Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | WAZAZI

Kuwafundisha Watoto Kutii

Kuwafundisha Watoto Kutii

KIKWAZO

Wewe na mwana wako mwenye umri wa miaka minne mnagombana, na inaonekana kwamba sikuzote mtoto wako hushinda.

  • Unapomwambia afanye jambo fulani anakataa na kukupuuza. *

  • Unapomwambia asifanye jambo fulani analotaka kufanya, hukasirika.

Unajiuliza, ‘Je, hii ni tabia ya kipindi tu? Nitarajie kwamba ataiacha baada ya muda?’

Unaweza kumfundisha mtoto wako kuwa na utii. Hata hivyo, kabla ya kuzungumzia jinsi ya kufanya hivyo, fikiria sababu moja inayomfanya awe na tabia hiyo isiyofaa.

KWA NINI HILO HUTUKIA

Mtoto wako alipokuwa mchanga ulikuwa na wajibu wa kumtunza. Ulimfanyia mtoto jambo lolote alilotaka. Alipolia, ulikuja haraka na kuhakikisha kwamba unampa chochote alichohitaji. Kwa kweli, jambo hilo lilikuwa lenye kufaa na muhimu. Mtoto mchanga huhitaji uangalizi wa wazazi wake daima.

Hata hivyo, baada ya kutendewa hivyo kwa miezi kadhaa, mtoto huanza kutenda kana kwamba ni mkuu wa nyumba na kuwafanya wazazi wake kuwa watumishi walio tayari kutimiza mahitaji yake. Kisha, anapofikisha umri wa miaka miwili hivi, mtoto huyo anagundua ukweli huu wa mambo: “Utawala” wake umeisha. Wazazi wake hawafuati tena maagizo yake; wanatarajia yeye afuate maagizo yao. Hilo linamshtua sana mtoto! Baadhi ya watoto huitikia hali hiyo kwa kukasirika. Wengine hujaribu mamlaka ya wazazi wao kwa kutowatii.

Katika kipindi hicho kigumu, wazazi wanahitaji kudhihirisha wazi mamlaka yao mpya, yaani, kutoa mwongozo ulio wazi wa kile ambacho wanatarajia kutoka kwa mtoto. Lakini, namna gani ikiwa mtoto anapuuza au anakataa mwongozo huo, kama ilivyoonyeshwa katika kisa kilichotangulia?

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Ongoza mambo. Mtoto wako hawezi kutii mamlaka yako ikiwa hataona kwamba unaongoza mambo. Hivyo, unahitaji kuonyesha mamlaka yako kwa usawaziko. Katika miaka iliyopita, baadhi ya watu wanaojiita wataalamu wamedai kwamba neno “mamlaka” lina maana isiyofaa. Mmoja wao hata alidai kwamba mamlaka ya wazazi “haifai” na “hailingani na maadili.” Hata hivyo, ikiwa wazazi watawapa uhuru mwingi, jambo hilo linaweza kuwafanya watoto wakose mwelekeo, wawe walioendekezwa, na wahisi kwamba wana haki ya kupata chochote wanachotaka. Kufanya hivyo hakutamsaidia mtoto kujiandaa na majukumu akiwa mtu mzima.—Kanuni ya Biblia: Methali 29:15.

Toa nidhamu. Kamusi moja inafafanua nidhamu kuwa “mazoezi yanayotokeza utii au kujidhibiti, na mara nyingi adhabu hutolewa sheria zinapovunjwa.” Hata hivyo, nidhamu haipaswi kamwe kuwa yenye kupita kiasi au kwa ukali. Kwa upande mwingine, inapaswa kuwa wazi au inayofaa ili kumsaidia mtoto kujua jambo la kufanyia kazi.—Kanuni ya Biblia: Methali 23:13.

Eleza mambo waziwazi. Baadhi ya wazazi huwaomba tu watoto wao watii. (“Ningependa usafishe chumba chako—Sawa?”) Huenda wazazi wakahisi kwamba hiyo ni njia nzuri. Hata hivyo, mbinu hiyo huenda ikamfanya mzazi asiwe na mamlaka na kumpa mtoto uhuru wa kufikiria faida na hasara za ombi hilo na kisha kuamua iwapo atatii. Badala ya kuacha mamlaka yako, toa mwongozo kwa kueleza mambo waziwazi.—Kanuni ya Biblia: 1 Wakorintho 14:9.

Uwe na msimamo. Ukisema hapana, shikamana na uamuzi huo na hakikisha kwamba wewe na mwenzi wako mnashirikiana. Ikiwa umeamua kutoa nidhamu, shikamana na uamuzi wako. Usijiingize katika makubaliano au mazungumzo ya muda mrefu kuhusu kwa nini ulifanya uamuzi huo. Hivyo itakuwa rahisi sana kwa mtoto wako na kwako, ikiwa ‘utaacha Ndiyo yako imaanishe Ndiyo, na Siyo yako, Siyo.’—Yakobo 5:12.

Uwe mwenye upendo. Familia haipaswi kuongozwa kidemokrasia au kidikteta. Badala yake, ni mpango wa Mungu ambao watoto wanaweza kuongozwa kwa upendo na hivyo kuwa watu wazima wenye kutegemeka. Ikiwa sehemu ya jambo hilo, nidhamu itamfundisha mtoto wako kutii na kumsaidia kuhisi salama chini ya uangalizi wako wenye upendo.

^ fu. 5 Ingawa mtoto anayetajwa ni mvulana, kanuni zinazozungumziwa katika makala hii zinawahusu pia wasichana.