Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi ya Kuzungumza na Kijana Wako Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu

Jinsi ya Kuzungumza na Kijana Wako Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu

KIKWAZO

Umesikia kwamba ni kawaida kwa vijana kutuma ujumbe mchafu. Huenda ukajiuliza hivi: ‘Je, kijana wangu anaweza kufanya hivyo?’

Unataka kuzungumzia jambo hilo na mtoto wako lakini unajiuliza utafanyaje hivyo. Kwanza fikiria kwa nini vijana fulani hutuma ujumbe mchafu na kwa nini hupaswi kupuuza jambo hilo. *

KWA NINI HILI HUTUKIA

  • Vijana fulani hutuma ujumbe mchafu wa ngono ili kumchezea kimapenzi mtu wanayempenda.

  • Katika visa vingine, msichana hutuma picha yake akiwa uchi kwa sababu anashinikizwa na mvulana kufanya hivyo.

  • Nyakati nyingine mvulana atawatumia watu wengine picha ya msichana akiwa uchi ili kuwafurahisha rafiki zake au kulipiza kisasi uhusiano wao unapovunjika.

Vyovyote vile, kijana mwenye simu ya mkononi anaweza kuingia matatani. “Maisha ya mtu yanaweza kubadilika milele kwa sababu tu ya kutuma ujumbe,” kinasema kitabu CyberSafe (Kutumia Intaneti kwa Njia Salama).

Watu wengi hawatambui kwamba mara tu picha inapoingizwa kwenye Intaneti, mtumaji hawezi tena kudhibiti jinsi picha hiyo itakavyotumiwa. Ripoti moja ya Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) ilielezea kisa cha msichana mwenye umri wa miaka 18 ambaye “alijiua baada ya kugundua kwamba picha yake akiwa uchi aliyokuwa amemtumia rafiki yake wa kiume kupitia simu ya mkononi ilisambazwa kwa mamia ya vijana shuleni. Inasemekana kwamba wanafunzi wengine waliendelea kusambaza picha hiyo na pia walimsumbua msichana huyo.”

Masuala ya kisheria hutokea pia mtu anapotuma ujumbe mchafu. Kwa mfano, katika maeneo fulani, watoto ambao wamewatumia watoto wengine picha chafu za ngono wameshtakiwa kwa kosa la ponografia zinazohusisha watoto na wamelazimika kujiandikisha katika orodha ya wahalifu wa makosa ya kingono. Ukiwa mzazi, wewe pia unaweza kuwajibika kisheria ikiwa simu ya mtoto wako imesajiliwa chini ya jina lako, au ikiwa hukuchukua hatua yoyote kumzuia mtoto wako kutuma ujumbe mchafu.

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Weka sheria zilizo wazi. Ingawa huwezi kudhibiti kikamili jinsi kijana wako anavyotumia simu ya mkononi, unaweza kuhakikisha kwamba anajua sheria zako na pia matokeo ya kuvunja sheria hizo. Pia, kumbuka kwamba ukiwa mzazi, una haki ya kuchunguza jinsi kijana wako anavyotumia simu.Kanuni ya Biblia: Waefeso 6:1.

Msaidie kijana wako afikirie kuhusu tatizo hilo. Unaweza kusema: “Watu wana maoni yanayotofautiana kuhusu ni nini kinachoamua ikiwa ujumbe ni mchafu. Wewe una maoni gani?” “Unadhani ni picha gani ambazo mtu hapaswi kutuma?” “Katika maeneo fulani ni hatia kwa mtoto kutuma picha ya mtoto mwingine akiwa uchi. Wewe unafikiri kufanya hivyo ni vibaya?” “Kwa nini kutuma ujumbe mchafu ni upotovu wa maadili?” Msikilize kijana wako kwa makini anapojieleza, na umsaidie afikirie madhara ya kutuma ujumbe wa aina hiyo.Kanuni ya Biblia: Waebrania 5:14.

Fikiria madhara ya kutuma ujumbe mchafu

Zungumzia kisa kinachoweza kutokea. Unaweza kumwambia binti yako hivi: “Wazia msichana anashinikizwa na mvulana amtumie ujumbe mchafu. Msichana huyo anapaswa kufanya nini? Je, akubali ili urafiki wao usivunjike? Akatae kufanya hivyo lakini aendelee kucheza naye kimapenzi? Akatize uhusiano? Je, amwambie mtu mzima?” Msaidie binti yako achanganue hali hizo. Bila shaka, unaweza kutumia njia hiyohiyo unapozungumza na mwana wako.Kanuni ya Biblia: Wagalatia 6:7.

Mchochee kijana wako afikirie faida ya kuwa na sifa nzuri. Uliza maswali kama haya: Unafikiri kuwa na sifa nzuri ni muhimu kadiri gani? Unataka ujulikane kwa sifa gani? Ungehisije ikiwa ungemwaibisha mtu mwingine kwa kusambaza picha yake chafu? Ungehisije ikiwa ungesimama imara na kutetea lililo sawa?’ Msaidie kijana wako ‘awe na dhamiri njema.’1 Petro 3:16.

Mwekee mfano mzuri. Biblia inasema hekima ya kimungu ni safi kiadili na si ya kinafiki. (Yakobo 3:17) Je, maadili yako yanaonyesha kwamba unakubaliana na hilo? Kitabu CyberSafe kinasema hivi: “Sisi wenyewe tunapaswa kuweka mfano mzuri wa kutotazama picha na vituo vya Intaneti vinavyoonwa kuwa vimepotoka kimaadili au haramu.”

^ fu. 5 Kutuma ujumbe mchafu, “sexting” katika Kiingereza kunarejelea kutuma ujumbe wa maneno, picha, na video za ngono kupitia simu ya mkononi. Kwa habari zaidi, tembelea Tovuti ya jw.org/sw na usome makala yenye kichwa “Vijana Huuliza—Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma Ujumbe Mchafu?”—Angalia chini ya—MAFUNDISHO YA BIBLIA > MATINEJA.