Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuwa na Imani ya Kweli

Unaweza Kuwa na Imani ya Kweli

Unaweza Kuwa na Imani ya Kweli

Wakati Sarah Jayne alipokuwa na umri wa miaka 19, aligundua kwamba ana kansa ya ovari. Baada ya kufanyiwa upasuaji, alipata nafuu na akawa na matumaini mema ya wakati ujao. Alikuwa na matumaini mema sana hivi kwamba alipofika umri wa miaka 20, alichumbiwa na akaanza kufanya mipango ya arusi. Mwaka huohuo, alishikwa tena na kansa hiyo, na akagundua kwamba angekufa baada ya majuma machache tu. Sarah Jayne alikufa mnamo Juni 2000, kabla tu hajafikisha umri wa miaka 21.

WAGENI walioenda kumwona Sarah Jayne hospitalini walivutiwa sana na uhakika aliokuwa nao kuhusu wakati ujao, pamoja na imani yake thabiti katika Mungu na katika Neno lake, Biblia. Licha ya msiba aliokuwa akikabili, alikuwa na tumaini hakika la ufufuo—kwamba angewaona tena marafiki wake wote. (Yohana 5:28, 29) Alisema, “nitawaona nyinyi nyote katika ulimwengu mpya wa Mungu.”

Watu wengine huona imani hiyo kuwa ndoto tu. Ludovic Kennedy asema kwamba ‘watu wasio na uhakika huamini kwamba wakati wa maisha ya baada ya kifo kutakuwa na mlio wa mwisho wa tarumbeta, kutakuwa na maziwa na asali na kwamba mahali fulani huko Edeni watu watafurahia kuwa pamoja na wale waliokufa kabla yao na wengine ambao huenda wakafa baada yao.’ Kupatana na taarifa hiyo, lazima tuzushe swali la kuipinga, Ni jambo gani lililo la busara—kuamini kwamba “uzima ndio uu huu tu, kwa hiyo tuufurahie kadiri tuwezavyo,” kama adokezavyo Kennedy, au tuamini Mungu na ahadi yake ya ufufuo? Sarah Jayne aliamua kumwamini Mungu na ahadi yake ya ufufuo. Alisitawishaje imani hiyo?

‘Mtafute Mungu na kwa Kweli Umpate’

Ili umtumaini mtu fulani, unahitaji kumjua na kujifunza jinsi anavyofikiri na kutenda. Kufanya hivyo kwahusisha moyo na akili. Ni kweli kwamba unahitaji kufanya hivyo ili kusitawisha imani ya kweli katika Mungu. Unahitaji kumjua, kujifunza sifa zake na utu wake, kufahamu jinsi ambavyo amethibitika kuwa mwenye kutumainika na kutegemeka katika mambo yote ambayo amesema na kufanya.—Zaburi 9:10; 145:1-21.

Wengine wanahisi kwamba jambo hilo haliwezekani. Wanasema, iwapo kweli Mungu yuko, yeye yuko mbali sana, huwezi kumwelewa. “Ikiwa Mungu ni halisi kama anavyoonwa na Wakristo kama vile Sarah Jayne, kwa nini hajifunui kwetu?” auliza mtu fulani mwenye kutilia shaka. Lakini je, kweli Mungu yuko mbali sana na hatafutikani? Katika hotuba aliyowatolea wanafalsafa na wasomi huko Athene, mtume Paulo alisema kwamba “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyo katika huo” ameandaa pia kila kitu kinachohitajiwa ili ‘kumtafuta yeye . . . na kwa kweli kumpata.’ Kwa kweli, Paulo alisema: “Yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:24-27.

Basi, unawezaje ‘kumtafuta Mungu na kweli umpate’? Wengine wamefanya hivyo kwa kuchunguza tu ulimwengu unaowazunguka. Wengi wanaona kwamba ulimwengu pekee unatoa uthibitisho wa kutosha kuwasadikisha kwamba lazima kuwe na Muumba. * (Zaburi 19:1; Isaya 40:26; Matendo 14:16, 17) Wanahisi kama mtume Paulo kwamba “sifa [za Mungu] zisizoonekana zaonwa waziwazi tangu uumbaji wa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa, hata nguvu zake za milele na Uungu.”—Waroma 1:20; Zaburi 104:24.

Unahitaji Biblia

Hata hivyo, ili usitawishe imani thabiti katika Muumba, unahitaji kitu kingine ambacho ameandaa. Unahitaji nini? Biblia—Neno la Mungu lililopuliziwa, ambamo amefunua kusudi na mapenzi yake. (2 Timotheo 3:16, 17) Wengine watasema, “unawezaje kuamini yale Biblia isemayo unapoona mambo mabaya sana yanayofanywa na watu wanaodai kuifuata Biblia?” Ni kweli kwamba Jumuiya ya Wakristo ina sifa mbaya sana ya unafiki, ukatili, na ukosefu wa maadili. Lakini mtu yeyote mwenye busara anaweza kuona kwamba Jumuiya ya Wakristo hujifanya tu kwamba inatii kanuni za Biblia.—Mathayo 15:8.

Biblia yenyewe ilionya kwamba watu wengi wangedai kuwa wanamwabudu Mungu, hata hivyo, kwa kweli ‘wangekana hata mmiliki aliyewanunua.’ Mtume Petro alisema, “kwa sababu ya hao njia ya kweli itasemewa kwa maneno yenye kuudhi.” (2 Petro 2:1, 2) Yesu Kristo alisema kwamba watu hao ni “wafanyakazi wa uasi-sheria” ambao wangejulikana waziwazi kwa sababu ya matendo yao maovu. (Mathayo 7:15-23) Kukataa Neno la Mungu kwa sababu ya sifa mbaya ya Jumuiya ya Wakristo ni sawa na kutupa barua inayotoka kwa rafiki unayemtumaini eti kwa sababu tu imeletwa na mtu mwenye sifa mbaya.

Haiwezekani kusitawisha imani ya kweli bila Neno la Mungu. Yehova hutujulisha habari zake kupitia Biblia. Yeye hutoa majibu kwa maswali yanayoulizwa daima, kama vile kwa nini ameruhusu mateso na maumivu na atafanya nini kuhusu hali hizo. (Zaburi 119:105; Waroma 15:4) Sarah Jayne alipata kufahamu kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa. (1 Wathesalonike 2:13; 2 Petro 1:19-21) Jinsi gani? Si kwa sababu wazazi wake walimwambia tu aamini hivyo, bali kwa sababu alichunguza kwa unyofu uthibitisho wote unaoonyesha kwamba Biblia ni ufunuo wa kipekee kutoka kwa Mungu. (Waroma 12:2) Kwa mfano, aliona jinsi Biblia ilivyo na uvutano wenye nguvu katika maisha ya wale wanaotii kanuni zake. Pia kwa msaada wa vichapo kama vile Biblia—Neno la Mungu au la Mwanadamu?, * alichunguza kwa makini uthibitisho mwingi sana unaoonyesha kwamba Biblia imepuliziwa na Mungu.

Imani Hufuata Jambo Lisikiwalo”

Hata hivyo, haitoshi tu kuwa na Biblia au hata kuamini tu kwamba imepuliziwa. Mtume Paulo aandika kwamba “imani hufuata jambo lisikiwalo.” (Waroma 10:17) Imani hujengwa kwa kuisikia Biblia si kuwa na Biblia tu. “Unasikia” yale ambayo Mungu anataka kusema kwa kusoma na kujifunza Neno lake. Hata vijana wanaweza kufanya hivyo. Paulo asema kwamba “tangu utoto sana” Timotheo alifundishwa “maandishi matakatifu” na mama yake na nyanya yake. Je, hilo lamaanisha kwamba alipumbazwa kiakili kwa njia fulani? La! Timotheo hakuhadaiwa au kudanganywa kwa njia yoyote ile. Alikuwa ‘ameshawishwa kuamini’ mambo aliyosikia na kujifunza.—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.

Sarah Jayne alikuwa ameshawishiwa jinsi hiyo. Kama Waberoya wa karne ya kwanza, ‘alilipokea neno kutoka kwa wazazi wake kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana.’ Akiwa mtoto mdogo, bila shaka alitumaini mambo aliyoambiwa na wazazi wake. Baadaye, alipoendelea kukua, hakukubali tu kila jambo alilofundishwa. ‘Aliyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.’—Matendo 17:11.

Unaweza Kusitawisha Imani ya Kweli

Wewe pia unaweza kusitawisha imani ya kweli—imani iliyofafanuliwa na mtume Paulo katika barua yake kwa Wakristo Waebrania. Alisema imani hiyo ni “taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” (Waebrania 11:1) Ukiwa na imani kama hiyo, utakuwa na uhakika kabisa kwamba tumaini na mataraja yako yote, kutia ndani ahadi ya Mungu ya ufufuo itatimizwa. Utakuwa na hakika kwamba tumaini hilo linategemea mambo hakika, si mambo ya kuwaziwa tu. Utajua kwamba Yehova hajawahi kukosa kamwe kutimiza ahadi zake. (Yoshua 21:45; 23:14; Isaya 55:10, 11; Waebrania 6:18) Ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu utakuwa halisi kwako kana kwamba umetokea tayari. (2 Petro 3:13) Na utaona waziwazi kwa macho ya imani kwamba Yehova Mungu, Yesu Kristo, na Ufalme wa Mungu ni mambo halisi, si ndoto tu.

Hauko peke yako unapositawisha imani ya kweli. Mbali na kufanya Neno lake lipatikane kwa urahisi, Yehova pia ameandaa kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote ambalo limejitoa kusaidia watu wenye mioyo minyofu kusitawisha imani katika Mungu. (Yohana 17:20; Waroma 10:14, 15) Kubali msaada wote unaotolewa na Yehova kupitia tengenezo hilo. (Matendo 8:30, 31) Na kwa kuwa imani ni tunda la roho takatifu ya Mungu, sali daima upate roho hiyo ili ikusaidie kusitawisha imani ya kweli.—Wagalatia 5:22.

Usivunjwe moyo na watu wenye kutilia shaka ambao hudhihaki mtu yeyote anayeonyesha imani katika Mungu na katika Neno lake. (1 Wakorintho 1:18-21; 2 Petro 3:3, 4) Kwa hakika, imani ya kweli ni yenye thamani kubwa sana katika kuimarisha msimamo wako dhidi ya mashambulizi hayo. (Waefeso 6:16) Sarah Jayne aliona ukweli wa jambo hilo, na sikuzote aliwatia moyo wale waliomtembelea hospitalini wasitawishe imani yao. Alikuwa akisema, “Fanya ukweli uwe njia yako ya maisha. Jifunze Neno la Mungu. Kaa karibu na tengenezo la Mungu. Sali daima. Uwe mwenye bidii katika utumishi wa Yehova.”—Yakobo 2:17, 26.

Alipoona imani ya Sarah Jayne katika Mungu na katika ufufuo, muuguzi mmoja alisema hivi: “Ni kweli kwamba unaamini mambo hayo.” Alipoulizwa ni nini kilichomsaidia kuwa na mtazamo mzuri namna hiyo licha ya majaribu yaliyompata, alijibu: “Ni kuwa na imani katika Yehova. Yeye ni rafiki yangu wa kweli, nami nampenda sana.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 12 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Kutoka utoto sana” Timotheo alifundishwa “maandishi matakatifu” na mama yake na nyanya yake

[Picha katika ukurasa wa 6]

Waberoya walisifiwa kwa kuyachunguza Maandiko kila siku

[Hisani]

From “Photo-Drama of Creation,” 1914

[Picha katika ukurasa wa 7]

Imani husitawishwa kwa kuisikia na kuifuata Biblia, si kuwa nayo tu

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Nitawaona nyinyi nyote katika ulimwengu mpya wa Mungu”