Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufufuo wa Yesu Wachunguzwa

Ufufuo wa Yesu Wachunguzwa

Ufufuo wa Yesu Wachunguzwa

“Naweza kuwaambia waziwazi kwamba ingawa tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yesu aliishi . . . , hatuwezi kusema kwa uhakika huohuo kwamba twajua Yeye alifufuliwa na Mungu kutoka kwa wafu.” Ndivyo alivyosema Askofu Mkuu wa Canterbury wa Kanisa la Anglikana.

MTUME Mkristo Paulo hakuwa na shaka lolote kuhusu ufufuo huo. Katika sura ya 15 ya barua yake ya kwanza iliyopuliziwa ambayo aliandikia Wakristo wenzake katika Korintho la kale, Paulo aliandika hivi: “Niliwapa nyinyi, miongoni mwa mambo ya kwanza, lile nililolipokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba amefufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.”—1 Wakorintho 15:3, 4.

Imani katika ufufuo wa Yesu Kristo iliwachochea wanafunzi wahubiri gospeli katika maeneo yote yaliyokaliwa na Wagiriki na Waroma—“katika viumbe vyote chini ya mbingu.” (Wakolosai 1:23) Kwa hakika, ufufuo wa Yesu ndio msingi hasa wa imani ya Kikristo.

Hata hivyo, tangu mwanzo kabisa, wengi walitilia shaka na kutoamini ufufuo wa Yesu. Kwa ujumla, Wayahudi waliona kuwa wafuasi wa Yesu walikufuru kwa kudai kwamba yule mtu aliyetundikwa alikuwa Mesiya. Nao Wagiriki wengi walioelimika ambao waliamini katika nafsi isiyoweza kufa, walichukizwa na wazo hilo la ufufuo.—Matendo 17:32-34.

Watu Wenye Shaka Leo

Katika miaka ya majuzi, wasomi fulani wanaodai kuwa Wakristo, wamechapisha vitabu na makala zinazotilia shaka ufufuo wa Yesu kuwa uvumi tu na kuanzisha mijadala mikali kuhusu habari hiyo. Katika jitihada zao za kutafuta ‘Yesu anayesimuliwa katika historia,’ wasomi kadhaa hudai kwamba masimulizi ya Gospeli kuhusu kaburi tupu na kutokea kwa Yesu mara kadhaa baada ya kufufuliwa ni uzushi mtupu ulioanzishwa muda mrefu baada ya kifo chake ili kuunga mkono madai ya mamlaka aliyo nayo mbinguni.

Kwa mfano, fikiria maoni ya msomi Mjerumani Gerd Lüdemann, ambaye ni profesa wa Agano Jipya na mwandishi wa kitabu What Really Happened to Jesus—A Historical Approach to the Resurrection. Anadai kwamba ufufuo wa Yesu ni “jambo lisilo na msingi” linalopasa kukataliwa na mtu yeyote mwenye “maoni ya kisayansi kuhusu ulimwengu.”

Profesa Lüdemann asisitiza kwamba Petro aliona ono tu lililosababishwa na huzuni na hatia kubwa sana ya kumkana Yesu kisha akafikiri Kristo aliyefufuliwa ndiye aliyemtokea. Na kulingana na Lüdemann, pindi ambapo Yesu aliwatokea waumini zaidi ya 500 ilikuwa tu “upeo wa shangwe wa umati.” (1 Wakorintho 15:5, 6) Kwa ufupi, wasomi wengi huunganisha masimulizi ya Biblia kuhusu ufufuo wa Yesu na mfululizo tu wa mambo ya kuwazia ambayo yaliwapa wanafunzi uhakika wa kiroho na kuwafanya wawe na bidii katika kazi ya mishonari.

Bila shaka, wengi hawapendezwi na mabishano ya kitaaluma. Hata hivyo, sote twapaswa kupendezwa na mazungumzo yanayohusu ufufuo wa Yesu. Kwa nini? Kwa sababu, ikiwa kwa upande mmoja Yesu hakufufuliwa, Ukristo hauna msingi wa kweli. Kwa upande mwingine, ikiwa ufufuo wa Yesu kwa kweli ni jambo hakika la kihistoria, Ukristo unategemea msingi kweli. Chini ya hali hizo, madai ya Kristo yalitetewa na ahadi zake zikathibitishwa kuwa sahihi. Isitoshe, ikiwa kuna ufufuo, kifo si mshindi mkuu bali ni adui anayeweza kushindwa.—1 Wakorintho 15:55.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

From the Self-Pronouncing Edition of the Holy Bible, containing the King James and the Revised versions