Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kifo—Jinsi Kitakavyoangamizwa

Kifo—Jinsi Kitakavyoangamizwa

INGAWA kosa la kutotii lililofanywa na wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, liliwaletea wanadamu wote dhambi na kifo, kosa hilo halikubadili kusudi la Mungu la kuwaumba wanadamu. Katika Neno lake, Biblia, Mungu anathibitisha tena na tena kwamba kusudi lake halijabadilika.

  • “Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.”​Zaburi 37:29.

  • “Atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova atafuta kabisa machozi katika nyuso zote.”​Isaya 25:8.

  • “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”​1 Wakorintho 15:26.

  • “Kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”​Ufunuo 21:4.

Mungu atatumia njia gani ‘kukimeza kifo,’ yaani, ‘kukiangamiza’ kabisa? Kama tulivyoona, Biblia inafunua wazi kwamba ‘waadilifu wataishi milele.’ Lakini inasema pia kwamba “hakuna mtu mwadilifu duniani anayefanya mema sikuzote.” (Mhubiri 7:20) Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu atakiuka viwango vyake ili wanadamu ambao si waadilifu waishi milele? La hasha! Hatafanya hivyo kwa sababu “Mungu [hawezi] kusema uwongo.” (Tito 1:2) Hivyo, Mungu atafanya nini ili kutimiza kusudi zuri alilokuwa nalo alipowaumba wanadamu?

MUNGU “ATAMEZA KIFO MILELE.”​—ISAYA 25:8

KUKOMESHA KIFO KWA KULIPA FIDIA

Akichochewa na upendo, Yehova Mungu alilipa fidia ili awakomboe wanadamu kutokana na kifo. Kimsingi, fidia ni kitu chenye thamani inayotosha kurekebisha uharibifu uliofanyika au kutimiza haki. Kwa kuwa wanadamu wote ni wenye dhambi na wanastahili kifo, Biblia inasema hivi kuwahusu: “Hakuna yeyote kati yao anayeweza kamwe kumkomboa ndugu yake wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake, (bei ya fidia kwa ajili ya uhai wao ni yenye thamani sana hivi kwamba hawawezi kamwe kulipa).”—Zaburi 49:7, 8

Mwanadamu asiye mkamilifu anapokufa, anaweza kulipia tu dhambi zake mwenyewe; hawezi kujikomboa, wala kulipia dhambi za mtu mwingine. (Waroma 6:7) Tulihitaji mtu ambaye ni mkamilifu na asiye na dhambi, atoe uhai wake kulipia dhambi zetu, na si dhambi zake.—Waebrania 10:1-4.

Mungu alichukua hatua ili kufanya jambo hilo liwezekane. Alimtuma Mwana wake, Yesu, aje kutoka mbinguni na kuzaliwa duniani akiwa mwanadamu mkamilifu asiye na dhambi. (1 Petro 2:22) Yesu alisema alikuja “kutoa uhai wake uwe fidia badala ya wengi.” (Marko 10:45) Alikufa ili alipie dhambi zetu na hivyo kutukomboa kutokana na kifo, na kutuwezesha kupata uzima.—Yohana 3:16.

KIFO KITAKOMESHWA LINI?

Leo, sambamba na unabii wa Biblia, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” kuthibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa mambo. (2 Timotheo 3:1) Siku za mwisho zitafikia tamati katika “siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Petro 3:3, 7) Lakini watu wanaompenda Mungu wataokoka uharibifu huo na kupewa “uzima wa milele.”—Mathayo 25:46.

Yesu alikuja “kutoa uhai wake uwe fidia badala ya wengi.”​—Marko 10:45

Mamilioni ya watu wengine watapata fursa ya kufurahia uzima wa milele watakapofufuliwa. Yesu alimfufua mtu aliyekufa, alipotembelea jiji la Naini. Mjane fulani alikuwa amefiwa na mwana pekee aliyekuwa naye. Yesu “akamsikitikia,” na kumfufua mwana wake. (Luka 7:11-15) Pia, mtume Paulo alisema hivi: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Tumaini hilo la kweli, linatuonyesha wazi jinsi ambavyo Mungu anawapenda wanadamu.—Matendo 24:15.

Mabilioni ya watu wanaweza kutazamia kuishi milele. Biblia inasema hivi: “Waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.” (Zaburi 37:29).Wakati huo, kila mmoja wao atajionea utimizo wa maneno yanayofurahisha na kufariji, yaliyoandikwa na mtume Paulo miaka 2,000 hivi iliyopita: “Kifo, uko wapi ushindi wako? Kifo, uko wapi mchomo wako?” (1 Wakorintho 15:55) Adui mkubwa wa wanadamu atakuwa ameangamizwa!