Je, Useja ni Takwa la Wahudumu Wakristo?
DINI nyingi duniani, kama vile Kanisa Katoliki, makanisa mbalimbali ya Othodoksi, dini ya Budha, na zingine, zimeweka sheria kwamba viongozi wa kanisa na makasisi wanapaswa kuwa waseja. Kwa upande mwingine, watu wengi wanahisi kwamba takwa hilo la useja ni chanzo kikuu cha tuhuma nyingi za ngono zinazowahusu viongozi wa kidini.
Hivyo basi, kulingana na Maandiko, Je, useja ni takwa ili mtu astahili kuwa mhudumu Mkristo? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze historia ya zoea hilo na maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo.
USEJA KATIKA HISTORIA YA DINI
Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema kwamba, useja “ni hali ya mtu kubaki bila kufunga ndoa, na hivyo, kujizuia kufanya ngono, hasa inapohusu cheo cha mtu anayejitoa kwa ajili ya dini.” Alipokuwa akihutubia Roman Curia mwaka wa 2006, Papa Benedict wa XVI alisema kwamba sheria ya useja kwa viongozi wa kidini ni “desturi ambayo imekuwepo tangu zamani, karibu na kipindi cha Mitume.”
Hata hivyo, useja haukuwa desturi ya kidini kwa Wakristo wa karne ya kwanza. Kwa kweli, mtume Paulo, ambaye aliishi wakati huo, aliwaonya Wakristo kuhusu watu ambao wangesema “maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha” na ‘kukataza kufunga ndoa.’—1 Timotheo 4:1-3.
Katika karne ya pili zoea la useja lilianza kuingia kwenye makanisa ya “Kikristo” ambayo baadaye yalifanyiza Kanisa Katoliki. Kulingana na kitabu Celibacy and Religious Traditions, zoea hilo “liliendana na mtindo wa kujizuia kufanya ngono uliokuwa umeibuka katika Milki ya Roma.”
Katika karne zilizofuata, mabaraza ya kanisa pamoja na wale wanaoitwa Mababa wa Kanisa, waliunga mkono viongozi wa kidini kuwa waseja. Walifikiri kwamba mahusiano ya ngono yanamtia mtu unajisi na hayapatani na majukumu ya viongozi wa kidini. Ingawa hivyo, kitabu Encyclopædia Britannica kinasema kwamba, “hadi kufikia karne ya 10 makasisi wengi na hata baadhi ya maaskofu walikuwa na wake.”
Mpango wa useja kwa viongozi wa kidini ulipitishwa rasmi kwenye Mabaraza ya Lateran ya mwaka wa 1123 na 1139, yaliyofanywa jijini Roma, na zoea hilo limefuatwa na Kanisa Katoliki mpaka leo. Kwa kuweka sheria hiyo, kanisa lilizuia upotevu wa mali na kipato uliotokana na tabia ya makasisi waliofunga ndoa, kuwarithisha watoto wao mali za kanisa.
MAONI YA MUNGU KUHUSU USEJA
Neno la Mungu, Biblia, linaeleza waziwazi maoni yake kuhusu useja. Katika Biblia, tunasoma maneno ya Yesu kuhusu wale waliobaki waseja, kama alivyokuwa, “kwa sababu ya Ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 19:12) Vivyo hivyo, mtume Paulo alizungumza kuhusu Wakristo waliofuata mfano wake na kubaki waseja “kwa ajili ya habari njema.”—1 Wakorintho 7:37, 38; 9:23.
Hata hivyo, Yesu na Paulo hawakuweka sheria kwa wahudumu Wakristo kubaki wakiwa waseja. Yesu alisema kwamba useja ni “zawadi” ya baadhi tu ya wanafunzi wake. Paulo alipoandika kuhusu “mabikira,” au wale ambao hawajawahi kufunga ndoa, alikiri hivi waziwazi: “Sina amri kutoka kwa Bwana, lakini natoa maoni yangu.”—Mathayo 19:11; 1 Wakorintho 7:25.
Kwa kuongezea, Biblia inaonyesha kwamba wahudumu wengi Wakristo katika karne ya kwanza, kutia ndani mtume Petro, walikuwa wameoa. (Mathayo 8:14; Marko 1:29-31; 1 Wakorintho 9:5) Kwa kweli, kutokana na kuenea kwa mwenendo mpotovu kingono katika milki ya Roma, Paulo aliandika kwamba ikiwa mwangalizi Mkristo ameoa, alipaswa kuwa “mume wa mke mmoja” na awe “mwenye watoto wanaojitiisha.”—1 Timotheo 3:2, 4.
Hizo hazikuwa ndoa zisizohusisha mahusiano ya ngono, kwa kuwa Biblia inasema moja kwa moja kwamba, “mume na ampe mke wake haki yake,” na kwamba wenzi wa ndoa hawapaswi ‘kunyimana haki’ ya ndoa. (1 Wakorintho 7:3-5) Ni wazi kwamba Mungu hajaweka sheria ya useja na wala si takwa la lazima kwa wahudumu Wakristo.
KWA AJILI YA HABARI NJEMA
Ikiwa si lazima kubaki mseja, kwa nini Yesu na Paulo walionyesha kwamba wanaunga mkono useja? Kwa sababu useja unampa mtu uhuru mkubwa wa kushiriki katika kazi ya kueneza habari njema. Waseja wanaweza kujitoa zaidi kwa kuwa wao hawana mahangaiko yanayowakabili wale waliofunga ndoa.—1 Wakorintho 7:32-35.
Fikiria mfano wa David, ambaye aliacha kazi yenye mshahara mnono jijini Mexico na kuhamia eneo la kijijini huko Kosta Rika ili awafundishe wengine Biblia. Je, David anaona kwamba useja ulimwezesha kuchukua hatua hiyo? “Bila shaka,” anasema. “Haikuwa rahisi kuzoea utamaduni mpya na hali tofauti za maisha, lakini kwa kuwa nilikuwa mseja, sikupata shida sana.”
Claudia, Mkristo mseja ambaye amehamia eneo lenye uhitaji wa wahubiri wa habari njema, anasema hivi: “Ninafurahia utumishi wangu kwa Mungu. Imani na uhusiano wangu pamoja na Mungu umeimarika zaidi kadiri ninavyoona jinsi anavyonitunza.”
“Vyovyote vile, iwe umefunga ndoa au ni mseja, utakuwa na furaha ikiwa utajitoa kabisa kwa Yehova Mungu.”
Kuwa mseja hakumaanishi kwamba hutakuwa na furaha. Claudia anaongeza hivi: “Vyovyote vile, iwe umefunga ndoa au ni mseja, utakuwa na furaha ikiwa utajitoa kabisa kwa Yehova Mungu.”