Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Sanamu

Sanamu

Mamilioni ya watu wanyoofu hutumia sanamu katika ibada yao. Lakini je, Biblia inakubali zoea hilo? Je, linampendeza Mungu?

Je, Wayahudi waaminifu nyakati za Biblia walitumia sanamu katika ibada?

“Usijifanyie sanamu ya kuchongwa wala umbo lililo kama kitu chochote kilicho juu mbinguni wala kilicho chini duniani wala kilicho ndani ya maji chini ya dunia. Usiviinamie wala kushawishiwa kuvitumikia.”—Kutoka 20:4, 5.

Kutumia sanamu katika ibada kumekatazwa tena na tena katika Maandiko ya Kiebrania ambayo pia huitwa Agano la Kale

MAONI YA WENGI

Kulingana na kitabu New Catholic Encyclopedia, Wayahudi walitumia sanamu nyingi katika ibada “na sanamu hizo ziliheshimiwa, kustahiwa na kuabudiwa.” * Kitabu hicho kinataja mifano ya michongo mingi ya matunda, maua, na wanyama iliyopamba hekalu la Yerusalemu.—1 Wafalme 6:18; 7:36.

UNACHOPASWA KUJUA

Tofauti na vile kitabu New Catholic Encyclopedia kinavyosema, Wayahudi waaminifu hawakuabudu michongo na michoro iliyokuwa hekaluni. Kwa kweli, Biblia haitaji Mwisraeli yeyote mwaminifu aliyeabudu kwa kutumia sanamu.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mungu alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe, wala sitazipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.”—Isaya 42:8.

 Je, Wakristo wa mapema walitumia sanamu katika ibada?

“Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu? . . . Mwache kugusa kitu kilicho najisi.” —2 Wakorintho 6:16, 17.

“Wakristo wa mapema hawangethubutu kuweka sanamu katika makanisa, na wangeona kusujudu au kusali mbele yazo kuwa sawa na kuabudu sanamu.” —Kitabu History of the Christian Church

MAONI YA WENGI

Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema: “Hatuwezi kutilia shaka kwamba Wakristo wa mapema walitumia sanamu katika ibada.” Kinaendelea kusema: “Makaburi ya Wakristo hao yana vitu vingi vya kuchongwa. . . . Sanamu pia zilipamba vyumba vitakatifu vya ibada na vya mazishi.” *

UNACHOPASWA KUJUA

Sanamu za kale zaidi zinazopatikana katika makaburi hayo, ambayo yalikuwa vijia vilivyochimbwa ardhini, zilitengenezwa karne ya tatu. Yaani, miaka 200 hivi baada ya Yesu kufa. Kwa hiyo, ibada inayorejezewa na kitabu New Catholic Encyclopedia kuwa “ibada ya Ukristo wa mapema” si ibada ya Ukristo wa mapema zaidi, yaani, Ukristo wa wanafunzi wa karne ya kwanza na inayoelezewa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo au Agano Jipya. Kwa kuwa sanamu zilikuwa kwenye makaburi hayo, basi kufikia karne ya tatu zoea la wapagani la kutumia sanamu lilikuwa limeingizwa katika Ukristo, labda ili kuwavuta wapagani wajiunge na Ukristo. *

BIBLIA INASEMA NINI?

 “Ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 10:14.

Je, sanamu inapaswa kutumiwa kama kifaa cha ibada?

“Jilindeni na sanamu.”—1 Yohana 5:21.

Kutumia sanamu katika ibada ni zoea la kidini ambalo haliungwi mkono na Biblia. Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova hawatumii sanamu katika ibada, wala hawana sanamu za kidini nyumbani au mahali wanapoabudia

MAONI YA WENGI

“Kwa kuwa ibada inayopewa sanamu humfikia mtu anayewakilishwa na sanamu . . . , basi ni sawa kuabudu sanamu kwa sababu inamwakilisha mtu huyo,” kinasema kitabu New Catholic Encyclopedia.

UNACHOPASWA KUJUA

Yesu alipowafundisha wafuasi wake kusali hakuwaambia watumie sanamu. Fundisho la kutumia sanamu kumwabudu Mungu wa kweli halipatikani katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

BIBLIA INASEMA NINI?

 “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Mathayo 4:10.

^ fu. 7 Kitabu New Catholic Encyclopedia kinafafanua kuheshimu sanamu kuwa “tendo la kidini, na pia ni tendo la ibada.”

^ fu. 13 Katika habari hii, sanamu zinatia ndani alama, picha, michoro, michongo, au chochote kinachoabudiwa.

^ fu. 14 Zamani sanamu zilitumiwa katika maeneo mengi kama vile Misri, Ugiriki, na India.