Kutoka Utumwani —Nyakati za Kale na Sasa
Blessing * alifika Ulaya akiwa na tumaini la kufanya kazi ya kusuka nywele. Lakini baada ya kupigwa kwa siku kumi mfululizo, na kutishiwa kwamba familia yake ingetendewa vibaya, hatimaye alikubali kufanya kazi ya ukahaba.
Michoro ya watumwa katika Misri ya kale
Blessing alitarajiwa kupata euro 200 hadi 300 kwa usiku mmoja ili kulipa deni alilowekewa na mwajiri wake la euro 40,000. * Anaeleza hivi: “Mara kwa mara nilifikiria kutoroka, lakini niliogopa kwamba wangeidhuru familia yangu. Sikuwa na la kufanya.” Kisa cha Blessing kinaonyesha hali ambayo watu zaidi ya milioni nne wanaotumikishwa katika biashara ya ngono wanakabili katika mataifa mbalimbali.
Karibu miaka 4,000 iliyopita, kijana aliyeitwa Yosefu aliuzwa utumwani na ndugu zake. Huko alitumikia kwenye nyumba ya mtu mwenye cheo cha juu nchini Misri. Tofauti na Blessing, mwanzoni Yosefu hakutendewa vibaya na bwana wake. Lakini alipokataa kufanya ngono na mke wa bwana wake, alihukumiwa isivyo haki kwamba alijaribu kumbaka. Kisha, akatupwa gerezani na kufungwa katika vyuma.—Mwanzo 39:1-20; Zaburi 105:17, 18.
Yosefu alikuwa mtumwa wa nyakati za kale; Blessing ni mtumwa wa karne ya 21. Lakini wote wawili waliathiriwa na biashara ya watumwa, ambayo imedumu kwa muda mrefu. Kwenye biashara hiyo, watu huonwa kuwa bidhaa, na wale wanaoifanya hawajali chochote zaidi ya kupata pesa.
VITA HUCHOCHEA BIASHARA YA WATUMWA
Vita vilifanya iwe rahisi kwa nchi kupata watumwa. Inasemekana kwamba Mfalme wa Misri, Thutmose wa III, alirudi na wafungwa 90,000 baada ya mapigano huko Kanaani. Wamisri waliwatumikisha wafungwa hao katika kazi za uchimbaji wa madini, mifereji na ujenzi wa mahekalu.
Katika Milki ya Roma, vita vilitokeza watumwa wengi, na nyakati nyingine uhitaji wa kupata watumwa
zaidi ulisababisha vita. Inakadiriwa kwamba kufikia karne ya kwanza, karibu nusu ya wakazi wa jiji la Roma, walikuwa watumwa. Watumwa wengi wa Misri na Roma walitendewa vibaya sana. Kwa mfano, urefu wa maisha ya watumwa katika migodi ya Waroma, ulikadiriwa kuwa miaka 30 tu.Kadiri muda ulivyopita, biashara ya watumwa ilizidi kuongezeka. Kuanzia karne ya 16 hadi ya 19, biashara ya watumwa iliyofanywa kati ya Afrika na Marekani ilikuwa moja ya biashara zenye faida kubwa duniani. Ripoti ya UNESCO inasema hivi: ‘Inakadiriwa kwamba kati ya wanaume, wanawake, na watoto milioni 25 hadi 30 walitekwa na kuuzwa.’ Inasemekana kwamba mamia ya maelfu ya watu walikufa walipokuwa wakivuka bahari ya Atlantiki. Olaudah Equiano, mtumwa ambaye alifanikiwa kufika akiwa hai, alisema hivi: “Vilio vya uchungu vya wanawake vilivyoambatana na miguno ya watu wanaokufa vilifanya mandhari yote iwe yenye kutisha sana.”
Kwa kusikitisha, utumwa bado unaendelea. Kulingana na Shirika la Kimataifa la Wafanyakazi (ILO), wanaume, wanawake, na watoto milioni 21 hivi bado wanafanya kazi wakiwa watumwa, baadhi yao wakilipwa pesa kidogo sana na wengine hawalipwi kabisa. Watumwa wa kisasa wanafanya kazi kwenye migodi, viwanda vya nguo na matofali, madanguro, na katika nyumba za watu. Ingawa si halali kisheria, utumwa bado unazidi kuongezeka.
Bado mamilioni ya watu wanafanya kazi wakiwa watumwa
KUTOKA UTUMWANI
Matendo ya kikatili yamefanya watumwa wengi wapiganie uhuru wao. Katika karne ya kwanza K.W.K., Spartacus pamoja na watumwa wengine 100,000, waliasi na kupigana na jeshi la Roma, lakini hawakufanikiwa. Kwenye karne ya 18, watumwa katika kisiwa cha Karibea cha Hispaniola waliasi dhidi ya mabwana zao. Kwa sababu ya kutendewa kikatili katika mashamba ya miwa, walianzisha vita vilivyodumu kwa miaka 13 na hatimaye taifa la Haiti lilipata uhuru wake mwaka wa 1804.
Hata hivyo, tunaweza kusema kwamba kisa cha Waisraeli Kutoka Misri ndio kisa cha watu waliofanikiwa kikamili kutoka utumwani, katika historia ya wanadamu. Taifa zima, lililokuwa na watu milioni tatu hivi, liliachiliwa huru kutoka utumwani Misri. Kwa kweli, walistahili kuwa huru. Biblia inaeleza kwamba Wamisri “waliwatumia [Waisraeli] wakiwa watumwa chini ya uonevu.” (Kutoka 1:11-14) Farao fulani hata alianzisha kampeni ya kuwauwa watoto wa Waisraeli ili kudhibiti idadi yao iliyokuwa ikiongezeka.—Kutoka 1:8-22.
Kisa cha Waisraeli kuachiliwa huru kutokana na uonevu walioupata Misri, kilikuwa cha pekee kwa Kutoka 3:7, 8) Mpaka leo, Wayahudi katika sehemu mbalimbali duniani, husherehekea Pasaka kila mwaka ili kukumbuka tukio hilo.—Kutoka 12:14.
sababu Mungu aliingilia kati. Mungu alimwambia Musa hivi: “Nayajua vizuri maumivu waliyo nayo. Nami ninashuka ili kuwakomboa.” (KUKOMESHA UTUMWA KABISA
Biblia inasema kuwa “hakuna ukosefu wowote wa uadilifu . . . kwa upande wa Yehova Mungu wetu,” na inatuhakikishia kwamba Mungu hajabadilika. (2 Mambo ya Nyakati 19:7; Malaki 3:6) Mungu alimtuma Yesu “kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka . . . , kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru.” (Luka 4:18) Je, hilo lilimaanisha kwamba kila mtu aliye utumwani kihalisi angeachiliwa? Hapana. Yesu alitumwa kuwaachilia huru watu kutoka kwenye utumwa wa dhambi na kifo. Baadaye alisema hivi: “Kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) Hadi leo, kweli ambayo Yesu alifundisha inawaweka watu huru katika njia nyingi.—Soma sanduku lenye kichwa “ Kutoka Katika Aina Nyingine ya Utumwa.”
Mungu alimsaidia Yosefu na Blessing kutoka utumwani katika njia zilizotofautiana. Unaweza kusoma simulizi lenye kuvutia la Yosefu katika sura ya 39 hadi 41 ya kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Vivyo hivyo, harakati za Blessing za kutafuta uhuru zilikuwa na matokeo mazuri.
Baada ya kufukuzwa kutoka nchi fulani ya Ulaya, Blessing alienda Hispania. Akiwa huko alikutana na Mashahidi wa Yehova na akaanza kujifunza nao Biblia. Akiwa ameazimia kurekebisha maisha yake, alitafuta kazi ya kawaida na kumwomba mwajiri wake wa awali ampunguzie kiasi cha pesa alichopaswa kurejesha kila mwezi. Siku moja, Blessing alipigiwa simu na yule mwajiri wake wa awali. Alitaka kufuta deni la Blessing na kumwomba msamaha. Kwa nini aliamua kufanya hivyo? Yeye pia alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova! Blessing anasema hivi: “Kweli inakuweka huru katika njia za kustaajabisha sana.”
Yehova Mungu alihisi uchungu alipoona ukatili waliotendewa Waisraeli utumwani Misri; bila shaka, anahisi hivyohivyo anapoona ukosefu wa haki kama huo leo. Ni kweli kwamba ili kukomesha aina zote za utumwa, mabadiliko makubwa sana yanahitajika katika jamii ya wanadamu. Lakini, Mungu anaahidi kuleta mabadiliko hayo. “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13