Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IGENI IMANI YAO | REBEKA

“Mimi Niko Tayari Kwenda”

“Mimi Niko Tayari Kwenda”

REBEKA alitazama eneo lenye mawemawe kadiri vivuli vilipozidi kuongezeka. Baada ya kusafiri kwa majuma kadhaa hatimaye akaanza kuzoea mwendo wa ngamia akiwa amekaa mgongoni mwa mnyama huyo. Walikuwa mbali sana na Harani, mji aliokulia uliokuwa kaskazini-mashariki. Huenda hataiona tena familia yao. Bila shaka alijiuliza maswali mengi kuhusu wakati ujao hasa kadiri alivyokaribia mwisho wa safari yake.

Msafara wao ulipita eneo kubwa la Kanaani na kukatisha katika Negebu. (Mwanzo 24:62) Labda Rebeka aliwaona kondoo. Kwa sababu ya ukame, huenda eneo hilo halikufaa kwa kilimo, lakini lilikuwa na malisho ya kutosha kwa ajili ya mifugo. Kiongozi wa msafara mwenye umri mkubwa zaidi alilifahamu vizuri eneo hilo. Alikuwa na hamu sana ya kumweleza bwana wake habari njema, kwamba Rebeka angekuwa mke wa Isaka! Inawezekana Rebeka alikuwa akifikiria jinsi maisha yatakavyokuwa katika nchi hiyo. Bwana-arusi wake, Isaka, yukoje? Hakumfahamu. Je, atafurahi kumwona? Atahisi jinsi gani atakapomwona Isaka?

Katika nchi nyingi watu huona kuchaguliwa mwenzi wa ndoa kuwa jambo la ajabu. Katika maeneo mengine ni kawaida watu kufunga ndoa za aina hiyo. Hata uwe na maoni gani, huenda ukakubali kwamba Rebeka alikuwa akiingia katika hali asiyojua. Alikuwa mwanamke mwenye ujasiri na imani yenye nguvu. Tunahitaji sifa hizo tunapokabili mabadiliko maishani. Hata hivyo, kuna sifa nyingine nzuri na za pekee ambazo Rebeka alizionyesha kupitia imani yake.

“NITATEKA MAJI PIA KWA AJILI YA NGAMIA ZAKO”

Badiliko kubwa katika maisha ya Rebeka lilianza katika njia ambayo aliiona kuwa ya kawaida. Inawezekana aliishi ndani au karibu na eneo la Harani lililokuwa katika jiji la Mesopotamia. Wazazi wake walikuwa tofauti na watu wengi wa Harani. Hawakumwabudu mungu-mwezi aliyeitwa Sin. Badala yake, Mungu wao alikuwa Yehova.—Mwanzo 24:50.

Rebeka alikuwa mwanamke mrembo sana na urembo wake haukuwa wa nje tu. Alikuwa mwenye bidii na safi kiadili. Kwa kuwa familia yao ilikuwa tajiri, walikuwa na watumishi, lakini Rebeka hakudekezwa au kutendewa kama binti wa mfalme; alifundishwa kufanya kazi kwa bidii. Kama ilivyokuwa kwa wanawake wengi wa wakati huo, Rebeka alifanya kazi ngumu zilizotia ndani kuteka maji kwa ajili ya familia yao. Wakati wa jioni, angebeba mtungi begani na kwenda kwenye chemchemi.—Mwanzo 24:11, 15, 16.

Jioni moja baada ya kujaza mtungi wake, mwanaume mzee alimkimbilia. Akamwambia hivi: “Tafadhali, nipe maji kidogo katika mtungi wako.” Mtu huyo alitoa ombi hilo kwa upole sana! Rebeka aliona kuwa mwanaume huyo alikuwa amesafiri kutoka mbali sana. Hivyo akashusha mtungi wake begani na kumpa mwanaume huyo maji baridi yenye kuburudisha. Pia alitambua kwamba mwanamume huyo alikuwa na ngamia kumi waliopiga magoti karibu na chombo cha kunyweshea wanyama ambacho hakikuwa kimejazwa maji. Isitoshe, Rebeka alitaka kumwonyesha ukarimu mwanamume huyo kadiri alivyoweza. Hivyo, akamwambia: “Nitateka maji pia kwa ajili ya ngamia zako mpaka wamalize kunywa.”—Mwanzo 24:17-19.

Ona kwamba Rebeka hakujitolea tu kuwapa ngamia kumi maji kidogo ya kunywa, bali alitaka kuwapa maji mengi hadi watakapotosheka. Ngamia mmoja mwenye kiu sana anaweza kunywa zaidi ya lita 95 za maji! Ikiwa ngamia wote kumi walikuwa na kiu sana, basi Rebeka alifanya kazi hiyo ngumu kwa saa nyingi. Hata hivyo, inaonekana ngamia hao hawakuwa na kiu sana. * Je, Rebeka alijua jambo hilo alipojitolea kuwapa maji? Hapana. Alikuwa tayari, hata alikuwa na hamu ya kufanya kazi kwa bidii sana ili kumwonyesha ukarimu mzee huyo mgeni. Mwanamume huyo alikubali msaada wake. Kisha alimtazama kwa makini kila mara alipokuwa akifanya kazi ya kwenda na kurudi ili kujaza mtungi wake na kumimina maji katika chombo cha kunyweshea wanyama.—Mwanzo 24:20, 21.

Rebeka alikuwa mwenye bidii na mkarimu

Mfano wa Rebeka unatufundisha jambo muhimu sana. Tunaishi katika ulimwengu ambao watu ni wabinafsi sana. Kama ilivyotabiriwa, watu wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe,” wasio tayari kujidhabihu kwa ajili ya wengine. (2 Timotheo 3:1-5) Wakristo wanaotaka kuepuka mwelekeo huo watafaidika sana wakitafakari bidii ya msichana huyo kama Biblia inavyosimulia.

Inaonekana Rebeka aligundua kuwa mzee huyo alikuwa akimtazama. Si kwamba Rebeka alionekana kwa njia isiyofaa bali mwanaume huyo alikuwa akistaajabu na kufurahia bidii yake. Rebeka alipomaliza kazi, mwanamume huyo alimpa zawadi, yaani, vito vyenye thamani! Kisha akamuuliza: “Wewe ni binti ya nani? Tafadhali niambie. Je, mna nafasi yoyote nyumbani kwa baba yako tukae usiku huu?” Mwanaume huyo alifurahi sana alipoelezwa kuhusu familia yao. Labda akiwa amesisimka sana, Rebeka akajibu hivi: “Tuna majani na chakula kingi cha mifugo, pia mahali pa kukaa usiku,” hilo lilikuwa jambo zuri kwa kuwa mwanaume huyo mzee alikuwa na watu wengine aliosafiri nao. Kisha Rebeka akatangulia nyumbani ili kumwambia mama yake kilichotokea.—Mwanzo 24:22-28, 32.

Ni wazi kwamba Rebeka alifundishwa na wazazi wake kuwa mkarimu. Hiyo ni sifa ambayo watu wengi leo hawana na hiyo ni sababu nyingine inayotufanya tuige imani ya mwanamke huyo mwenye fadhili. Imani yetu kwa Mungu inapaswa kutuchochea tuwe wakarimu. Yehova ni mkarimu kwa watu wote na anataka waabudu wake wafanye hivyo pia. Tunapokuwa wakarimu hata kwa wale ambao huenda wasitulipe chochote, tunamfurahisha Baba yetu wa mbinguni.—Mathayo 5:44-46; 1 Petro 4:9.

“UMCHUKULIE MWANANGU MKE”

Mwanaume huyo mzee aliyekuwa katika kisima alikuwa nani? Alikuwa mtumishi wa Abrahamu, kaka ya babu ya Rebeka. Hivyo, alikaribishwa nyumbani kwa baba ya Rebeka, aliyeitwa Bethueli. Huenda mtumishi huyo aliitwa Eliezeri. * Alikataa kula chakula alichopewa na wenyeji wake kwa kuwa alitaka kwanza kueleza kusudi la safari yake. (Mwanzo 24:31-33) Tunaweza kuwazia jinsi alivyoongea kwa msisimko kwa kuwa aliona uthibitisho mkubwa kwamba Mungu wake, Yehova, alimbariki katika mgawo huo muhimu. Jinsi gani?

Wazia Eliezeri akisimulia kisa chake huku Bethueli baba ya Rebeka, na Labani kaka yake, wakimsikiliza kwa makini. Aliwaambia kwamba Yehova alimbariki sana Abrahamu huko Kanaani na kwamba Abrahamu na Sara walikuwa na mwana, Isaka, ambaye angerithi kila kitu. Abrahamu alimpa mtumishi wake mgawo muhimu sana: Alipaswa kumtafutia Isaka mke miongoni mwa ndugu za Abrahamu huko Harani.—Mwanzo 24:34-38.

Abrahamu alimwapisha Eliezeri kwamba asimtafutie Isaka mke miongoni mwa wanawake wa Kanaani. Kwa nini? Kwa sababu Wakanaani hawakumheshimu wala kumwabudu Yehova Mungu. Abrahamu alijua kwamba Yehova angewaangamiza watu hao kwa sababu ya uovu wao. Abrahamu hakutaka mwana wake mpendwa, Isaka, ashirikiane na watu hao na kuiga maadili yao mabaya. Pia alijua kwamba mwana wake alikuwa na sehemu muhimu katika utimizo wa ahadi za Mungu.—Mwanzo 15:16; 17:19; 24:2-4.

Eliezeri aliendelea kuwaeleza wenyeji wake kwamba alisali kwa Yehova Mungu alipofika kwenye kisima kilichokuwa karibu na Harani. Alimwomba Yehova amsaidie kumchagulia Isaka mke anayefaa. Jinsi gani? Eliezeri alimwomba Mungu amhakikishie kuwa mwanamke ambaye anafaa kuolewa na Isaka aje kwenye kisima hicho. Akimwomba maji, ajitolee pia kuwanywesha ngamia zake. (Mwanzo 24:12-14) Ni nani aliyekuja na kufanya hayo yote? Ni Rebeka! Wazia jinsi Rebeka alivyohisi ikiwa alisikia mazungumzo ya Eliezeri akiwasimulia washiriki wa familia yake!

Bethueli na Labani walivutiwa sana na simulizi la Eliezeri. Walisema hivi: “Jambo hili limetoka kwa Yehova.” Kama ilivyokuwa desturi, walifanya mapatano ya ndoa, na kumruhusu Rebeka aolewe na Isaka. (Mwanzo 24:50-54) Je, hilo linamaanisha kwamba Rebeka hakuwa na la kusema katika jambo hilo?

Majuma kadhaa yaliyopita, Eliezeri alimuuliza Abrahamu, kwa kusema hivi: “Itakuwaje ikiwa mwanamke huyo hatakuja pamoja nami?” Abrahamu alimjibu: “Utakuwa bila wajibu kwangu kwa kiapo.” (Mwanzo 24:39, 41) Katika familia ya Bethueli maoni ya mwanamke huyo yalithaminiwa pia. Eliezeri alisisimuka sana kwa kuwa alifanikiwa katika mgawo wake hivi kwamba asubuhi iliyofuata, aliomba ruhusa arudi na Rebeka mara moja hadi Kanaani. Hata hivyo, familia ilitaka Rebeka abaki angalau kwa siku kumi zaidi. Mwishowe walisuluhisha jambo hilo kwa njia hii: “Na tumwite huyo mwanamke kijana tusikie kutoka kinywani mwake.”—Mwanzo 24:57.

Rebeka alikuwa njia panda. Angesema nini? Je, angewaonea huruma baba na kaka yake na kukataa kwenda mahali asipopajua? Au angeona kuwa ni pendeleo kushiriki katika matukio yaliyoongozwa na Yehova? Alipojibu, alionyesha jinsi alivyohisi kuhusu mabadiliko hayo makubwa na ya ghafla katika maisha yake. Alisema hivi: “Mimi niko tayari kwenda.”—Mwanzo 24:58.

Rebeka alikuwa na mtazamo mzuri sana! Leo, huenda desturi zetu kuhusu ndoa ni tofauti, lakini tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa Rebeka. Maoni ya Mungu wake, Yehova, yalikuwa muhimu zaidi kuliko maoni yake. Neno la Mungu hutoa mwongozo unaofaa kuhusu ndoa katika siku zetu, yaani, mtu wa kufunga naye ndoa na jinsi ya kuwa mume au mke bora. (2 Wakorintho 6:14, 15; Waefeso 5:28-33) Ni jambo linalofaa kuiga mfano wa Rebeka na kufanya mambo yanayompendeza Mungu.

‘YULE MWANAMUME NI NANI?’

Familia ya Bethueli ilimbariki mtoto wao mpendwa Rebeka. Kisha, yeye pamoja na Debora, mtunzaji wake tangu alipokuwa mtoto na baadhi ya watumishi wake wanawake, wakaondoka pamoja na Eliezeri na wanaume wake. (Mwanzo 24:59-61; 35:8) Baada ya muda mfupi, waliiacha Harani mbali sana. Ilikuwa safari ndefu ya kilometa 800 au zaidi ambayo huenda ilichukua majuma matatu. Yawezekana kwamba haikuwa safari yenye kustarehesha. Ingawa Rebeka aliona ngamia wengi maishani mwake, huenda hakuwa na uzoefu wa kusafiri kwa ngamia. Biblia inaitaja familia yao kuwa ya wachungaji wala si wafanyabiashara walioendesha misafara ya ngamia. (Mwanzo 29:10) Mara nyingi, wapanda ngamia hulalamika kuhusu maumivu wanayopata wanaposafiri hata ikiwa ni safari fupi!

Vyovyote vile, Rebeka alikazia fikira mambo ya mbele, huenda kwa kujifunza mambo mengi kutoka kwa Eliezeri kuhusu Isaka na familia yake. Wazia mwanaume huyo mzee akizungumza na Rebeka wanapoota moto jioni, akimweleza kuhusu ahadi ya Yehova aliyompa rafiki Yake Abrahamu. Mungu angetokeza uzao kutoka katika ukoo wa Abrahamu ambao ungewaletea wanadamu wote baraka. Wazia jinsi Rebeka alivyostaajabu alipotambua kuwa ahadi ya Yehova ingetimia kupitia mume wake mtarajiwa, Isaka na yeye pia!—Mwanzo 22:15-18.

Rebeka alikuwa mnyenyekevu, sifa ambayo ni adimu lakini yenye thamani sana

Mwishowe, siku tuliyoitaja mwanzoni mwa makala hii ilifika. Msafara ulipokuwa ukikaribia eneo la Negebu na giza kuanza kuingia, Rebeka alimwona mwanaume akitembea shambani. Alikuwa akitafakari. Simulizi hilo linasema, “Akaruka chini kutoka kwenye ngamia,” huenda bila hata kusubiri ngamia apige magoti kisha akamuuliza mtumishi: “Yule mwanamume anayetembea pale shambani kuja kutupokea, ni nani?” Alipojua kwamba ni Isaka, akachukua kitambaa cha kichwani na kujifunika. (Mwanzo 24:62-65) Kwa nini? Inaonekana alifanya hivyo kama ishara ya heshima kwa mume wake mtarajiwa. Huenda wengine wakaona kuwa heshima ya aina hiyo imepitwa na wakati. Hata hivyo, wanaume na wanawake wanaweza kujifunza kutokana na unyenyekevu wa Rebeka kwa kuwa sote tunahitaji kuboresha sifa hiyo nzuri.

Isaka, alikuwa na umri wa miaka 40 hivi wakati huo na bado alikuwa akiomboleza kifo cha mama yake, Sara, aliyekufa miaka mitatu iliyopita. Hivyo, tunaweza kusema kwamba Isaka alikuwa mwanaume mwenye hisia mwenzi. Ilikuwa baraka kubwa kwa mwanaume huyo kupata mke mwenye bidii, mkarimu na mnyenyekevu! Mambo yalikuwaje walipokutana? Biblia inasema Isaka “Akampenda.”—Mwanzo 24:67; 26:8.

Ingawa karne 39 hivi zimepita, bado tunaweza kuiga mtazamo wa Rebeka. Tunavutiwa na jinsi alivyokuwa mwenye bidii, jasiri, mkarimu, na mnyenyekevu. Sote, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, waliofunga ndoa na waseja, tutanufaika tukiiga imani yake!

^ fu. 10 Tayari ilikuwa jioni. Simulizi halitaji kwamba Rebeka alibaki kisimani kwa saa nyingi. Halionyeshi kwamba familia yake ilikuwa imelala usingizi alipomaliza kuchota maji au kama kuna mtu yeyote aliyemtafuta kwa sababu alichelewa kurudi.

^ fu. 15 Eliezeri hatajwi katika simulizi hilo, lakini huenda ndiye mtumishi aliyehusika katika kisa hicho. Wakati mmoja, Abrahamu alikusudia kumrithisha Eliezeri mali zake zote ikiwa hangepata mtoto, hivyo Eliezeri alikuwa mtumishi mwenye umri mkubwa na aliyeaminiwa zaidi na Abrahamu. Mtumishi anayetajwa katika kisa hiki anaelezwa kwa njia hiyo pia.—Mwanzo 15:2; 24:2-4.