Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Yehova Anavyotuongoza

Jinsi Yehova Anavyotuongoza

Jinsi Yehova Anavyotuongoza

‘Uniongoze katika njia iliyonyoka.’—ZABURI 27:11.

1, 2. (a) Yehova anawaongozaje watu wake leo? (b) Kunufaika kikamili na mikutano kwahusisha nini?

KAMA tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, Yehova ndiye Chanzo cha nuru na kweli. Neno lake hutuangazia tutembeapo kwenye njia iliyonyoka. Yehova hutuongoza kwa kutufundisha njia zake. (Zaburi 119:105) Kama mtunga-zaburi wa kale, sisi hufuata kwa shukrani miongozo ya Mungu na kusali: “Ee BWANA, unifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia iliyonyoka.”—Zaburi 27:11.

2 Njia mojawapo ambayo Yehova hutumia kutufundisha leo ni mikutano ya Kikristo. Je, sisi hunufaika kikamili na uandalizi huo wenye upendo kwa (1) kuhudhuria kwa ukawaida, (2) kusikiliza programu kwa makini, na (3) kushiriki kwa utayari katika sehemu zinazohusisha wasikilizaji? Na zaidi, je, sisi hushukuru tunapopokea madokezo ambayo yatatuwezesha kubaki “katika njia iliyonyoka”?

Unahudhuriaje Mikutano?

3. Mtumishi mmoja wa wakati wote alikuzaje mazoea mazuri ya kuhudhuria mikutano kwa ukawaida?

3 Wahubiri wengine wa Ufalme wamekuwa wakihudhuria mikutano kwa ukawaida tangu utotoni. “Mimi na dada zangu tulipokuwa tukikua katika miaka ya 1930,” akumbuka mhudumu mmoja wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, “hatukuwa tukiwauliza wazazi wetu kama tutaenda mkutano. Tulijua tunaenda ila tu tuwe wagonjwa. Familia yetu haikuwa ikikosa mikutano.” Kama nabii wa kike Ana, dada huyu ‘hakukosa kamwe’ penye ibada ya Yehova.—Luka 2:36, 37.

4-6. (a) Kwa nini wahubiri wengine wa Ufalme hukosa mikutano? (b) Kwa nini ni muhimu sana kuhudhuria mikutano?

4 Je, wewe ni mmojawapo wa wale wanaohudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, ama wewe si wa kawaida? Wakristo fulani waliofikiri kwamba wanafanya vizuri waliamua kuhakikisha jambo hilo. Kwa majuma kadhaa, waliandika kila mkutano waliohudhuria. Walipopitia maandishi hayo baada ya kipindi fulani walichokuwa wameweka, walishangaa kuona ni mikutano mingapi waliyokuwa wamekosa.

5 ‘Si ajabu,’ huenda mtu akasema. ‘Watu wana mikazo mingi sana leo hivi kwamba si rahisi wahudhurie mikutano kwa ukawaida.’ Ni kweli kwamba twaishi katika nyakati zenye mikazo. Na bila shaka mikazo hiyo itaongezeka. (2 Timotheo 3:13) Lakini, je, hali hiyo haifanyi iwe muhimu hata zaidi kuhudhuria mikutano kwa ukawaida? Bila lishe ya daima ya chakula kifaacho cha kiroho cha kutuendeleza, hatuwezi kutumaini kushinda mikazo ya mfumo huu. Kwani, bila kushirikiana kwa ukawaida tunaweza kushawishika kuacha “njia iliyonyoka”! (Mithali 4:18) Ni kweli kwamba tunapofika nyumbani baada ya siku ngumu, huenda nyakati nyingine tusijisikie kuhudhuria mkutano. Hata hivyo, tunapohudhuria japo tumechoka, tunanufaika na kuwatia moyo Wakristo wenzetu kwenye Jumba la Ufalme.

6 Andiko la Waebrania 10:25 ladokeza sababu nyingine muhimu inayofanya tuhudhurie mikutano kwa ukawaida. Katika andiko hilo mtume Paulo awahimiza Wakristo wenzake wakusanyike pamoja ‘zaidi sana kwa kadiri waonavyo siku ikikaribia.’ Ndiyo, hatupaswi kusahau kwamba “siku ya Yehova” inakaribia. (2 Petro 3:12) Tukikata kauli ya kwamba mwisho wa mfumo huu uko mbali sana, huenda tukaanza kufuatia mambo ya kibinafsi na kuacha utendaji muhimu wa kiroho, kama vile kuhudhuria mikutano. Kisha, kama alivyoonya Yesu, ‘kwa ghafula siku hiyo iwe juu yetu mara hiyo.’—Luka 21:34.

Sikiliza kwa Makini

7. Kwa nini ni muhimu watoto wasikilize kwenye mikutano?

7 Haitoshi tu kuhudhuria mikutano. Ni lazima tusikilize kwa makini mambo yasemwayo huko. (Mithali 7:24) Jambo hili lawahusu watoto wetu pia. Mtoto anapoenda shuleni, inatarajiwa amsikilize mwalimu, hata kama hapendi somo fulani au kama inaonekana haelewi somo hilo. Mwalimu ajua kwamba mtoto huyo akijaribu kusikiliza, angalau atapata manufaa fulani kutokana na somo hilo. Basi, je, si jambo linalopatana na akili kwa watoto wenye umri wa kwenda shuleni kusikiliza mafundisho kwenye mikutano ya kutaniko badala ya kuachiliwa kulala usingizi mara tu mikutano inapoanza? Ni kweli kwamba baadhi ya kweli zenye thamani katika Maandiko ni “mambo fulani magumu kuelewa.” (2 Petro 3:16) Lakini tusipuuze uwezo wa mtoto kujifunza. Mungu haupuuzi. Katika nyakati za Biblia, aliwaamuru watumishi wake wachanga ‘wasikie na kujifunza na kumcha BWANA, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii,’ ambayo bila shaka ilikuwa na sehemu zilizokuwa ngumu kwa watoto kuelewa. (Kumbukumbu la Torati 31:12; linganisha Mambo ya Walawi 18:1-30.) Je, Yehova hatarajii watoto wetu wafanye vivyo hivyo leo?

8. Wazazi wengine huchukua hatua zipi ili kuwasaidia watoto wao wawe wasikivu kwenye mikutano?

8 Wazazi Wakristo hutambua kwamba mahitaji fulani ya kiroho ya watoto wao hutoshelezwa na yale wanayojifunza kwenye mikutano. Kwa hiyo, wazazi wengine hupanga watoto wao walale usingizi kwa muda mfupi kabla ya kwenda mikutanoni ili wafike kwenye Jumba la Ufalme wakiwa wamepumzika na tayari kujifunza. Wazazi wengine wanaweza kuzuia kabisa au kuwakataza kwa hekima watoto wao wasitazame televisheni jioni ambayo kuna mkutano. (Waefeso 5:15, 16) Na wazazi kama hao hufanya watoto wasikengeushwe, wakiwatia moyo wasikilize na kujifunza, kulingana na umri wao na uwezo wao.—Mithali 8:32.

9. Ni nini kiwezacho kutusaidia kukuza uwezo wetu wa kusikiliza?

9 Yesu alikuwa akizungumza na watu wazima aliposema: “Kazieni uangalifu jinsi msikilizavyo.” (Luka 8:18) Jambo hilo si rahisi siku hizi. Ni kweli kwamba ni kazi ngumu kusikiliza kwa makini, lakini tunaweza kukuza uwezo wa kusikiliza. Usikilizapo hotuba inayotegemea Biblia au sehemu fulani ya mkutano, jaribu kutambua mambo makuu. Fikiria jambo ambalo msemaji atafuatia kusema. Jaribu kutafuta mambo uwezayo kutumia katika huduma yako au kutumia maishani. Pitia akilini mambo hayo yanapozungumziwa. Andika mambo mafupi.

10, 11. Wazazi wengine wamewasaidiaje watoto wao wawe wasikivu zaidi, na ni njia zipi ambazo wewe umeona kuwa zenye msaada?

10 Mazoea mazuri ya kusikiliza hukuzwa kwa njia bora wakati wa utoto. Hata kabla hawajajifunza kusoma na kuandika, watoto fulani ambao hawajaanza kwenda shuleni hutiwa moyo na wazazi wao “kuandika” wakati wa mikutano. Wao hutia alama fulani kwenye karatasi wakati maneno ya kawaida kama “Yehova,” “Yesu,” au “Ufalme” yanapotumiwa. Kwa njia hiyo, watoto wanaweza kuwa makini kusikiliza yale yanayosemwa jukwaani.

11 Nyakati nyingine hata watoto wakubwa huhitaji kutiwa moyo wasikilize. Baba mmoja alipotambua kwamba mawazo ya mwana wake mwenye umri wa miaka 11 yalikuwa mbali wakati wa mkusanyiko wa Kikristo, alimpa Biblia na kumwambia afungue maandiko yaliyokuwa yakitajwa na wasemaji. Baba yake, aliyekuwa akiandika mambo makuu, alikuwa akimtazama mwana wake akitumia Biblia hiyo. Basi, mwana huyo akafuata programu ya mkusanyiko kwa shauku zaidi.

Toa Maelezo

12, 13. Kwa nini ni muhimu kushiriki kuimba kutanikoni?

12 Mfalme Daudi aliimba: ‘Nitaizunguka madhabahu yako, Ee BWANA, ili niitangaze sauti ya kushukuru.’ (Zaburi 26:6, 7) Mikutano ya Mashahidi wa Yehova hutuandalia fursa bora za kutangaza imani yetu kwa sauti. Njia mojawapo ya kufanya hivyo ni kuimba pamoja kutanikoni. Hiyo ni sehemu muhimu ya ibada yetu, lakini inaweza kupuuzwa kwa urahisi.

13 Watoto wengine ambao bado hawajui kusoma hukariri maneno ya nyimbo za Ufalme zitakazoimbwa kwenye mikutano kila juma. Wao husisimka kuweza kuimba pamoja na watu wazima. Lakini, watoto waendeleapo kukua kidogo huenda wasipende sana kuimba nyimbo za Ufalme pamoja na wengine. Pia watu wazima wengine husita kuimba kwenye mikutano. Lakini kuimba ni sehemu ya ibada yetu, kama tu huduma ya shambani ilivyo sehemu ya ibada yetu. (Waefeso 5:19) Sisi hujitahidi sana kumsifu Yehova katika huduma ya shambani. Je, hatuwezi pia kumtukuza kwa kuimba kwa sauti—iwe tamu au la—nyimbo za sifa kwa hisia za moyoni?—Waebrania 13:15.

14. Kwa nini habari tunazojifunza kwenye mikutano ya kutaniko zinahitaji kutayarishwa vizuri mapema?

14 Sisi pia humsifu Mungu tunapotoa maelezo yenye kujenga katika sehemu za mikutano zinazohitaji wasikilizaji washiriki. Hilo lataka matayarisho. Inachukua muda kutafakari mambo ya ndani ya Neno la Mungu. Mtume Paulo, ambaye alikuwa msomaji mwenye bidii wa Maandiko, alitambua jambo hilo. Aliandika: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!” (Waroma 11:33) Enyi vichwa vya familia, ni muhimu kusaidia kila mmoja katika familia yenu atafute hekima ya Mungu kama inavyofunuliwa katika Maandiko. Tenga wakati fulani wakati wa funzo la Biblia la familia kueleza mambo magumu na kusaidia familia yako kujitayarishia mikutano.

15. Ni madokezo gani yanayoweza kumsaidia mtu atoe maelezo kwenye mikutano?

15 Kama ungependa kutoa maelezo mara nyingi kwenye mikutano, mbona usitayarishe mapema jambo unalotaka kusema? Si lazima ueleze mambo mengi. Andiko lifaalo la Biblia lisomwalo kwa usadikisho au maneno machache yaliyochaguliwa vizuri na yanayotoka moyoni yathaminiwa. Wahubiri wengine humwomba kiongozi wa funzo awape nafasi ya kutoa maelezo ya kwanza kwenye fungu fulani ili wasikose fursa ya kutangaza imani yao.

Asiye na Uzoefu Hupata Hekima

16, 17. Mzee mmoja alimpa mtumishi mmoja wa huduma shauri gani, na kwa nini shauri hilo lilikuwa na matokeo?

16 Kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, mara nyingi sisi hukumbushwa kusoma Neno la Mungu kila siku. Inaburudisha kufanya hivyo. Pia kufanya hivyo hutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima, kurekebisha kasoro za utu, kushinda vishawishi, na kupata tena usawaziko wa kiroho ikiwa tumechukua hatua isiyofaa.—Zaburi 19:7.

17 Wazee wa kutaniko wenye uzoefu wako tayari kuandaa mashauri yanayotokana na Maandiko ambayo yanahusu mahitaji yetu. Sisi twahitaji tu ‘kuyateka’ kwa kutafuta mashauri yanayotegemea Biblia. (Mithali 20:5) Siku moja mtumishi mmoja wa huduma mwenye shauku alimwomba mzee mmoja madokezo ya jinsi awezavyo kuwa mwenye mafaa zaidi kutanikoni. Mzee huyo, ambaye alimjua ndugu huyo kijana vizuri sana, alifungua andiko la 1 Timotheo 3:3 kwenye Biblia yake, ambalo linasema kwamba wanaume waliowekwa rasmi ni lazima wawe ‘wenye kukubali sababu.’ Alitaja kwa fadhili njia ambazo kijana huyo angeweza kuwa mwenye kukubali sababu katika uhusiano wake na wengine. Je, ndugu huyo kijana aliudhiwa na shauri hilo la wazi alilopokea? La hasha! “Mzee huyo alitumia Biblia,” alieleza, “basi nikatambua kwamba shauri hilo linatoka kwa Yehova.” Mtumishi huyo wa huduma alitumia shauri hilo kwa shukrani na anafanya maendeleo mazuri.

18. (a) Ni nini kilichomsaidia kijana mmoja Mkristo ashinde kishawishi shuleni? (b) Wewe hukumbuka maandiko gani ya Biblia unapokabili kishawishi?

18 Neno la Mungu pia linaweza kuwasaidia vijana ‘wakimbie tamaa zenye kutukia ujanani.’ (2 Timotheo 2:22) Kijana mmoja Shahidi wa Yehova ambaye majuzi alimaliza shule ya sekondari aliweza kushinda kishawishi miaka yake yote ya masomo kwa kutafakari na kutumia maandiko fulani ya Biblia. Mara nyingi alifikiria shauri lililoandikwa kwenye Mithali 13:20: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa mwenye hekima.” Basi, yeye alitahadhari kufanya urafiki na wale tu wanaostahi sana kanuni za Maandiko. Aliwaza hivi: “Mimi si bora kuliko watu wengine. Nikijihusisha na watu wabaya, nitataka kuwapendeza rafiki zangu, na hilo laweza kutokeza matatizo.” Shauri la Paulo lililoandikwa kwenye 2 Timotheo 1:8 pia lilimsaidia. Aliandika: “Usiwe mwenye kuaibikia ushahidi juu ya Bwana wetu, . . . bali chukua sehemu yako katika kupatwa na uovu kwa ajili ya habari njema.” Kwa kupatana na shauri hilo, yeye aliwatangazia wanadarasa wenzake kwa ujasiri itikadi zake zinazotegemea Biblia kwenye kila pindi iliyofaa. Wakati wowote alipopewa mgawo wa kutoa ripoti mbele ya darasa, yeye alichagua habari ambayo ilimwezesha kutoa ushahidi kwa busara kuhusu Ufalme wa Mungu.

19. Kwa nini kijana mmoja alishindwa na misongo ya ulimwengu huu, lakini ni nini kilichompa nguvu za kiroho?

19 Tukikengeuka kutoka kwenye “njia iliyonyoka,” Neno la Mungu laweza kutusaidia kurekebisha hatua zetu. (Mithali 4:18) Kijana mmoja aishiye Afrika alijionea ukweli wa jambo hilo. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipomzuru, alikubali funzo la Biblia. Alifurahia yale aliyokuwa akijifunza lakini upesi akaanza kuwa na mashirika mabaya shuleni. Baada ya muda, akaanza kuishi maisha yasiyo ya adili. “Dhamiri yangu ilinitesa daima, ikanibidi niache kuhudhuria mikutano,” yeye akiri. Baadaye, akaanza kuhudhuria mikutano tena. Kijana huyo alitaja maneno haya yenye kufunua mambo wazi: “Niligundua kwamba mambo hayo yote yalisababishwa hasa na njaa ya kiroho. Sikuwa na funzo la kibinafsi. Hiyo ndiyo sababu iliyofanya nishindwe na kishawishi. Kisha nikaanza kusoma Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hatua kwa hatua, nikapata tena nguvu za kiroho na kurekebisha maisha yangu. Huo ukawa ushahidi mzuri kwa wale walioona mabadiliko ambayo nilikuwa nimefanya. Nilibatizwa, na sasa nina furaha.” Ni nini kilichompa kijana huyo nguvu za kushinda udhaifu wake wa kimwili? Yeye alipata nguvu za kiroho kwa kuwa na funzo la kibinafsi la Biblia la kawaida.

20. Kijana anawezaje kukinza mashambulizi ya Shetani?

20 Enyi vijana Wakristo, mwashambuliwa leo! Ni lazima mle chakula cha kiroho kwa ukawaida ikiwa mtashinda mashambulizi ya Shetani. Mtunga-zaburi, ambaye yaonekana vilevile alikuwa kijana, alielewa jambo hili. Alimshukuru Yehova kwa kuandaa Neno lake, ili ‘kijana aisafishe njia yake.’—Zaburi 119:9.

Kokote Kule Mungu Atuongozako, Tutafuata

21, 22. Kwa nini tusikate kauli ya kwamba njia ya kweli ni ngumu sana?

21 Yehova aliongoza taifa la Israeli kutoka Misri hadi Bara Lililoahidiwa. Kwa maoni ya wanadamu huenda njia aliyochagua ilionekana kuwa ngumu isivyo lazima. Badala ya kufuata njia iliyoonekana kuwa rahisi, na ya moja kwa moja kandokando ya Bahari ya Mediterania, Yehova aliwaongoza watu wake katika njia ngumu jangwani. Lakini, kumbe hiyo ilikuwa tu fadhili ya Mungu. Ingawa njia hiyo ya kandokando ya bahari ilikuwa fupi, hiyo ingewafanya Waisraeli wapitie nchi ya Wafilisti wenye uhasama. Kwa kuchagua njia nyingine, Yehova aliwaepusha watu hao wasikabiliane na Wafilisti mapema.

22 Vivyo hivyo, njia ambayo Yehova anatuongozea leo huenda ikaonekana kuwa ngumu nyakati nyingine. Kila juma, tuna ratiba kamili ya utendaji wa Kikristo, kutia ndani mikutano ya kutaniko, funzo la kibinafsi, na utumishi wa shambani. Huenda njia nyinginezo zikaonekana kuwa rahisi. Lakini ni kwa kufuata tu mwongozo wa Mungu ndipo tutakapofikia mradi wetu tunaojitahidi sana kuufikia. Basi, na tuendelee kutwaa mafundisho muhimu kutoka kwa Yehova na kubaki kwenye “njia iliyonyoka” milele!—Zaburi 27:11.

Unaweza Kueleza?

Kwa nini twahitaji hasa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida?

Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wawe wasikivu kwenye mikutano?

Ni nini kinachohusika katika kuwa msikilizaji mzuri?

Ni nini kinachoweza kutusaidia kutoa maelezo kwenye mikutano?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Kuhudhuria mikutano ya Kikristo hutusaidia kukumbuka siku ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuna njia kadhaa za kumsifu Yehova kwenye mikutano ya Kikristo