Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari​—Madagaska

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari​—Madagaska

SYLVIANA, painia mwenye umri wa miaka 27 anasema hivi:“Nilipokuwa nikiwasikiliza marafiki wangu wakisimulia mambo waliyojionea walipokuwa wakitumikia katika maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa wa mapainia, nilitamani sana kuwa na shangwe kama wao. Lakini nilihisi kwamba siwezi kujitolea katika eneo lenye uhitaji.”

Je, hali yako ni kama ya Sylviana? Je, wewe pia unatamani sana kutumikia mahali ambapo wahubiri wa Ufalme wanahitajika, lakini una wasiwasi ikiwa utawahi kufikia lengo hilo? Ikiwa unahisi hivyo, usife moyo! Kwa msaada wa Yehova, maelfu ya ndugu na dada wamefanikiwa kushinda mambo yaliyokuwa yakiwazuia wasipanue huduma yao. Ili kujua jinsi Yehova alivyowasaidia baadhi yao kushinda vizuizi, tutatembelea nchi ya Madagaska, kisiwa cha nne kwa ukubwa duniani.

Katika kipindi cha miaka kumi, zaidi ya wahubiri na mapainia 70 wenye bidii kutoka nchi 11 * wametumikia katika shamba hili lenye matokeo lililopo barani Afrika, ambapo watu wengi huiheshimu Biblia. Pia, wahubiri wengi wenyeji wamejitoa kwa hiari kuhamia maeneo mengine katika kisiwa hiki kikubwa ili kueneza ujumbe wa Ufalme. Acheni tuwafahamu baadhi yao.

KUSHINDA WOGA NA HISIA ZA KUVUNJIKA MOYO

Perrine na Louis

Louis na Perrine, wenzi wa ndoa wenye umri wa miaka 30 hivi, walihama Ufaransa na kwenda kuishi Madagaska. Kwa miaka mingi, walikuwa wakifikiria kuhusu kupanua utumishi wao kwa kuhamia nchi nyingine, lakini Perrine alisita kuhama. Anaeleza hivi: “Niliogopa kwenda mahali nisipokujua. Niliogopa kuwaacha watu wa familia, kutaniko, nyumba yetu, maeneo niliyozoea, na mambo niliyozoea kufanya. Kwa kweli, kizuizi kikubwa nilichohitaji kushinda ni wasiwasi niliokuwa nao.” Mwaka wa 2012, Perrine alijipa ujasiri, naye pamoja na Louis, mume wake, wakahama. Anahisije kuhusu uamuzi waliofanya? “Ninapotafakari jambo hilo, sina budi kusema kwamba imani yetu imeimarika kwa kuona mkono wa Yehova maishani mwetu.” Louis anasema hivi: “Hebu wazia, katika Ukumbusho wetu wa kwanza nchini Madagaska, kati ya wanafunzi wa Biblia tuliokuwa nao, kumi walihudhuria!”

Ni nini kilichowapa wenzi hao nguvu za kuendelea kubaki katika mgawo wao matatizo yalipozuka? Walisali kwa Yehova kwa bidii ili awape nguvu za kuvumilia. (Flp. 4:13) Louis anaeleza hivi: “Tulijionea Yehova akijibu sala zetu na kutupatia ‘amani ya Mungu.’ Hivyo, tulifaulu kukazia fikira shangwe tuliyokuwa tukipata katika utumishi wetu. Pia, marafiki wetu nchini Ufaransa walitutumia barua zilizotusaidia tusife moyo.”—Flp. 4:6, 7; 2 Kor. 4:7.

Yehova aliwathawabisha sana Louis na Perrine kwa uvumilivu wao. Louis anasema hivi: “Mwezi wa Oktoba 2014, tulihudhuria Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo * nchini Ufaransa. Kuhudhuria shule hiyo ilikuwa zawadi isiyoweza kusahaulika kutoka kwa Yehova.” Baada ya kuhitimu, wenzi hao wa ndoa walifurahi sana kupokea mgawo wa kurudi nchini Madagaska.

“TUTAWAONEA FAHARI!”

Nadine na Didier

Didier na Nadine, wenzi wa ndoa kutoka Ufaransa, walihamia Madagaska mwaka wa 2010, walipokuwa na umri wa miaka 50 hivi. Didier anaeleza hivi: “Tulifanya upainia tulipokuwa vijana, kisha tukawalea watoto wetu watatu. Walipokuwa watu wazima, tulifikiria uwezekano wa kutumikia katika nchi nyingine.” Nadine anakiri hivi: “Nilipofikiria kwamba nitakuwa mbali na watoto wangu, nilisita, lakini walituambia hivi: ‘Mkijitolea kwenda kutumikia nchi nyingine, tutawaonea fahari!’ Maneno yao yalitutia moyo hivi kwamba tukaamua kuhama. Ingawa tunaishi mbali sana na watoto wetu, tunafurahi kwamba tunaweza kuwasiliana nao kwa ukawaida.”

Didier na Nadine, walipata changamoto kubwa sana kujifunza Kimalagasi. Nadine anasema hivi huku akitabasamu: “Sisi si vijana wenye umri wa miaka 20.” Walifaulu jinsi gani? Kwanza, walijiunga na kutaniko la lugha ya Kifaransa. Baadaye, walipohisi kwamba wako tayari kujifunza lugha ya wenyeji, walihamia kutaniko la Kimalagasi. Nadine anaendelea kusema hivi: “Watu wengi tunaokutana nao tunapohubiri wanapenda kujifunza Biblia. Mara nyingi wanatushukuru kwa kuwatembelea. Mwanzoni, nilidhani ninaota. Ninafurahia kufanya upainia katika eneo hili. Ninapoamka asubuhi, mimi husema, ‘Safi sana—ninaenda kuhubiri leo!’”

Didier anatabasamu anapokumbuka wakati alipoanza kujifunza Kimalagasi. Anaeleza hivi: “Nilikuwa nikiongoza mkutano fulani wa kutaniko lakini sikuelewa maelezo yoyote yaliyotolewa na akina ndugu. Nilikuwa nikiwaambia tu, ‘Asante.’ Baada ya kumshukuru dada mmoja kwa maelezo aliyotoa, wale waliokuwa wameketi nyuma yake walianza kunionyesha ishara kwamba maelezo yake hayakuwa sahihi. Mara moja nikamchagua ndugu, naye akatoa jibu sahihi—natumaini lilikuwa sahihi.”

ALIKUBALI MWALIKO KWA FURAHA

Katika kusanyiko mwaka wa 2005, Thierry na Nadia, mke wake, walitazama drama “Fuatia Miradi Inayomletea Mungu Heshima.” Drama hiyo ya Biblia kuhusu Timotheo iligusa mioyo yao na kuongeza tamaa yao ya kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Thierry anasema hivi: “Mwishoni mwa drama hiyo tulipokuwa tukipiga makofi, nilimnong’oneza mke wangu na kumuuliza, ‘Sisi twende wapi?’ Mke wangu aliniambia alikuwa akifikiria jambo hilohilo pia.” Muda mfupi baada ya kusanyiko hilo, wakaanza kupanga mikakati ya kutimiza lengo lao. Nadia anaeleza hivi: “Hatua kwa hatua, tulipunguza mali zetu mpaka tukabaki na vitu vilivyotoshea katika masanduku manne tu!”

Kushoto kabisa: Nadia na Marie-Madeleine; Kulia kabisa: Thierry

Walifika Madagaska mwaka 2006 na mara moja wakaanza kufurahia huduma yao. Nadia anasema hivi: “Watu tunaokutana nao wanatufanya tuwe na shangwe nyingi sana.”

Hata hivyo, miaka sita baadaye wenzi hao wa ndoa walipata changamoto. Marie-Madeleine, mama ya Nadia, aliyekuwa akiishi Ufaransa, alianguka, akavunjika mkono na kujeruhiwa kichwani. Baada ya wenzi hao kuzungumza na daktari wa Marie-Madeleine, walimwomba mama yao aje kuishi nao nchini Madagaska. Ingawa wakati huo alikuwa na umri wa miaka 80, alikubali mwaliko huo kwa furaha. Anahisije kuhusu kuishi katika nchi ya kigeni? Anaeleza hivi: “Nyakati nyingine si rahisi kuzoea hali, lakini licha ya udhaifu mbalimbali nilionao, ninahisi kwamba ninatimiza mengi kutanikoni. Na kinachonifurahisha hata zaidi kuhusiana na mpango huu wa kuhamia huku ni kwamba watoto wangu wanaweza kuendelea na utumishi wao wenye matokeo.”

“NILIJIONEA MKONO WA YEHOVA UKINISAIDIA”

Riana akitoa hotuba katika lugha ya Tandroy

Riana ni ndugu mwenye umri wa miaka 20 hivi. Alilelewa Alaotra Mangoro, eneo lenye rutuba lililoko mashariki mwa Madagaska. Alifanya vizuri katika masomo yake na alitaka kufuatilia elimu ya juu. Hata hivyo, baada ya kujifunza Biblia alibadili mawazo yake. Anasema hivi: “Nilimaliza masomo yangu ya sekondari na kumwahidi Yehova hivi: ‘Ikiwa nitafaulu mtihani wangu wa mwisho, nitaanza upainia.’” Baada ya kuhitimu shule, Riana alitimiza ahadi yake. Alianza kuishi na ndugu mwingine painia, akapata kazi ya muda, na kuanza upainia. Anasema hivi: “Huo ndio uamuzi bora zaidi niliowahi kufanya.”

Hata hivyo, watu wake wa ukoo hawakuelewa kwa nini hakufuatilia kazi nzuri yenye mshahara mnono. Anaeleza hivi: “Baba yangu, mjomba wangu, na mdogo wa kike wa nyanya (bibi) yangu walinitia moyo nifuatilie elimu ya juu. Lakini sikutaka kuruhusu chochote kinifanye niache upainia.” Baada ya muda mfupi, Riana alitamani kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ni nini kilichofanya atamani kufanya hivyo? Anasema hivi: “Wezi walivunja na kuingia mahali tulipoishi na kuiba vitu vyangu vingi. Tukio hilo lilinifanya nitafakari maneno ya Yesu kuhusu kujiwekea ‘hazina mbinguni.’ Niliamua kutafuta kwa bidii utajiri wa kiroho.” (Mt. 6:19, 20) Alihamia eneo la mbali sana kusini mwa nchi ya Madagaska—eneo lenye ukame lililo umbali wa kilomita 1,300 kutoka mahali alipokuwa akiishi. Watandroy wanaishi eneo hilo. Kwa nini alihamia huko?

Mwezi mmoja kabla ya tukio la wizi, Riana alikuwa ameanza kujifunza Biblia na wanaume wawili Watandroy. Alijifunza maneno kadhaa ya lugha yao na akaanza kufikiria kuhusu Watandroy wengi ambao hawakuwa wamepata ujumbe wa Ufalme. Anaeleza hivi: “Nilisali kwa Yehova anisaidie nihamie eneo hilo la watu wanaozungumza lugha ya Tandroy.”

Riana alihamia eneo hilo na mara moja akakumbana na changamoto. Hakuweza kupata kazi. Mwanamume mmoja alimwambia hivi: “Kwa nini ulikuja huku? Watu wa sehemu hii huenda kutafuta kazi huko ulikotoka!” Baada ya majuma mawili, Riana alienda kuhudhuria kusanyiko la eneo akiwa na pesa kidogo sana, bila kujua atafanya nini. Siku ya mwisho ya kusanyiko hilo, ndugu mmoja aliingiza kitu fulani katika mfuko wa koti la Riana. Kilikuwa kiasi kikubwa cha pesa kilichomwezesha kusafiri kurudi eneo la Antandroy na kuanzisha biashara ndogo ya maziwa ya mgando. Riana anasema hivi: “Nilijionea mkono wa Yehova ukinisaidia kwa wakati mwafaka. Ningeweza kuendelea kuwasaidia wale ambao hawakuwa wamepata fursa ya kujifunza kumhusu Yehova!” Pia, kulikuwa na kazi nyingi kutanikoni. Riana anaendelea kusema hivi: “Nilipewa mgawo wa kutoa hotuba ya watu wote kila baada ya majuma mawili. Yehova alikuwa akinizoeza kupitia tengenezo lake.” Leo, Riana anaendelea kuwahubiria ujumbe wa Ufalme watu wengi wanaozungumza lugha ya Tandroy, wanaotaka kujifunza kumhusu Yehova.

‘ABARIKIWA NA MUNGU WA KWELI’

Yehova anatuhakikishia kwamba ‘kila mtu anayejitafutia baraka duniani atabarikiwa na Mungu wa kweli.’ (Isa. 65:16) Tunapojitahidi kushinda mambo yanayotuzuia kupanua utumishi wetu, tunajionea baraka za Yehova. Mfikirie Sylviana, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii. Kumbuka kwamba alihisi hangeweza kujitolea katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Kwa nini alihisi hivyo? Anaeleza hivi: “Mguu wangu wa kushoto ni mfupi kuliko mguu wa kulia kwa sentimita 9. Hivyo, mimi huchechemea na ninachoka haraka.”

Sylviana (kushoto) na Sylvie Ann (kulia) pamoja na Doratine kwenye siku yake ya ubatizo

Hata hivyo, katika mwaka wa 2014, Sylviana aliungana na Sylvie Ann, dada kijana painia kutanikoni, nao wakahamia katika kijiji kidogo kilichoko umbali wa kilomita 85 kutoka nyumbani kwao. Licha ya changamoto hizo, Sylviana alitimiza ndoto yake—naye akapata baraka kubwa! Anaeleza hivi: “Mwaka mmoja tu baada ya kufika katika mgawo wangu, Doratine, mwanamke niliyejifunza naye Biblia alibatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko.”

“NITAKUSAIDIA”

Kama tunavyoona kutokana na maelezo ya wajitoleaji hao wenye imani, tunapojitahidi kushinda kizuizi fulani ili kupanua huduma yetu tunajionea kibinafsi ukweli wa ahadi hii ambayo Yehova amewapa watumishi wake: “Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.” (Isa. 41:10) Tunapojionea jinsi Yehova anavyotimiza ahadi yake, uhusiano wetu pamoja naye unakuwa imara zaidi. Zaidi ya hayo, kujitoa kwa hiari katika nchi tunayoishi au katika nchi ya kigeni, hututayarisha kwa ajili ya utendaji wa kitheokrasi katika ulimwengu mpya. Kama Didier, aliyetajwa awali anavyosema, “kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa ni mazoezi mazuri kwa ajili ya wakati ujao!” Tunawatia moyo wahubiri wengi zaidi waanze mazoezi hayo bila kukawia!

^ fu. 4 Wajitoleaji hao walitoka Guadeloupe, Jamhuri ya Cheki, Kanada, Luxembourg, Marekani, New Caledonia, Sweden, Ufaransa, Uingereza, Ujerumani, na Uswisi.

^ fu. 8 Sasa Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme imechukua mahali pa shule hiyo. Watumishi wa wakati wote wanaotumikia katika nchi ya kigeni na ambao wanatimiza matakwa wanaweza kujiandikisha wahudhurie shule hii nchini mwao au katika nchi nyingine ambapo shule hiyo inafanywa katika lugha yao ya mama.