Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fikiri kwa Njia Inayofaa—Tenda kwa Hekima

Fikiri kwa Njia Inayofaa—Tenda kwa Hekima

Fikiri kwa Njia Inayofaa—Tenda kwa Hekima

FIKIRIA kisa hiki: Yesu Kristo anaeleza kwamba maadui wa kidini huko Yerusalemu watamtesa na mwishowe wamuue. Mtume Petro ambaye ni rafiki yake wa karibu haamini jambo hilo. Anampeleka Yesu kando na kumkemea. Bila shaka Petro anafanya hivyo kwa sababu yeye ni mnyofu na anamjali. Lakini Yesu anaonaje njia ya Petro ya kufikiri? Yesu anamwambia: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kipingamizi chenye kukwaza kwangu, kwa sababu wewe wafikiri, si fikira za Mungu, bali zile za wanadamu.”—Mathayo 16:21-23.

Ni lazima jambo hilo lilimshangaza sana Petro. Badala ya kuwa msaada kwa Bwana wake aliyempenda sana, alikuwa “kipingamizi chenye kukwaza.” Ilikuwaje hivyo? Huenda Petro alikuwa na kasoro fulani ambayo huathiri sana kufikiri kwa wanadamu, yaani, kuamini tu yale aliyotaka kuamini.

Usijitumaini Kupita Kiasi

Hatari tunayokabili tunapotaka kufikiri kwa njia inayofaa ni mwelekeo wa kujitumaini kupita kiasi. Mtume Paulo aliwaonya hivi Wakristo wenzake huko Korintho la kale: “Acheni yeye ambaye afikiri kuwa amesimama ajihadhari kwamba asianguke.” (1 Wakorintho 10:12) Kwa nini Paulo alisema hivyo? Yaelekea ni kwa sababu alijua jinsi ilivyo rahisi kwa mwanadamu kufikiri kwa njia iliyopotoka, na hata akili za Wakristo ‘kufisidiwa kutoka kwenye weupe wa moyo na usafi wa kiadili ambao wamstahili Kristo.’—2 Wakorintho 11:3.

Jambo hilo lilikuwa limekipata kizazi chote cha mababu wa Paulo. Wakati huo, Yehova aliwaambia: “Mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu.” (Isaya 55:8) Walikuwa “wenye hekima katika macho yao wenyewe,” na matokeo yakawa mabaya sana. (Isaya 5:21) Kwa kweli basi, ni jambo la akili kujichunguza ili tuendelee kufikiri kwa njia inayofaa na hivyo kuepuka matokeo mabaya kama hayo.

Jihadhari na Kufikiri kwa Njia ya Kimwili

Watu fulani huko Korintho waliathiriwa vibaya kwa kufikiri kwa njia ya kimwili. (1 Wakorintho 3:1-3) Walitilia mkazo falsafa za wanadamu badala ya Neno la Mungu. Hapana shaka kwamba wasomi Wagiriki walikuwa watu wenye akili nyingi. Hata hivyo, Mungu aliwaona kuwa wapumbavu. Paulo alisema: “Imeandikwa: ‘Hakika nitafanya hekima ya watu wenye hekima iangamie, na akili ya watu wenye akili hakika nitaisukuma kando.’ Yuko wapi mtu mwenye hekima? Wapi mwandishi? Wapi mshindania-maneno wa mfumo huu wa mambo? Je, Mungu hakuifanya hekima ya ulimwengu iwe pumbavu?” (1 Wakorintho 1:19, 20) Wasomi kama hao waliongozwa na “roho ya ulimwengu” badala ya roho ya Mungu. (1 Wakorintho 2:12) Falsafa zao na maoni yao hayakupatana na kufikiri kwa Yehova.

Chanzo hasa cha kufikiri kwa njia ya kimwili ni Shetani Ibilisi, aliyetumia nyoka kumshawishi Hawa. (Mwanzo 3:1-6; 2 Wakorintho 11:3) Je, yeye bado ni tisho kwetu? Ndiyo! Kulingana na Neno la Mungu, Shetani “amepofusha akili” za watu sana hivi kwamba sasa ‘anaiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.’ (2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9) Jinsi ilivyo muhimu kuzijua mbinu zake!—2 Wakorintho 2:11.

Jihadhari na “Hadaa ya Watu”

Mtume Paulo alionya pia dhidi ya “hadaa ya watu.” (Waefeso 4:14) Alikutana na “wafanyakazi wenye udanganyifu” waliodai kuhubiri kweli lakini kwa hakika waliipotosha. (2 Wakorintho 11:12-15) Ili kutimiza malengo yao, huenda watu hao wakaamua kutumia mambo yanayounga mkono kufikiri kwao, lugha inayovutia hisia, kweli nusu-nusu zenye kupotosha, ujanja, na hata kusema uwongo waziwazi.

Mara nyingi wale wanaowapotosha watu kimakusudi hutumia neno kama vile “madhehebu” ili kuwashutumu wengine. Katika pendekezo fulani lililotolewa kwenye Mkutano wa Baraza la Bunge la Ulaya, ilidokezwa kwamba inafaa maofisa wanaochunguza dini mpya “washauriwe wasitumie neno hilo.” Kwa nini? Ilionekana kwamba neno “madhehebu” lina maana mbaya sana. Vivyo hivyo, wasomi Wagiriki walimwita mtume Paulo kimakosa “mpiga-domo” au ‘mwokota mbegu.’ Kwa kusema hivyo walimaanisha kwamba alikuwa mtu mvivu mwenye kuropoka, aliyeokota na kurudia-rudia tu mambo aliyosikia kwa wengine. Kwa kweli Paulo “alikuwa akitangaza habari njema ya Yesu na ufufuo.”—Matendo 17:18.

Je, mbinu za watu hao wanaopotosha wengine zimefanikiwa? Ndiyo. Wamesababisha chuki ya kikabila na kidini kwa kupotosha maoni ya watu kuhusu mataifa mengine au dini nyingine. Wengi wametumia mbinu hizo ili kuvipuuza vikundi vidogo katika jamii. Adolf Hitler alitumia mbinu kama hizo kwa mafanikio aliposema kwamba Wayahudi na wengineo walikuwa “watu wa hali ya chini,” “waovu,” na “tisho” kwa Taifa. Usiruhusu kamwe hadaa kama hiyo ya watu iharibu kufikiri kwako.—Matendo 28:19-22.

Usijidanganye

Pia ni rahisi kujidanganya wenyewe. Kwa kweli, inaweza kuwa vigumu sana kuacha au hata kushuku maoni yetu tunayoyapenda sana. Kwa nini? Kwa sababu tunashikilia sana maoni yetu. Kisha tunaweza kujidanganya kwa kufikiri kimakosa, yaani, kutafuta sababu za kutetea mambo yasiyo ya kweli na yenye kupotosha.

Jambo hilo liliwapata Wakristo fulani wa karne ya kwanza. Walijua Neno la Mungu, lakini hawakuliruhusu liongoze kufikiri kwao. Wakaishia ‘kujidanganya wenyewe kwa kuwazawaza kusiko kwa kweli.’ (Yakobo 1:22, 26) Ikiwa tunakasirika imani yetu inaposhambuliwa, basi inaonyesha kwamba tumenaswa katika aina hiyo ya kujidanganya. Badala ya kukasirika, ni vizuri kuwa na busara na kusikiliza kwa makini yale ambayo wengine wanasema, hata tunapohisi kwamba maoni yetu ni sawa.—Mithali 18:17.

Chimba Upate “Kumjua Mungu”

Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kufikiri kwa njia inayofaa? Msaada unapatikana, lakini ni lazima tujitahidi kuupata. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu.” (Mithali 2:1-5) Naam, ikiwa sisi binafsi tutajitahidi kujaza ukweli wa Neno la Mungu katika akili na mioyo yetu, tutapata hekima halisi, ufahamu, na busara. Kwa hakika, tutakuwa tunachimba ili tupate vitu vyenye thamani sana kuliko fedha au hazina yoyote ya kimwili.—Mithali 3:13-15.

Hekima na ujuzi ni sifa muhimu ili kufikiri kwa njia inayofaa. Neno la Mungu linasema: “Maana hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi. Ili kukuokoa na njia ya uovu, na watu wanenao yaliyopotoka; watu waziachao njia za unyofu, ili kuziendea njia za giza.”—Mithali 2:10-13.

Ni muhimu hasa kuacha maoni ya Mungu yaongoze kufikiri kwetu wakati wa mikazo au hatari. Hisia zenye nguvu kama vile hasira au woga zinaweza kufanya iwe vigumu kufikiri kwa njia inayofaa. “Jeuri humpumbaza mwenye hekima,” akasema Sulemani. (Mhubiri 7:7) Hata inaweza kumfanya mtu ‘amnunie BWANA.’ (Mithali 19:3) Namna gani? Kwa kumlaumu Mungu tunapokuwa na matatizo na kuyatumia kuwa kisingizio cha kufanya mambo yaliyo kinyume cha sheria na kanuni zake. Na tuwasikilize kwa unyenyekevu washauri wenye hekima wanaotaka kutusaidia kwa kutumia Maandiko, badala ya kufikiri kwamba sisi hufanya maamuzi yanayofaa kila wakati. Na ikiwezekana, tuwe tayari kuacha maoni yetu ambayo tumeshikilia sana yanapothibitishwa kuwa yenye kupotosha.—Mithali 1:1-5; 15:22.

‘Fuliza Kumwomba Mungu’

Tunaishi katika wakati wenye msukosuko na hatari. Ikiwa tunataka kutenda inavyofaa na kwa hekima, ni muhimu kumwomba Yehova uongozi. Paulo anaandika: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Ikiwa tunakosa hekima ya kushughulikia matatizo au vishawishi vyenye kutatanisha, tunahitaji ‘kufuliza kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu.’—Yakobo 1:5-8.

Kwa kuwa alijua kwamba Wakristo wenzake walihitaji kuwa na hekima, mtume Petro alitaka ‘kuamsha uwezo wao mwangavu wa kufikiri.’ Alitaka ‘wakumbuke semi zilizosemwa hapo awali na manabii watakatifu na amri ya Bwana na Mwokozi,’ Yesu Kristo. (2 Petro 3:1, 2) Tukifanya hivyo na kuendelea kufikiri kupatana na Neno la Yehova, tutafikiri kwa njia inayofaa na kutenda kwa hekima.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wakristo wa mapema waliruhusu hekima ya kimungu iongoze kufikiri kwao wala si maoni ya wanadamu

[Hisani]

Philosophers left to right: Epicurus: Photograph taken by courtesy of the British Museum; Cicero: Reproduced from The Lives of the Twelve Caesars; Plato: Roma, Musei Capitolini

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kusali na kujifunza Neno la Mungu ni muhimu