Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanya Kazi Katika “Shamba” Kabla ya Mavuno

Kufanya Kazi Katika “Shamba” Kabla ya Mavuno

Kufanya Kazi Katika “Shamba” Kabla ya Mavuno

WANAFUNZI wa Mwalimu Mkuu walishangaa. Yesu alikuwa ametoka tu kusimulia hadithi fupi juu ya ngano na magugu. Ilikuwa mojawapo ya mifano kadhaa aliyozungumzia siku hiyo. Alipomaliza wasikilizaji wengi waliondoka. Lakini wafuasi wake walijua kwamba lazima mifano yake ilikuwa na maana hususa—hasa ule unaohusu ngano na magugu. Walijua kwamba Yesu hakuwa msimuliaji hadithi mwenye kupendeza tu.

Mathayo aripoti kwamba waliuliza hivi: “Tueleze kile kielezi cha magugu katika shamba.” Kwa kujibu, Yesu alifasiri mfano huo, akitabiri uasi-imani mkubwa ambao ungetokea miongoni mwa watu waliodai kuwa wanafunzi wake. (Mathayo 13:24-30, 36-38, 43) Uasi-imani ulitokea na kuenea haraka baada ya kifo cha mtume Yohana. (Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:6-12) Uasi-imani ulienea kote hivi kwamba swali alilouliza Yesu, kwenye Luka 18:8 lilifaa sana: “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?”

Kuwasili kwa Yesu kungeashiria mwanzo wa “mavuno” ya Wakristo wanaofananishwa na ngano. Kungekuwa ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” ulioanza 1914. Kwa hiyo hatupaswi kushangaa kwamba wengine walianza kupendezwa na kweli ya Biblia katika kipindi kilichotangulia mwanzo wa mavuno.—Mathayo 13:39.

Tunapochunguza historia twaona uthibitisho kwamba kuanzia hasa karne ya 15 na kuendelea, watu wengi walianza kupendezwa na kweli, hata miongoni mwa washiriki wengi wa Jumuiya ya Wakristo waliokuwa kama “magugu,” au Wakristo bandia. Biblia na konkodansi za Biblia zilipoanza kupatikana bila kizuizi chochote, watu wenye mioyo minyofu walianza kuchunguza Maandiko kwa makini.

Nuru Yaangaza Zaidi

Miongoni mwa watu hao mwanzoni mwa karne ya 19, kulikuwako Henry Grew (1781-1862), kutoka Birmingham, Uingereza. Alipokuwa na umri wa miaka 13, alisafiri kwa meli pamoja na familia yake kuvuka Atlantiki na kuwasili Marekani Julai 8, 1795. Wakaanza kuishi Providence, Rhode Island. Wazazi wake walimfundisha hatua kwa hatua kuipenda Biblia. Akiwa na umri wa miaka 25 mwaka wa 1807, Grew alialikwa atumikie akiwa pasta wa Kanisa la Baptisti, katika Hartford, Connecticut.

Alichukua madaraka yake ya kufundisha kwa uzito na kujaribu kusaidia wale waliokuwa chini ya utunzaji wake waishi kupatana na Maandiko. Hata hivyo, aliamini kwamba lazima kutaniko libaki safi bila kuchafuliwa na mtu yeyote aliyezoea dhambi kimakusudi. Nyakati fulani, yeye pamoja na watu wengine wenye madaraka katika kanisa, walilazimika kuwafukuza (kuwatenga na ushirika) wale waliofanya uasherati au waliokuwa na mazoea machafu.

Kulikuwa na matatizo mengine kanisani yaliyomsumbua. Walikuwa na watu walioshughulikia mambo ya kifedha ya kanisa na kuongoza nyimbo kwenye ibada ilhali hawakuwa washiriki wa kanisa. Watu hao wangeweza kutoa maoni kuhusu mambo mazito ya kutaniko na hivyo kudhibiti mambo ya kanisa kwa kiasi fulani. Akitegemea kanuni ya kujitenga na ulimwengu, Grew aliamini kwa dhati kwamba ni wanaume waaminifu peke yao wanaopaswa kufanya kazi hizo. (2 Wakorintho 6:14-18; Yakobo 1:27) Kulingana na maoni yake, kuruhusu wasioamini waimbe nyimbo za kumsifu Mungu ni kukufuru. Kwa sababu ya msimamo huo, Henry Grew alikataliwa na kanisa mwaka wa 1811. Washiriki wengine waliokuwa na maoni kama yake walijitenga na kanisa wakati huohuo.

Kujitenga na Jumuiya ya Wakristo

Washiriki wa kikundi hiki, kutia ndani Henry Grew walianza kujifunza Biblia wakiwa na lengo la kupatanisha maisha na matendo yao na shauri la Biblia. Baada ya muda mfupi, funzo lao liliwapa uelewevu zaidi wa Biblia na wakaanza kufunua makosa ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa mfano, mwaka wa 1824, Grew aliandika hati yenye sababu nzuri ya kukanusha Utatu. Ona jinsi kifungu hiki kutoka kwa maandishi yake kinavyopatana na akili: “‘Habari ya siku ile, na saa ile hakuna [mtu] aijuaye, wala malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila BABA.’ [Marko 13:32] Ona hapa tofauti iliyopo kati ya vyeo vya watu hao. Mwanadamu, Malaika, Mwana, Baba. . . . Bwana wetu anatufundisha kwamba ni Baba pekee aliyejua siku hiyo. Lakini hiyo si kweli, ikiwa, kama wengine wanavyodhani, Baba, Neno, na Roho Takatifu ni watu watatu katika Mungu mmoja; kwa kuwa kulingana na hili [fundisho la Utatu,] . . . Mwana aliijua kama vile Baba.”

Grew alifunua unafiki wa makasisi na makamanda wa kijeshi waliojidai kuwa wanamtumikia Kristo. Mwaka wa 1828 alitangaza hivi: “Je, twaweza kuona jambo baya kushinda kumwona Mkristo akitoka katika chumba chake cha faragha, alipokuwa akiwaombea maadui wake, na baada ya hapo kuamrisha jeshi lake litumie silaha kwa ukatili kuua maadui haohao? Kwa upande mmoja, inafurahisha kwamba anafanana na Bwana wake anayekufa; lakini anafanana na nani kwa upande mwingine? Yesu aliwaombea wale waliomwua. Wakristo huwaombea watu na kuua watu haohao.”

Grew aliandika hivi kwa mkazo hata zaidi: “Ni lini tutakapomwamini Mweza Yote anayetuhakikishia kwamba ‘hadhihakiwi?’ Ni lini tutakapoelewa asili, mtazamo, wa ile dini takatifu inayotaka tujiepushe hata na ‘kuonekana tu kwa uovu?’ . . . Je, huko si kumkashifu Mwana wa Mungu, kudhani kwamba dini yake hutaka mtu atende kama malaika kwa upande mmoja, na kumruhusu atende kama roho mwovu kwa upande mwingine?”

Uhai wa Milele Si Jambo la Asili

Katika miaka hiyo wakati ambapo hakukuwa na redio na televisheni, njia mashuhuri ya kueleza maoni ilikuwa kuandika na kugawanya vijitabu. Yapata mwaka wa 1835, Grew aliandika kijitabu cha maana kilichofunua kwamba mafundisho ya kutokufa kwa nafsi na moto wa mateso si ya Kimaandiko. Alihisi kwamba mafundisho hayo yalimkufuru Mungu.

Kijitabu hicho kingekuwa na matokeo makubwa sana. Mwaka wa 1837, George Storrs mwenye umri wa miaka 40 alipata nakala moja kwenye garimoshi. Storrs alikuwa mzaliwa wa Lebanon, New Hampshire, lakini wakati huo alikuwa anaishi Utica, New York.

Alikuwa mhudumu mashuhuri sana katika Kanisa la Methodisti-Episkopali. Aliposoma kijitabu hicho, alivutiwa kuona jinsi hoja nzuri zilivyotolewa kupinga mafundisho ya msingi ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo hakuwa amepata kuyatilia shaka. Hakujua mwandishi wa kijitabu hicho, na alikuja kukutana tu na Henry Grew miaka kadhaa baadaye, mwaka wa 1844, wakati ambapo wote wawili walikuwa wanaishi Philadelphia, Pennsylvania. Hata hivyo, Storrs alichunguza jambo hilo mwenyewe kwa miaka mitatu, na kulizungumzia tu na wahudumu wengine.

Hatimaye, kwa kuwa hakuna mtu aliyeweza kukanusha mambo aliyokuwa akijifunza, George Storrs aliamua kwamba hangeweza kuwa mwaminifu kwa Mungu kama angeendelea kushirikiana na Kanisa la Methodisti. Alijiuzulu mwaka wa 1840 na kuhamia Albany, New York.

Katika masika ya mwanzo-mwanzo wa mwaka wa 1842, kwa muda wa majuma sita, Storrs alitoa mfululizo wa hotuba sita wenye kichwa “Uchunguzi—Je, Waovu Ni Wasioweza Kufa?” Watu walipendezwa sana na hotuba hizo hivi kwamba alizisahihisha na kuzichapisha, na kwa miaka 40 iliyofuata, nakala 200,000 ziligawanywa Marekani na Uingereza. Storrs na Grew walifanya mijadala pamoja kupinga fundisho la kutokufa kwa nafsi. Grew aliendelea kuhubiri kwa bidii hadi alipokufa Agosti 8, 1862, huko Philadelphia.

Muda mfupi tu baada ya Storrs kutoa hotuba zile sita zilizotoka tu kutajwa, alipendezwa na mahubiri ya William Miller, aliyekuwa akitarajia kurudi kwa Kristo kunakoonekana mwaka wa 1843. Kwa miaka miwili hivi, Storrs alijihusisha sana katika kuhubiri ujumbe huo kotekote katika kaskazini-mashariki mwa Marekani. Baada ya 1844, hakuunga mkono tena kuweka tarehe yoyote ya kurudi kwa Kristo, hata hivyo hakupinga wale waliotaka kuchunguza kronolojia. Storrs aliamini kwamba kurudi kwa Kristo kulikuwa karibu na kwamba ilikuwa muhimu Wakristo waendelee kuwa macho kiroho, wakiwa tayari kwa ajili ya siku ya kukaguliwa. Lakini aliacha kushirikiana na kikundi cha Miller kwa sababu kilikubali mafundisho yasiyo ya Kimaandiko, kama vile kutokufa kwa nafsi, kuchomwa kwa ulimwengu, na kwamba wale wanaokufa kabla ya kujifunza hawana tumaini lolote la kuishi milele.

Upendo wa Mungu Ungeongoza Kwenye Nini?

Storrs alichukizwa na wazo la Waadventisti kwamba Mungu atafufua waovu akiwa na kusudi pekee la kuwaua tena. Hakupata uthibitisho wowote katika Maandiko kwamba Mungu angeweza kufanya tendo la aina hiyo lisilo na msingi na la kutaka kulipiza kisasi. Storrs na washiriki wake walishikilia maoni yaliyokuwa kinyume kabisa cha hayo na kukata kauli kwamba waovu hawatafufuliwa kamwe. Ingawa ilikuwa vigumu kwao kueleza maandiko fulani yaliyorejezea ufufuo wa wasio waadilifu, waliona mkataa wao kuwa unapatana zaidi na upendo wa Mungu. Punde si punde wangechukua hatua nyingine ya kuelewa kusudi la Mungu.

Mwaka wa 1870, Storrs akawa mgonjwa sana na hakuweza kufanya kazi kwa miezi kadhaa. Katika kipindi hicho, aliweza kuchunguza upya yote aliyokuwa amejifunza katika miaka yake yote 74. Alikata kauli kwamba alikuwa amekosa kusudi muhimu la Mungu kuhusu wanadamu kama lionyeshwavyo katika agano la Kiabrahamu—kwamba ‘familia zote za dunia zitabarikiwa kwa sababu Abrahamu alisikiliza sauti ya Mungu.’— Mwanzo 22:18; Matendo 3:25.

Jambo hilo lilimpa wazo jipya. Ikiwa “familia zote” zingebarikiwa, je, watu wote hawangehitaji kusikia habari njema? Wangeisikiaje? Je, mamilioni hawakuwa wamekufa tayari? Kwa kuchunguza Maandiko zaidi, alifikia mkataa kwamba kuna vikundi viwili vya watu “waovu” waliokufa: wale waliokataa katakata upendo wa Mungu na wale waliokufa kabla ya kujifunza.

Storrs alifikia mkataa kwamba kikundi cha pili kingehitaji kufufuliwa kutoka kwa wafu na kupewa fursa ya kunufaika na dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu. Wale ambao wangeikubali wangeishi milele duniani. Wale ambao wangeikataa wangeharibiwa. Naam, Storrs aliamini kwamba hakuna mtu ambaye angefufuliwa na Mungu bila kupewa tumaini naye. Hatimaye, hakuna mtu ambaye angekufa kutokana na dhambi ya Adamu isipokuwa Adamu! Lakini namna gani wale wanaoishi wakati wa kurudi kwa Bwana Yesu Kristo? Hatimaye Storrs aliona kwamba kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote ingehitaji kufanywa ili kuwafikia. Hakujua kwa vyovyote jinsi ambavyo kazi hiyo ingefanywa, lakini aliandika hivi kwa imani: “Watu wengi sana, wasipoelewa jinsi jambo fulani linavyopasa kufanywa hulikataa, kana kwamba Mungu hawezi kulifanya kwa sababu hawawezi kuona hatua hiyo.”

George Storrs alikufa Desemba 1879, nyumbani kwake Brooklyn, New York, majengo machache tu kutoka sehemu ambayo ingekuja kuwa kitovu cha kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote aliyokuwa ameitazamia kwa hamu.

Nuru Zaidi Ilihitajiwa

Je, watu kama vile Henry Grew na George Storrs walielewa ile kweli waziwazi kama tunavyoielewa leo? La. Walifahamu pambano lao kama alivyosema Storrs mwaka wa 1847: “Twapaswa kukumbuka kwamba tumetoka tu kwenye enzi za giza za kanisa; na hatutashangaa hata kidogo tukitambua kwamba tunaona mafundisho fulani ya Babiloni kuwa kweli.” Kwa mfano, Grew, alielewa kwamba fidia ilitolewa na Yesu, lakini hakuelewa kwamba ilikuwa “fidia inayolingana,” yaani, uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Yesu uliotolewa badala ya uhai mkamilifu wa kibinadamu uliopotezwa na Adamu. (1 Timotheo 2:6) Pia Henry Grew aliamini kwa makosa kwamba Yesu angerudi na kutawala duniani kwa kuonekana. Hata hivyo, Grew alihangaikia kutakaswa kwa jina la Yehova, jambo ambalo halikuwapendeza watu wengi tangu karne ya pili W.K.

Vivyohivyo, George Storrs hakuelewa kwa usahihi mambo fulani muhimu. Aliweza kutambua mafundisho bandia yaliyofundishwa na makasisi, lakini nyakati fulani alichukua msimamo ulio kinyume kabisa. Kwa mfano, yaonekana baada ya kukasirishwa sana na imani inayokubaliwa na makasisi kuhusu Shetani, Storrs alipinga wazo la kwamba Ibilisi ni mtu halisi. Alikataa Utatu; hata hivyo, hakuwa na uhakika kama roho takatifu ni mtu ama sivyo hadi alipokaribia kufa. Ingawa George Storrs alitarajia kwamba kurudi kwa Kristo hakungeonekana hapo kwanza, hatimaye alifikiri kwamba kungeonekana. Hata hivyo, yaonekana kwamba watu hao wawili walikuwa na moyo mnyoofu na mweupe, na walikaribia kuielewa ile kweli zaidi kuliko watu wengi.

“Shamba” ambalo Yesu alieleza katika ule mfano wa ngano na magugu halikuwa tayari kabisa kuvunwa. (Mathayo 13:38) Grew, Storrs, na wengineo walikuwa wakifanya kazi katika “shamba” ili kulitayarisha kwa ajili ya mavuno.

Charles Taze Russell, aliyeanza kuchapisha gazeti hili mwaka wa 1879, aliandika hivi kuhusu miaka yake ya mapema: “Bwana alitupa misaada mingi ya kujifunza neno Lake; mmojawapo ya misaada hiyo mikubwa ni ndugu yetu mpendwa na mzee, George Storrs ambaye kupitia neno na maandishi alitupa msaada mkubwa sana; lakini hatukutaka kamwe kuwa wafuasi wa wanadamu, hata wawe wazuri na wenye hekima namna gani, bali kuwa ‘Wafuasi wa Mungu kama watoto wapendwa.’” Naam, wanafunzi wa Biblia wenye moyo mweupe walifaidika na jitihada za watu kama vile Grew na Storrs, lakini bado ni jambo la maana kuchunguza Neno la Mungu, Biblia, kuwa chanzo halisi cha ile kweli.—Yohana 17:17.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Mambo Aliyoamini Henry Grew

Jina la Yehova limeshutumiwa, na lahitaji kutakaswa.

Utatu, kutokufa kwa nafsi, na moto wa mateso ni mafundisho bandia.

Lazima kutaniko la Kikristo lijitenge na ulimwengu.

Wakristo hawapaswi kushiriki katika vita vya mataifa.

Wakristo hawako chini ya sheria ya Sabato ya Jumamosi au Jumapili.

Wakristo hawapaswi kujihusisha na vikundi vya siri, kama vile Freemasons.

Hakupaswi kuwa na jamii ya makasisi na ya watu wa kawaida miongoni mwa Wakristo.

Vyeo vya kidini vyatokana na mpinga-Kristo.

Makutaniko yote yanapaswa kuwa na baraza la wazee.

Wazee wanapaswa kuwa watakatifu katika mwenendo wao wote, bila shutuma.

Lazima Wakristo wote wahubiri habari njema.

Kutakuwa na watu watakaoishi milele katika Paradiso duniani.

Nyimbo za Kikristo zapasa kumsifu Yehova na Kristo.

[Hisani]

Picha: Collection of The New-York Historical Society/69288

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

Mambo Aliyoamini George Storrs

Yesu alitoa uhai wake kuwa fidia kwa ajili ya wanadamu.

Habari njema hazijahubiriwa bado (mwaka wa 1871).

Kwa sababu hiyo, mwisho haukuwa karibu wakati huo (mwaka wa 1871). Habari njema zingehubiriwa katika kizazi ambacho kingefuata.

Kutakuwa na watu watakaorithi uhai wa milele duniani.

Kutakuwa na ufufuo wa watu wote waliokufa kabla ya kujifunza. Wale wanaokubali dhabihu ya fidia ya Kristo watapokea uhai wa milele duniani. Wale wanaoikataa wataharibiwa.

Kutokufa kwa nafsi na moto wa mateso ni mafundisho bandia yanayomshushia Mungu heshima.

Mlo wa Jioni wa Bwana ni sherehe ya kila mwaka inayofanywa Nisani 14.

[Hisani]

Picha: SIX SERMONS, by George Storrs (1855)

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mwaka wa 1909, C. T. Russell, mhariri wa “Zion’s Watch Tower,” alihamia Brooklyn, New York, Marekani