Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Wengine Walivyopata Majibu

Jinsi Wengine Walivyopata Majibu

Jinsi Wengine Walivyopata Majibu

WATU wengi husali. Baadhi yao wanaamini kwamba sala zao hujibiwa. Wengine hutilia shaka kama sala zao husikiwa. Na bado wengine hutafuta majibu lakini hawajafikiria kusali kwa Mungu ili kuyapata.

Biblia husema kwamba Mungu wa kweli ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Unaposali, je, una hakika kwamba sala zako zinamwendea Mungu wa kweli? Je, sala zako ni baadhi ya zile anazojibu?

Sala za watu wengi duniani zimejibiwa. Zimejibiwa jinsi gani? Nao wamejifunza nini?

Mungu, Yeye Ni Nani?

Mwalimu mmoja wa shule huko Ureno aliyekuwa amesomea katika shule ya Wakatoliki, alifuata dini yake kwa moyo mweupe. Mwalimu huyo alichanganyikiwa baada ya kanisa kubadili msimamo wake na kuacha desturi ambazo alikuwa amefundishwa kuwa muhimu. Aliposafiri katika nchi moja ya Mashariki, alipata kujua jinsi watu wa nchi hiyo wanavyoabudu na akaanza kujiuliza kama kuna Mungu mmoja wa kweli. Alipaswa kuabudu jinsi gani? Alipomwuliza kasisi wa kanisa lake kuhusu mambo fulani katika Biblia, kasisi huyo alipuuza maswali yake, naye akavunjika moyo.

Kanisa Katoliki lilikuwa limesambaza vijitabu katika jiji anakoishi mwalimu huyo vilivyowaonya Wakatoliki wa jiji hilo wasizungumze na Mashahidi wa Yehova. Lakini bado alitaka kujibiwa maswali yake. Siku moja Mashahidi walipomtembelea aliwasikiliza na akapendezwa na habari aliyosikia. Ilikuwa mara yake ya kwanza kuzungumza nao.

Ili apate kujibiwa maswali yake yaliyokuwa mengi, mwanamke huyo alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Kila juma alikuwa na maswali mengi sana ya kuwauliza. Alitaka kujua jina la Mungu, iwapo kuna Mungu mmoja tu wa kweli, na kama Mungu anakubali watu watumie mifano katika ibada, na kadhalika. Alitambua kwamba walitumia Biblia wala si maoni yao kujibu maswali yake yote, kwa hiyo, alishangaa na kufurahia habari aliyokuwa akijifunza. Hatua kwa hatua, alijibiwa maswali yake yaliyokuwa mengi. Leo, anamwabudu Yehova kwa roho na kweli, kama vile Yesu Kristo alivyosema “waabudu wa kweli” wangefanya.—Yohana 4:23.

Huko Sri Lanka, washiriki wa familia moja walisoma Biblia pamoja kwa ukawaida, lakini hawakupata majibu kwa maswali mengi ambayo waliyaona kuwa muhimu. Ingawa walihitaji msaada, kasisi wao hakuweza kuwasaidia. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova waliwatembelea na kuwaachia vichapo vya Biblia ambavyo vingewasaidia. Baadaye, walikubali kujifunza Biblia baada ya Mashahidi wa Yehova kujibu maswali yao ya Biblia kwa njia yenye kuridhisha. Walipendezwa sana na mambo waliyojifunza.

Hata hivyo, kwa sababu ya mambo aliyokuwa amefundishwa kanisani tangu utotoni, mke alishindwa kuelewa kwamba Baba ya Yesu Kristo ndiye “Mungu wa pekee wa kweli,” kama vile Yesu mwenyewe alivyosema. (Yohana 17:1, 3) Alikuwa amefundishwa kwamba Yesu ni sawa na Baba na kwamba “fumbo” hilo halipaswi kupingwa. Alisali kwa Yehova kwa unyofu na kwa bidii, akitumia jina lake, na kumwomba amwonyeshe Yesu ni nani. Kisha akayachunguza tena maandiko yanayozungumzia jambo hilo. (Yohana 14:28; 17:21; 1 Wakorintho 8:5, 6) Ilikuwa kana kwamba macho yake yalifunguliwa, akaona waziwazi kwamba Yehova—Muumba wa mbingu na dunia na Baba ya Yesu Kristo—ndiye Mungu wa kweli.—Isaya 42:8; Yeremia 10:10-12.

Kwa Nini Watu Huteseka?

Ayubu aliteseka sana. Watoto wake wote waliuawa na dhoruba, naye akawa maskini. Pia alipatwa na ugonjwa wenye maumivu makali na kuvumilia mikazo kutoka kwa marafiki bandia. Chini ya hali hizo, wakati mwingine Ayubu alisema bila kufikiri. (Ayubu 6:3) Lakini Mungu alifikiria hali zake. (Ayubu 35:15) Alijua kilichokuwa katika moyo wa Ayubu na akampa ushauri aliohitaji. Leo pia Mungu huwashauri watu.

Castro anayeishi nchini Msumbiji alifiwa na mama yake akiwa na umri wa miaka kumi tu. Aliumia sana. Aliuliza, “Kwa nini alikufa na kutuacha?” Ingawa alilelewa na wazazi wanaomwogopa Mungu, hakuelewa kwa nini mama yake alikufa. Ni nini ambacho kingeweza kumtuliza akili na moyo? Alipata faraja kwa kusoma Biblia ndogo ya Chichewa na kuizungumzia na kaka zake.

Hatua kwa hatua, Castro alipata kuelewa kwamba mama yake alikufa si kwa sababu Mungu hafuati haki, bali kwa sababu ya dhambi tuliyorithi. (Waroma 5:12; 6:23) Alifarijiwa sana na ahadi ya Biblia ya ufufuo kwa sababu tumaini hilo lilimpa uhakika wa kwamba atamwona mama yake tena. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Kwa kusikitisha, baba yake alikufa miaka minne tu baadaye. Lakini wakati huu Castro aliweza kukabiliana na msiba huo vizuri zaidi. Leo, anampenda Yehova na anamtumikia kwa uaminifu. Wote wanaomjua wanaona kwamba yeye ni mwenye shangwe.

Watu wengi ambao wamefiwa na wapendwa wao, hupata faraja kutokana na kweli za Biblia zilizomfariji Castro. Wengi ambao wamepatwa na magumu makubwa yanayosababishwa na waovu huuliza kama Ayubu: “Mbona waovu wanaishi?” (Ayubu 21:7) Watu wanaposikiliza jibu ambalo Mungu anatoa kupitia Neno lake, wanajifunza kwamba njia ya Mungu ya kushughulikia mambo huwanufaisha.—2 Petro 3:9.

Barbara, aliyelelewa Marekani, hakuwa amejionea ukatili wa vita. Lakini alipokuwa akikua, nchi nyingi zilikuwa zikipigana. Ripoti kuhusu ukatili wa vita zilichapishwa kila siku katika magazeti. Alipokuwa shuleni alishangazwa na matukio ya kihistoria yasiyoeleweka. Yalisababishwa na nini? Je, Mungu alijali kuhusu yale yaliyokuwa yakitukia? Aliamini kwamba kuna Mungu, lakini hakumwelewa vizuri sana.

Hata hivyo, hatua kwa hatua, mtazamo wa Barbara kuhusu maisha ulibadilika kwa sababu ya kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Aliwasikiliza na kujifunza Biblia pamoja nao. Alihudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Hata alihudhuria mojawapo ya makusanyiko yao makubwa. Isitoshe alipouliza maswali, alitambua kwamba Mashahidi hawakumpa majibu yenye kutofautiana. Badala yake, Mashahidi walinena kwa upatano kwa sababu kufikiri kwao kulitegemea Biblia.

Mashahidi walitumia Biblia kumthibitishia kwamba Shetani Ibilisi ndiye mtawala wa ulimwengu, na kwa sababu hiyo ulimwengu hudhihirisha roho yake. (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4; Waefeso 2:1-3; 1 Yohana 5:19) Walieleza kwamba mambo yaliyomtatanisha Barbara, yametabiriwa katika Biblia. (Danieli, sura ya 2, 7, na 8) Mungu aliyatabiri kwa sababu anaweza kujua matukio ya wakati ujao anapotaka. Baadhi ya mambo hayo yalisababishwa na Mungu. Mengine aliruhusu tu yatukie. Mashahidi pia walimwambia Barbara kwamba Biblia inatabiri matukio mazuri na mabaya ya wakati wetu na inaeleza maana yake. (Mathayo 24:3-14) Walimwonyesha ahadi za Biblia kuhusu ulimwengu mpya wenye uadilifu na usio na mateso.—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Hatua kwa hatua, Barbara alielewa kwamba Yehova Mungu hasababishi kuteseka kwa wanadamu, wala hazuii mateso hayo kwa kuwalazimisha wanadamu watii sheria zake iwapo hawataki kufanya hivyo. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Mungu amefanya maandalizi ili tuweze kuishi milele kwa furaha, lakini sasa anatupatia fursa ya kuonyesha kama tutaishi kupatana na njia zake za uadilifu. (Ufunuo 14:6, 7) Barbara aliazimia kujifunza matakwa ya Mungu na kuyafuata. Pia aliona kwamba Mashahidi wa Yehova wanadhihirisha upendo ambao Yesu alisema ungewatambulisha wafuasi wake wa kweli.—Yohana 13:34, 35.

Wewe pia unaweza kunufaika kutokana na maandalizi yaliyomsaidia Barbara.

Maisha Yenye Kusudi

Huenda hata wale wanaoonekana kuwa wamefanikiwa maishani wakataka kupata majibu kwa maswali ambayo huwatatanisha. Kwa mfano, Matthew, mwanamume kijana nchini Uingereza, alitamani sana kumjua Mungu wa kweli na kusudi la maisha. Baba yake alikufa Matthew akiwa na umri wa miaka 17. Baadaye, Matthew alipata shahada ya digrii katika somo la muziki. Kisha akaanza kuhisi kwamba maisha yake ya kufuatia vitu vya kimwili hayakuwa na maana yoyote. Aliondoka nyumbani kwenda kuishi London ambako alianza kutumia dawa za kulevya, kwenda kwenye klabu za usiku, kujiingiza katika utabiri wa kutumia nyota, kuwasiliana na roho, na kufuatia falsafa za Kibudha na falsafa nyinginezo. Alifanya hayo yote ili kupata maisha yenye kuridhisha. Kwa kukata tamaa alimlilia Mungu ili amsaidie kupata kweli.

Siku mbili baadaye, Matthew alikutana na rafiki yake wa zamani na kumweleza matatizo yake. Rafiki huyo alikuwa amejifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Matthew alipoonyeshwa andiko la 2 Timotheo 3:1-5, alishangaa kuona jinsi Biblia inavyoeleza kwa usahihi hali zilizopo ulimwenguni. Aliguswa moyo aliposoma kuhusu Mahubiri ya Mlimani. (Mathayo, sura ya 5-7) Matthew aliamua kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa karibu, ingawa mwanzoni alisita kufanya hivyo kwa sababu alikuwa amesoma habari zenye kuwachambua Mashahidi wa Yehova.

Matthew alifurahia mambo aliyosikia kwenye mikutano na akaanza kujifunza Biblia na mmoja wa wazee wa kutaniko. Baada ya muda mfupi alitambua kwamba sala aliyotoa kwa Mungu ilikuwa inajibiwa kupitia mambo aliyokuwa anajifunza. Alinufaika kwa kuacha mazoea yasiyompendeza Yehova. Alipositawisha hofu inayofaa kwa Mungu, alichochewa kuishi kupatana na amri za Mungu. Matthew alijifunza kwamba maisha hayo yana kusudi halisi.—Mhubiri 12:13.

Haikuwa imeamuliwa kimbele kwamba Matthew au wengine waliotajwa katika makala hii wangepata kuishi maisha yenye kuridhisha. Hata hivyo, walijifunza kwamba Yehova Mungu ana kusudi lenye upendo kwa wale wote wanaoamua kwa hiari kutii amri zake. (Matendo 10:34, 35) Kusudi hilo linatia ndani uhai wa milele katika ulimwengu usio na vita, magonjwa, njaa, na hata kifo. (Isaya 2:4; 25:6-8; 33:24; Yohana 3:16) Je, ungependa kuishi maisha kama hayo? Ikiwa ndivyo, unaweza kujifunza mengi kuhusu jinsi unavyoweza kupata maisha yenye kuridhisha kwa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova ambako Biblia huzungumziwa. Unakaribishwa kwa uchangamfu kuhudhuria mikutano hiyo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Sali kwa Mungu kwa bidii ukitumia jina lake

[Picha katika ukurasa wa 7]

Jifunze Biblia pamoja na wale ambao hufundisha kweli ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 7]

Hudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 4]

Hiker: Chad Ehlers/Index Stock Photography