Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema za Amani Zafika Kwenye Milima ya Chiapas

Habari Njema za Amani Zafika Kwenye Milima ya Chiapas

Habari Njema za Amani Zafika Kwenye Milima ya Chiapas

“Katika mauaji ya kinyama yasiyoweza kusahauliwa na mtu yeyote kwenye jimbo la Chiapas, wakulima wadogo 45 wasioweza kujihami, kutia ndani watoto wachanga 13, waliuawa na kikundi cha . . . wanaume wenye silaha.” Likaripoti gazeti “El Universal” kuhusu yaliyotokea huko Acteal, Jimbo la Chiapas, Desemba 22, 1997.

CHIAPAS ni jimbo la Mexico lililo kusini kabisa, ambalo linapakana na Guatemala. Kikundi cha Wahindi wa Maya, wenyeji ambao wameishi kwa umaskini na uhitaji kwa muda mrefu, walianzisha maasi kwa kutumia silaha mnamo Januari 1994, wakijiita Ejército Zapatista de Liberación Nacional (EZLN, Jeshi la Kitaifa la Ukombozi la Zapatista). Majadiliano ya kutafuta amani yamechukua muda mrefu. Uvamizi na mashambulizi yaliyofanywa na waasi na pia askari wa serikali, yamesababisha umwagikaji wa damu na vifo. Msukosuko huo ulifanya wakulima wengi katika eneo hilo wakimbilie usalama.

Chini ya hali hizo zenye wasiwasi, kuna kikundi kimoja cha wapenda-amani ambao hawaungi mkono upande wowote wa pambano hilo la kisiasa. Huku wakiwa na bidii, wanaelekeza fikira kwenye Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la kutatua matatizo yanayowapata watu katika eneo hilo na ulimwenguni pote. (Danieli 2:44) Wao ni nani? Ni Mashahidi wa Yehova. Kwa kutii amri ya Yesu, wanajitahidi kupeleka habari njema za Ufalme wa Mungu hadi sehemu za mbali zaidi za milima ya Chiapas. (Mathayo 24:14) Ilikuwaje kuhubiri chini ya hali hizo, na matokeo yalikuwaje?

“Mimi Ni Mmoja wa Mashahidi wa Yehova”

Adolfo, kijana mmoja ambaye hivi majuzi alipata kuwa mhubiri wa Ufalme, alikuwa akifanya kazi siku moja kwenye kituo cha redio huko Ocosingo. Kwa ghafula akasikia mlango ukibishwa kwa nguvu. Kikundi cha wanaume waliokuwa wamejifunika vichwa waliingia na kumwelekezea bunduki zao kichwani. Waliingia mbio-mbio kwenye chumba cha matangazo, wakatwaa vifaa kwa nguvu, na kutangaza kwenye redio kwamba wameanzisha vita dhidi ya serikali.

Wanaume hao wenye silaha walimgeukia Adolfo na kumwamuru ajiunge na harakati yao. “Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova,” akajibu Adolfo, hata ingawa hakuwa amebatizwa bado. Aliwaeleza kwamba tumaini pekee la amani ni Ufalme wa Mungu, akakataa katakata yunifomu na bunduki waliyompa. Walipoona msimamo wake imara, walimruhusu aende. Akikumbuka tukio hilo, Adolfo asema: “Tukio hilo liliimarisha imani yangu kwelikweli.”

Hatimaye hali ilitulia, lakini eneo hilo likawa bado linasimamiwa na majeshi. Licha ya hali hiyo, Adolfo alikubali kwa furaha ombi la wazee wa kutaniko la kwao afanye kazi na kikundi cha Wakristo waliokuwa mbali na eneo hilo. Katika vituo vya ukaguzi alivyolazimika kupitia, askari-jeshi walimstahi alipojitambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baadaye alibatizwa na amepata uradhi wa kusaidia kikundi hicho kilicho mbali kuwa kutaniko la Mashahidi wa Yehova. “Kwa kuwa sasa nimebatizwa,” akasema Adolfo, “naweza kusema kwa usadikisho kamili kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova!”

“Yehova Alituimarisha”

Muda mfupi baada ya kikundi cha EZLN kutangaza vita dhidi ya serikali kupitia redio, wakazi wa mjini walitoroka. Francisco, mhudumu wa wakati wote, au painia, alieleza jinsi Yehova alivyowaimarisha yeye na mkewe katika mambo yaliyowapata.

“Tuliamua kukimbilia eneo ambalo tulitembea kwa muda wa saa tatu kufika huko. Kulikuwa na kutaniko huko, kwa hiyo tungekaa na akina ndugu. Punde si punde wakati wa kufanya kusanyiko letu la mzunguko huko Palenque ukafika. Mimi na mke wangu hatukutaka kukosa mkutano wa pekee kwa ajili ya mapainia, lakini tulipata habari kwamba njia ya kuelekea kwenye kusanyiko ilikuwa imefungwa na kikundi cha EZLN. Tuliamua kupitia njia ya msituni, iliyotuchukua muda wa saa tisa. Tulifika kwa wakati na kuhudhuria programu nzima ya kusanyiko na vilevile mkutano wa mapainia ambao tulifurahia sana.

“Tuliporudi, tulikuta nyumba yetu imechomwa na mifugo yetu imeibwa. Mfuko mdogo tu wa mavazi ndio ulioachwa. Tulihuzunika kwa sababu ya hasara tuliyopata, lakini ndugu wa Ocosingo walitukaribisha nyumbani kwao kwa fadhili. Walitufunza pia kazi mbalimbali ambazo sisi wakulima hatukuwa tumepata kuzifanya hapo awali. Ndugu mmoja alinifunza kupiga picha, mwingine akanifunza kushona viatu. Kwa njia hiyo mimi na mke wangu tumeweza kujitegemeza hadi sasa, bila kulazimika kuacha utumishi wa painia. Tunapokumbuka yaliyotukia, twaweza kuona kwamba ingawa haikuwa rahisi kuvumilia, Yehova alituimarisha.”

Matokeo ya Kuhubiri

Mashahidi katika Jimbo la Chiapas hawakuzuiwa na magumu na hatari wasishiriki katika jitihada ya pekee ya kupelekea watu wa eneo hilo habari njema. Kwa mfano, mnamo Aprili na Mei 1995, walijiunga na Wakristo wenzao ulimwenguni pote katika kampeni ya kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 34, yenye kichwa kinachofaa Kwa Nini Maisha Yamejaa Matatizo Sana?

Wakati wa kampeni hiyo—katika sehemu iitwayo Pueblo Nuevo, Ciro—ambaye ni painia wa kawaida, alipata familia iliyoonyesha upendezi. Aliporudi siku tatu baadaye, alianzisha funzo la Biblia pamoja na familia hiyo. Lakini Ciro aliporudi akiwa na rafiki fulani ili kuendeleza funzo na familia hiyo, mwenye nyumba hakuwako. Badala yake, kulikuwa na kikundi cha wanaume waliokuwa wamejifunika vichwa wakimngojea ili wamwumize. Walimwuliza Ciro na mwandamani wake ni nini walichokuwa wakitafuta na wakatisha kuwaua. Baada ya kusali kwa Yehova kwa ukimya, Wakristo hao wawili waliwaeleza kwa ujasiri kwamba walikuwa wamekuja kufundisha familia hiyo Biblia. Baada ya kusikia mambo hayo, wanaume hao waliojifunika vichwa waliwaachilia. Kwa sababu fulani, mwenye nyumba hakurudi nyumbani siku hiyo.

Siku moja yapata miaka mitatu baadaye, Ciro alishangaa kumwona mwanamume huyo mlangoni pake. Ciro alifurahi kama nini kupata habari kwamba familia nzima ilikuwa imebatizwa na kwamba sasa ilikuwa ikishirikiana na kutaniko fulani nchini Guatemala! Hata mmoja wa mabinti wake alikuwa akitumikia akiwa painia wa kawaida.

Kuthamini Chakula cha Kiroho

Licha ya kuendelea kwa magumu katika Chiapas, mwangalizi mmoja wa wilaya aripoti kwamba Mashahidi katika eneo hilo huthamini kwelikweli umuhimu wa kukutanika pamoja. (Waebrania 10:24, 25) Asimulia kilichotukia kwenye siku ya kusanyiko la pekee iliyofanywa hivi majuzi, ambayo ilipangiwa kuanza mapema asubuhi ili wahudhuriaji waweze kurudi nyumbani salama kukiwa bado na nuru. Ijapokuwa wengi wao walilazimika kutembea kwa muda unaozidi saa tatu kupitia msituni ili kufika kwenye kusanyiko, kila mtu alikuwa ameketi ilipofika saa 1:00 asubuhi. Miongoni mwa wasikilizaji kulikuwemo washiriki sita wa kikundi cha EZLN, wakisikiliza na kupiga makofi, huku wakionekana kuwa wanafurahia programu. Wao pia walitembea kwa muda wa saa tatu ili kuhudhuria kusanyiko. Ishirini kati yao walihudhuria pia Ukumbusho wa kifo cha Kristo, uliofanywa katika Jumba la Ufalme la hapo.

Kijana mwingine aliyeshirikiana na harakati ya wapiganaji wa kuvizia alipewa mgawo na wakubwa wake wa kulinda doria katika eneo fulani la msituni. Alipofika kwenye jumuiya hiyo, alikuta wakazi wote, ambao wengi wao walikuwa Mashahidi wa Yehova wametoroka. Kwa hiyo akaanza kuishi katika mojawapo ya makao yaliyokuwa yameachwa. Kwa kuwa hakuwa na mengi ya kufanya, alichukua vitabu fulani alivyopata katika nyumba hiyo na kuanza kuvisoma. Vichapo hivyo vilikuwa vya Watch Tower vilivyoachwa na Mashahidi. Akiwa peke yake, kijana huyo alikuwa na wakati wa kutafakari mambo aliyokuwa akisoma. Aliamua kwamba ni lazima abadili maisha yake na kusalimisha silaha zake. Alitafuta Mashahidi haraka iwezekanavyo na kuanza kujifunza Biblia. Kwa muda wa miezi sita, alikuwa akihubiria wengine habari njema. Yeye na washiriki wengine watatu wa familia yake waliokuwa wakiunga mkono harakati ya wapiganaji wa kuvizia sasa ni Wakristo waliobatizwa.

Kuwa na Matumaini Mema

Hata ingawa vita hivyo vilisababisha magumu mengi, kwa kweli viliathiri ifaavyo mtazamo wa watu kuelekea kazi ya kuhubiri. Mzee mmoja katika jiji ambamo vita vilianza asimulia hivi: “Karibu siku tano baada ya vita kuanza, tulipanga kazi ya kuhubiri ndani na nje ya jiji. Watu walikuwa na hamu ya kutusikiliza. Tuliangusha vichapo vingi vya Biblia na kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia. Katika eneo moja, watu wengi walikuwa wakipinga kweli, lakini kwa sababu ya vita, sasa wanasikiliza, wanajifunza Biblia, na kuhudhuria mikutano na makusanyiko.”

Akina ndugu wanafurahi kwamba wamefaulu kuendelea na utendaji wao wa kitheokrasi licha ya hali hizo zenye wasiwasi. Wanaendelea kufanya makusanyiko yao ambayo huwajenga kiroho, licha ya kwamba jambo hilo lajulikana na wanajeshi wa serikali na wa kikundi cha EZLN. Ziara za waangalizi wasafirio pia zimekuwa kichocheo kikubwa cha kuendelea kuhubiri. Jambo linalopendeza ni kwamba, Mashahidi wanatiwa moyo hata na watu wanaohusika katika pambano hilo, ambao mara nyingi huwahimiza waendelee na kazi yao ya kuhubiri.

Ijapokuwa majaribu na magumu ambayo yamewapata watu wa Chiapas yamepungua kwa kiasi fulani baada ya muda, bado hayajakoma. Vyovyote iwavyo, jambo moja ni hakika—Mashahidi wa Yehova wameazimia kuendelea bila kuacha katika jitihada yao ya kupelekea watu habari njema za amani kutoka katika Neno la Mungu, Biblia. (Matendo 10:34-36; Waefeso 6:15) Kama alivyosema nabii Yeremia, wanatambua kwamba, “njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Ni Ufalme wa Mungu pekee kupitia Mwana wake, Yesu Kristo, unaoweza kutatua udhalimu na umaskini ulimwenguni.—Mathayo 6:10.

[Ramani katika ukurasa wa 9]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ghuba ya Mexico

CHIAPAS

GUATEMALA

Bahari ya Pasifiki

[Hisani]

Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mashahidi wakielekea katika huduma kwenye milima ya Chiapas