Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Usali?

Kwa Nini Usali?

Kwa Nini Usali?

“MWAOMBA, na bado hampokei, kwa sababu mwaomba kwa kusudi baya . . . Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:3, 8) Maneno hayo ya Yakobo, mwanafunzi wa Yesu, yaweza kutuchochea tufikirie sababu zinazofanya tusali.

Sala si namna tu ya kumwambia Mungu mahitaji yetu. Katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Baba yenu ajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla nyinyi hamjamwomba.” Hata hivyo, Yesu pia alisema: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa.” (Mathayo 6:8; 7:7) Kwa hiyo Yehova hutaka tumwambie yale tunayohisi tunahitaji. Lakini sala yahusisha mengi zaidi.

Marafiki wa kweli hawawasiliani tu wanapohitaji kitu fulani. Kila mmoja hupendezwa na mwenzake, na urafiki wao hukua wanapodhihirisha hisia zao. Vivyo hivyo, sala ina kusudi kubwa zaidi kuliko kuomba tu yale tunayohitaji. Hutupa fursa ya kuimarisha uhusiano wetu na Yehova kwa kumweleza ujitoaji wetu kutoka moyoni.

Naam, Mungu ametupa pendeleo la sala ili tuweze kumkaribia. Twaweza kuwa na uhusiano huo ikiwa tu, tutadhihirisha hisia zetu kwa Mungu badala ya kurudia-rudia sala zilizokaririwa. Inapendeza kama nini kuzungumza na Yehova katika sala! Isitoshe, mithali moja ya Biblia husema: “Maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.”—Mithali 15:8.

“Nami kumkaribia Mungu ni kwema kwangu,” akaimba mtunga-zaburi Asafu. (Zaburi 73:28) Lakini ili tumkaribie Mungu, lazima tufanye mengi zaidi kuliko kusali tu. Ona jinsi simulizi lifuatalo linavyoonyesha hivyo:

“Mtu fulani kati ya wanafunzi wake [Yesu] alimwambia: ‘Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.’” Yesu alijibu kwa kusema: “Wakati wowote msalipo, semeni, ‘Baba, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje.’” (Luka 11:1, 2) Je, tunaweza kwa njia hiyo kutoa sala zenye maana kabla ya kujifunza kwanza jina la Mungu ni nani na jinsi litakavyotakaswa? Na je, tunaweza kusali kupatana na maneno hayo ya Yesu ikiwa hatuelewi Ufalme wa Mungu ni nini? Tunaweza kuelewa mambo hayo tukichunguza Biblia kwa makini. Kisha ujuzi tutakaopata utatusaidia kumjua Mungu na kuelewa njia zake. Zaidi ya hayo, kumjua Yehova Mungu kutatufanya tuhisi kuwa karibu zaidi naye na kujitoa kwake zaidi. Halafu, hiyo itatusaidia kuzungumza naye kwa uhuru zaidi katika sala.

Sala Yaweza Kutatua Matatizo

Kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kutatusaidia kutatua matatizo. Ona uthibitisho wa jambo hilo katika visa vifuatavyo. Vinaonyesha kwamba wale waliosali waliweza kuimarisha uhusiano wao pamoja na Yehova.

Nchini Brazili mwanamke mmoja anayeitwa Maria alisali kwa Mungu ili kupata msaada. Alitaka kuasi viwango vya mwenendo vinavyokubalika, kwa kiasi fulani kwa sababu ya unafiki alioona katika jamii. Maria hata alikuwa amemwacha mume wake, watoto wake, na nyumba yake. Alianza pia kutumia dawa za kulevya. Lakini alipokosa furaha, alimweleza Mungu hisia zake kwa uhuru, akisali asaidiwe.

Punde si punde, Mashahidi wawili wa Yehova wakamtembelea na kumwachia Maria toleo moja la Mnara wa Mlinzi lililokuwa na habari kuhusu faida ya kukubali mwongozo kutoka kwa Mungu. Liligusa moyo wake, akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi hao siku iyo hiyo. Funzo hilo hatimaye lilimfanya arudi kuishi na familia yake. Alipoendelea kujifunza juu ya Yehova, alitaka kumwonyesha upendo wake. “Nikafanya mabadiliko yanayofaa,” akasema Maria. “Kwanza mume na familia yangu walinipinga nisijifunze Biblia. Lakini walipoona mabadiliko niliyokuwa nikifanya, wakaanza kunitia moyo.” Baadaye, Maria aliweka maisha yake wakfu kwa Msikiaji wa sala ili amtumikie.

Ingawa José alikuwa na mke mrembo na biashara yenye kusitawi nchini Bolivia, hakuwa na furaha. Kwa sababu ya kufanya ngono nje ya ndoa, mke wake alimwacha. Alikunywa kupindukia na kuhisi hafai kitu. José asema hivi: “Nilianza kusali kwa moyo mweupe, nikijiuliza ninalopaswa kufanya ili nimpendeze Mungu. Punde si punde, Mashahidi wa Yehova walizuru mahali pangu pa biashara wakiwatolea watu funzo la Biblia la nyumbani bila malipo, lakini nikawafukuza. Niliwafukuza mara tatu. Kila mara niliposali ili nipate msaada, Mashahidi walikuja. Hatimaye, nikaazimia kwamba wakija mara nyingine tena, nitawasikiliza. Nilikuwa nimeisoma Biblia yote na nilikuwa na maswali mengi, lakini sikuzote walikuwa na majibu yaliyoniridhisha. Kujifunza juu ya Yehova kulinipa kusudi jipya maishani, na marafiki wangu Mashahidi walikuwa vielelezo vyenye kutia moyo kama nini! Nilimwacha rafiki yangu msichana na marafiki wangu nilioshirikiana nao kunywa. Baada ya muda mfupi, nikarudia mke na watoto wangu. Nilibatizwa mwanzo-mwanzo wa mwaka wa 1999.”

Nchini Italia, ndoa ya Tamara ilikuwa taabani, kwa hiyo alisali ili kupata hekima. Baada ya kupigwa na kufukuzwa na familia yao alipokuwa na umri wa miaka 14, akawa mchokozi. Tamara asema hivi: “Nilipata Biblia nikaanza kuisoma. Jioni moja, nilisoma kwamba ‘kutafuta busara ni kama kutafuta hazina iliyositirika.’ Nilisali ili kupata hekima hiyo. (Mithali 2:1-6) Asubuhi iliyofuata, Mashahidi wa Yehova walinitembelea. Nikaanza kujifunza Biblia pamoja nao, lakini ilinichukua muda kabla ya kutumia yale niliyojifunza. Hatimaye, nikaamua kufuata njia ya maisha ya Kikristo na kubatizwa. Sasa, nikiwa pamoja na mume wangu, ninasaidia wengine wajinufaishe na hekima ya Mungu.”

Beatriz alikuwa miongoni mwa watu mashuhuri katika jamii ya Caracas, Venezuela. Hata hivyo, alitalikiwa na kupatwa na msononeko. Akiwa amekata tumaini, wakati mmoja alitumia saa kadhaa akisali. Asubuhi iliyofuata akasikia kengele ya mlango ikilia. Akiwa ameudhika, alitazama kwenye tundu la kuchungulia na kuona watu wawili wenye mikoba. Akajifanya hayuko nyumbani, lakini kabla wenzi hao wa ndoa hawajaondoka, waliingiza kikaratasi cha kukaribisha watu chini ya mlango. Kilisema “Ijue Biblia Yako.” Je, ziara yao ilihusiana na sala alizotoa usiku uliotangulia? Akawaita warudi. Punde si punde, akaanza kujifunza Biblia, na baadaye akabatizwa. Akiwa mwenye furaha hatimaye, sasa Beatriz anafundisha wengine jinsi ya kupata furaha.

Carmen alisali kuhusu pambano lake dhidi ya umaskini. Alikuwa na watoto kumi na mume mlevi, Rafael. “Nilijaribu kuchuma fedha kwa kufua nguo,” akasema Carmen. Lakini zoea la Rafael la kunywa likawa baya zaidi. “Mume wangu alianza kubadilika wakati tu tulipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Tukajifunza juu ya ahadi ya Ufalme—kwamba hivi karibuni Yehova ataondoa umaskini na uonevu ulimwenguni. Hatimaye sala zangu kwa Mungu zikajibiwa!” Kujifunza juu ya njia za Yehova kulimsaidia Rafael aache kunywa, na “[akavaa] utu mpya.” (Waefeso 4:24) Yeye na familia yake waliweza kuboresha maisha yao. Rafael asema hivi: “Ijapokuwa sisi si matajiri, na hatuna nyumba yetu wenyewe, tunapata mahitaji ya msingi, na tuna furaha.”

Wakati Sala Zote Zitakapojibiwa

Je, sala zilikuwa na manufaa yoyote kwa watu hao? Bila shaka! Na je, uliona kwamba katika visa vingi sala zao zilijibiwa wakati mtu fulani kutoka kutaniko la Kikristo alipowasaidia kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu kwa kujifunza Biblia?—Matendo 9:11.

Kwa hiyo, basi, tuna sababu nzuri za kusali. Hivi karibuni, sala kuhusu kuja kwa Ufalme wa Mungu na kufanywa kwa mapenzi yake hapa duniani kama mbinguni itajibiwa. (Mathayo 6:10) Baada ya Mungu kusafisha dunia yetu kwa kuondoa watu wanaompinga, “dunia itajawa na kumjua BWANA.” (Isaya 11:9) Kisha wale wote wanaompenda Yehova watafurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu”—na bila shaka sala zao zitajibiwa.—Waroma 8:18-21.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, unajua ni kwa nini tunapaswa kusali?