Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ushirikina Unaongoza Maisha Yako?

Je, Ushirikina Unaongoza Maisha Yako?

Je, Ushirikina Unaongoza Maisha Yako?

USHIRIKINA upo ulimwenguni pote. Nyakati nyingine, ushirikina huthaminiwa sana, ukionwa kuwa urithi wa kitamaduni. Au huenda ukaonwa kuwa udadisi tu unaofanya maisha yawe yenye kusisimua. Katika nchi za Magharibi, ushirikina hauchukuliwi kwa uzito. Kwingineko—kwa mfano, barani Afrika—ushirikina unaweza kuathiri vibaya sana maisha ya watu.

Utamaduni mwingi wa Kiafrika unategemea sana ushirikina. Mara nyingi sinema, majadiliano ya redio, na vitabu vinavyotolewa barani Afrika hukazia ushirikina na mambo ya mafumbo, kama vile uchawi, kuabudu wazazi wa kale, na hirizi. Kwa nini watu huathiriwa sana na ushirikina, na chanzo cha ushirikina ni nini?

Chanzo cha Ushirikina Ni Nini?

Ushirikina hasa unatokana na kuogopa roho za wafu au roho za aina nyinginezo. Matukio fulani huonwa kuwa njia ambazo roho hao hutumia kujaribu kuwasiliana na watu walio hai kwa kuwatisha, kuwaonya, au hata kuwabariki.

Ushirikina pia unahusianishwa sana na uponyaji na dawa. Dawa za kisasa ni za bei ya juu sana hivi kwamba, watu wengi katika nchi zinazoendelea hawawezi kuzinunua. Hivyo, wengi wanageukia tamaduni za wazazi wao wa kale, uwasiliani-roho, na ushirikina ili kupata ponyo au kinga. Pia, wanastarehe zaidi wanapoenda kumwona mchawi anayejua tamaduni zao na anayezungumza lugha yao kuliko kwenda kumwona daktari. Hivyo, ushirikina huzidi kuenea.

Wanaofuata ushirikina wanaamini kwamba ugonjwa na aksidenti hazitokei tu, bali husababishwa na nguvu fulani ya roho. Huenda wachawi wakadai kwamba mzazi fulani wa kale amechukizwa na jambo fulani. Au huenda wawasiliani-roho wakadokeza kwamba mtu aliyepatwa na ugonjwa au aksidenti alilaaniwa na mchawi fulani anayeshindana nao.

Kuna ushirikina wa aina nyingi ulimwenguni, na kuenezwa kwa ushirikina hutegemea utamaduni, hekaya, na hali ya mahali fulani. Lakini ile imani kwamba mtu fulani au kiumbe fulani kutoka ulimwengu wa roho anataka kutulizwa ndiyo sababu kuu ambayo hufanya ushirikina uenee.

Je, Ushirikina Ni Zoea Lisilodhuru au Ni Zoea Hatari?

Familia nyingi huona kuzaliwa kwa mapacha kuwa jambo la pekee na lenye kufurahisha. Hata hivyo, huenda mtu anayeamini ushirikina akaona tukio hilo kuwa ishara ya jambo fulani. Katika maeneo fulani huko Afrika Magharibi, watu wengi huona tukio hilo kuwa kuzaliwa kwa miungu, nao huabudu mapacha hao. Iwapo pacha mmoja au wote wawili wanakufa sanamu ndogo za mapacha hao hutengenezwa, nazo familia zinapaswa kuzipa sanamu hizo chakula. Kwingineko, watu huona kuzaliwa kwa mapacha kuwa laana, na hata wazazi fulani huua angalau mmoja wa mapacha hao. Kwa nini? Wanaamini kwamba ikiwa mapacha wote wawili wataishi, watawaua wazazi wao siku moja.

Mifano kama hiyo inaonyesha kwamba ingawa huenda ushirikina fulani ukaonekana kuwa usiodhuru na usioudhi, kuna aina nyingine za ushirikina zinazoweza kuwa hatari—hata zenye kuleta kifo. Tukio fulani lisilodhuru linaweza kugeuzwa kuwa jambo hatari ikiwa litaeleweka vibaya.

Naam, kwa kweli ushirikina ni imani, aina fulani ya dini. Kwa kufikiria hatari zinazohusiana na ushirikina, inafaa kuuliza hivi: Ni nani anayenufaika kutokana na imani na desturi za kishirikina?

Chanzo cha Ushirikina

Watu wengi hawakubali kwamba kuna Shetani na roho waovu ingawa kuna uthibitisho wa kutosha wa jambo hilo. Hata hivyo, wakati wa vita, kukataa kutambua kwamba kuna adui hatari kunaweza tu kuleta msiba. Inaweza kuwa vivyo hivyo tunapopambana na viumbe wa roho wenye nguvu nyingi kuliko za mwanadamu kwa kuwa mtume Paulo aliandika: “Tuna kushindana mwereka . . . dhidi ya majeshi ya roho waovu.”—Waefeso 6:12.

Roho waovu wako hata ingawa hatuwezi kuwaona. Biblia inasema kwamba roho mwovu fulani asiyeonekana alitumia nyoka kuwasiliana na mwanamke wa kwanza Hawa na hivyo roho huyo mwovu akafanya mwanamke huyo amwasi Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Biblia humtambulisha kiumbe huyo wa roho kuwa “nyoka wa awali, yeye aitwaye Ibilisi na Shetani, anayeiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Shetani alifanikiwa kushawishi malaika wengine wamwasi Mungu. (Yuda 6) Malaika hao wakawa roho waovu, adui za Mungu.

Yesu na wanafunzi wake walifukuza roho waovu waliopagaa watu. (Marko 1:34; Matendo 16:18) Roho hao si wazazi wa kale, kwa kuwa “wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Bali, hao ni malaika waasi waliopotoshwa na Shetani. Kuwasiliana nao au kuacha watuongoze ni jambo lisilopaswa kuchukuliwa vivi hivi. Hiyo ni kwa sababu roho hao, kama kiongozi wao Shetani Ibilisi, wanaweza kutuangamiza. (1 Petro 5:8) Lengo lao ni kutufanya tukose tumaini pekee kwa wanadamu—Ufalme wa Mungu.

Biblia hufunua mojawapo ya njia ambazo Shetani na roho wake waovu hutumia: “Shetani mwenyewe hufuliza kujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Shetani angependa kutupumbaza tuamini kwamba anaweza kufanya maisha yetu yawe bora. Kwa hiyo, huenda ikaonekana kana kwamba roho waovu wanaleta manufaa fulani za muda. Lakini roho waovu hawawezi kutatua matatizo yetu kabisa. (2 Petro 2:4) Hawawezi kutupatia uhai wa milele, nao wataharibiwa hivi karibuni. (Waroma 16:20) Muumba wetu ndiye pekee anayeweza kutupatia uhai wa milele, furaha ya kweli, na kinga bora zaidi dhidi ya roho waovu.—Yakobo 4:7.

Mungu hushutumu kuwasiliana na roho ili kutafuta msaada. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; 2 Wafalme 21:6) Kufanya hivyo ni kushirikiana na adui, kufanya urafiki na wasaliti wa Mungu! Kufanya uaguzi kwa kutumia nyota, kutafuta habari fulani kwa mganga wa kienyeji, au kujiingiza katika ushirikina wa aina yoyote ile humaanisha kwamba unawaruhusu roho waovu wakuongoze katika maamuzi unayofanya maishani mwako. Hiyo ni sawa na kuwaunga mkono katika kumwasi Mungu.

Je, Unaweza Kupata Ulinzi Dhidi ya Uovu?

Ade, * mwanamume anayeishi huko Niger, alikuwa akijifunza Biblia na mhubiri wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Ade alimweleza ni kwa nini aliweka hirizi fulani kwenye duka lake: “Nina adui wengi.” Lakini mwalimu wake wa Biblia akamweleza kwamba, Yehova peke yake ndiye anayeweza kuandaa ulinzi kamili. Alimsomea Ade andiko la Zaburi 34:7, linalosema: “Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.” Naye Ade akamalizia kwa kusema: “Ikiwa kwa kweli Yehova anaweza kunilinda, basi nitaondoa hirizi hiyo.” Sasa, baada ya miaka mingi, Ade anatumikia akiwa mzee wa kutaniko na mhubiri wa wakati wote. Hakuna hata mmoja wa adui zake ambaye amemdhuru.

Biblia inaonyesha kwamba wakati na matukio yasiyotazamiwa hutupata sote, tuwe tunaamini ushirikina au la. (Mhubiri 9:11) Lakini Yehova hatujaribu kwa maovu. (Yakobo 1:13) Kifo na hali ya kutokamilika husababishwa na dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu. (Waroma 5:12) Kwa sababu hiyo, sote huwa wagonjwa mara kwa mara, na hufanya makosa yanayoweza kuleta msiba. Kwa hiyo, ingekuwa makosa kusema kwamba magonjwa yote au matatizo yote husababishwa na roho waovu. Imani kama hiyo inaweza kutushawishi tujaribu kuwatuliza roho hao kwa njia fulani. * Tunapokuwa wagonjwa tunapaswa kutafuta matibabu yanayofaa, wala si ushauri kutoka kwa ‘mwongo na baba ya uwongo,’ Shetani Ibilisi. (Yohana 8:44) Takwimu zinaonyesha kwamba watu wanaoishi katika nchi ambako ushirikina unaohusianishwa na wazazi wa kale umeenea sana, hawaishi maisha marefu na bora kuliko watu wa nchi nyinginezo. Basi, ni wazi kwamba ushirikina hauna manufaa yoyote kiafya.

Mungu ni mwenye nguvu kuliko roho mwovu yeyote, Naye anatutakia mema. “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao.” (1 Petro 3:12) Sali kwake ili upate ulinzi na hekima. (Mithali 15:29; 18:10) Jitahidi kuielewa Biblia, Neno lake Takatifu. Ujuzi sahihi wa Biblia ndio ulinzi bora tuwezao kupata. Utatusaidia kufahamu ni kwa nini mambo mabaya hutokea na jinsi ya kupata kibali cha Mungu Mweza Yote.

Manufaa za Kumjua Mungu

Ujuzi sahihi juu ya Yehova na makusudi yake—kinyume cha ushirikina na kutojua—ndio ufunguo wa kupata ulinzi wa kweli. Jambo hilo linathibitishwa na kisa cha Jean, mwanamume mmoja kutoka Benin. Familia ya Jean iliamini sana ushirikina. Kulingana na tamaduni za kishirikina za kabila lao, mwanamke aliyezaa mtoto wa kiume anapaswa kukaa kwa siku tisa katika kibanda kilichojengwa kwa njia maalumu. Akizaa mtoto wa kike, anapaswa kukaa kwenye kibanda hicho kwa siku saba.

Katika mwaka wa 1975, mke wa Jean alizaa mtoto mzuri wa kiume ambaye walimwita Marc. Kwa kuwa walikuwa na ujuzi wa Biblia, Jean na mke wake hawakutaka kujihusisha na roho waovu. Lakini je, woga na mkazo ungewafanya wafuate ushirikina na kumfanya mama ya Marc akae kwenye kibanda? La—walikataa katakata kufuata ushirikina wa kabila lao.—Waroma 6:16; 2 Wakorintho 6:14, 15.

Je, familia ya Jean ilipatwa na madhara yoyote? Miaka mingi imepita, na Marc sasa anatumikia akiwa mtumishi wa huduma katika kutaniko la kwao la Mashahidi wa Yehova. Familia nzima inafurahi kwamba hawakuruhusu ushirikina uongoze maisha yao na kuhatarisha hali yao njema ya kiroho.—1 Wakorintho 10:21, 22.

Wakristo wa kweli wanapaswa kuepuka kabisa mambo maovu yanayohusiana na ushirikina na kukubali nuru ya kiroho inayoangazwa na Muumba, Yehova, na Mwana wake, Yesu Kristo. Hivyo wanaweza kufurahia amani ya kweli ya akili inayotokana na kujua kwamba wanafanya yanayofaa machoni pa Mungu.—Yohana 8:32.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 21 Ona makala “Je, Ibilisi Hutufanya Tuwe Wagonjwa?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1999.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

Ushirikina Ambao Umeenea Ulimwenguni

• Vijiti vilivyosimama juu ya bakuli la wali ni ishara ya kifo.

• Kuona bundi mchana huleta bahati mbaya

• Mshumaa ukizimika wakati wa sherehe ni ishara kwamba roho waovu wako karibu

• Kuangusha mwavuli sakafuni ni ishara kwamba mtu fulani atauawa katika nyumba hiyo

• Kuweka kofia juu ya kitanda huleta bahati mbaya

• Mlio wa kengele hufukuza roho waovu

• Kuzima mishumaa yote kwenye keki ya siku ya kuzaliwa kwa kupuliza mara moja tu, humaanisha kwamba utatimiziwa unachotaka

• Ufagio unaoegemea kitanda huruhusu roho waovu kwenye ufagio huo kuroga kitanda hicho

• Paka mweusi akipita mbele yako ni ishara ya bahati mbaya

• Kuangusha uma wa kulia ni ishara kwamba mwanamume atakutembelea

• Picha ya tembo ikiwekwa kuelekea mlangoni huleta bahati nzuri

• Kiatu cha farasi huleta bahati nzuri kikiwekwa kwenye mlango

• Mmea wa mwefeu ukimea kwenye nyumba huikinga na uovu

• Ni bahati mbaya kutembea chini ya ngazi

• Kuvunja kioo ni ishara ya miaka saba ya bahati mbaya

• Ukimwaga pilipili ni ishara kwamba utagombana na rafiki yako wa karibu

• Ukimwaga chumvi utakuwa na bahati mbaya usiporusha kiasi kidogo cha chumvi hiyo nyuma yako juu ya bega la kushoto

• Kuacha kiti cha bembea kikibembea bila mtu hukaribisha roho waovu kuketi juu yake

• Kuacha viatu upande wa chini ukiwa juu huleta bahati mbaya

• Mtu akifa, madirisha yanapaswa kufunguliwa ili nafsi yake itoke nje

[SandukuPicha katika ukurasa wa 6]

Kuwekwa Huru na Ushirikina

Mashahidi wa Yehova walikuwa wakihubiri katika eneo fulani huko Afrika Kusini. Walibisha mlango fulani na ulipofunguliwa, mwanamke aliyevalia mavazi ya Sangoma (mchawi) akatokea. Mashahidi hao walitaka kuondoka, lakini mwanamke huyo akasisitiza wamweleze ujumbe waliokuwa nao. Mmoja wa Mashahidi hao alimsomea Kumbukumbu la Torati 18:10-12 ili kumwonyesha maoni ya Mungu kuhusu kuwasiliana na roho waovu. Mchawi huyo alikubali ujumbe huo na akakubali kujifunza Biblia. Alisema kwamba ataacha uchawi ikiwa kwa kujifunza Biblia atathibitishiwa kwamba zoea hilo ni kinyume cha mapenzi ya Yehova.

Baada ya kujifunza sura ya 10 ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani pamoja na Biblia, aliteketeza vitu vyote vya uchawi na akaanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Zaidi ya hayo, alihalalisha ndoa yake, ingawa alikuwa ametengana na mume wake kwa miaka 17. Sasa, yeye na mume wake ni Mashahidi wa Yehova waliobatizwa.

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Sangoma” atupa mifupa anapoagua ili apate kujua ni nini kinachosababisha matatizo ya mgonjwa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ujuzi sahihi juu ya Mungu huleta ulinzi na furaha ya kweli