Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Watu Wanawezaje Kuishi kwa Amani?

Watu Wanawezaje Kuishi kwa Amani?

Frank na Jerry walikuwa majirani wazuri, lakini mambo yalibadilika Jerry alipofanya sherehe usiku. * Frank alilalamika kuhusu kelele naye Jerry akakasirika sana. Wakaanza kubishana. Mwishowe wakaacha kushirikiana.

FRANK na Jerry walikabili jambo la kawaida. Watu wanapokosana, mara nyingi wanakasirikiana, au hata kulaumiana. Na wakishindwa kusuluhisha matatizo yao, urafiki wao unaweza kuvunjika.

Labda umewahi kupatwa na hali kama hiyo. Ikiwa ndivyo, bila shaka hukuifurahia! Kwa kweli, wengi wetu tungependa kuishi na rafiki na jirani zetu kwa amani na umoja. Tunawezaje kufanya hivyo hata tunapokosana? Je, tunaweza kushinda hisia zisizofaa na kuwasamehe wanaotukosea? Je, tunaweza kutatua matatizo kwa amani?

Fikiria tena tatizo la Frank na Jerry. Urafiki wao ulianza kusambaratika hatua kwa hatua: (1) Jerry hakujali, (2) Frank alilalamika kwa njia iliyomkasirisha Jerry, (3) wote walikasirika, na (4) wote walikataa kukubaliana.

Hata hivyo, baada ya muda walielewana. Walitatua tofauti zao na kufanya amani. Ni nini kilichowasaidia? Walitumia kanuni ambazo zimewasaidia marafiki wengi kushinda hali ngumu na vilevile kuimarisha urafiki wao.

Kanuni hizo zinapatikana katika kitabu ambacho kimesambazwa zaidi duniani, yaani, Biblia. Inatutia moyo tusitawishe sifa zinazoleta amani na kutuliza maumivu ya kihisia—sifa kama utambuzi, ufahamu, fadhili, upendo, na subira.—Methali 14:29; 1 Wakorintho 13:4, 5.

Frank na Jerry ni mifano miwili tu inayoonyesha jinsi Biblia ilivyo na nguvu za kubadili maisha. Kuna mifano mingine  mingi, kutia ndani watu walioshinda tabia mbaya zilizokita mizizi. Kwa mfano, Robert anayeishi huko Australia, alishinda hasira yake kali. Nelson, anayeishi huko Timor Mashariki, alishinda chuki na akafanya amani na adui yake wa zamani. Biblia iliwasaidiaje Robert na Nelson? Mwandishi wa Amkeni! aliwahoji kuhusu hilo.

MAHOJIANO YA 1

ROBERT, unaweza kutueleza kuhusu malezi yako?

Nililelewa katika familia isiyo na furaha. Kwa mfano, baba yangu alikuwa na hasira kali na alinipiga mara kwa mara. Nyakati nyingine alinipiga mpaka nikatokwa damu na kuzimia. Matokeo yake, nikawa mwenye hasira na mjeuri. Nilipokuwa tineja, nilipelekwa kwenye shule ya watoto watukutu na nikakaa huko miaka miwili. Baadaye, nilimpiga mtu vibaya na nikafungwa katika gereza lenye ulinzi mkali. Nilipotoka gerezani, nilienda Australia ili kuanza maisha upya.

Robert alikuwa kijana mwenye hasira na mjeuri na hata alifungwa gerezani

Je, kwenda Australia kulibadili tabia yako?

Kilichonibadili si kuhama, bali ni mambo niliyojifunza katika Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, bado nilipambana ili kudhibiti hasira yangu na wakati mwingine nilivunjika moyo na kujihisi sifai. Lakini siku moja nilitafakari andiko la Methali 19:11, linalosema: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” Nikitamani kusitawisha ufahamu huo, nilianza kufikiria kile kinachochochea hisia, maneno, na matendo yetu. Hivyo, pole kwa pole nikaanza kuwa mwenye subira, mwenye kusamehe na kuwaelewa watu.

Unaweza kutoa mfano?

Siku moja nilimuudhi rafiki yangu bila kukusudia, na akanifokea kwa hasira mbele ya watu. Kwa kweli, niliaibika sana! Hata hivyo, nilikumbuka shauri la Biblia linalosema, “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu” na nikaomba msamaha haraka. (Waroma 12:17) Rafiki yangu alipotulia, nilizungumza naye faraghani na nikatambua alikuwa akipambana na matatizo ya kifamilia. Tulifikia mapatano na baadaye alinipa koti zuri sana kama zawadi. Sijui ingekuwaje kama ningetenda kwa hasira kama zamani.

Unashughulikiaje matatizo ya familia?

Mimi na mke wangu tuna kijana mwenye umri wa miaka 20, na kama familia nyingine, nyakati nyingine tunakosana. Lakini nimejifunza mengi kutoka katika Biblia, kutia ndani umuhimu wa kusema, “Samahani.” Inashangaza kuona jinsi maneno hayo ya unyoofu yanavyoweza kuzuia au kutatua ugomvi.

MAHOJIANO YA 2

 NELSON, wewe ni mchangamfu na mwenye urafiki. Lakini zamani ulikuwa mwenye chuki sana. Je, ni kweli?

Ndiyo! Nilipokuwa kijana, nilijiunga na kikundi cha kisiasa kilichopinga serikali. Pia, nilikichukia chama cha kisiasa cha upinzani kilichokuwa kikiwania kuongoza wilaya yetu. Ili niwe mpiganaji hodari, nilijifunza kupigana na nilimpiga mtu yeyote aliyeniudhi.

Alipokuwa kijana, Nelson alijiunga na kikundi cha kisiasa kilichopinga serikali

Kwa nini ulibadilika?

Nilianza kujifunza Biblia na kutumia mafundisho yake, na mambo mawili yalinigusa moyo sana. Jambo la kwanza ni hili: “Mambo yote . . . mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Pili: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Niliwaona Mashahidi walionifundisha Biblia wakionyesha upendo huo, bila kuzingatia rangi au jamii ya mtu. Nilitaka kuwa kama wao. Kwa kweli , nilifanikiwa, kwa kuwa watu walionifahamu zamani walishangaa sana na wakaacha kuniogopa.

Je, uliwahi kurudia tena tabia yako ya zamani?

Sijawahi kurudia hadharani. Lakini wakati mwingine nilishindwa kudhibiti hasira yangu nyumbani. Pindi moja, nilikasirika na kumpiga mke wangu, jambo ambalo ninajutia sana. Ingawa alinisamehe, jambo hilo lilinifanya nijitahidi zaidi kudhibiti hisia zangu.

Ulisema watu waliacha kukuogopa. Unaweza kutoa mfano?

Ndiyo. Siku moja, nilikutana na Augusto, mwanachama mashuhuri wa chama cha upinzani nilichokitaja mwanzoni. Alikuwa na wasiwasi sana. Lakini nilimsalimu kwa uchangamfu, nikamwomba tusahau tofauti zetu na nikamkaribisha nyumbani. Alikubali na alishangaa kuona mabadiliko niliyofanya, hivi kwamba akaanza pia kujifunza Biblia. Sasa mimi na Augusto ni marafiki wa karibu na vilevile ndugu kiroho.

 “Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”

Vyanzo vya ugomvi hutofautiana, na si kila mtu atakayeitikia vizuri jitihada zako za kufanya amani. Hivyo, kwa kufaa Biblia inashauri hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.

Watu waliotajwa katika makala hii wanathibitisha kwamba hekima inayopatikana katika Biblia inafaa kabisa—na tukiitumia inaweza kupindua hata mitazamo isiyofaa ‘yenye nguvu.’ (2 Wakorintho 10:4) Methali 3:17, 18 inasema hivi kuhusu hekima hiyo: “Njia zake ni njia za uzuri, na barabara zake zote ni amani. Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.”

Nelson na Augusto sasa ni marafiki

Je, ungependa kuwa mwenye amani na furaha zaidi? Je, ungependa kuwa na urafiki wenye kudumu utakaostahimili hali ngumu? Ikiwa ndivyo, fuata ushauri wa Biblia nawe utajifunza jinsi ya kufanya hivyo.

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.