Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unafanyaje Kunapotokea Kutoelewana?

Unafanyaje Kunapotokea Kutoelewana?

Unafanyaje Kunapotokea Kutoelewana?

SISI hushughulika kila siku na watu wenye nyutu mbalimbali. Mara nyingi hilo hutuletea furaha na maoni mapya. Nyakati nyingine hilo pia hutokeza ukosefu wa maelewano, mengine makubwa ilhali mengine ni mikwaruzano midogomidogo tu katika maisha yetu ya kila siku. Hata kutoelewana kwetu kuweje, jinsi tunavyokushughulikia hutuathiri kiakili, kihisia-moyo, na kiroho.

Kufanya kadiri tuwezavyo ili kutatua kutoelewana kwa njia nzuri kutatusaidia kuishi maisha yenye afya zaidi na kuwa na mahusiano yenye amani zaidi na wengine. Mithali moja ya kale yasema hivi: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili.”—Mithali 14:30.

Kinyume kabisa cha andiko lililo juu ni ukweli wa maneno haya: “Asiyetawala roho yake ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.” (Mithali 25:28) Ni nani kati yetu angependa kutawaliwa na mawazo mabaya yanayoweza kufanya atende kwa njia zisizofaa—njia ziwezazo kutudhuru na kudhuru wengine? Majibu ya hasira, yasiyodhibitiwa yaweza kusababisha mambo hayo. Kwenye Mahubiri ya Mlimani, Yesu alipendekeza kwamba tuuchunguze mtazamo wetu, ambao waweza kuathiri jinsi tunavyotatua hali zozote za kutoelewana ziwezazo kutokea kati yetu na wengine. (Mathayo 7:3-5) Badala ya kuwachambua wengine, ni vema tufikirie jinsi tuwezavyo kusitawisha na kudumisha urafiki pamoja na wale wenye maoni na malezi tofauti.

Mtazamo Wetu

Hatua ya kwanza ya kutatua hitilafu iliyopo au inayodhaniwa ipo ni kutambua kwamba ni rahisi kuwe na fikira na mitazamo mibaya. Maandiko yatukumbusha kuwa sote hufanya dhambi “na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Zaidi ya hayo, huenda ufahamu ukafunua kwamba sisi ndio chanzo cha tatizo. Hebu tuyachunguze yaliyompata Yona kwa habari hiyo.

Yehova alimwagiza Yona aende mjini Ninawi kuhubiri hukumu ya Mungu iliyokuwa inakaribia juu ya wakazi wake. Matokeo yakawa kwamba mji mzima wa Ninawi ulitubu na kumwamini Mungu wa kweli. (Yona 3:5-10) Yehova aliona kwamba mtazamo wao wenye toba uliwastahilisha kusamehewa, basi hakuwaangamiza. “Lakini jambo hili lilimchukiza Yona sana, naye akakasirika.” (Yona 4:1) Itikio la Yona kwa rehema ya Yehova lilishangaza. Mbona Yona amkasirikie Yehova? Yaonekana kwamba Yona alizingatia sana maoni yake mwenyewe, akaona kuwa ameaibika katika jumuiya. Hakutambua rehema ya Yehova. Kwa fadhili, Yehova alimfundisha Yona kupitia mambo yaliyompata ambayo yalimsaidia kubadili mtazamo wake na kuona thamani bora ya rehema ya Mungu. (Yona 4:7-11) Ni wazi kwamba mtazamo wa Yona, wala si wa Yehova, ndio uliohitaji kubadilishwa.

Je, nyakati nyingine sisi pia huhitaji kubadili mtazamo wetu kuhusu jambo fulani? Mtume Paulo atushauri hivi: “Katika kuonyeshana heshima iweni wenye kuongoza.” (Waroma 12:10) Alimaanisha nini? Kwa upande mmoja, anatutia moyo tuwe wenye kusababu na kuwatendea Wakristo wengine kwa heshima na adhama. Hiyo yamaanisha kutambua kwamba kila mtu ana pendeleo la kufanya maamuzi yake. Paulo pia atukumbusha: “Kila mmoja atachukua mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5) Basi, kabla kutoelewana hakujasababisha mgawanyiko, ni jambo la hekima kama nini kuona kama twahitaji kubadili mtazamo wetu! Lazima tujitahidi sana kudhihirisha maoni ya Yehova na kudumisha amani na wengine wanaompenda Mungu kikweli.—Isaya 55:8, 9.

Mfikio Wetu

Hebu wazia watoto wawili waking’ang’ania mwanasesere mmoja, huku kila mmoja akimvuta kwa nguvu. Huenda wakatukanana kwa hasira hadi mmoja anapoachilia au mtu mwingine aingilie.

Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yatuambia kuwa Abrahamu alisikia kwamba mabishano yametokea kati ya wachungaji wake na wa Loti mpwa wake. Abrahamu alichukua hatua ya kwanza kumfikia Loti na kusema: “Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu.” Abrahamu aliazimia kutoruhusu ugomvi wowote uharibu uhusiano wao. Kwa hasara gani? Alikuwa tayari kuachilia pendeleo lake la kuchagua japo yeye ndiye aliyekuwa na umri mkubwa zaidi; alikuwa tayari kuachilia jambo fulani. Abrahamu alimruhusu Loti ajichagulie alikotaka kwenda pamoja na familia na mifugo yake. Basi Loti akajichagulia eneo lenye malisho mema la Sodoma na Gomora. Abrahamu na Loti wakaachana kwa amani.—Mwanzo 13:5-12.

Ili kudumisha mahusiano ya amani na wengine, je, tuko tayari kutenda kama Abrahamu? Kisa hicho cha Biblia ni kigezo bora cha kuiga tunapotatua kutoelewana. Abrahamu alisihi hivi: “Usiwepo ugomvi.” Abrahamu alitamani kikweli kupata suluhisho la amani. Kwa hakika usemi huo wa kuendeleza mahusiano ya amani waweza kutusaidia kuachilia mbali kutoelewana kwokwote. Kisha Abrahamu akahitimisha kwa kusema “maana sisi tu ndugu.” Mbona aharibu uhusiano bora kwa sababu tu ya mapendezi ya kibinafsi au kiburi? Abrahamu alizingatia kabisa jambo muhimu. Alifanya hivyo kwa kujiheshimu na kujistahi, naye akamheshimu mpwa wake vilevile.

Ingawa nyakati nyingine huenda kukahitajika msaada wa watu wengine ili kutatua hali fulani ya kutoelewana, ni jambo bora kama nini kutatua tatizo faraghani! Yesu atutia moyo tuwe wa kwanza kufanya amani na ndugu yetu, na kuomba msamaha ikihitajika. * (Mathayo 5:23, 24) Itahitaji tuwe wanyenyekevu, au tuwe na hali ya akili ya kujishusha chini. Petro aliandika hivi: “Jifungeni hali ya akili ya kujishusha chini kuelekea mtu na mwenzake, kwa sababu Mungu hupinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.” (1 Petro 5:5) Jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu huathiri moja kwa moja uhusiano wetu na Mungu.—1 Yohana 4:20.

Huenda tukahitajika kuachilia haki fulani ili kudumisha amani katika kutaniko la Kikristo. Wengi ambao sasa wanashirikiana na Mashahidi wa Yehova wamejiunga na familia ya waabudu wa kweli wa Mungu katika miaka mitano iliyopita. Hilo latufurahisha kama nini! Kwa hakika, namna tunavyojiendesha huwaathiri wao pamoja na wengine kutanikoni. Hiyo ni sababu nzuri ya kufikiria kwa makini uchaguzi wetu wa vitumbuizo, hobi, vikusanyiko vya kijamii, au kazi ya kuajiriwa, tukizingatia jinsi wengine wanavyotuona. Je, baadhi ya matendo na maneno yetu yaweza kueleweka vibaya na hivyo yawakwaze wengine?

Mtume Paulo atukumbusha hivi: “Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yenye faida. Mambo yote yaruhusika kisheria; lakini si mambo yote yajengayo. Acheni kila mmoja afulize kutafuta sana, si faida yake mwenyewe, bali ya mtu yule mwingine.” (1 Wakorintho 10:23, 24) Tukiwa Wakristo, tunahangaikia kikweli kujenga upendo na umoja wa udugu wa Kikristo.—Zaburi 133:1; Yohana 13:34, 35.

Maneno Yanayoponya

Maneno yaweza kuleta matokeo mema sana. “Maneno yapendezayo ni kama sega la asali; ni tamu nafsini, na afya mifupani.” (Mithali 16:24) Simulizi la jinsi Gideoni alivyoepuka pambano ambalo lingeweza kutokea kati yake na Waefraimu huonyesha ukweli wa mithali hiyo.

Gideoni, aliyekuwa akipigana vikali na Wamidiani, aliwaita Waefraimu wamsaidie. Hata hivyo, baada ya vita, Waefraimu walimgeuka Gideoni na kulalamika kwamba hakuwaita mwanzoni mwa vita. Masimulizi yasema kwamba ‘waliteta naye sana.’ Gideoni akawajibu hivi: “Je! mimi nimefanya nini sasa kama mlivyofanya ninyi? Hayo masazo ya zabibu za Efraimu si mema kuliko mavuno ya Abiezeri? Mungu amewatia hao wakuu wa Midiani, Orebu na Zeebu, mikononi mwenu; na mimi nilipata kufanya nini kama mlivyofanya ninyi?” (Waamuzi 8:1-3) Kwa maneno yake yaliyoteuliwa vizuri na yenye kutuliza, Gideoni aliepuka jambo ambalo lingekuwa vita vikali kati ya makabila. Huenda watu wa kabila la Efraimu walikuwa wenye majivuno na kiburi. Hata hivyo, hilo halikumzuia Gideoni asijitahidi kupata suluhisho la amani. Je, nasi twaweza kufanya hivyo?

Huenda wengine wakapandwa na hasira na kuwa wakali kwetu. Tambua hisia zao, na ujitahidi kuelewa maoni yao. Je, labda tumechangia hisia zao kwa njia fulani? Ikiwa ndiyo, basi na tukubali kwamba tulichangia tatizo hilo na tuombe msamaha kwa sababu ya kulizidisha. Maneno machache yaliyoteuliwa vizuri yaweza kurudisha uhusiano ulioharibika. (Yakobo 3:4) Wengine ambao wameudhika huenda wakataka tu tuwape uhakikishio kwa fadhili. Biblia yasema kuwa “moto hufa kwa kukosa kuni.” (Mithali 26:20) Naam, maneno yaliyoteuliwa vizuri na kusemwa kwa roho nzuri yaweza ‘kugeuza hasira’ na kuponya.—Mithali 15:1.

Mtume Paulo apendekeza hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” (Waroma 12:18) Ni kweli kwamba hatuwezi kudhibiti hisia za wengine, lakini twaweza kutimiza wajibu wetu ili kuendeleza amani. Badala ya kutawaliwa na maelekeo yetu yasiyo makamilifu au yale ya wengine, twaweza kuchukua hatua sasa ili kutumia kanuni imara za Biblia. Kutatua kutoelewana kama Yehova anavyotuagiza kutatupatia amani na furaha ya milele.—Isaya 48:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ona makala “Samehe Kutoka Katika Moyo Wako” na “Unaweza Kumpata Ndugu Yako,” katika Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1999.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, sisi hung’ang’ania mambo yafanywe kwa njia yetu wenyewe?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Abrahamu aliweka mfano mzuri wa kuachilia mambo ili kutatua kutoelewana