Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ni Nini Hutambulisha Haki ya Yehova?”

“Ni Nini Hutambulisha Haki ya Yehova?”

“Ni Nini Hutambulisha Haki ya Yehova?”

KATIKA Biblia, haki inafafanuliwa kuwa udumishaji na utekelezaji wa yaliyo sawa kwa njia ifaayo na isiyo na ubaguzi, na kwa kupatana na kiwango fulani kilichowekwa. Neno la Kiebrania mish·patʹ, ambalo mara nyingi hutafsiriwa “haki” au “hukumu” (NW, UV), laweza pia kumaanisha mpango fulani maalum (Kutoka 26:30), desturi (Mwanzo 40:13), kanuni (2 Mambo ya Nyakati 4:20, NW), au utaratibu fulani wa kawaida (Mambo ya Walawi 5:10, NW) wa kufanya mambo.

Ingawa neno haki hutumiwa katika mambo yanayohusiana na kesi za mahakama, kimsingi hakuna tofauti kati ya neno haki na uadilifu.—Linganisha Amosi 5:24.

Yehova Mungu ni Mwamuzi mkuu na Mfanya-Sheria (Isaya 33:22), naye “apenda uadilifu na haki.” (Zaburi 33:5, BHN) “Hatapuuza haki wala wingi wa uadilifu.” (Ayubu 37:23, NW) Jambo hilo linatuhakikishia kwamba yeye hataacha waaminifu-washikamanifu wake. (Zaburi 37:28) Yehova habagui anaposhughulika na viumbe wake, bali yeye huwakubali na kuwabariki wote wanaomwogopa na kutenda uadilifu. (Matendo 10:34, 35) Mtu mmoja-mmoja au mataifa huadhibiwa au kuthawabishwa kupatana na matendo yao. (Waroma 2:3-11; Waefeso 6:7-9; Wakolosai 3:22-4:1) Haki ya Yehova ina rehema pia, hivyo huwapa wanadamu na mataifa fursa ya kuacha mienendo yao mibaya na hivyo kuepuka hukumu kali.—Yeremia 18:7-10; Ezekieli 33:14-16.

Yehova ana hekima nyingi kuliko wanadamu wasio wakamilifu, hivyo wanadamu ndio wanaopaswa kujifunza njia za haki wala si Mungu. (Isaya 40:14, BHN) Hivyo, mwanadamu hawezi kuhukumu matendo ya Mungu kuwa ya haki au yasiyo haki, bali anapaswa kujifunza kupatanisha maoni yake na kiwango cha haki ambacho Yehova amefunua katika Neno lake. Mungu aliwaambia hivi Waisraeli: “Ee nyumba ya Israeli, je! njia zangu sizo zilizo sawa? njia zenu sizo zisizo sawa?” (Ezekieli 18:29) Pia, kwa kuwa Yehova ndiye Muumba hatuna sababu yoyote ya kutilia shaka uhalali wa matendo yake.—Waroma 9:20, 21; ona pia Ayubu 40:8-41:34.

Hivyo, kwa kufaa sikuzote Yehova ametaka wale wanaotamani kibali chake wajue kiwango chake cha haki na kukifuata. (Isaya 1:17, 18; 10:1, 2; Yeremia 7:5-7; 21:12; 22:3, 4; Ezekieli 45:9, 10; Amosi 5:15; Mika 3:9-12; 6:8; Zekaria 7:9-12) Kama Mungu, hawapaswi kuwa na ubaguzi, kwa kuwa sifa hiyo si ya haki na huvunja sheria ya upendo. (Yakobo 2:1-9) Hata hivyo, si vigumu kufuata haki kupatana na kiwango cha Mungu. Mwanadamu anakuwa mwenye furaha anapofanya hivyo. (Zaburi 106:3; linganisha Isaya 56:1, 2.) Blackstone, mwanasheria mashuhuri Mwingereza, alikiri jambo hilo kuwa kweli aliposema hivi: ‘[Mungu] amefanya isiwezekane kabisa kwa mtu yeyote kuwa na furaha isipokuwa afuate sheria zake za haki.’—Chadman’s Cyclopedia of Law, 1912, Buku la Kwanza, ukurasa wa 88.