Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uwe Mwenye Kujitolea?

Kwa Nini Uwe Mwenye Kujitolea?

Kwa Nini Uwe Mwenye Kujitolea?

Bill ni mwanamume mwenye umri wa miaka 50 hivi, ana familia naye ni mwalimu wa ufundi wa ujenzi. Kwa mwaka mzima, yeye hutumia majuma mengi akisaidia katika kupanga na kujenga Majumba ya Ufalme ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kwa gharama yake mwenyewe. Emma ni mwanamke mseja mwenye umri wa miaka 22 na ameelimika sana na kuhitimu vema. Badala ya kufuatia miradi ya kibinafsi tu, yeye hutumia zaidi ya saa 70 kila mwezi katika huduma, akiwasaidia watu waijue Biblia. Maurice na Betty wamestaafu. Badala ya kuishi maisha ya starehe tu sasa, wamehamia nchi nyingine ili kusaidia watu huko wajifunze kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia.

WATU hao hawajioni kuwa wa pekee au wa ajabu. Wao ni watu wa kawaida tu wanaofanya mambo ambayo wanaona yanafaa. Mbona wao hutumia wakati wao, nguvu zao, uwezo wao mbalimbali, na mali zao kwa ajili ya masilahi ya wengine? Kinachowachochea ni upendo mkubwa kwa Mungu na kwa jirani zao. Upendo huu umechochea roho ya kweli ya kujitolea katika kila mmoja wao.

Tunamaanisha nini tusemapo roho ya kujitolea? Kuwa na roho ya kujitolea hakumaanishi kuishi maisha ya kujinyima kupita kiasi. Si lazima kuhusishe kujinyima sana kunakotufanya tukose shangwe au uradhi. Kama isemavyo kamusi ya The Shorter Oxford English Dictionary, kujitolea humaanisha tu “kutofuatia masilahi, furaha, na tamaa zako mwenyewe ili uwahudumie wengine.”

Yesu Kristo—Mfano Bora

Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, Yesu Kristo, ndiye mfano bora wa mtu aliye na roho ya kujitolea. Katika kuwako kwake kabla ya kuwa mwanadamu, hapana budi maisha yake yalikuwa yenye kuchangamsha na kuridhisha sana. Alikuwa na uhusiano mzuri, wa karibu na Baba yake na pia viumbe wa roho. Zaidi ya hayo, Mwana wa Mungu alitumia uwezo wake katika utendaji mbalimbali wenye kusisimua akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:30, 31) Hapana shaka aliishi katika hali bora sana kuliko hali zozote awezazo kupata hata yule mtu aliye tajiri zaidi duniani. Akiwa wa pili kutoka kwa Yehova Mungu, alikuwa na cheo cha juu na kisicho na kifani huko mbinguni.

Licha ya hayo, Mwana wa Mungu “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu na kuchukua umbo la mtumwa na kuja kuwa katika ufanani wa wanadamu.” (Wafilipi 2:7) Kwa kuja kuwa mwanadamu, aliachilia kwa hiari masilahi yake ya kibinafsi na kutoa uhai wake uwe fidia ili kuondoa madhara ambayo Shetani amesababisha. (Mwanzo 3:1-7; Marko 10:45) Hilo lilimaanisha kuja kuishi miongoni mwa wanadamu wenye dhambi katika ulimwengu ulio chini ya uwezo wa Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Lilimaanisha pia kuvumilia usumbufu ambao ungempata kibinafsi. Hata hivyo, haidhuru ilimgharimu nini, Yesu Kristo aliazimia kufanya mapenzi ya Baba yake. (Mathayo 26:39; Yohana 5:30; 6:38) Hilo lilikuwa jaribu kali sana kwa upendo na uaminifu-mshikamanifu wa Yesu. Alikuwa tayari kujitolea kadiri gani? “Alijinyenyekeza mwenyewe akawa mtiifu hadi kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso,” akasema mtume Paulo.—Wafilipi 2:8.

“Tunzeni Mtazamo Huu wa Akili Ndani Yenu”

Tunatiwa moyo tufuate mfano wa Yesu. “Tunzeni mtazamo huu wa akili ndani yenu uliokuwa pia ndani ya Kristo Yesu,” akasihi Paulo. (Wafilipi 2:5) Twaweza kufanyaje hivyo? Njia moja ni kwa ‘kufuliza kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.’ (Wafilipi 2:4) Upendo wa kweli “hautafuti masilahi yao wenyewe.”—1 Wakorintho 13:5.

Mara nyingi watu wanaojali wamejitolea pasipo ubinafsi ili kuwahudumia wengine. Leo, hata hivyo, watu wengi huelekea kujifikiria wenyewe tu. Ulimwengu una mtazamo wa mimi-kwanza. Twahitaji kujilinda dhidi ya roho ya ulimwengu kwa sababu ikifaulu kuufinyanga mtazamo wetu, yaelekea tutafanya tamaa zetu kuwa mambo ya maana zaidi. Ndipo kila kitu tunachofanya—jinsi tunavyotumia wakati wetu, nguvu zetu, mali zetu—kitatawaliwa na mahangaiko ya ubinafsi. Basi twahitaji kupiga vita vikali dhidi ya uvutano huo.

Hata huenda nyakati nyingine ushauri unaotolewa kwa nia nzuri ukavunja roho yetu ya kujitolea. Mtume Petro alipotambua mahali ambapo mwendo wa kujitolea wa Yesu ulikuwa ukimwongoza, alisema hivi: “Uwe mwenye fadhili kwako mwenyewe, Bwana.” (Mathayo 16:22) Labda alishindwa kukubali utayari wa Yesu wa kujitolea kufa ili kutimiza masilahi ya enzi kuu ya Baba yake na wokovu wa wanadamu. Kwa hiyo akajaribu kumshawishi Yesu asiufuatie mwendo huo.

‘Jikane Mwenyewe’

Yesu aliitikiaje? Masimulizi hayo yasema hivi: “Akageuka, akatazama wanafunzi wake akamkemea Petro, na kusema: ‘Nenda nyuma yangu, Shetani, kwa sababu wewe wafikiri, si fikira za Mungu, bali [zile za] wanadamu.’” Kisha Yesu akauita umati na wanafunzi wake na kusema: “Ikiwa yeyote ataka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso na kunifuata kwa kuendelea.”—Marko 8:33, 34.

Miaka 30 hivi baada ya kumpa Yesu ushauri huo, Petro alionyesha kwamba tayari alikuwa ameelewa maana ya kujitolea. Hakuwatia moyo waamini wenzake wastarehe tu na kujitendea kwa fadhili. Badala yake, Petro aliwahimiza wakaze akili zao kwa utendaji na wakome kufanyizwa kulingana na tamaa zao za awali za kilimwengu. Licha ya majaribu,walipaswa kutangulizautendaji wamapenziyaMungu maishani mwao.—1 Petro 1:6, 13, 14; 4:1, 2.

Mwendo wenye thawabu zaidi ambao yeyote kati yetu aweza kuufuatia ni kujikabidhi wenyewe kwa Yehova, tukimfuata Yesu Kristo kwa uaminifu na kumruhusu Mungu aelekeze utendaji wetu. Kuhusu mambo hayo, Paulo aliweka mfano mzuri. Hisi yake ya uharaka na shukrani yake kwa Yehova zilimchochea aachilie mbali miradi au matazamio ya kilimwengu ambayo yangemkengeusha asifanye mapenzi ya Mungu. “Kwa upande wangu,” yeye akasema, “hakika mimi nitatumia kwa mteremo zaidi sana na kutumiwa kabisa” katika kuhudumia masilahi ya wengine. (2 Wakorintho 12:15) Paulo alitumia uwezo wake mbalimbali kuendeleza masilahi ya Mungu, wala si yake binafsi.—Matendo 20:24; Wafilipi 3:8.

Twaweza kujichunguzaje wenyewe ili tuone kama tuna mtazamo kama ule wa mtume Paulo? Huenda tukajiuliza maswali haya: Mimi hutumiaje wakati wangu, nguvu zangu, uwezo wangu mbalimbali, na mali zangu? Je, mimi huvitumia vitu hivyo pamoja na vipawa vingine vyenye thamani ili kuendeleza masilahi yangu binafsi, au mimi huvitumia kuwasaidia wengine? Je, nimefikiria kuishiriki kikamilifu kazi iokoayo uhai ya kutangaza habari njema, labda nikiwa mhubiri wa Ufalme wa wakati wote? Je, naweza kushiriki kikamilifu zaidi katika utendaji kama vile ujenzi na udumishaji wa Majumba ya Ufalme? Je, mimi hutumia nafasi kuwasaidia wenye uhitaji? Je, mimi humpa Yehova yaliyo bora?—Mithali 3:9.

“Furaha Zaidi Katika Kutoa”

Lakini je, kujitolea ni jambo la hekima kweli? Ndiyo! Paulo alijionea mwenyewe kwamba roho ya aina hiyo huleta thawabu tele. Ilimpa furaha nyingi na kumridhisha sana. Aliwaeleza wanaume wazee kutoka Efeso mambo hayo alipokutana nao kule Mileto. Paulo akasema: “Nimewaonyesha wazi nyinyi katika mambo yote kwamba kwa kufanya kazi ya jasho hivyo [kwa njia ya kujitolea] ni lazima msaidie wale walio dhaifu, na lazima mzingatie akilini maneno ya Bwana Yesu, wakati yeye mwenyewe aliposema, ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.’” (Matendo 20:35) Mamilioni ya watu wamegundua kwamba kuonyesha roho ya aina hiyo huleta furaha nyingi leo. Pia italeta shangwe wakati ujao Yehova atakapowapa thawabu wale wanaotanguliza masilahi yake na yale ya wengine kabla ya masilahi yao binafsi.—1 Timotheo 4:8-10.

Alipoulizwa sababu ya kujitahidi sana kusaidia wengine kujenga Majumba ya Ufalme, Bill alieleza hivi: “Kuyasaidia makutaniko madogo kwa njia hiyo huniridhisha sana. Napata uradhi ninapotumia stadi na ujuzi wowote nilio nao kwa faida ya wengine.” Kwa nini Emma ameamua kutumia nguvu zake na uwezo wake mbalimbali ili kuwasaidia wengine wajifunze kweli ya Kimaandiko? “Sikuwazia kufanya jambo jingine lolote. Nataka nifanye kadiri niwezavyo ili kumpendeza Yehova na kuwasaidia wengine wakati ningali mchanga na bado nina uwezo. Kujinyima mambo fulani ya kimwili si jambo kubwa. Ninafanya tu wajibu wangu kwa kuzingatia yale ambayo Yehova amenifanyia.”

Maurice na Betty hawajuti kamwe kwa kujiepusha na maisha ya starehe baada ya miaka mingi ya kazi ngumu ya kulea na kukidhi familia yao. Kwa vile sasa wamestaafu, wanataka kuendelea kutumia maisha yao kufanya jambo lenye manufaa na maana. “Hatutaki kupumzika na kustarehe tu sasa,” wanasema. “Kusaidia wengine wajifunze juu ya Yehova katika nchi ya kigeni hutupa nafasi ya kuendelea kufanya jambo lenye kusudi.”

Je, umeazimia kuwa mwenye kujitolea? Kujitolea si rahisi. Sikuzote kuna pambano baina ya tamaa zetu za kibinadamu zisizo kamilifu na tamaa yetu nzuri ya kutaka kumpendeza Mungu. (Waroma 7:21-23) Lakini twaweza kushinda pambano hilo tukimruhusu Yehova aongoze maisha yetu. (Wagalatia 5:16, 17) Hapana shaka atakumbuka kazi yetu ya kujitolea katika utumishi wake naye atatubariki sana. Kwa kweli, Yehova Mungu ‘atayafungua madirisha ya mbinguni, na kutumwagia baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.’—Malaki 3:10; Waebrania 6:10.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yesu alikuwa na roho ya kujitolea. Vipi wewe?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Paulo alitumia nguvu zake katika kazi ya kuhubiri Ufalme