. (a) Ni mambo gani ya ukuu wa Yehova ambayo yameonyeshwa kuhusiana na Yesu Kristo? (b) Ufufuo wa Yesu unapaswa kuwa na matokeo gani juu ya imani yetu?

9 Fikiria mambo mengine kuhusu ukuu wa Yehova—yale ambayo yanahusu Yesu Kristo. Ukuu wa Mungu ulionyeshwa alipomuumba Mwana wake na kumtumia kwa muda mrefu sana akiwa ‘stadi Wake wa kazi.’ (Methali 8:22-31) Upendo mwingi wa Yehova ulionyeshwa alipomtoa Mwana wake mzaliwa-pekee awe dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; 1 Yohana 2:1, 2) Nao wanadamu hawawezi kamwe kuuelewa mwili mtukufu wa roho usioweza kufa ambao Yehova alimuumbia Yesu wakati wa ufufuo.—1 Petro 3:18.

10 Ufufuo wa Yesu ulihusisha mambo mengi yenye kuvutia ya ukuu wa Yehova usiochunguzika. Bila shaka, Mungu alimkumbusha Yesu kazi iliyohusika katika kuumba vitu visivyoonekana na vinavyoonekana. (Wakolosai 1:15, 16) Vitu hivyo vinatia ndani viumbe wengine wa roho, ulimwengu, dunia yenye kuzaa, na viumbe wengine wote wenye uhai duniani. Zaidi ya kumkumbusha Mwana wake historia yote ya maisha ya mbinguni na duniani ambayo aliona kabla ya kuwa mwanadamu, Yehova pia alimkumbusha Yesu mambo yaliyompata alipokuwa mwanadamu mkamilifu. Ndiyo, ukuu usiochunguzika wa Yehova unaonekana katika ufufuo wa Yesu. Isitoshe, tendo hilo kuu ni uhakikisho kwamba wengine wanaweza kufufuliwa. Linapaswa kuimarisha imani yetu kwamba Mungu anaweza kuwafufua mamilioni ya wafu walio katika kumbukumbu lake kamilifu.—Yohana 5:28, 29; Matendo 17:31.

Kazi za Ajabu na Matendo Yenye Nguvu

11. Ni kazi gani kubwa ya Yehova iliyoanza Pentekoste 33 W.K.?

11 Tangu ufufuo wa Yesu, Yehova amefanya kazi nyingine kuu na za ajabu. (Zaburi 40:5) Siku ya Pentekoste 33 W.K., Yehova alitokeza taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” ambalo lilifanyizwa na wanafunzi wa Kristo waliotiwa mafuta kwa roho takatifu. (Wagalatia 6:16) Katika njia yenye nguvu, taifa hilo jipya lilipanuka katika ulimwengu wote wa wakati huo. Ingawa baada ya kifo cha mitume wa Yesu uasi-imani ulitokeza dini zinazojiita za Kikristo, Yehova aliendelea kufanya kazi za ajabu ili kuhakikisha kwamba kusudi lake linatimia.

12. Kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha zote kuu duniani kunashuhudia nini?

12 Kwa mfano, Biblia nzima ilihifadhiwa na mwishowe ikatafsiriwa katika lugha zote kuu duniani leo. Mara nyingi Biblia ilitafsiriwa chini ya hali ngumu na vitisho vya kuuawa kutoka kwa wawakilishi wa Shetani. Bila shaka, haingewezekana kuitafsiri Biblia katika lugha zaidi ya 2,000 kama hayakuwa mapenzi ya Mungu mkuu, Yehova, asiyechunguzika!

13. Tangu mwaka wa 1914, ukuu wa Yehova umeonyeshwaje kuhusiana na makusudi yake ya Ufalme?

13 Ukuu wa Yehova umeonyeshwa kuhusiana na makusudi ya Ufalme wake. Kwa mfano, katika mwaka wa 1914, alimweka Mwana wake Yesu Kristo awe Mfalme wa kimbingu. Muda mfupi baadaye, Yesu aliwachukulia hatua Shetani na roho wake waovu.Walifukuzwa kutoka mbinguni na kuzuiwa kwenye ujirani wa dunia ambako sasa wanangojea kutiwa ndani ya abiso. (Ufunuo 12:9-12; 20:1-3) Tangu wakati huo, kuteswa kwa wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu kumeongezeka. Hata hivyo, Yehova amewategemeza wakati huu wa kuwapo kwa Kristo kusikoonekana.—Mathayo 24:3; Ufunuo 12:17.

14. Yehova alifanya kazi gani ya ajabu mwaka wa 1919, na kazi hiyo ilitimiza nini?

14 Katika mwaka wa 1919, Yehova alifanya kazi nyingine ya ajabu iliyoonyesha ukuu wake. Wafuasi-watiwa mafuta wa Yesu ambao walikuwa katika hali ya kutotenda walipewa nguvu mpya. (Ufunuo 11:3-11) Tangu wakati huo, watiwa-mafuta wamehubiri kwa bidii habari njema kuhusu Ufalme wa kimbingu uliosimamishwa. Watiwa-mafuta wengine wamekusanywa ili kukamilisha hesabu ya 144,000. (Ufunuo 14:1-3) Na kupitia wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo, Yehova aliweka msingi wa “dunia mpya,” yaani, jamii ya wanadamu waadilifu. (Ufunuo 21:1) Lakini itakuwaje kwa “dunia mpya” baada ya watiwa-mafuta waaminifu wote kwenda mbinguni?

15. Ni kazi gani ambayo imekuwa ikiongozwa na Wakristo watiwa-mafuta na matokeo yamekuwaje?

15 Mnamo 1935, matoleo ya gazeti hili ya Agosti 1 na Agosti 15 yalikuwa na makala muhimu zilizozungumzia “umati mkubwa” unaotajwa katika Ufunuo sura ya 7. Wakristo watiwa-mafuta walianza kuwaalika kwa bidii waabudu hao wenzao kutoka katika mataifa yote, kabila, watu, na lugha ili washirikiane nao. ‘Umati huo mkubwa’ wa watu wataokoka “dhiki kuu” inayokaribia nao watakuwa na tazamio la kuishi milele katika Paradiso wakiwa wakaaji wa kudumu wa “dunia mpya.” (Ufunuo 7:9-14) Kwa sababu ya kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi inayoongozwa na Wakristo watiwa-mafuta, sasa watu zaidi ya milioni sita wana tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani. Ni nani anayepaswa kusifiwa kwa ongezeko hilo ijapokuwa upinzani kutoka kwa Shetani na ulimwengu wake mpotovu? (1 Yohana 5:19) Yehova tu ndiye anayeweza kutimiza yote hayo akitumia roho yake takatifu.—Isaya 60:22; Zekaria 4:6.

Fahari Tukufu na Utukufu wa Yehova

16. Kwa nini wanadamu hawawezi kuona kihalisi ‘fahari tukufu ya utukufu wa Yehova’?

16 ‘Kazi za ajabu’ na ‘matendo yenye nguvu’ ya Yehova hayatasahaulika kamwe, hata yawe ya aina gani. Daudi aliandika hivi: “Kizazi baada ya kizazi kitazipongeza kazi zako, nao watatangaza juu ya matendo yako ya nguvu. Fahari tukufu ya utukufu wako na mambo ya kazi zako za ajabu nitayafanya yawe hangaiko langu. Nao wataongea juu ya nguvu za mambo yako yenye kuogopesha; nami nitautangaza ukuu wako.” (Zaburi 145:4-6) Lakini Daudi angeweza kujua mambo mengi kadiri gani kuhusu fahari tukufu ya Yehova kwa kuwa “Mungu ni Roho” naye hawezi kuonekana na wanadamu?—Yohana 1:18; 4:24.

17, 18. Daudi angewezaje kuzidisha uthamini wake kwa ‘fahari tukufu ya utukufu wa Yehova’?

17 Ingawa Daudi hangeweza kumuona Mungu, kuna njia ambazo angeweza kuzidisha uthamini wake kwa utukufu wa Yehova. Kwa mfano, angeweza kusoma Maandiko kuhusu matendo yenye nguvu ya Mungu, kama vile kuharibiwa kwa ulimwengu mwovu kupitia gharika ya ulimwengu wote. Yaelekea Daudi alijua jinsi miungu ya uwongo ya Misri ilivyoaibishwa wakati Mungu alipowakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri. Matukio hayo hushuhudia utukufu na ukuu wa Yehova.

18 Bila shaka, Daudi alizidisha uthamini kwa utukufu wa Mungu kwa kusoma Maandiko na pia kwa kuyatafakari. Kwa mfano, huenda alitafakari kuhusu yaliyotukia Yehova alipowapa Waisraeli Sheria. Kulikuwa na mingurumo, umeme, wingu zito, na sauti kubwa sana ya pembe. Mlima Sinai ulitetemeka na kutoa moshi. Waisraeli waliokuwa wamekusanyika chini ya mlima huo walisikia “Maneno Kumi” kutoka katikati ya moto na wingu Yehova aliposema nao kupitia mwakilishi wa kimalaika. (Kumbukumbu la Torati 4:32-36; 5:22-24; 10:4; Kutoka 19:16-20; Matendo 7:38, 53) Huo ni wonyesho ulioje wa utukufu wa Yehova! Wapendao Neno la Mungu ambao hutafakari masimulizi hayo huchochewa na ‘fahari tukufu ya utukufu wa Yehova.’ Bila shaka, leo tuna Biblia nzima ambayo ina maono mbalimbali ya utukufu yanayofanya tuvutiwe na ukuu wa Yehova.—Ezekieli 1:26-28; Danieli 7:9, 10; Ufunuo, sura ya 4.

19. Ni nini kitakachozidisha uthamini wetu kwa utukufu wa Yehova?

19 Njia nyingine ambayo Daudi angeweza kuvutiwa na utukufu wa Mungu ni kwa kujifunza sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli. (Kumbukumbu la Torati 17:18-20; Zaburi 19:7-11) Kwa kutii sheria za Yehova, taifa la Israeli liliheshimiwa na kutengwa na watu wengine wote. (Kumbukumbu la Torati 4:6-8) Kama ilivyokuwa kuhusu Daudi, kusoma Maandiko kwa ukawaida, kuyatafakari kwa undani, na kuyachunguza kwa bidii kutazidisha uthamini wetu kwa utukufu wa Yehova.

Sifa za Kiadili za Mungu Ni Kuu Sana

20, 21. (a) Zaburi ya 145:7-9 hutukuza ukuu wa Yehova kuhusiana na sifa gani? (b) Sifa za Mungu zilizotajwa hapa zina matokeo gani juu ya wote wanaompenda?

20 Kama ambavyo tumeona, mistari sita ya kwanza ya Zaburi ya 145 hutupa sababu nzuri za kumsifu Yehova kwa mambo yanayohusu ukuu wake usiochunguzika. Mstari wa 7 hadi 9 hutukuza ukuu wa Mungu kwa kutaja sifa zake za kiadili. Daudi anaimba: “Watabubujikwa na maneno wakitaja wingi wa wema wako, na kwa sababu ya uadilifu wako watapiga vigelegele vya shangwe. Yehova ni mwenye neema na mwenye rehema, si mwepesi wa hasira naye ni mkuu katika fadhili zenye upendo. Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.”

21 Hapa Daudi anakazia wema na uadilifu wa Yehova kwanza, sifa ambazo Shetani Ibilisi alitilia shaka. Sifa hizo zina matokeo gani kwa wote wanaompenda Mungu na kujitiisha kwa utawala wake? Wema wa Yehova na njia yake ya uadilifu ya kutawala huwafurahisha sana waabudu wake hivi kwamba hawawezi kuacha kumsifu. Isitoshe, Yehova huonyesha wema wake “kwa wote.” Tunatumaini kwamba wema huo utawasaidia wengi zaidi watubu na kuwa waabudu wa Mungu wa kweli kabla ya kuchelewa mno.—Matendo 14:15-17.

22. Yehova huwatendeaje watumishi wake?

22 Daudi pia alithamini sifa ambazo Mungu mwenyewe alikazia ‘Alipopita karibu mbele ya uso wa Musa na kutangaza: “Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.”’ (Kutoka 34:6) Hivyo, Daudi angeweza kusema: “Yehova ni mwenye neema na mwenye rehema, si mwepesi wa hasira naye ni mkuu katika fadhili zenye upendo.” Ingawa ukuu wa Yehova hauchunguziki, yeye huwaheshimu watumishi wake wanadamu kwa kuwatendea kwa neema. Yeye ana rehema nyingi na yuko tayari kuwasamehe watenda-dhambi wenye kutubu kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Pia Yehova si mwepesi wa hasira, kwa kuwa huwapa watumishi wake nafasi ya kushinda udhaifu unaoweza kuwazuia wasiingie katika ulimwengu wake mpya wenye uadilifu.—2 Petro 3:9, 13, 14.

23. Ni sifa gani nzuri itakayozungumziwa katika makala inayofuata?

23 Daudi anamsifu Mungu kwa fadhili zake zenye upendo, au upendo mshikamanifu. Kwa kweli, mistari inayobaki ya Zaburi ya 145 inaonyesha jinsi Yehova hudhihirisha sifa hiyo na jinsi watumishi wake washikamanifu huitikia fadhili zake zenye upendo. Mambo hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Kuna nafasi gani za kumsifu Yehova “mchana kutwa”?

• Ni mifano gani inayoonyesha kwamba ukuu wa Yehova hauchunguziki?

• Tunawezaje kuzidisha uthamini wetu kwa fahari yenye utukufu ya Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Makundi ya nyota katika ulimwengu hushuhudia ukuu wa Yehova

[Hisani]

Courtesy of Anglo-Australian Observatory, photograph by David Malin

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ukuu wa Yehova umeonyeshwaje kuhusiana na Yesu Kristo?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Waisraeli walipopokea Sheria kwenye Mlima Sinai, waliona utukufu wenye fahari wa Yehova