Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Mafanikio ya Kweli Yanapatikana Jinsi Gani?

Mafanikio ya Kweli Yanapatikana Jinsi Gani?

JE, KUNA jambo baya kuliko kushindwa? Ndiyo, jambo hilo ni mafanikio ya uwongo. Unaposhindwa kutimiza jambo fulani, unaweza kujitahidi kulirekebisha. Hata unaweza kuazimia kuliboresha jambo hilo.

Hali ni tofauti na mafanikio ya uwongo. Mtu anaweza kudhani amefanikiwa ilhali ameshindwa. Lakini anapotambua anahitaji kufanya marekebisho, huenda ikawa kuchelewa mno.

Fikiria mfano ufuatao. Yesu Kristo aliuliza hivi: “Mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote lakini aipoteze nafsi yake?” (Mathayo 16:26) Hoja hiyo ya Yesu inawahusu wale ambao wanadhani kwamba mafanikio ya kweli yanaletwa na pesa na mali nyingi, ambacho ni chanzo kikuu cha mafanikio ya uwongo. Tom Denham, mshauri wa mambo ya kazi alisema: “Kufikiria tu cheo, kupata pesa zaidi au kutafuta mali nyingi, hakumfanyi mtu aridhike. Kupima mafanikio kwa njia hiyo si sahihi na hakuleti furaha ya kweli.”

Bila shaka, watu wengi wanakubaliana na maneno hayo. Utafiti uliofanywa nchini Marekani kuhusu “mambo yanayochangia maisha yenye mafanikio,” uliorodhesha “kuwa na pesa nyingi” katika nafasi ya 20 kati ya mambo 22. Kati ya mambo yaliyoorodheshwa kwanza ni afya njema, mahusiano mema, na kazi unayoipenda.

Bila shaka, watu wengi wanaweza kutofautisha kati ya mafanikio ya kweli na mafanikio ya uwongo, wanapoombwa kufanya hivyo. Hata hivyo ni vigumu kufanya uamuzi sahihi kuhusiana na mafanikio ya kweli.