Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kwa Kweli Bwana Alifufuliwa!”

“Kwa Kweli Bwana Alifufuliwa!”

“Kwa Kweli Bwana Alifufuliwa!”

Hebu wazia jinsi wanafunzi wa Yesu walivyosononeka Bwana wao alipouawa. Tumaini lao halikuwa hai, lilikuwa kama mwili ambao Yosefu wa Arimathea aliuweka kaburini. Mataraja yao pia kwamba Yesu angewakomboa Wayahudi kutoka katika utumwa wa Waroma yalikoma.

IKIWA mambo yangeishia hapo, labda wanafunzi wa Yesu wangetoweka kama wafuasi wa watu wengi wanaodai kuwa Mesiya. Lakini Yesu alikuwa hai! Kulingana na Maandiko, aliwatokea wafuasi wake pindi kadhaa muda mfupi baada ya kufa. Kwa hiyo, baadhi yao walichochewa kutangaza hivi: “Kwa kweli Bwana alifufuliwa!”—Luka 24:34.

Wanafunzi walilazimika kutetea imani yao kwamba Yesu ndiye Mesiya. Kwa kufanya hivyo, walikazia hasa ufufuo wake kutoka kwa wafu kuwa uthibitisho usioweza kutiliwa shaka kwamba alikuwa Mesiya. Kwa kweli, ‘wakiwa na nguvu kubwa mitume waliendelea kutoa ushahidi kuhusu ufufuo wa Bwana Yesu.’—Matendo 4:33.

Ikiwa mtu yeyote angethibitisha kwamba ufufuo huo haukutokea—labda kwa kufanya mwanafunzi mmoja akiri kwamba haukutokea, au kwa kuonyesha kwamba mwili wa Yesu ulibaki kaburini—Ukristo ungekuwa umeambulia patupu tokea mwanzo. Lakini haukuambulia patupu. Wakijua kwamba Kristo alikuwa hai, wafuasi wa Yesu walienda kila mahali wakitangaza ufufuo wake, na watu wengi wakamwamini Kristo aliyefufuliwa.

Kwa nini wewe pia unaweza kuamini ufufuo wa Yesu? Kuna uthibitisho gani kwamba ufufuo huo ulikuwa halisi?

Kwa Nini Tuchunguze Uthibitisho Huo?

Masimulizi yote manne ya Gospeli huripoti ufufuo wa Yesu. (Mathayo 28:1-10; Marko 16:1-8; Luka 24:1-12; Yohana 20:1-29) * Sehemu nyingine za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo husema kwa uhakika kuhusu kufufuliwa kwa Kristo.

Basi haishangazi kwamba wafuasi wa Yesu wamekuwa wakiutangaza ufufuo wake! Ikiwa kwa kweli alifufuliwa na Mungu, basi hizo ni habari zenye kushangaza zaidi ambazo ulimwengu umepata kusikia. Inamaanisha kwamba Mungu yuko. Isitoshe, inamaanisha kwamba Yesu yu hai hata sasa.

Hilo latuathirije? Yesu alisali hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Naam, tunaweza kupata ujuzi unaotoa uhai kuhusu Yesu na Baba yake. Kwa kutumia ujuzi huo, hata tukifa, twaweza kufufuliwa, kwa kuwa Yesu alifufuliwa. (Yohana 5:28, 29) Tunaweza kuwa na tumaini la uhai udumuo milele katika paradiso duniani chini ya Ufalme wa kimbingu wa Mungu unaoongozwa na Mwana wake aliyetukuzwa, Yesu Kristo, Mfalme wa wafalme.—Isaya 9:6, 7; Luka 23:43; Ufunuo 17:14.

Kwa hiyo, basi, suala la kama kwa kweli Yesu alifufuka kutoka kwa wafu ni muhimu. Linaathiri maisha yetu sasa na mataraja yetu ya wakati ujao. Ndiyo sababu twakualika uchunguze sababu nne za uthibitisho wenye kusadikisha kwamba Yesu alikufa na kufufuliwa.

Kwa Kweli Yesu Alikufa Kwenye Mti

Watu fulani wenye shaka hudai kwamba, ijapokuwa Yesu alitundikwa mtini kwa kweli yeye hakufa kwenye mti. Wanasema kwamba alikuwa amekaribia kufa na kwamba alihuishwa na baridi iliyokuwa ndani ya kaburi. Hata hivyo, uthibitisho uliopo waonyesha kwamba mwili wa Yesu uliokufa ndio uliowekwa kaburini.

Kwa kuwa Yesu aliuawa hadharani, kulikuwa na mashahidi walioshuhudia kwamba kwa kweli alikufa kwenye mti. Kifo chake kilithibitishwa na ofisa wa jeshi la Roma aliyekuwa akisimamia mauaji hayo. Ofisa huyo wa kijeshi alikuwa mtaalamu ambaye kazi yake ilitia ndani kuhakikisha kwamba kwa kweli Yesu alikuwa amekufa. Isitoshe, ni baada tu ya kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa amekufa ndipo Gavana Mroma Pontio Pilato alipotoa mwili wa Yesu kwa Yosefu wa Arimathea ili auzike.—Marko 15:39-46.

Kaburi Lilipatikana Likiwa Tupu

Kaburi lililokuwa tupu liliwapa wanafunzi wa Yesu uthibitisho wa kwanza kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa, na uthibitisho huo haujawahi kutiliwa shaka. Yesu alizikwa katika kaburi jipya, ambalo halikuwa limepata kutumiwa. Lilikuwa karibu na mahali alipotundikwa na wakati huo lingeweza kutambuliwa kwa usahihi na kwa urahisi sana. (Yohana 19:41, 42) Gospeli zote nne hupatana zinaposimulia kwamba wakati marafiki wa Yesu walipofika kwenye kaburi asubuhi ya pili baada ya yeye kufa, mwili wake haukuwapo.—Mathayo 28:1-7; Marko 16:1-7; Luka 24:1-3; Yohana 20:1-10.

Kaburi tupu liliwashangaza maadui na vilevile marafiki wa Yesu. Maadui wake walikuwa wamejaribu kwa muda mrefu uhakikisha kwamba amekufa na kuzikwa. Baada ya kutimiza mradi wao, walichukua tahadhari kwa kuweka mlinzi na kuziba kaburi. Hata hivyo, asubuhi ya siku ya kwanza ya juma, kaburi lilikuwa tupu.

Je, marafiki wa Yesu walikuwa wamechukua mwili wake kutoka kaburini? Haielekei walifanya hivyo, kwa kuwa Gospeli zaonyesha kwamba walisononeka sana baada ya Yesu kuuawa. Zaidi ya hayo, wanafunzi wake hawangekubali kuendelea kunyanyaswa na kuuawa kwa sababu ya jambo walilojua kuwa ni udanganyifu.

Ni nani aliyeutoa mwili kutoka kaburini? Haielekei kabisa kwamba maadui wa Yesu ndio waliouchukua mwili huo. Hata kama wangeuchukua, bila shaka wangeutoa baadaye ili kukanusha madai ya wanafunzi kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa na alikuwa hai. Lakini jambo kama hilo halikupata kutukia kamwe, kwa kuwa Mungu ndiye aliyechukua hatua.

Majuma kadhaa baadaye, maadui wa Yesu hawakupinga kwa kutoa ushahidi mwingi wa kukanusha ufufuo Petro aliposhuhudia hivi: “Wanaume wa Israeli, sikieni maneno haya: Yesu Mnazareti, mwanamume aliyeonyeshwa hadharani na Mungu kwenu kupitia kazi zenye nguvu na mambo ya ajabu na ishara ambazo Mungu alifanya kupitia yeye katikati yenu, kama vile nyinyi wenyewe mjuavyo, mwanamume huyu, kama aliyetolewa kwa shauri lililoamuliwa na kwa ujuzi wa kimbele wa Mungu, mlimfunga kwenye mti kwa mkono wa watu waasi-sheria na kumwondolea mbali. Lakini Mungu alimfufua kwa kuyafungua maumivu makali ya ghafula ya kifo, kwa sababu haikuwezekana yeye kuendelea kushikwa sana nacho. Kwa maana Daudi asema kwa habari yake, ‘Nilikuwa na Yehova mbele ya macho yangu daima . . . Zaidi ya hayo, hata mwili wangu utakaa katika tumaini; kwa sababu hutaacha nafsi yangu katika Hadesi, wala hutaruhusu mwaminifu-mshikamanifu wako aone uharibifu.’”—Matendo 2:22-27.

Wengi Walimwona Yesu Aliyefufuliwa

Luka, mwandishi wa Gospeli, alisema hivi katika kitabu cha Matendo: “Kwa [mitume hawa] pia kwa ithibati zilizo hakika [Yesu] alijionyesha yeye mwenyewe kuwa hai alipokuwa ameteseka, akionwa nao wakati wote wa siku arobaini na kusema mambo juu ya ufalme wa Mungu.” (Matendo 1:2, 3) Wanafunzi kadhaa walimwona Yesu aliyefufuliwa katika pindi mbalimbali—kwenye bustani, barabarani, wakati wa kula, kando ya Bahari ya Tiberiasi.—Mathayo 28:8-10; Luka 24:13-43; Yohana 21:1-23.

Wachambuzi hupinga ukweli wa kutokea huko katika pindi mbalimbali. Wanasema kwamba waandishi hao walitunga mambo hayo au wanataja mambo yanayoonekana kuwa yanapingana. Kwa kweli, tofauti ndogondogo katika masimulizi ya Gospeli huthibitisha kwamba hayapingani. Tunapata kumfahamu Yesu zaidi wakati mwandishi mmoja anapotoa habari ambazo huelezea zaidi masimulizi mengine yanayohusu matukio ya maisha ya kidunia ya Kristo.

Je, kutokea kwa Yesu katika pindi mbalimbali baada ya kufufuliwa, kulikuwa maono ya uwongo? Hoja yoyote ya aina hiyo si ya kweli, kwa kuwa alionekana na watu wengi sana. Miongoni mwao walikuwemo wavuvi, wanawake, mtumishi mmoja wa serikali, na hata Tomasi, mtume mwenye kutilia shaka, ambaye alikuja kusadiki tu alipoona uthibitisho usioweza kukanushwa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu. (Yohana 20:24-29) Katika pindi kadhaa, wanafunzi wa Yesu hawakumtambua mara moja Bwana wao aliyefufuliwa. Pindi moja, zaidi ya watu 500 walimwona, wengi wao walikuwa wangali hai wakati mtume Paulo alipotumia tukio hilo kuwa uthibitisho alipotetea ufufuo.—1 Wakorintho 15:6.

Yesu Aliye Hai Huathiri Watu

Habari inayohusu ufufuo wa Yesu haipasi kuonwa kama jambo la udadisi au la kujadiliwa tu. Uhakika wa kwamba yu hai umeathiri watu kila mahali kwa njia nzuri. Tangu karne ya kwanza, watu wengi sana wameacha kuwa na ubaridi au kupinga Ukristo kabisa na wamekuwa na uhakika kabisa kwamba Ukristo ndio dini ya kweli. Ni nini kilichowabadili? Kwa kujifunza Maandiko walipata uthibitisho kwamba Mungu alimfufua Yesu na kumpa uhai akiwa kiumbe wa kiroho mwenye utukufu huko mbinguni. (Wafilipi 2:8-11) Wamedhihirisha imani katika Yesu na maandalizi ya Yehova Mungu ya wokovu kupitia dhabihu ya fidia ya Kristo. (Waroma 5:8) Watu hao wamepata furaha ya kweli kwa kufanya mapenzi ya Mungu na kuishi kupatana na mafundisho ya Yesu.

Fikiria kilichomaanishwa na kuwa Mkristo katika karne ya kwanza. Hungefaidika kwa kupata umashuhuri, mamlaka, au mali. Kinyume cha hilo, Wakristo wengi wa mapema ‘walikubali kwa shangwe kuporwa mali zao’ kwa ajili ya imani yao. (Waebrania 10:34) Ukristo ulitaka mtu aishi maisha ya kujidhabihu na kunyanyaswa ambako mara nyingi kulisababisha kufia-imani.

Kabla ya kuwa wafuasi wa Kristo, wengine walikuwa na mataraja mazuri ya kuwa mashuhuri na kupata mali. Sauli wa Tarso alifundishwa na Gamalieli mwalimu wa Sheria aliyekuwa maarufu na alikuwa ameanza kupata umashuhuri miongoni mwa Wayahudi. (Matendo 9:1, 2; 22:3; Wagalatia 1:14) Hata hivyo, Sauli alipata kuwa mtume Paulo. Yeye pamoja na wengine wengi walikataa umashuhuri na mamlaka yanayopatikana katika ulimwengu. Kwa nini? Kusudi waeneze ujumbe wa tumaini la kweli linalotegemea ahadi za Mungu na uhakika wa kwamba Yesu Kristo alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu. (Wakolosai 1:28) Walikuwa tayari kuteseka kwa sababu ya jambo walilojua lilitegemea kweli.

Ndivyo ilivyo kwa mamilioni ya watu leo. Unaweza kuwapata katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Mashahidi wanakualika kwa uchangamfu kwenye ukumbusho unaofanywa kila mwaka wa kifo cha Kristo, utakaofanywa baada ya jua kutua Jumapili, Aprili 8, 2001. Watafurahi ukihudhuria sherehe hiyo na pia mikutano yao yote ya kujifunza Biblia inayofanywa kwenye Majumba yao ya Ufalme.

Kwa nini usijifunze zaidi, si kuhusu tu kifo na ufufuo wa Yesu bali pia kuhusu maisha na mafundisho yake? Anatualika twende kwake. (Mathayo 11:28-30) Chukua hatua sasa ya kujipatia ujuzi sahihi kuhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kufanya hivyo kwaweza kumaanisha uhai udumuo milele chini ya Ufalme wa Mungu utakaotawalwa na Mwana wake mpendwa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ili kupata uthibitisho kuhusu ukweli wa Gospeli nne, ona “Gospeli—Je, Ni za Kweli au Ni Hekaya Tu?” katika Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 2000.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mamilioni ya watu hupata furaha ya kweli wakiwa wafuasi wa Yesu Kristo

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]

From the Self-Pronouncing Edition of the Holy Bible, containing the King James and the Revised versions