Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wachochewa Kutumikia

Wachochewa Kutumikia

Wachochewa Kutumikia

NI NINI ambacho kingewachochea wenzi 24 waliofunga ndoa wakiwa katika upeo wa maisha yao kuacha familia zao, marafiki, na mazingira waliyozoea ili kwenda kufanya kazi ya umishonari katika nchi za kigeni? Kwa nini wapendezwe na kwenda katika nchi kama vile Papua New Guinea na Taiwan, na vilevile nchi za Afrika na za Amerika ya Kusini? Je, ni kutaka tu mambo ya kujasiria? La. Badala yake, wanachochewa na upendo halisi kwa Mungu na jirani.—Mathayo 22:37-39.

Watu hao ni nani? Ni wahitimu wa darasa la 109 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Jumamosi, Septemba 9, 2000, jumla ya watu 5,198 walikusanyika kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower—huko Patterson, New York—na katika sehemu mbalimbali zilizounganishwa kwa simu ili kusikiliza shauri lenye upendo linaloweza kuwasaidia wahitimu kuwa mishonari wenye matokeo.

Mwenyekiti wa programu alikuwa Stephen Lett, mshiriki wa Halmashauri ya Kufundisha ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Maelezo yake ya kufungua yalitegemea Mathayo 5:13, “Nyinyi ndio chumvi ya dunia.” Ndugu Lett alieleza kwamba maneno ya Yesu bila shaka yanahusu wanafunzi wanaohitimu. Mathalani, chumvi inaweza kufanya vitu viwe na ladha nzuri. Vivyo hivyo, wanapohubiri kwa njia yenye matokeo, mishonari wanakuwa kama chumvi kwa njia ya mfano.

Kitia-Moyo cha Kuagana

Kisha Ndugu Lett akakaribisha baadhi ya watumishi wa Yehova ambao wametumikia kwa muda mrefu kutoa hotuba fupi za Kimaandiko lakini zenye matokeo. Wa kwanza alikuwa John Wischuk, anayetumikia katika Idara ya Kuandika. Kichwa cha hotuba yake, iliyotegemea Zaburi 117, NW, kilikuwa “Zaburi Fupi Zaidi Huchochea Roho ya Umishonari.” Leo, kuna uhitaji ulimwenguni pote wa kutoa ushahidi kwa “mataifa” na “mbari” kuhusu Yehova na Ufalme wake. Wanafunzi walitiwa moyo watimize yale yanayosemwa katika Zaburi 117, NW, kwa kuhimiza wengine “Wamsifu Yah.”

Kisha mwenyekiti akamkaribisha Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza. Alizungumzia kichwa “Uwe Mwenye Kubadilikana, Lakini Imara.” Neno la Mungu ni thabiti. Yehova Mungu huitwa Mwamba kwenye Kumbukumbu la Torati 32:4, hata hivyo Neno lake hubadilikana kwa sababu liliandikwa kwa ajili ya watu wa lugha na tamaduni zote—naam, kwa ajili ya wanadamu wote. Wanafunzi walishauriwa wahubiri Neno la Mungu, na kuruhusu ujumbe wake uguse mioyo na dhamiri za watu. (2 Wakorintho 4:2) “Mwe imara kuhusiana na kanuni zinazofaa, lakini mbadilikane. Msidharau watu wa nchi ambayo mnatumikia kwa sababu utamaduni wao ni tofauti,” akahimiza Ndugu Pierce.

Karl Adams, mmoja wa wafunzi wa Gileadi, ambaye ametumikia kwenye makao makuu ya ulimwengu kwa miaka 53 hivi, alizungumzia kichwa chenye kuamsha fikira “Utaenda Wapi Utokapo Hapa?” Ni kweli kwamba wenzi 24 waliofunga ndoa walipokea migawo ya umishonari katika nchi 20 tofauti-tofauti ulimwenguni pote, lakini swali liliulizwa, Utakapofika huko na kuona nchi utakayotumikia, utafanya nini hatimaye? Tunaishi katika ulimwengu ambamo watu hawatulii. Watu wanataka kusafiri katika nchi za kigeni na kufanya mambo mapya ili kujifurahisha. Kwa upande mwingine, wanafunzi walipokea mgawo kutoka kwa Yehova waende mahali ambako anataka watumikie “kondoo” zake bila ubinafsi. Hawapaswi kuwa kama watu wa Israeli la kale ambao kwa sababu ya ubinafsi walipoteza fursa ya kutumiwa na Yehova kubariki wanadamu wote. Badala yake, wanapaswa kumwiga Yesu Kristo, ambaye alifanya mapenzi ya Baba yake sikuzote bila ubinafsi na kumtii chini ya hali zote.—Yohana 8:29; 10:16.

Kichwa cha hotuba ya Wallace Liverance, msajili wa Shule ya Gileadi kilikuwa “Thaminini Sana Mambo Yenye Kina Kirefu ya Mungu.” Mara nyingi, Maandiko hutaja Neno la Mungu kuwa utajiri, vito vyenye thamani, metali zenye thamani, na vitu vya thamani ya juu na vinavyotafutwa sana. Mithali 2:1-5 huonyesha kwamba ili “kupata kumjua Mungu,” lazima tuutafute ujuzi huo kama “hazina iliyositirika.” Msemaji aliwatia moyo wanafunzi waendelee kuchimba katika mambo yenye kina kirefu ya Mungu wanapotumikia katika migawo yao mipya. Ndugu Liverance alisababu hivi: “Jambo hilo ni la busara, kwa kuwa linajenga imani na uhakika katika Yehova nalo litaimarisha azimio lenu la kushikamana na mgawo wenu. Litawasaidia kusema kwa usadikisho na kuwa walimu wenye matokeo zaidi mnapowaeleza wengine makusudi ya Mungu.”

Akitumia kikao cha darasa, mfunzi mwingine wa Shule ya Gileadi alitoa muhtasari wa jinsi ambavyo Yehova alibariki utumishi wa shambani wa wanafunzi katika miezi mitano iliyopita. Lawrence Bowen alitaja maneno ya mtume Paulo kwenye Matendo 20:20 kuhusu huduma yake ya watu wote huko Efeso, akikazia kwamba Paulo alitumia fursa zote kutoa ushahidi. Mambo yaliyoonwa ya wanafunzi yalionyesha kwamba, kama mtume Paulo, wale wanaochochewa na upendo kwa Mungu na jirani katika wakati wetu hawakosi kusema kweli na kuruhusu nguvu za Neno la Mungu ziathiri wengine. Hilo huleta baraka tele kutoka kwa Yehova.

Ndugu Wenye Uzoefu Wanena

Wakati wa muhula wao wa shule, wanafunzi wa darasa hili la Gileadi walinufaika hasa kwa kushirikiana na washiriki wa Halmashauri ya Tawi kutoka nchi 23, ambao pia walikuwa katika Kituo cha Elimu cha Patterson ili kupokea elimu ya pekee. Leon Weaver na Merton Campbell wa Idara ya Utumishi walihoji washiriki kadhaa wa Halmashauri ya Tawi, ambao baadhi yao walikuwa wahitimu wa Gileadi. Wanafunzi, familia na marafiki wao, walitiwa moyo baada ya kusikia mishonari wenye uzoefu wakihojiwa.

Shauri walilopewa wahitimu ili kuwasaidia wafaane na migawo yao katika nchi za kigeni lilitia ndani maelezo kama: “Mwe wenye kutazamia mema. Ukiona jambo lisilo la kawaida au usiloelewa, usikate tamaa. Mtegemee Yehova”; “jifunze kufurahia kile ulicho nacho, na kutumaini kwamba Yehova atakupa mahitaji ya lazima maishani.” Maelezo mengine yalikazia jinsi ya kusaidia wanafunzi wadumishe shangwe katika mgawo wao. Mambo machache yalisemwa kama vile: “Usilinganishe nchi ambayo unatumikia na mahali ulipotoka”; “jifunze lugha ya wenyeji na kuizungumza vizuri ili uweze kuwasiliana na watu”; “jifunze desturi na utamaduni wa watu, kwa kuwa hilo litakusaidia kushikamana na mgawo wako.” Maneno hayo yaliwatia moyo sana mishonari wapya.

Baada ya mahoji, David Splane, aliyekuwa mishonari na mhitimu wa darasa la 42 la Gileadi ambaye sasa anatumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alitoa hotuba kuu yenye kichwa chenye kuvutia “Wanafunzi au Wahitimu—Nyinyi Ni Nani?” Aliuliza darasa la wahitimu, “Mtajionaje wenyewe mtakapoenda kwenye mgawo wenu wa umishonari? Je, mtajiona kuwa wahitimu wanaojua kila kitu kuhusu kazi ya umishonari au kama wanafunzi ambao bado wanahitaji kujifunza mengi?” Ndugu Splane alisema kwamba mhitimu mwenye hekima hujiona kuwa mwanafunzi. Mishonari wapaswa kuwa na maoni kwamba kila mtu wanayekutana naye katika mgawo wao wa umishonari anaweza kuwafundisha jambo fulani. (Wafilipi 2:3) Wanafunzi walitiwa moyo washirikiane kwa ukaribu na mishonari wenzao, ofisi ya tawi, na kutaniko. “Mmepita mitihani yenu ya mwisho, lakini mngali wanafunzi. Acheni kila mtu ajue kwamba mnataka kujifunza,” akahimiza Ndugu Splane.

Baada ya hotuba hiyo, wanafunzi walipokea diploma zao, na migawo yao ikatangazwa kwa wasikilizaji. Wahitimu waliguswa moyo wakati mwakilishi wa darasa aliposoma azimio lililosema kwamba wanafunzi walikuwa wameamua kuruhusu mambo waliyojifunza kutoka kwa Neno la Mungu yawachochee kufanya mengi zaidi katika utumishi mtakatifu.

Wote waliohudhuria walikubali kwamba shauri lililotolewa liliimarisha azimio la wahitimu la kumpenda Mungu na jirani. Liliwafanya pia waazimie hata zaidi kuliko wakati mwingine wowote kusaidia watu kiroho katika mgawo wao wa umishonari.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 10

Idadi ya nchi walikogawiwa: 20

Idadi ya wanafunzi: 48

Wastani wa umri: 33.7

Wastani wa miaka katika kweli: 16.2

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12.5

[Picha katika ukurasa wa 26]

Darasa la 109 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Collins, E.; Miles, L.; Alvarado, A.; Lake, J. (2) Van Dusen, L.; Biharie, A.; Heikkinen, H.; Koós, S.; Smith, H. (3) Ashford, J.; Ashford, C.; Boor, C.; Richard, L.; Wilburn, D.; Lake, J. (4) Chichii, K.; Chichii, H.; Ramirez, M.; Baumann, D.; Becker, G.; Biharie, S.; Ramirez, A. (5) Van Dusen, W.; Lemâtre, H.; Pisko, J.; Cutts, L.; Russell, H.; Johnson, R. (6) Becker, F.; Baumann, D.; Johnson, K.; Pifer, Á.; Madsen, C.; Lemâtre, J.; Heikkinen, P. (7) Smith, R.; Russell, J.; Collins, A.; Pisko, D.; Wilburn, R.; Koós, G. (8) Cutts, B.; Boor, J.; Madsen, N.; Pifer, S.; Richard, E.; Miles, B.; Alvarado, R.