Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?

Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?

Je, Hii Yaweza Kuwa Kazi-Maisha Inayokufaa Zaidi?

IKIWA wewe ni Mkristo aliyebatizwa, bila shaka kumpenda Mungu hukuchochea kufanya mapenzi yake. Isitoshe, bila shaka huduma yapasa kuwa wito wako. Kwani, Yesu Kristo aliagiza wafuasi wake wote wafanye wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Naam, huenda sasa ukawa unafanya kazi ya kimwili ili kujiruzuku. Lakini ukiwa mfuasi wa Yesu na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, wewe hasa ni mhudumu Mkristo—mtu ambaye hutanguliza kazi ya kuhubiri Ufalme maishani.—Mathayo 24:14.

Labda una umri wa miaka 17 hadi 19 au unaanza miaka ya 20. Huenda umefikiria sana jambo utakalofanya maishani. Unapochanganua mambo unayoweza kufanya, labda utafikiria sana jinsi unavyoweza kujipatia uradhi.

Basi, fikiria yale asemayo Jørgen wa Denmark kuhusu chaguo alilofanya. Jørgen afafanua chaguo alilofanya kuwa “njia bora zaidi ya maisha ambapo unaweza kukazia fikira kazi iliyo ya maana zaidi.” Eva, mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 31 huko Ugiriki, asema: “Ninapolinganisha maisha yangu na ya marika wangu, sikuzote mimi hukata kauli kwamba yana kusudi zaidi, yanaridhisha zaidi na yanasisimua zaidi.” Ni kazi-maisha gani inayotokeza uradhi kama huo? Unawezaje kufuatia kazi-maisha kama hiyo?

Je, Mungu Hukuelekeza?

Huenda ikawa vigumu sana kuchagua kazi-maisha. Kwa kweli, huenda wengine wakatamani Mungu awaonyeshe waziwazi jambo analotaka wafanye.

Musa alipokuwa Midiani, Yehova alimwelekeza arudi Misri na kuwaongoza Waisraeli kutoka utumwani. (Kutoka 3:1-10) Malaika wa Mungu alimtokea Gideoni, aliyekuwa amewekwa rasmi kuokoa Waisraeli kutoka kwa uonezi. (Waamuzi 6:11-14) Daudi alikuwa akichunga kondoo wakati Mungu alipomwambia Samweli amtie mafuta kuwa mfalme wa Israeli ambaye angefuata. (1 Samweli 16:1-13) Hatuelekezwi kwa njia kama hizo leo. Badala yake, twapaswa kuchunguza mambo kwa uangalifu na kuamua jinsi ya kutumia uwezo wetu mbalimbali tuliopewa na Mungu.

Yehova amewafungulia vijana Wakristo leo “mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji.” (1 Wakorintho 16:9) Jinsi gani? Katika mwongo uliopita, idadi ya watangazaji wa Ufalme imeongezeka kutoka watu zaidi ya 2,125,000 hadi kufikia watu zaidi ya 6,000,000 duniani pote. Ni nani ambao husaidia kuandaa mamilioni ya Biblia, vitabu, broshua, magazeti, na trakti zinazohitajiwa ili kujilisha kiroho na pia kusaidia katika kazi ya kuhubiri habari njema inayofanywa ulimwenguni pote? Pendeleo hilo lenye baraka hufurahiwa na washiriki wa familia ya Betheli ulimwenguni pote.

Maisha Yenye Kuthawabisha

Neno Betheli, lamaanisha “Nyumba ya Mungu,” na makao ya Betheli ni mahali wanapoishi wajitoleaji Wakristo wanaotumikia katika makao makuu na kwenye ofisi mbalimbali za tawi za Watch Tower Society. (Mwanzo 28:19, NW, kielezi-chini) Familia za Betheli za siku ya kisasa zaweza kulinganishwa na ‘nyumba zilizojengwa kwa hekima’ na kuimarishwa kwa upendo kuelekea Yehova.—Mithali 24:3.

Ni nini kinachoweza kusemwa kuhusu hali iliyo kama ya familia katika Betheli? Mshiriki mmoja wa Betheli mwenye umri wa miaka 25 huko Estonia asema: “Ninafurahia kuwa miongoni mwa marafiki wa Yehova kila siku. Bado hilo laendelea kuwa jambo lenye thamani zaidi kwangu Betheli.”—Zaburi 15:1, 2.

Kwa sasa, watu wapatao 19,500 hufurahia pendeleo la utumishi wa Betheli ulimwenguni pote. (Zaburi 110:3) Nchini Marekani, asilimia 46 ya wale wanaotumikia Betheli ni wenye umri wa kati ya miaka 19 na 29. Kama Isaya, wamesema: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Isaya—ambaye tayari alikuwa amejiweka wakfu kwa Yehova—alikuwa akijitoa kwa pendeleo zaidi la utumishi. Yaonekana jambo hilo lilimaanisha kudhabihu mambo fulani ya kibinafsi yenye manufaa. Wale wanaotumikia Betheli huacha nyumba na hali walizozoea, na vilevile mama, baba, ndugu, dada, na marafiki. Wanajidhabihu kwa hiari “kwa ajili ya habari njema.”—Marko 10:29, 30.

Wanapata baraka zilizoje Betheli wanapofanya hivyo! Mshiriki mmoja mchanga wa familia ya Betheli huko Urusi aeleza: “Kwa kuwa wenye kujidhabihu, twaweza kujifunza mengi ambayo yaweza kutusaidia kuishi katika ulimwengu mpya. Naweza kusema kwamba kwa upande wangu baraka za Yehova ni nyingi zaidi ya mambo niliyodhabihu.”—Malaki 3:10.

Maisha ya Betheli

Maisha ya Betheli yakoje? Washiriki wa familia ya Betheli wanakubali kwamba ni yenye kujenga, na hata yenye kufurahisha. Jens, ambaye ana umri wa miaka 43, hufurahia utumishi wa Betheli. Kwa nini? Asema: “Kwa sababu ya kuhisi kwamba tunafanya jitihada kuu ili kutekeleza kazi muhimu. Naweza kuhisi jinsi kazi ya Yehova ilivyo kuu na muhimu.”

Kuanzia Jumatatu hadi Jumamosi, siku katika Betheli huanza kwa ibada ya asubuhi. Ibada hiyo ni mazungumzo ya Biblia, yanayoongozwa na mzee fulani mwenye uzoefu. Muda wa saa moja hutengwa jioni za Jumatatu kwa ajili ya funzo la Biblia la familia kupitia Mnara wa Mlinzi, nyakati nyingine likifuatwa na hotuba inayotegemea habari fulani za Kimaandiko zinazohusu hasa familia ya Betheli.

Ni nini hutukia mtu anapokuja Betheli mara ya kwanza? Ili kusaidia washiriki wapya wazoee maisha ya Betheli, ndugu wakomavu wa familia hutoa hotuba zinazohusu sehemu mbalimbali za utumishi wa Betheli. Kwa majuma kadhaa katika mwaka wa kwanza, mshiriki mpya wa familia ya Betheli huhudhuria shule bora inayofanywa kila juma ambayo imekusudiwa kupanua uelewevu wake wa Maandiko. Washiriki wapya hufurahia pia programu ya pekee ya usomaji wa Biblia. Katika mwaka wao wa kwanza wa utumishi wa Betheli, washiriki wapya wa familia husoma Biblia nzima.

Mazoezi hayo yote huwa na matokeo gani? Joshua, mshiriki wa Betheli mwenye umri wa miaka 33 huko Hong Kong, ajibu: “Kwa kweli Betheli imefanya nimthamini Yehova zaidi. Naweza kushirikiana na ndugu wengi wazoefu ambao wametumia miaka mingi maishani kumtumikia Yehova. Ninafurahia hasa programu za kiroho, kama vile ibada ya asubuhi na Funzo la familia la Mnara wa Mlinzi. Zaidi ya hayo, ninapenda maisha yenye utaratibu na sahili. Maisha hayo huniepusha na mahangaiko yasiyo ya lazima. Ninajifunza pia jinsi ya kushughulika na mambo kwa njia ya Kikristo, na kufanya hivyo kumeninufaisha sikuzote.”

Washiriki wa Betheli hutumia muda na jitihada nyingi kufanya kazi waliyojitolea kufanya. Yaani, kutumia uwezo wao wa kimwili na kiakili hasa kutunza migawo wanayopewa Betheli. Kuna kazi za aina mbalimbali zinazohitaji kufanywa. Wengine hufanya kazi kwenye matbaa au katika sehemu ya kujalidi vitabu, wakitengeneza vitabu ambavyo hupelekwa kwa makutaniko mengi. Wengine hufanya kazi jikoni, kwenye chumba cha kulia, au mahali pa kufulia na kupigia nguo pasi. Migawo inatia ndani kutunza usafi, kulima, kujenga, na kadhalika. Wengine wana daraka la kutunza vifaa katika idara hizo. Wengine hushughulikia mambo ya afya au kufanya kazi ofisini. Kazi zote za Betheli ni ngumu lakini ni zenye kufurahisha na huthawabisha sana. Kazi inayofanywa Betheli huridhisha hasa kwa sababu huendeleza masilahi ya Ufalme nayo hufanywa kwa sababu ya kumpenda Mungu.

Washiriki wa familia ya Betheli hupewa mgawo wa kushirikiana na makutaniko mbalimbali, ambako hupata kuona moja kwa moja manufaa ya kazi yao. Wanafurahia kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki kazi ya kuhubiri. Kwa sababu hiyo, washiriki wa familia ya Betheli wamesitawisha urafiki wa karibu sana pamoja na ndugu na dada wa makutaniko wanayoshirikiana nayo.—Marko 10:29, 30.

Rita, mshiriki fulani wa familia ya Betheli nchini Uingereza, asema: “Nalishukuru sana kutaniko! Ninapokuwa mikutanoni na katika huduma, imani yangu huimarishwa sana kuona ndugu wapendwa, dada, watoto, na wazee-wazee wamekuja! Hata hali ziweje, wanakuwepo. Hiyo hunisaidia niwe na bidii zaidi katika utumishi wangu wa Betheli.”

Maisha ya Betheli hayahusishi tu kazi, mikutano, utumishi wa shambani, na kujifunza wakati wote. Familia hufurahia vipindi vya mapumziko vilevile. Pindi kwa pindi, kunakuwa na programu za tafrija zenye kuburudisha na kuthawabisha kiroho, ambazo hutokeza fursa za kufurahia vipawa vya wengine na kujifunza mambo yajengayo kuhusu maisha ya wengine wanaotumikia Betheli. Pia kutembeleana hufurahisha na kujenga. Kuna vifaa kadhaa vya tafrija na vilevile maktaba, kwa ajili ya usomaji na utafiti wa kibinafsi. Kunakuwa pia na mazungumzo yenye kufurahisha mezani wakati wa chakula.

Tom, ambaye ni mshiriki wa familia ya Betheli huko Estonia, asema: “Karibu na Betheli kuna bahari, na karibu nayo kuna msitu mzuri ambapo mimi na mke wangu hufurahia kwenda matembezi kwa muda mfupi. Pindi kwa pindi pia, mimi hucheza gofu, mpira wa magongo, na tenisi pamoja na akina ndugu wa kutaniko na wa Betheli. Na wakati hali ya hewa inapokuwa nzuri, tunaendesha baiskeli.”

Unaweza Kufanya Nini Ili Ustahili?

Bila shaka, Betheli ni mahali hasa ambapo Wakristo wakomavu hutoa utumishi mtakatifu kwa Yehova na kufanya kazi kwa niaba ya waamini wenzao ulimwenguni pote. Wale wanaopata kuwa washiriki wa Betheli lazima watimize sifa fulani. Unaweza kufanya nini ili ustahili kutumika Betheli?

Kama Timotheo, aliyetumikia pamoja na mtume Paulo, wale wanaokubaliwa kwa utumishi wa Betheli lazima wawe na msimamo mzuri kutanikoni. (1 Timotheo 1:1) Timotheo “aliripotiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu.” (Matendo 16:2) Ijapokuwa alikuwa mchanga, Timotheo alijua Maandiko na alikuwa thabiti katika kweli. (2 Timotheo 3:14, 15) Vivyo hivyo, wale wanaokubaliwa kutumika Betheli wanatarajiwa wawe na ujuzi wa Biblia.

Washiriki wa familia ya Betheli wanahitaji kuwa na roho ya kujidhabihu. Timotheo alidhihirisha waziwazi roho ya kujidhabihu na utayari wa kutanguliza masilahi ya Ufalme badala ya masilahi yake hivi kwamba Paulo angeweza kusema hivi kumhusu: “Sina mwingine yeyote mwenye mwelekeo kama wake atakayejali kihalisi mambo yanayohusiana nanyi. Kwa maana wale wengine wote wanatafuta sana masilahi yao wenyewe, si yale ya Kristo Yesu. Lakini nyinyi mwaijua ithibati aliyoitoa juu yake mwenyewe, kwamba kama vile mtoto na baba yeye alitumikia kama mtumwa pamoja nami katika kuendeleza habari njema.”—Wafilipi 2:20-22.

Utumishi wa Betheli hutaka wanaume na wanawake wa kiroho. Mipango inayofanywa kwa ajili ya washiriki wa Betheli huwawezesha wakue kiroho kupitia funzo la Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki huduma ya shambani kwa ukawaida, na kushirikiana na Wakristo wakomavu. Kwa hiyo wale walio Betheli wanasaidiwa kutii shauri hili la Paulo: “Endeleeni kutembea katika muungano na yeye [Kristo Yesu], mkiwa wenye kutia mizizi na kujengwa katika yeye na kuimarishwa katika imani, kama vile mlivyofundishwa, mkifurikwa na imani katika utoaji-shukrani.”—Wakolosai 2:6, 7.

Kazi inayofanywa Betheli hutaka wale wanaopewa pendeleo hilo la utumishi wawe na nguvu za kimwili na afya nzuri. Ikiwa umetimiza sifa ambazo tumetaja, una umri wa miaka 19 au zaidi, na umebatizwa kwa angalau mwaka mmoja, twakutia moyo ufikirie utumishi wa Betheli.

Sote Tunashiriki Fungu Fulani

Tukiwa Wakristo, kwa kweli sote tunatamani kutanguliza masilahi ya Ufalme maishani na kumtolea Yehova utumishi wa nafsi yote. (Mathayo 6:33; Wakolosai 3:23) Twaweza kuwatia moyo pia wale wanaotumikia Betheli waendelee kutoa utumishi mtakatifu huko. Na hasa ndugu wachanga wanaostahili kutumikia Betheli wapaswa kuhimizwa wafikie pendeleo hilo lenye baraka.

Utumishi wa Betheli ni njia ya maisha inayothawabisha kiroho—inaweza kuwa kazi-maisha inayokufaa zaidi. Nick aliyeanza utumishi wa Betheli akiwa na umri wa miaka 20 amefuatia njia hiyo ya maisha. Baada ya kutumikia katika Betheli kwa miaka kumi, asema hivi: “Mara nyingi mimi husali kwa Yehova ili kumshukuru kwa ajili ya fadhili zake zisizostahiliwa. Nitake nini zaidi? Hapa, twazungukwa na Wakristo waaminifu wanaofanya yote wawezayo kumtumikia Yehova.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

WAZEE NA WAZAZI WANAWEZA KUFANYA NINI?

Wazee na waangalizi wasafirio hasa wapaswa kuwatia moyo vijana wajaze ombi la kutumikia Betheli. Hivi karibuni, uchunguzi usio rasmi uliofanyiwa washiriki wachanga wa familia ya Betheli ulionyesha kwamba asilimia 34 kati yao walihimizwa hasa na waangalizi Wakristo waweke mradi wa kutumikia Betheli. Ndiyo, huenda kutaniko wanaloshirikiana nalo likakosa kunufaika na utumishi wao. Lakini ni vizuri kukumbuka kwamba ingawa pasipo shaka Timotheo alikuwa na uvutano mzuri kwa vijana wengine huko Listra na Ikoniamu, wazee wa huko hawakumzuia asitumikie pamoja na Paulo. Hawakukata kauli kwamba kutaniko lao lingepata hasara kubwa sana Timotheo akiandamana na mtume huyo.—1 Timotheo 4:14.

Wazazi Wakristo hasa wapaswa kuwa na uvutano mzuri kwa watoto wao kuhusiana na jambo hilo. Katika uchunguzi uliotajwa, asilimia 40 ya wale walioulizwa walitaja kwamba wazazi wao hasa ndio waliowatia moyo waanze utumishi wa Betheli. Dada mmoja ambaye amekuwa akitumikia katika Betheli kwa miaka michache alisema: “Nilichochewa sana kuanza utumishi wa Betheli nilipoangalia maisha ya wazazi wangu ambao walikuwa wakimtumikia Yehova. Kwa kutazama kielelezo chao katika huduma ya wakati wote, nilijua kwamba hiyo ndiyo ingekuwa njia bora zaidi ya maisha na yenye kuridhisha ninayopaswa kuchagua.”

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

WANATHAMINI UTUMISHI WA BETHELI

“Ninathamini sana utumishi wangu Betheli. Ninaridhika kujua kwamba nimemtumikia Yehova siku nzima na kwamba nitafanya vivyo hivyo kesho, keshokutwa, na kuendelea. Hiyo hufanya niwe na dhamiri nzuri na kujaza akili yangu mambo yanayofaa.”

“Betheli ni mahali ambapo unaweza kutumia nguvu na wakati wako wote kumtumikia Yehova bila kukengeushwa. Hilo huleta furaha ya moyoni. Unaweza pia kuwa na mtazamo tofauti kuhusu tengenezo la Yehova. Unahisi ukiwa karibu zaidi na kitovu cha utendaji wa tengenezo hilo, na jambo hilo husisimua sana.”

“Utumishi wa Betheli ndio jambo bora zaidi ambalo nimepata kufanya. Elimu haikomei hapa. Na hapa elimu si ya kujipatia sifa ya kibinafsi, bali kumpa Yehova sifa. Hapa kazi yangu haitakuwa ya bure kamwe.”

“Mimi ninaridhika na kupata amani ninapotumia vipawa vyangu katika Betheli kwa sababu ninavitumia kwa ajili ya Yehova na kwa ajili ya akina ndugu.”

“Singeweza kupata uradhi na furaha ya kweli katika kazi niliyofanya hapo awali. Nilikuwa nimetamani kwa miaka mingi kufanya kazi pamoja na ndugu na dada zangu na pia kufanya kazi kwa niaba yao. Ndiyo sababu nikaja Betheli. Ninapata uradhi wa kweli kujua kwamba jitihada zangu zote zitanufaisha wengine kiroho na kumletea Yehova sifa.”