Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mjifunze Kutoka Kwangu”

“Mjifunze Kutoka Kwangu”

“Mjifunze Kutoka Kwangu”

“Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—MATHAYO 11:29.

1. Kwa nini kujifunza kutoka kwa Yesu kunaweza kupendeza na kuthawabisha?

SIKUZOTE Yesu Kristo alifikiri, akafundisha, na kutenda inavyofaa. Hakuishi muda mrefu duniani, lakini alifurahia kazi yenye kuthawabisha na yenye kuridhisha, na aliendelea kuwa mwenye furaha. Aliwakusanya wanafunzi wake na kuwafundisha jinsi ya kumwabudu Mungu, kuwapenda wanadamu, na kuushinda ulimwengu. (Yohana 16:33) Alijaza mioyo yao tumaini na ‘kutoa nuru juu ya uhai na kutoharibika kupitia habari njema.’ (2 Timotheo 1:10) Iwapo wewe ni mmoja wa wanafunzi wake, unafikiri inamaanisha nini kuwa mwanafunzi? Kwa kuchunguza mambo ambayo Yesu anasema kuhusu wanafunzi, tunaweza kujua jinsi ya kuboresha maisha yetu. Hiyo inamaanisha kukubali maoni yake na kufuata kanuni fulani za msingi.— Mathayo 10:24, 25; Luka 14:26, 27; Yohana 8:31, 32; 13:35; 15:8.

2, 3. (a) Mwanafunzi wa Yesu ni nani? (b) Kwa nini ni muhimu kujiuliza, ‘Mimi nimekuwa mwanafunzi wa nani?’

2 Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno linalotafsiriwa “mwanafunzi” linamaanisha hasa mtu anayekazia akili jambo fulani, au mtu anayejifunza. Neno linalohusiana na hilo linapatikana kwenye andiko letu la msingi, Mathayo 11:29: “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Naam, mwanafunzi ni mtu anayejifunza. Kwa kawaida vitabu vya Injili hutumia neno “mwanafunzi” kurejezea wafuasi wa karibu wa Yesu, ambao walisafiri naye alipohubiri, na waliofundishwa naye. Huenda wengine walikubali tu mafundisho ya Yesu, wakifanya hivyo kisiri. (Luka 6:17; Yohana 19:38) Waandikaji wa vitabu vya Injili pia waliwataja “wanafunzi wa Yohana [Mbatizaji] na wanafunzi wa Mafarisayo.” (Marko 2:18) Kwa kuwa Yesu aliwaonya wafuasi wake ‘wajiangalie na fundisho la Mafarisayo,’ tunaweza kujiuliza, ‘Mimi nimekuwa mwanafunzi wa nani?’—Mathayo 16:12.

3 Ikiwa sisi ni wanafunzi wa Yesu na tumejifunza kutoka kwake, basi wengine wanapaswa kuhisi wameburudika kiroho wanapokuwa nasi. Wanapaswa kutambua kwamba tumekuwa wenye tabia-pole zaidi na wenye hali ya chini moyoni. Iwapo sisi ni wasimamizi kazini, au ni wazazi, au ni wachungaji katika kutaniko la Kikristo, je, wale walio chini ya uangalizi wetu wanahisi kwamba tunawatendea kama Yesu alivyowatendea wale waliokuwa chini ya uangalizi wake?

Jinsi Yesu Alivyowatendea Watu

4, 5. (a) Kwa nini si vigumu kujua jinsi Yesu alivyowatendea watu waliokuwa na matatizo? (b) Ni nini kilitukia kwa Yesu alipokuwa akila nyumbani mwa Farisayo mmoja?

4 Tunahitaji kujua jinsi Yesu alivyowatendea watu, hasa wale waliokuwa na matatizo makubwa. Si vigumu kujua jambo hilo kwa kuwa Biblia ina ripoti nyingi kuhusu jinsi Yesu alivyowatendea wengine, ambao baadhi yao walikuwa na matatizo. Na tuone pia jinsi viongozi wa kidini, hasa Mafarisayo walivyowatendea watu wenye matatizo. Ulinganisho huo utatufunza mambo fulani.

5 Katika mwaka wa 31 W.K., wakati Yesu alipokuwa katika safari ya kuhubiri huko Galilaya, “mtu mmoja wa Mafarisayo alifuliza kumwomba ili ale mlo-mkuu pamoja naye.” Yesu alikubali mwaliko huo. “Basi akaingia katika nyumba ya huyo Farisayo na kuegama kwenye meza. Na, tazama! mwanamke aliyejulikana katika jiji kuwa mtenda-dhambi akapata habari kwamba alikuwa akiegama kwenye mlo katika nyumba ya Farisayo, naye akaleta chupa ya alabasta iliyo na mafuta yenye marashi, na, akichukua kikao nyuma kwenye miguu yake, akatoa machozi na kuanza kulowesha miguu yake kwa machozi yake naye akawa akiyafuta kwa nywele za kichwa chake. Pia, alibusu miguu yake kwa wororo na kuipaka mafuta yenye marashi.”—Luka 7:36-38.

6. Huenda ni kwa nini mwanamke aliyekuwa “mtenda-dhambi” alikuwa nyumbani kwa Farisayo?

6 Hebu wazia jambo hilo. Kitabu kimoja cha marejezo chasema: “Mwanamke huyo (mstari wa 37) alitumia pindi hiyo ambayo kidesturi watu wenye uhitaji waliruhusiwa kuwepo kwenye karamu hizo ili kuchukua chakula kilichobaki.” Hilo linaonyesha jinsi ambavyo mtu angeweza kuingia kwenye karamu kama hiyo bila kualikwa. Huenda kulikuwa na wengine waliotazamia kuchukua mabaki baada ya mlo huo. Hata hivyo, tabia ya mwanamke huyo haikuwa ya kawaida. Yeye hakutazama mambo tu akiwa pembeni, akingojea wakati wa mlo uishe. Alikuwa “mtenda-dhambi” mwenye sifa mbaya, aliyejulikana sana, hivi kwamba Yesu alisema kuwa alizijua “dhambi zake, ingawa [zilikuwa] nyingi.”—Luka 7:47.

7, 8. (a) Tungetendaje kama tungekabili hali kama zile zilizoripotiwa katika Luka 7:36-38? (b) Simoni alitendaje?

7 Hebu wazia kwamba uliishi wakati huo na ulikabili hali kama hiyo aliyokabili Yesu. Ungetendaje? Je, ungekuwa na wasiwasi kukaribiwa na mwanamke huyo? Hali hiyo ingekuathiri namna gani? (Luka 7:45) Je, ungeudhika au kushtuka?

8 Kama ungekuwa mmoja wa wageni hao, je, ungekuwa na maoni kama ya Farisayo aliyeitwa Simoni? “Kwa kuona hayo yule Farisayo aliyemwalika [Yesu] akajisemea ndani yake mwenyewe: ‘Mtu huyu, kama angekuwa ni nabii, angejua ni nani na ni wa aina gani mwanamke anayemgusa, kwamba ni mtenda-dhambi.’” (Luka 7:39) Tofauti na Farisayo huyo, Yesu alikuwa mwenye huruma nyingi. Alielewa shida za mwanamke huyo na kufahamu jinsi alivyoteseka. Biblia haisemi jinsi alivyoanza maisha yake ya dhambi. Ikiwa kwa hakika yeye alikuwa kahaba, yaonekana watu wa mji huo, ambao walikuwa Wayahudi waliojitoa kwa Mungu, hawakumsaidia.

9. Yesu alitendaje, na yaelekea matokeo yalikuwa nini?

9 Lakini Yesu alitaka kumsaidia mwanamke huyo. Alimwambia: “Dhambi zako zimesamehewa.” Kisha akaongeza kusema: “Imani yako imekuokoa; shika njia yako uende kwa amani.” (Luka 7:48-50) Masimulizi hayo yanaishia hapo. Huenda mtu akabisha kwamba Yesu hakumsaidia sana mwanamke huyo. Alimbariki tu na kumwambia aende zake. Je, unafikiri aliendelea na maisha yake yenye kusikitisha? Ingawa hatuwezi kujua kwa hakika hali ilivyokuwa, ona maneno ya Luka yanayofuata. Alisema kwamba Yesu alisafiri “kutoka jiji hadi jiji na kutoka kijiji hadi kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme.” Luka pia aliripoti kwamba “wanawake fulani” walikuwa pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Wanawake hao ‘waliwahudumia kutokana na mali zao.’ Kuna uwezekano kwamba mwanamke huyu mwenye kutubu na mwenye uthamini alikuwa miongoni mwa wanawake hao, na aliishi maisha yanayompendeza Mungu akiwa na dhamiri safi, kusudi maishani, na upendo mwingi kwa Mungu.—Luka 8:1-3.

Tofauti Kati ya Yesu na Mafarisayo

10. Kwa nini inanufaisha kufikiria masimulizi juu ya Yesu na yule mwanamke kwenye nyumba ya Simoni?

10 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo yenye kuvutia? Yanachochea hisia zetu, sivyo? Hebu wazia ukiwa nyumbani kwa Simoni, ungehisije? Je, ungetenda kama Yesu, au ungehisi kidogo kama yule Farisayo aliyemkaribisha? Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, hivyo hatuwezi kuhisi na kutenda sawa kabisa na alivyotenda. Kwa upande mwingine, huenda hatungependa kuwa kama Simoni, aliyekuwa Farisayo. Ni watu wachache sana ambao wangejivunia kuwa Farisayo.

11. Kwa nini hatungetaka kufananishwa na Mafarisayo?

11 Kwa kuchunguza uthibitisho wa Kibiblia na wa kilimwengu, tunaweza kukata kauli kwamba Mafarisayo walijivuna kuwa waangalizi wa masilahi ya umma na ya taifa. Sheria ya Mungu ilikuwa wazi na yenye kueleweka kwa urahisi lakini hawakutosheka na jambo hilo. Walipoona kana kwamba Sheria haikueleza mambo fulani waziwazi, walijaribu kuongezea maelezo yao kuifanya iwe wazi zaidi ili kusiwe na uhitaji wa kutumia dhamiri. Viongozi hao wa kidini walijaribu kubuni sheria za kuongoza mwenendo wa watu katika kila jambo, hata mambo madogo-madogo. *

12. Mafarisayo walijionaje?

12 Mwanahistoria Myahudi Josephus wa karne ya kwanza anaonyesha wazi kwamba Mafarisayo walijiona kuwa watu wenye fadhili, wapole, wenye haki, na waliostahili kabisa kwa kazi yao. Hapana shaka kwamba baadhi yao walikuwa na sifa zinazokaribiana na hizo. Huenda ukamkumbuka Nikodemo. (Yohana 3:1, 2; 7:50, 51) Baada ya muda, baadhi yao waliukubali Ukristo. (Matendo 15:5) Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani, kama vile Mafarisayo: “Wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Hata hivyo, vitabu vya Injili vinaonyesha jinsi watu wa kawaida walivyowaona. Waliwaona kuwa watu wenye majivuno, wenye kiburi, wenye kujiona kuwa waadilifu, wenye kutafuta-tafuta makosa, wenye kushutumu, na kuwadharau wengine.

Maoni ya Yesu

13. Yesu alisema nini kuhusu Mafarisayo?

13 Yesu aliwakemea waandishi na Mafarisayo kuwa wanafiki. “Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka juu ya mabega ya watu, lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza kwa kidole chao.” Naam, mzigo ulikuwa mzito, nayo nira ambayo watu walibebeshwa haikuwa ya fadhili. Yesu aliwaita waandishi na Mafarisayo “wapumbavu.” Mtu mpumbavu husumbua jamii. Yesu pia aliwaita waandishi na Mafarisayo “viongozi vipofu” na kusisitiza kwamba ‘walipuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’ Hakuna mtu ambaye angetaka Yesu amlinganishe na Farisayo.—Mathayo 23:1-4, 16, 17, 23.

14, 15. (a) Yesu anafunua nini kuhusu Mafarisayo kupitia jinsi alivyomtendea Mathayo Lawi? (b) Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi haya?

14 Karibu wasomaji wote wa masimulizi ya vitabu vya Injili wanaweza kuona kwamba Mafarisayo walikuwa wachambuzi. Baada ya Yesu kumwalika Mathayo Lawi, aliyekuwa mkusanya-kodi, awe mwanafunzi wake, Lawi alimwandalia Yesu karamu kubwa. Masimulizi hayo yanasema: “Ndipo Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kunung’unikia wanafunzi wake, wakisema: ‘Ni kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya-kodi na watenda-dhambi?’ Yesu aliwajibu hivi: ‘. . . Nimekuja kuita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi waje kwenye toba.’”— Luka 5:27-32.

15 Lawi mwenyewe alielewa jambo jingine ambalo Yesu alisema wakati huo: “Nendeni, basi, na mjifunze kile ambacho hili lamaanisha, ‘Mimi nataka rehema, wala si dhabihu.’” (Mathayo 9:13) Ingawa Mafarisayo walidai kwamba waliamini maandishi ya manabii Waebrania, wao hawakukubali maneno hayo kutoka katika andiko la Hosea 6:6. Waliona ni afadhali washikilie mapokeo kuliko kuonyesha rehema. Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza, ‘Je, mimi nina sifa ya kusisitiza sheria fulani zifuatwe, kama zile zinazounga mkono maoni yangu binafsi au njia za kawaida za kushughulikia mambo? Au je, wengine wanaona kwamba mimi ni mwenye rehema na mwema?’

16. Mafarisayo walikuwa na mazoea gani na tunawezaje kuepuka kuwa kama wao?

16 Mafarisayo walikuwa na mazoea ya kuwachambua wengine. Walitafuta kila kasoro—iwe ya kweli au ya kuwaziwa tu. Walishutumu watu kila wakati na kuwakumbusha kasoro zao. Mafarisayo walijivuna kwa kutoa sehemu ya kumi ya mimea iliyo midogo zaidi kama vile mnanaa, dili, na jira. Kwa mavazi yao walijionyesha kuwa watu wenye kumcha Mungu na walijaribu kuliongoza taifa. Kwa kweli, ili matendo yetu yapatane na kielelezo cha Yesu, ni lazima tuepuke mwelekeo wa kutafuta na kutia chumvi kasoro za wengine.

Yesu Alishughulikaje na Matatizo

17-19. (a) Eleza jinsi Yesu alivyoshughulika na hali ambayo ingekuwa na matokeo mabaya sana. (b) Ni nini kilichofanya hali hiyo iwe yenye wasiwasi na isiyopendeza? (c) Kama ungekuwepo wakati mwanamke huyo alipomfikia Yesu, ungetendaje?

17 Yesu alishughulika na matatizo kwa njia tofauti kabisa na Mafarisayo. Fikiria jinsi Yesu alivyoshughulika na hali ambayo ingekuwa na matokeo mabaya sana. Ilihusu mwanamke mmoja aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka kumi na miwili. Unaweza kusoma masimulizi hayo katika andiko la Luka 8:42-48.

18 Masimulizi ya Marko yanasema kwamba mwanamke huyo ‘aliogopa na kutetemeka.’ (Marko 5:33) Kwa nini? Bila shaka ni kwa sababu alijua kwamba alikuwa amevunja Sheria ya Mungu. Kulingana na andiko la Mambo ya Walawi 15:25-28, mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu usio wa kawaida angeendelea kuwa asiye safi wakati wa mtiririko na hata juma moja baada ya mtiririko huo kuisha. Kila kitu alichogusa na kila mtu aliyemgusa angekuwa mchafu. Ili kumfikia Yesu, ingembidi mwanamke huyo ajikakamue kupita katikati ya umati. Tusomapo masimulizi hayo miaka 2,000 baadaye, tunamhurumia mwanamke huyo kwa tatizo lake.

19 Kama ungalikuwako siku hiyo, ungeonaje hali hiyo? Ungesema nini? Ona kwamba Yesu alimtendea mwanamke huyo kwa fadhili, upendo, na kwa kumjali, bila hata kutaja matatizo yoyote ambayo huenda alisababisha.—Marko 5:34.

20. Kama andiko la Mambo ya Walawi 15:25-28 lingekuwa takwa la Kikristo leo, ungekuwa na tatizo gani?

20 Je, tunaweza kujifunza jambo lolote kutokana na tukio hilo? Tuseme wewe ni mzee wa kutaniko la Kikristo leo. Isitoshe, tuseme andiko la Mambo ya Walawi 15:25-28 ni takwa la Kikristo leo na kwamba mwanamke Mkristo amelivunja takwa hilo kwa sababu ya kufadhaika na kutojua la kufanya. Ungetendaje? Je, ungemwaibisha mbele ya watu kwa kumshauri vikali? “Ah, mimi singeweza kamwe kufanya hivyo! Kwa kufuata kielelezo cha Yesu, ningejitahidi niwezavyo kuwa mwenye fadhili, upendo, ufikirio, na mwenye kujali.” Sawa! Lakini tatizo ni kuonyesha sifa hizo, kuiga kielelezo cha Yesu.

21. Yesu aliwafundisha watu nini kuhusu Sheria?

21 Kwa kawaida, watu walihisi wameburudishwa, wamechangamshwa, na kutiwa moyo na Yesu. Sheria ya Mungu ilipotaja mambo waziwazi, ilimaanisha tu kile ilichosema. Kama haikutaja mambo waziwazi, basi watu wangetumia dhamiri zao zaidi na wangeonyesha upendo wao kwa Mungu kupitia maamuzi yao. Sheria haikuwa na vizuizi vingi kupita kiasi. (Marko 2:27, 28) Mungu aliwapenda watu wake, akijishughulisha daima kwa manufaa yao, na alikuwa tayari kuwaonyesha rehema walipokosea. Yesu alikuwa hivyo pia.—Yohana 14:9.

Matokeo ya Mafundisho ya Yesu

22. Kujifunza kutoka kwa Yesu kuliwasaidia wanafunzi wake wawe na mtazamo gani?

22 Wale waliomsikiliza Yesu na kuwa wanafunzi wake walithamini sana ukweli wa maneno haya yake: “Nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:30) Hawakuhisi wamelemewa, wamenyanyaswa, au kukemewa naye. Walikuwa huru zaidi, wenye furaha zaidi na wenye uhakika zaidi kuhusu uhusiano wao na Mungu na miongoni mwao wenyewe. (Mathayo 7:1-5; Luka 9:49, 50) Walijifunza kutoka kwake kwamba kiongozi wa kiroho anahitaji kuwa mwenye kuburudisha kwa wengine na kuonyesha hali ya akili na ya moyo ya kujishusha chini.—1 Wakorintho 16:17, 18; Wafilipi 2:3.

23. Kuwa na Yesu kuliwafunza wanafunzi jambo gani muhimu na kuliwasaidia wafikie maamuzi gani?

23 Isitoshe, wengi waliona umuhimu wa kudumisha umoja pamoja na Kristo na kuiga mtazamo wake. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kama vile Baba amenipenda mimi nami nimewapenda nyinyi, kaeni katika upendo wangu. Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nimeshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” (Yohana 15:9, 10) Ili kufanikiwa wakiwa wahudumu na watumishi wa Mungu, wangepaswa kujitahidi sana kufuata mambo waliyofunzwa na Yesu kuhusu kuhubiri na kufundisha hadharani habari njema za Mungu, na kuhusu namna ya kuwatendea watu wa familia na rafiki. Makutaniko yalipoongezeka, mara kwa mara akina ndugu walihitaji kujikumbusha kwamba njia ya Yesu ya kufanya mambo ndiyo inayofaa. Alifundisha ile kweli, na kwa kweli wangehitaji kuazimia kuishi jinsi alivyoishi.—Yohana 14:6; Waefeso 4:20, 21.

24. Ni mambo gani ambayo tunapaswa kuweka moyoni kutokana na kielelezo cha Yesu?

24 Unapofikiria baadhi ya mambo ambayo tumezungumzia, je, unaona sehemu ambazo unaweza kufanyia maendeleo? Je, unakubali kwamba sikuzote Yesu alifikiri, kufundisha na kutenda inavyofaa? Basi, usife moyo. Yesu anatutia moyo kwa maneno haya: “Ikiwa mwajua mambo hayo, wenye furaha ni nyinyi ikiwa mwayafanya.”—Yohana 13:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 ‘Tofauti kuu kati ya Yesu na Mafarisayo inaonyeshwa waziwazi na maoni yao tofauti kuhusu Mungu. Kulingana na Mafarisayo, Mungu hasa ndiye mwenye kudai; kulingana na Yesu, Mungu ni mwenye neema na huruma. Bila shaka Mafarisayo wanakubali kwamba Mungu ni mwema na ni mwenye upendo, lakini kulingana nao, sifa hizo zinaonyeshwa katika zawadi ya Torati [Sheria] na katika uwezekano wa kutimiza matakwa ya Torati hiyo. Mafarisayo waliona kwamba Torati ingeweza kutimizwa kwa kufuata mapokeo ya mdomo, yaliyokuwa na kanuni zilizofafanua sheria. Yesu aliyakataa mapokeo ya mdomo na badala yake akaikweza sheria ya upendo kwa Mungu na jirani (Mathayo 22:34-40) kuwa msingi unaofaa wa kuifafanua Sheria. Ufafanuzi wake ulipingana na wa Mafarisayo.’—The New International Dictionary of New Testament Theology.

Unajibuje?

• Inamaanisha nini kwako kuwa mwanafunzi wa Yesu?

• Yesu alitendeaje watu?

• Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyofundisha?

• Kulikuwa na tofauti gani kati ya Mafarisayo na Yesu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mtazamo wa Yesu kuelekea watu ulikuwa tofauti kama nini na wa Mafarisayo!