Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza “Kutofautisha Lililo Sahihi na Lililo Kosa Pia”?

Je, Unaweza “Kutofautisha Lililo Sahihi na Lililo Kosa Pia”?

Je, Unaweza “Kutofautisha Lililo Sahihi na Lililo Kosa Pia”?

Fulizeni kuhakikisha ni nini lililo lenye kukubalika kwa Bwana.”—WAEFESO 5:10.

1. Maisha yanawezaje kuwa yenye kutatanisha leo, na kwa nini?

“EE, BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Jambo hili alilotambua Yeremia, lina maana kubwa zaidi kwetu leo. Kwa nini? Kwa sababu tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” kama ilivyotabiri Biblia. (2 Timotheo 3:1) Kila siku tunakabili hali zenye kutatanisha ambazo hutaka tufanye maamuzi fulani. Maamuzi hayo, yawe makubwa au madogo, yanaweza kuathiri sana hali yetu—ya kimwili, ya kihisia-moyo, na ya kiroho.

2. Ni uchaguzi gani mbalimbali unaoweza kuonwa kuwa usio wa maana, hata hivyo Wakristo waliojiweka wakfu huuonaje?

2 Uamuzi mwingi tunaofanya kila siku katika maisha yetu unaweza kuonwa kuwa wa kawaida au usio wa maana. Kwa mfano, kila siku ni lazima tuchague ni mavazi gani tutakayovaa, chakula tutakachokula, watu tutakaowatembelea, na kadhalika. Tunafanya mambo hayo pasipo kuyafikiria sana. Lakini je, kwa kweli mambo hayo hayana maana yoyote? Sisi Wakristo tuliojiweka wakfu, tunajali sana uchaguzi tunaofanya kuhusiana na mavazi na sura zetu, kula na kunywa, usemi na mwenendo wetu. Sikuzote mambo hayo yapasa kuonyesha kwamba sisi ni watumishi wa Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi Sana. Tunakumbushwa maneno ya mtume Paulo: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo jingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31; Wakolosai 4:6; 1 Timotheo 2:9, 10.

3. Ni uamuzi gani mbalimbali ambao ni mzito hata zaidi?

3 Kisha kuna uamuzi mbalimbali ambao ni mzito hata zaidi. Kwa mfano, uamuzi wa kufunga ndoa au kubaki mseja kwa kweli ni mzito na unaweza kuathiri sana maisha ya mtu kwa muda mrefu. Kwa hakika si jambo dogo wala rahisi kuchagua mtu anayefaa kufunga ndoa naye, yaani mwenzi wa maisha. * (Mithali 18:22) Kwa kuongezea, marafiki na watu tunaochagua kushirikiana nao shuleni, kazini, kwenye vitumbuizo na tafrija wanaweza kuathiri sana hali yetu ya kiroho na hivyo kuathiri hali yetu njema ya milele.—Waroma 13:13, 14; Waefeso 5:3, 4.

4. (a) Ni uwezo gani unaotamanika sana? (b) Twapaswa kuchunguza maswali gani?

4 Kwa kuwa tunakabili uamuzi huo mbalimbali, bila shaka tutanufaika tukiwa na uwezo wa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa au kati ya jambo linaloonekana kuwa sahihi na lile ambalo kwa kweli ni sahihi. Biblia huonya kwamba “iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwisho wake ni njia za mauti.” (Mithali 14:12) Kwa hiyo, huenda tukauliza: ‘Tunaweza kusitawishaje uwezo wa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa? Tunaweza kupata wapi mwongozo tunaohitaji ili kufanya maamuzi? Watu wamefanyaje kuhusiana na jambo hilo sasa na wakati uliopita, na matokeo yamekuwaje?’

“Falsafa na Udanganyo Mtupu” wa Ulimwengu

5. Wakristo wa mapema waliishi katika ulimwengu wa aina gani?

5 Wakristo wa karne ya kwanza waliishi katika ulimwengu uliodhibitiwa na kanuni na maadili ya Wagiriki na Waroma. Kwa upande mmoja, maisha ya Waroma yalikuwa yenye anasa na starehe, mambo yaliyoonekana na wengi kuwa yenye kutamanika sana. Kwa upande mwingine, wasomi wa siku hizo walichochewa na mawazo mengi ya kifalsafa ya Plato na Aristotle na pia falsafa za wanafunzi wapya, kama vile Waepikurea na Wastoa. Mtume Paulo alipofika Athene katika safari yake ya pili ya mishonari, alikutana na wanafalsafa Waepikurea na Wastoa waliohisi kwamba walikuwa bora kuliko “mpiga-domo huyu,” Paulo.—Matendo 17:18.

6. (a) Wakristo fulani wa mapema walishawishiwa kufanya nini? (b) Paulo alitoa onyo gani?

6 Kwa hiyo si vigumu kuelewa sababu iliyofanya Wakristo fulani wa mapema wavutiwe na njia na mitindo ya maisha ya kujionyesha ya watu waliowazunguka. (2 Timotheo 4:10) Wale waliokuwa sehemu ya mfumo huo walionekana walifurahia manufaa nyingi, na uamuzi waliofanya ulionekana kuwa mzuri. Ulimwengu ulionekana kuwa na kitu fulani chenye thamani kisichopatikana katika maisha ya Kikristo. Hata hivyo, mtume Paulo alionya: “Jihadharini: labda huenda kukawa na mtu fulani ambaye atawachukua nyinyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyo mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” (Wakolosai 2:8) Kwa nini Paulo alisema hivyo?

7. Kwa kweli hekima ya ulimwengu ina thamani gani?

7 Paulo alitoa onyo hilo kwa sababu aliona hatari ambayo ingekabili kufikiri kwa wale waliovutiwa na ulimwengu. Matumizi yake ya maneno “falsafa na udanganyo mtupu” yanafaa sana. Neno “falsafa” kihalisi lamaanisha “kupenda na kufuatia hekima.” Kufanya hivyo kwaweza kunufaisha. Kwa kweli, Biblia, hasa katika kitabu cha Mithali, hututia moyo tutafute sana ujuzi na hekima inayofaa. (Mithali 1:1-7; 3:13-18) Hata hivyo, Paulo alijumlisha “falsafa” na “udanganyo mtupu.” Yaani, Paulo aliona hekima ya ulimwengu kuwa tupu na yenye udanganyifu. Kama vile kibofu ambacho kimejazwa hewa, hekima hiyo ilionekana kuwa thabiti, lakini ilikuwa bure. Bila shaka, lingekuwa jambo la ubatili na hata lenye kuleta msiba, kuamua lililo sahihi na lililo kosa kwa kutegemea kitu bure kama vile “falsafa na udanganyo mtupu” wa ulimwengu.

Wale Wasemao Kwamba “Uovu Ni Wema na Wema Ni Uovu”

8. (a) Watu hutafuta mashauri wapi? (b) Ni mashauri ya aina gani yanayotolewa?

8 Mambo si tofauti sana leo. Karibu katika nyanja zote ambazo wanadamu wanajitahidi kutimiza mambo fulani, kuna wataalamu wengi. Washauri wa masuala ya ndoa na familia, waandishi wa habari, watu wanaojiita wanatiba, wanajimu, watu wanaowasiliana na roho, na wengineo wako tayari kutoa mashauri kwa kulipwa. Lakini wao hutoa mashauri ya aina gani? Mara nyingi, viwango vya Biblia vya maadili hupuuzwa, na badala yake maadili mapya kukaziwa zaidi. Kwa mfano, ikizungumzia jinsi serikali ilivyokataa kusajili “ndoa za watu wa jinsia moja,” tahariri ya gazeti moja linalozungumzia mambo kwa ujumla nchini Kanada, The Globe and Mail lasema: ‘Katika mwaka wa 2000, ni jambo la upumbavu kukataza wenzi wanaopendana na wanaowajibika kwa mmoja na mwenzake kufunga ndoa kwa sababu tu ni wa jinsia moja.’ Watu wana mwelekeo wa kuvumilia mambo, si kuyachambua. Hakuna sheria dhahiri kuhusu lililo sahihi na lililo kosa; kila jambo linaamuliwa kwa kutegemea matokeo yake.—Zaburi 10:3, 4.

9. Mara nyingi watu wanaoonekana kuwa wenye kuheshimika katika jamii hufanya nini?

9 Wengine huwaona watu ambao wamefanikiwa kijamii na kiuchumi—matajiri na watu mashuhuri—kuwa mifano ya kuigwa wanapofanya maamuzi yao. Ijapokuwa matajiri na watu mashuhuri huonwa kuwa watu wenye kuheshimika katika jamii ya leo, mara nyingi wao hutaja tu unyofu na kutumainika lakini hawadhihirishi sifa hizo. Wengi huvunja au kukwepa kanuni za maadili bila kujali, kusudi wapate mamlaka na faida za kifedha. Ili wapate sifa na wawe mashuhuri, watu fulani hupuuza kanuni na viwango vinavyokubaliwa na hupendelea tabia isiyo ya kawaida na yenye kutisha. Kwa sababu hiyo, kumekuwa na jamii ambayo hutaka kujifaidi na yenye uendekevu, ambayo wito wake ni, “Jambo lolote linaruhusiwa.” Je, inashangaza kwamba watu wametatanika na hawana uhakika kuhusu lililo sahihi na lililo kosa?—Luka 6:39.

10. Maneno ya Isaya kuhusu uovu na wema yamethibitikaje kuwa ya kweli?

10 Tunaona matokeo yenye kuhuzunisha ya maamuzi mabaya yanayofanywa kwa kutegemea mwongozo wenye makosa—ndoa na familia zilizovunjika, matumizi mabaya ya vileo na dawa za kulevya, vikundi vya vijana wenye jeuri, ngono za ovyoovyo, maradhi yanayoambukizwa kingono, kwa kutoa mifano michache tu. Kwa kweli, tunawezaje kutarajia matokeo tofauti na hayo iwapo watu wanapuuza mambo ya msingi yanayokubaliwa kuhusu lililo sahihi na lililo kosa? (Waroma 1:28-32) Ni kama alivyosema nabii Isaya: “Ole wao wasemao kwamba uovu ni wema, na kwamba wema ni uovu; watiao giza badala ya nuru, na nuru badala ya giza; watiao uchungu badala ya utamu, na utamu badala ya uchungu! Ole wao walio wenye hekima katika macho yao wenyewe, na wenye busara katika fikira zao wenyewe!”—Isaya 5:20, 21.

11. Kwa nini si jambo la hekima kujitegemea mwenyewe unapoamua lililo sahihi na lililo kosa?

11 Uhakika wa kwamba Mungu aliwatoza hesabu Wayahudi wa kale ambao walikuwa “wenye hekima katika macho yao wenyewe” hufanya liwe jambo muhimu sana kwetu kuepuka kujitegemea tunapoamua lililo sahihi na lililo kosa. Watu wengi leo hukubali maoni ya kwamba “fanya yale moyo wako unataka,” au “fanya lile unaloona kuwa sahihi.” Je, huo ni mtazamo wa hekima? Unapingana na Biblia, ambayo husema hivi waziwazi: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha [“na umekata tamaa,” NW]; nani awezaye kuujua?” (Yeremia 17:9) Je, unaweza kumtegemea mtu mdanganyifu na aliyekata tamaa akuongoze kufanya maamuzi? Sivyo. Kwa hakika, labda ungefanya kinyume cha vile mtu huyo angekuambia. Ndiyo sababu Biblia hutukumbusha: “Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga; bali yeye aendaye kwa busara ataokolewa.”—Mithali 3:5-7; 28:26.

Acheni Tujifunze Mambo Yenye Kukubalika kwa Mungu

12. Kwa nini tunahitaji kujithibitishia wenyewe “mapenzi ya Mungu”?

12 Kwa kuwa hatupaswi kutegemea hekima ya ulimwengu au kujitegemea wenyewe kuamua lililo sahihi na lililo kosa, twapaswa kufanya nini? Ona shauri hili lililo wazi la mtume Paulo: “Komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Kwa nini tunahitaji kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu? Katika Biblia, Yehova hutoa sababu iliyo wazi na thabiti, asemapo: “Kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” (Isaya 55:9) Hivyo, badala ya kutegemea akili zetu au jinsi tunavyohisi, tunashauriwa hivi: “Fulizeni kuhakikisha ni nini lililo lenye kukubalika kwa Bwana.”—Waefeso 5:10.

13. Maneno ya Yesu katika Yohana 17:3 yanakaziaje uhitaji wa kujua mambo yenye kukubalika kwa Mungu?

13 Yesu Kristo alikazia uhitaji huo aliposema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Usemi “kutwaa ujuzi” unamaanisha mengi zaidi ya “kujua” tu. Kulingana na Vine’s Expository Dictionary, ‘usemi huo unaonyesha uhusiano uliopo kati ya mtu na kitu anachojua; na kwa habari hii, kitu kinachojulikana ni chenye thamani au ni muhimu kwa mtu huyo, na hivyo kunakuwa na uhusiano huo wenye thamani.’ Kuwa na uhusiano na mtu fulani kunamaanisha si kujua jina lake tu, bali kujua mengi zaidi kumhusu. Pia kunatia ndani kujua mambo anayopenda na asiyopenda, kujua maadili na viwango vyake na kuviheshimu.—1 Yohana 2:3; 4:8.

Kuzoeza Nguvu Zetu za Ufahamu

14. Paulo alisema ni nini hasa kinachoweza kutofautisha watoto wa kiroho na watu wakomavu?

14 Hivyo, basi, tunawezaje kujipatia uwezo wa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa? Twapata jibu kutokana na maneno ya Paulo aliyowaandikia Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza. Aliandika: “Kila mtu ashirikiye maziwa halijui sana neno la uadilifu, kwa maana yeye ni kitoto. Lakini chakula kigumu ni cha watu wakomavu, cha wale ambao kupitia utumizi, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.” Hapa Paulo atofautisha “maziwa,” ambayo aliyataja katika mstari uliotangulia kuwa “mambo ya msingi ya matamko matakatifu ya Mungu,” na “chakula kigumu,” ambacho ni cha “watu wakomavu,” ambao “nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.”—Waebrania 5:12-14.

15. Kwa nini tunahitaji kujitahidi sana kupata ujuzi sahihi juu ya Mungu?

15 Hii yamaanisha kwamba, kwanza kabisa, lazima tujitahidi kutwaa uelewevu sahihi kuhusu viwango vya Mungu vilivyo katika Neno lake, Biblia. Hatutafuti orodha yenye sheria zinazotuonyesha mambo tunayoweza kufanya na mambo tusiyoweza kufanya. Biblia si kitabu cha namna hiyo. Badala yake, Paulo alieleza hivi: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Ili kunufaika na fundisho, karipio, na nidhamu hiyo, lazima tuanze kutumia akili zetu na nguvu zetu za kufikiri. Jambo hilo lahitaji jitihada, lakini jitihada hiyo inafaa ili tuwe ‘walioandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—Mithali 2:3-6.

16. Inamaanisha nini kuzoeza nguvu zako za ufahamu?

16 Kisha, kama Paulo alivyoonyesha, ‘nguvu za ufahamu za watu wakomavu zimezoezwa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.’ Hapa twafikia sehemu muhimu ya habari hiyo. Usemi “nguvu zao za ufahamu zimezoezwa” kihalisi wamaanisha “kuzoeza hisi za mwili (kama vile mwanasarakasi).” (Kingdom Interlinear Translation) Mwanasarakasi mwenye uzoefu anaweza kufanya sarakasi zake kwa sekunde chache sana na kuonekana kana kwamba anatenda kinyume cha nguvu za uvutano au sheria nyingine za asili. Anadhibiti kabisa viungo vya mwili wake nyakati zote, na anaweza kujua mara moja hatua anayopaswa kuchukua ili kukamilisha jambo analofanya kwa mafanikio. Anafaulu kufanya mambo hayo yote kwa sababu ya kujizoeza kwa bidii bila kuacha.

17. Tunapaswa kuwa wanasarakasi katika maana gani?

17 Lazima sisi pia tuzoezwe kama mwanasarakasi katika maana ya kiroho ikiwa twataka kuwa na uhakika kwamba sikuzote tutafanya maamuzi na uchaguzi mzuri. Ni lazima nyakati zote tudhibiti kikamili hisi zetu na viungo vya mwili wetu. (Mathayo 5:29, 30; Wakolosai 3:5-10) Kwa mfano, je, unadhibiti macho yako yasitazame mambo machafu au masikio yako yasisikie muziki au usemi wenye kushusha heshima? Ni kweli kwamba tunazungukwa na mambo hayo yasiyofaa. Hata hivyo, sisi ndio tutakaoamua kama tutaruhusu mambo hayo yasitawi mioyoni na akilini mwetu. Tunaweza kumwiga mtunga-zaburi aliyesema: “Sitaweka mbele ya macho yangu neno la uovu. Kazi yao waliopotoka naichukia, haitaambatana nami. . . . Asemaye uongo hatathibitika mbele ya macho yangu.”—Zaburi 101:3, 7.

Zoeza Nguvu Zako za Ufahamu kwa Kuzitumia

18. Ni nini kinachodokezwa na usemi “kupitia utumizi” katika maelezo ya Paulo kuhusu kuzoeza nguvu za ufahamu?

18 Kumbuka kwamba “kupitia utumizi” tunaweza kuzoeza nguvu zetu za ufahamu kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia. Yaani, kila mara tunapokabili uamuzi fulani, twapaswa kujifunza kutumia uwezo wetu wa akili ili kufahamu kanuni za Biblia zinazohusika na jinsi zinavyoweza kutumiwa. Uwe na zoea la kufanya utafiti katika vichapo vinavyotegemea Biblia ambavyo huandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Bila shaka, tunaweza kutafuta msaada kutoka kwa Wakristo wakomavu. Hata hivyo, hatimaye tutapata manufaa nyingi kutokana na jitihada ya kibinafsi tunayofanya kujifunza Neno la Mungu, pamoja na kusali kwa Yehova ili kupata mwongozo na roho yake.—Waefeso 3:14-19.

19. Tunaweza kupata baraka gani kwa kuzoeza nguvu zetu za ufahamu hatua kwa hatua?

19 Tunapozoeza nguvu zetu za ufahamu hatua kwa hatua, lengo ni “tusiwe tena vitoto, tukirushwa huku na huku kama vile na mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kwa njia ya mbinu ya hadaa ya watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Waefeso 4:14) Badala yake, kwa kutegemea ujuzi na uelewevu wa yale yanayokubalika kwa Mungu, tunaweza kufanya maamuzi ya hekima, yawe makubwa au madogo, ambayo yatatunufaisha, yatawajenga waabudu wenzetu, na zaidi ya yote yatampendeza Baba yetu wa kimbingu. (Mithali 27:11) Ni baraka na ulinzi ulioje katika nyakati hizi zenye hatari!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Katika orodha iliyotayarishwa na Dakt. Thomas Holmes na Dakt. Richard Rahe, kifo cha mwenzi wa ndoa, talaka, na kutengana ni mambo yanayochukua nafasi za kwanza 3 kati ya mambo zaidi ya 40 yanayosababisha mkazo mwingi zaidi katika maisha ya watu. Kufunga ndoa kunachukua nafasi ya saba kwenye orodha hiyo.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni uwezo gani unaohitajiwa ili kufanya maamuzi mazuri?

• Kwa nini si jambo la hekima kutegemea watu mashuhuri au kutegemea hisi zetu tunapoamua lililo sahihi na lililo kosa?

• Kwa nini twapaswa kuwa na hakika juu ya mambo yenye kukubalika kwa Mungu tunapofanya maamuzi, na tunawezaje kufanya hivyo?

• Inamaanisha nini ‘kuzoeza nguvu zetu za ufahamu’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ni jambo la ubatili kutafuta mwongozo kutoka kwa matajiri na watu mashuhuri

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kama vile mwanasarakasi, twapaswa kudhibiti kikamili hisi zetu zote na viungo vya mwili wetu