Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kumtumikia Yehova kwa Moyo Thabiti

Endelea Kumtumikia Yehova kwa Moyo Thabiti

Endelea Kumtumikia Yehova kwa Moyo Thabiti

“Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, moyo wangu u thabiti.”—ZABURI 57:7.

1. Kwa nini tunaweza kuwa na usadikisho kama wa Daudi?

YEHOVA anaweza kutufanya tuwe na imani thabiti ya Kikristo ili tushikamane na Ukristo wa kweli tukiwa watumishi wake waliojiweka wakfu. (Waroma 14:4) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na usadikisho kama wa mtunga-zaburi Daudi aliyechochewa kuimba: “Ee Mungu, moyo wangu u thabiti.” (Zaburi 108:1) Ikiwa moyo wetu ni thabiti, tutachochewa kuishi kupatana na wakfu wetu kwa Mungu. Na kwa kumtegemea ili kupata mwongozo na nguvu, tunaweza kuwa imara, wenye usadikisho thabiti tukiwa washika uaminifu-maadili, ‘sikuzote tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 Wakorintho 15:58.

2, 3. Himizo la Paulo katika 1 Wakorintho 16:13 linamaanisha nini?

2 Mtume Paulo alisema hivi kuwahimiza wafuasi wa Yesu huko Korintho la kale na pia Wakristo wa sasa: “Kaeni macho, simameni imara katika imani, endeleeni kama wanaume, kueni mwe wenye uweza.” (1 Wakorintho 16:13) Katika Kigiriki maagizo hayo yote yako katika hali ya wakati uliopo, kwa hiyo yatuhimiza tuendelee kutenda. Himizo hilo linamaanisha nini?

3 Tunaweza ‘kukaa macho’ kiroho kwa kumpinga Ibilisi na kumkaribia Mungu. (Yakobo 4:7, 8) Kumtegemea Yehova hutuwezesha kudumisha muungano na ‘kusimama imara katika imani ya Kikristo.’ Sisi—kutia ndani wanawake wengi walio miongoni mwetu—‘tunaendelea kama wanaume’ kumtumikia Mungu kwa ujasiri tukiwa watangazaji wa Ufalme. (Zaburi 68:11) ‘Tunakua wenye uweza’ kwa kuendelea kumtegemea Baba yetu wa kimbingu atupatie nguvu za kufanya mapenzi yake.—Wafilipi 4:13.

4. Ni matayarisho gani tuliyofanya ili kubatizwa na kuwa Wakristo?

4 Tulionyesha kwamba tumekubali kweli tulipojiweka wakfu kwa Yehova bila masharti na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Lakini ni matayarisho gani tuliyofanya hadi tukabatizwa? Kwanza, tulitwaa ujuzi sahihi wa Neno la Mungu. (Yohana 17:3) Ujuzi huo ulifanya tuwe na imani ambayo ilituchochea kutubu, tukadhihirisha sikitiko la kweli kuhusu makosa tuliyofanya awali. (Matendo 3:19; Waebrania 11:6) Kisha tukageuka, kwa kuacha mazoea mabaya ili kuishi maisha yanayopatana na mapenzi ya Mungu. (Waroma 12:2; Waefeso 4:23, 24) Baada ya hapo tulijiweka wakfu kwa Yehova kwa moyo wote kupitia sala. (Mathayo 16:24; 1 Petro 2:21) Tulimwomba Mungu atupatie dhamiri safi na tukabatizwa ili kuonyesha wakfu wetu kwake. (1 Petro 3:21) Kukumbuka hatua hizo kutatusaidia tusiache kukazia fikira uhitaji wa kuendelea kujitahidi ili kuishi kupatana na wakfu wetu na kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo thabiti.

Endelea Kutafuta Ujuzi Sahihi

5. Kwa nini twapaswa kuendelea kujifunza Maandiko?

5 Ili kuishi kupatana na wakfu wetu kwa Mungu, twapaswa kuendelea kujifunza Maandiko yanayoimarisha imani. Tulifurahi kama nini kula chakula cha kiroho tulipofahamu kweli ya Mungu mara ya kwanza! (Mathayo 24:45-47) “Vyakula” hivyo vilikuwa na ladha nzuri—navyo vilitujenga kiroho. Sasa ni muhimu tuendelee kula chakula chenye lishe ya kiroho ili tudumishe moyo thabiti tukiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu.

6. Huenda ulisaidiwaje uwe mwenye shukrani ya kutoka moyoni kwa ajili ya kweli ya Biblia?

6 Jitihada inahitajiwa ili kuongeza ujuzi wa Kimaandiko. Ni kama kutafuta hazina iliyofichwa—jambo linalohitaji jitihada nyingi. Lakini inathawabisha kama nini kupata “kumjua Mungu”! (Mithali 2:1-6) Mhubiri wa Ufalme alipojifunza Biblia pamoja nawe mara ya kwanza, huenda alitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Labda mlitumia wakati mwingi kumaliza kila sura, pengine mlijifunza sura hiyo zaidi ya pindi moja. Ulinufaika wakati maandiko yaliyotajwa yaliposomwa na kuzungumziwa. Ulielezwa mambo yaliyokuwa magumu kufahamu. Mtu aliyejifunza Biblia nawe alijitayarisha vizuri, akasali kupata roho ya Mungu, na kukusaidia uwe mwenye shukrani ya kutoka moyoni kwa ajili ya ile kweli.

7. Ni nini humsaidia mtu astahili kufundisha wengine kweli ya Mungu?

7 Jitihada hiyo ilifaa, kwa kuwa Paulo aliandika hivi: “Acheni yeyote afundishwaye neno kwa mdomo ashiriki katika mambo mema yote pamoja naye atoaye fundisho la mdomo la namna hiyo.” (Wagalatia 6:6) Hapa maandishi ya Kigiriki yanaonyesha kwamba mafundisho ya Neno la Mungu yalikaziwa kikiki katika akili na moyo wa mtu ‘aliyefundishwa kwa mdomo.’ Kufundisha kwa njia hiyo hukusaidia ustahili kufundisha wengine. (Matendo 18:25) Ili uwe mwaminifu kwa wakfu wako, lazima udumishe afya nzuri ya kiroho na uthabiti kwa kuendelea kujifunza Neno la Mungu.—1 Timotheo 4:13; Tito 1:13; 2:2.

Kumbuka Wakati Ulipotubu na Kugeuka

8. Unaweza kudumishaje mwenendo mtakatifu?

8 Je, unakumbuka jinsi ulivyohisi ulipojifunza kweli, ukatubu, na kuhisi kwamba umepata msamaha wa Mungu kwa sababu ya kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu? (Zaburi 32:1-5; Waroma 5:8; 1 Petro 3:18) Bila shaka hungependa kurudia maisha ya dhambi. (2 Petro 2:20-22) Kusali kwa Yehova kwa ukawaida ni mojawapo ya mambo yatakayokusaidia kudumisha mwenendo safi, kuishi kupatana na wakfu wako, na kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.—2 Petro 3:11, 12.

9. Baada ya kuacha mazoea ya dhambi, twapaswa kufuata njia gani?

9 Baada ya kugeuka na kuacha mazoea ya dhambi, endelea kutafuta msaada wa Mungu ili kudumisha moyo thabiti. Kwa kweli, ulikuwa ukifuata njia isiyo sawa lakini ukachunguza ramani iliyo sahihi na kuanza kusafiri katika njia iliyo sawa. Usipotee njia sasa. Endelea kutegemea mwongozo wa Mungu, na uazimie kudumu katika njia iongozayo kwenye uhai.—Isaya 30:20, 21; Mathayo 7:13, 14.

Usisahau Kamwe Wakfu na Ubatizo Wako

10. Tunapaswa kukumbuka mambo gani kuhusu wakfu wetu kwa Mungu?

10 Kumbuka kwamba ulijiweka wakfu kwa Yehova kupitia sala, ukiwa na tumaini la kumtumikia kwa uaminifu milele. (Yuda 20, 21) Kujiweka wakfu kunamaanisha kwamba umetengwa kwa kusudi takatifu. (Mambo ya Walawi 15:31; 22:2) Wakfu wako haukuwa makubaliano ya muda au kuwa na wajibu kwa mtu fulani. Ulikuwa wakfu wa kudumu kwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, na kuishi kupatana na wakfu huo kwataka mtu awe mwaminifu-mshikamanifu kwa Mungu muda wote wa maisha yake. Naam, ‘tuishi au tufe, sisi ni wa Yehova.’ (Waroma 14:7, 8) Ili tuwe wenye furaha tunapaswa kufanya mapenzi yake na kuendelea kumtumikia kwa moyo thabiti.

11. Kwa nini ukumbuke ubatizo wako na maana ya ubatizo huo?

11 Sikuzote kumbuka kuwa ubatizo huonyesha kwamba umejiweka wakfu kwa Mungu kwa moyo wako wote. Hukulazimishwa kubatizwa, kwa kuwa uliamua mwenyewe. Je, sasa umeazimia kuonyesha uamuzi wako kupatana na mapenzi ya Mungu kwa muda wote wa maisha yako? Ulimwomba Mungu akupe dhamiri safi na ukabatizwa ili kuonyesha kwamba umejiweka wakfu kwake. Dumisha dhamiri hiyo safi kwa kuishi kupatana na wakfu wako, nawe utapokea baraka nyingi za Yehova.—Mithali 10:22.

Hiari Yako Inahusika

12, 13. Hiari yetu inahusianaje na wakfu na ubatizo?

12 Kwa kweli, mamilioni ya watu duniani pote wamenufaika kwa kujiweka wakfu na kubatizwa. Tunapoonyesha wakfu wetu kwa Mungu kwa kubatizwa katika maji, tunakufa kwa kuacha mwenendo wetu wa zamani lakini hatuachi kufanya mambo kwa hiari. Kwa kweli, tulipojiweka wakfu kwa Mungu kupitia sala na kubatizwa tukiwa waumini waliofundishwa ifaavyo, tulifanya hivyo kwa hiari. Kuweka maisha yetu wakfu kwa Mungu na kubatizwa hutaka tujue mapenzi ya Mungu ni nini kisha tuamue kuyafanya. (Waefeso 5:17) Kwa kufanya hivyo tunamwiga Yesu, aliyeacha kazi ya useremala kwa hiari, akabatizwa, na kujitoa kabisa kufanya mapenzi ya Baba yake wa kimbingu.—Zaburi 40:7, 8; Yohana 6:38-40.

13 Yehova Mungu alikusudia Mwana wake afanywe kuwa “mkamilifu kupitia mateso.” Kwa hiyo Yesu alilazimika kuvumilia mateso hayo kwa uaminifu kwa hiari yake. Ili kutimiza hayo, alitoa “dua na pia maombi . . . na vilio vyenye kupaazwa kwa nguvu na machozi, naye akasikiwa kwa kupendelewa kwa sababu ya hofu yake ya kimungu.” (Waebrania 2:10, 18; 5:7, 8) Tukidhihirisha hofu hiyo yenye staha kwa Mungu, sisi pia tutakuwa na hakika kwamba ‘tutasikiwa kwa kupendelewa,’ na kwamba Yehova atatufanya tuwe thabiti tukiwa Mashahidi wake waliojiweka wakfu.—Isaya 43:10.

Unaweza Kudumisha Moyo Thabiti

14. Kwa nini tusome Biblia kila siku?

14 Ni nini kitakachokusaidia kudumisha moyo thabiti na hivyo kuishi kupatana na wakfu wako kwa Mungu? Soma Biblia kila siku ukiwa na kusudi la kuendelea kuongeza ujuzi wako wa Neno la Mungu. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hutuhimiza daima kufanya hivyo. Shauri hilo hutolewa kwa sababu kuishi kupatana na wakfu wetu hutaka tuendelee kutembea katika kweli ya Mungu. Ikiwa tengenezo la Yehova lingekubali kimakusudi mafundisho yasiyo ya kweli, Mashahidi wa Yehova na watu wanaowahubiria hawangeshauriwa kusoma Biblia.

15. (a) Ni nini kinachopaswa kufikiriwa tunapofanya maamuzi? (b) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Mkristo hatangulizi kazi ya kimwili maishani?

15 Unapofanya maamuzi, sikuzote fikiria jinsi yanavyoweza kuathiri azimio lako la kuishi kupatana na wakfu wako kwa Yehova. Huenda yakahusu kazi yako ya kimwili. Je, unajitahidi kufanya kazi hiyo ikusaidie kusongeza mbele ibada ya kweli? Ingawa kwa ujumla waajiri huona kwamba Wakristo waliojiweka wakfu ni wenye kutumainika na stadi, pia wanatambua kwamba Mashahidi wa Yehova hawana tamaa ya makuu ya kupata mafanikio ya ulimwengu na hawashindani na wenzao ili kupata vyeo vya mshahara mkubwa. Hii ni kwa sababu Mashahidi hawana nia ya kutajirika, kupata umashuhuri, sifa, au mamlaka. Jambo lililo muhimu zaidi kwa wale wanaoishi kupatana na wakfu wao kwa Mungu, ni kufanya mapenzi yake. Hawatangulizi kazi ya kimwili ambayo huwawezesha kupata mahitaji ya msingi. Kama mtume Paulo, kazi yao kuu ni huduma ya Kikristo. (Matendo 18:3, 4; 2 Wathesalonike 3:7, 8; 1 Timotheo 5:8) Je, unatanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwako?—Mathayo 6:25-33.

16. Tunaweza kufanya nini ikiwa mahangaiko yasiyo ya lazima yanafanya iwe vigumu kuishi kupatana na wakfu wetu kwa Mungu?

16 Huenda wengine walikuwa karibu kulemewa kabisa na mahangaiko mbalimbali kabla ya kujifunza kweli. Lakini mioyo yao ilijaa shangwe, shukrani, na upendo kwa Mungu kama nini walipokubali tumaini la Ufalme! Kukumbuka manufaa ambayo wamepata tangu wakati huo kwaweza kuwasaidia waishi kupatana na wakfu wao kwa Yehova. Kwa upande mwingine, namna gani mahangaiko yasiyofaa kuhusu matatizo ya kawaida ya maisha katika mfumo huu yakitisha kusonga “neno la Mungu,” kama vile miiba iwezavyo kuzuia miche isikomae na kuzaa? (Luka 8:7, 11, 14; Mathayo 13:22; Marko 4:18, 19) Ukiona kwamba hali hiyo imeanza kukupata wewe au familia yako, mtwike Yehova mahangaiko yako na umwombe akusaidie kukua katika upendo na shukrani. Ukimtwika mzigo wako, atakutegemeza na kukupa nguvu ya kuendelea kumtumikia kwa furaha ukiwa na moyo thabiti.—Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7; Ufunuo 2:4.

17. Inawezekanaje kuvumilia majaribu makali?

17 Endelea kusali kwa Yehova Mungu kwa ukawaida, kama ulivyosali wakati ulipojiweka wakfu kwake. (Zaburi 65:2) Unaposhawishiwa kufanya kosa, au unapokabili jaribu kali, tafuta mwongozo wa Mungu na umwombe akusaidie kuufuata. Kumbuka kwamba unahitaji imani kwa kuwa mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima [ya kuvumilia jaribu], acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo. Lakini acheni afulize kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo, kwa maana yeye atiaye shaka ni kama wimbi la bahari liendeshwalo na upepo na kupeperushwa huku na huku. Kwa kweli, acheni mtu huyo asidhani kwamba atapokea kitu chochote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu wa kusitasita kuamua, asiye imara katika njia zake zote.” (Yakobo 1:5-8) Ikiwa jaribu fulani laonekana kana kwamba litatushinda, twaweza kuwa na uhakika huu: “Hakuna kishawishi ambacho kimewapata nyinyi ila kilicho kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili, bali pamoja na hicho kishawishi ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kuvumilia hilo.”—1 Wakorintho 10:13.

18. Tunaweza kufanya nini ikiwa tumeficha dhambi nzito ambayo inadhoofisha azimio letu la kuishi kupatana na wakfu wetu kwa Yehova?

18 Namna gani ikiwa umeficha dhambi nzito ambayo inakusumbua dhamiri na kudhoofisha azimio lako la kuishi kupatana na wakfu wako kwa Mungu? Ikiwa umetubu, unaweza kupata faraja kwa kujua kwamba Yehova ‘hataudharau moyo uliovunjika na kupondeka.’ (Zaburi 51:17) Tafuta msaada wa wazee Wakristo wenye upendo, ukifahamu kwamba wazee hao—kwa kumwiga Yehova—hawatapuuza tamaa yako ya kurudisha tena uhusiano mzuri pamoja na Baba yako wa kimbingu. (Zaburi 103:10-14; Yakobo 5:13-15) Kisha ukiwa na nguvu mpya za kiroho na moyo thabiti, utaweza kunyoosha njia zako na kuweza kuishi kupatana na wakfu wako kwa Mungu.—Waebrania 12:12, 13.

Endelea Kutumikia kwa Moyo Thabiti

19, 20. Kwa nini ni muhimu tuendelee kuishi kupatana na wakfu wetu?

19 Katika nyakati hizi zenye hatari, lazima tujitahidi sana kuishi kupatana na wakfu wetu na kuendelea kumtumikia Mungu kwa moyo thabiti. Yesu alisema: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Kwa kuwa tunaishi katika “siku za mwisho,” mwisho unaweza kuja wakati wowote. (2 Timotheo 3:1) Isitoshe, hakuna mmoja kati yetu anayeweza kuwa na uhakika kwamba atakuwa hai kesho. (Yakobo 4:13, 14) Kwa hiyo, ni muhimu kuendelea kuishi kupatana na wakfu wetu sasa!

20 Mtume Petro alikazia jambo hilo katika barua yake ya pili. Alionyesha kwamba kama vile watu wasiomhofu Mungu walivyoangamia kabla ya Furiko, ndivyo dunia ya mfano, au jamii ya wanadamu waovu watakavyoharibiwa katika “siku ya Yehova.” Kwa hiyo Petro alisema hivi kwa mkazo: “Mwapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu”! Pia aliwahimiza hivi: “Wapendwa, mkiwa mnakuwa na ujuzi huu wa kimbele, iweni wenye kulinda ili msipate kuongozwa kando [na walimu wasio wa kweli na watu wasiomhofu Mungu] na kuanguka kutoka kwenye uimara wenu wenyewe.” (2 Petro 3:5-17) Lingekuwa jambo la kuhuzunisha kama nini iwapo mtu aliyebatizwa angeongozwa vibaya na kufa akiwa ameshindwa kudumisha moyo thabiti!

21, 22. Maneno ya Zaburi 57:7 yamethibitikaje kuwa ya kweli kuhusiana na Daudi na Wakristo wa kweli?

21 Azimio lako la kuishi kupatana na wakfu wako kwa Mungu laweza kuimarishwa ukikumbuka siku yenye furaha ambayo ulibatizwa, na kutafuta msaada wa Mungu ili ufurahishe moyo wake kwa maneno na matendo. (Mithali 27:11) Yehova hawatamaushi watu wake kamwe, na bila shaka twapaswa kuwa waaminifu kwake. (Zaburi 94:14) Alionyesha huruma na sikitiko kwa kuvuruga mbinu za maadui na kumwokoa Daudi. Akishukuru kwa wokovu huo, Daudi alitangaza jinsi upendo wake kwa Mkombozi wake ulivyokuwa thabiti na imara. Aliimba hivi akiwa na hisia nyingi: “Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, moyo wangu u thabiti. Nitaimba, nitaimba zaburi.”—Zaburi 57:7.

22 Kama Daudi, Wakristo wa kweli wako imara katika ujitoaji wao kwa Mungu. Wakiwa na mioyo thabiti, wanamsifu Yehova kwa kuwakomboa na kuwahifadhi na hivyo kumwimbia kwa shangwe. Ikiwa moyo wako ni thabiti, utamtegemea Mungu, na kwa msaada wake utaweza kuishi kupatana na wakfu wako. Naam, unaweza kuwa kama “mwenye haki” ambaye mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu: “Hataogopa habari mbaya; moyo wake u imara, ukimtumaini BWANA.” (Zaburi 112:6, 7) Kwa kuwa na imani katika Mungu na kumtegemea kabisa, unaweza kuishi kupatana na wakfu wako na kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo thabiti.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tuendelee kutwaa ujuzi sahihi wa Biblia?

• Kwa nini tukumbuke toba na kugeuka kwetu?

• Tunanufaikaje kwa kukumbuka wakfu wetu na ubatizo?

• Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kumtumikia Yehova kwa moyo thabiti?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unadumisha afya nzuri ya kiroho kwa kusoma Neno la Mungu kila siku?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kufanya huduma ya Kikristo iwe kazi kuu kutatusaidia tuendelee kumtumikia Yehova kwa moyo thabiti