Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Ifanyayo Wanadamu Wahitaji Msaidiaji

Sababu Ifanyayo Wanadamu Wahitaji Msaidiaji

Sababu Ifanyayo Wanadamu Wahitaji Msaidiaji

‘MIMI nilikuwa mnyanyasaji fidhuli,’ akakiri mtu mmoja aliyekuwa mwenye kiburi na mwenye ujeuri hapo awali. Alikuwa mkufuru mwenye matukano aliyewanyanyasa na kuwashambulia kikatili wafuasi wa Yesu Kristo wenye kumcha Mungu. “Hata hivyo,” akasema kwa shukrani, “nilionyeshwa rehema.” Amini usiamini, mnyanyasaji huyu mkatili akawa yule mtume Mkristo mwaminifu, Paulo.—1 Timotheo 1:12-16; Matendo 9:1-19.

Si kila mtu ambaye amefanya mambo kama yale aliyofanya Paulo. Lakini sisi sote hushindwa kufikia viwango vya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Isitoshe, ni rahisi sana kukata tamaa, labda tukihisi kwamba sisi ni wabaya sana tusiweze kupokea rehema ya Mungu. Alipotafakari mielekeo yake yenye dhambi, Paulo mwenyewe alisema hivi: “Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” Alijibu swali lake mwenyewe kwa kuandika: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!”—Waroma 7:24, 25.

Muumba mwadilifu anaweza kushughulikaje na watenda-dhambi? (Zaburi 5:4) Ona kwamba Paulo alisema: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu.” Mwingine aliyepokea rehema ya Mungu alieleza: “Ikiwa yeyote afanya hasa dhambi, tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo, aliye mwadilifu. Na yeye ni dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.”—1 Yohana 2:1, 2.

Kwa nini Yesu Kristo anaitwa “msaidiaji kwa Baba”? Na ni kwa njia gani Yesu ni “dhabihu yenye kufunika” kwa ajili ya dhambi?

Sababu Ifanyayo Msaidiaji Ahitajiwe

Yesu alikuja duniani “kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.” (Mathayo 20:28) Fidia ni bei inayolipwa kununua tena, au kusababisha kuachiliwa kwa mtu au kitu. Aina ya kitenzi cha neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fidia” latoa wazo la kufunika dhambi. (Zaburi 78:38) Neno la Kigiriki, kama lile lipatikanalo kwenye Mathayo 20:28, lilitumiwa hasa kurejezea bei iliyolipwa kuwafidi wafungwa wa vita au kuwaachilia watumwa. Ili kutimiza matakwa ya haki, kitu kimoja hutolewa kubadilishana na kingine cha thamani hiyohiyo.

Wanadamu walipata kuwa watumwa kwa sababu mtu wa kwanza alimwasi Mungu. Kama ionyeshwavyo katika Mwanzo sura ya 3, mtu mkamilifu—Adamu—alichagua kutotii Yehova Mungu. Kwa kufanya hivyo, akajiuza na kuuza wazao wake wasiozaliwa bado katika utumwa wa dhambi na kifo. Hivyo, Adamu akapoteza zawadi ya uhai mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili yake mwenyewe na wazao wake wote.—Waroma 5:12, 18, 19; 7:14.

Katika Israeli la kale, Mungu alipanga dhabihu za wanyama zitolewe ili kufunika dhambi za watu. (Mambo ya Walawi 1:4; 4:20, 35) Kwa kweli, uhai wa mnyama wa dhabihu ulitolewa badala ya ule wa mtenda-dhambi. (Mambo ya Walawi 17:11) Hivyo, “siku ya kufunika” ingeweza pia kurejezewa kuwa “siku ya fidia.”—Mambo ya Walawi 23:26-28, NW.

Hata hivyo, kwa kuwa wanyama ni wa hali ya chini wakilinganishwa na mwanadamu, ‘haingewezekana damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi [kabisa].’ (Waebrania 10:1-4) Ili dhabihu iwe na thamani inayotosha kufunika au kuondoa dhambi kabisa, ingepaswa kuwa na thamani sawa na kile alichopoteza Adamu. Haki inadai kwamba mtu mkamilifu (Yesu Kristo) asawazishe kile ambacho mtu mwingine mkamilifu (Adamu) alipoteza. Uhai mkamilifu wa kibinadamu tu ndio ungeweza kulipia bei ya fidia ya kukomboa uzao wa Adamu kutoka katika utumwa ambao baba yao wa kwanza aliwauza. Kutoza ‘uhai kwa uhai’ kungetimiza matakwa ya haki ya kweli.—Kutoka 21:23-25.

Adamu alipofanya dhambi na kuhukumiwa kifo, wazao wake wasiozaliwa bado walikuwa kiunoni mwake na hivyo wakafa naye. Kwa hiari, yule mtu mkamilifu Yesu, “Adamu wa mwisho,” hakupata watoto. (1 Wakorintho 15:45) Alikuwa na watoto wasiozaliwa bado kwenye kiuno alipokufa akiwa dhabihu kamilifu ya kibinadamu. Kwa hiyo, inaweza kusemwa kwamba jamii ya kibinadamu ambayo ingeweza kutoka kiunoni mwake ilikufa pamoja naye. Yesu aliichukua familia ya Adamu, yenye dhambi na yenye kufa, iwe yake mwenyewe. Alijinyima haki ya kuwa na familia yake mwenyewe. Kwa kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe dhabihu, Yesu aliwanunua wazao wote wa Adamu ili wawe familia Yake, wakimfanya Yesu kuwa ‘Baba yao wa milele.’—Isaya 9:6, 7.

Dhabihu ya fidia ya Yesu iliwawezesha wanadamu watiifu kupata rehema ya Mungu na uhai udumuo milele. Hivyo, mtume Paulo aliandika: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Tunachochewa kumsifu Yehova kwa upendo na huruma zinazohusiana na fidia ambayo yeye na Mwana wake ampendaye sana waliitoa kwa gharama kubwa sana. (Yohana 3:16) Na kwa kweli Yesu alikuwa “msaidiaji kwa Baba” alipofufuliwa kwenye uhai wa mbinguni na kuwasilisha thamani ya dhabihu yake ya fidia kwa Mungu mbinguni. * (Waebrania 9:11, 12, 24; 1 Petro 3:18) Lakini Yesu Kristo amekuwaje msaidiaji wetu mbinguni?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Ona sura ya 4 na ya 7 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Uhai mkamilifu wa Yesu ulipata kuwa bei ya kufidi wazao wa Adamu