Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Haki ya Kweli Chini ya Serikali ya Mungu

Haki ya Kweli Chini ya Serikali ya Mungu

Haki ya Kweli Chini ya Serikali ya Mungu

UNABII wa Biblia unaonyesha kwamba hivi karibuni ulimwengu uliopo utaondolewa na mahali pake patachukuliwa na ulimwengu mpya uliofanyizwa na Mungu. Isitoshe, ulimwengu huo mpya utakuwa na serikali moja tu—Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo akiwa Mfalme wake. (Ufunuo 11:15) Ufalme wa Mungu utaondoaje ukosefu wa haki? Utafanya hivyo katika njia mbili.

1. Ufalme wa Mungu utaondoa utawala wa wanadamu wenye ukosefu wa haki na usio na uwezo wa kutawala. Danieli 2:44 inasema: “Katika siku za wafalme hao [serikali] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za kibinadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

2. Ufalme wa Mungu utawaharibu waovu na kuwakomboa wenye haki. Zaburi 37:10 inasema: “Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena.” Mstari wa 28 unasema: “Yehova ni mpenda-haki, naye hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo.”

“Washikamanifu” hao watajionea utimizo wa maneno ambayo Yesu alisema katika sala yake ya kielelezo. Alisema hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Mapenzi ya Mungu ni nini kuhusiana na dunia?

Ufalme wa Mungu Utakapotawala Dunia . . .

Ufisadi na ukandamizaji utakwisha. Waebrania 1:9 inasema hivi kumhusu Yesu Kristo: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria.” Yesu akiwa Mtawala mwenye haki kabisa “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. . . . Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.”—Zaburi 72:12-14.

Wote watakuwa na chakula kingi. “Hakika dunia itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.” (Zaburi 67:6) “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Wakati mmoja Yesu aliwalisha kimuujiza maelfu ya watu, akionyesha kimbele yale atakayotimiza kupitia Ufalme wa Mungu.—Mathayo 14:15-21; 15:32-38.

Haki haitazuiwa na udhaifu wa wanadamu. “Hakuna kiumbe kisichokuwa wazi machoni pake [Mungu], bali vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Tunasoma hivi kumhusu Kristo: “Hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.”—Isaya 11:3, 4.

Utawala wa Ufalme Uko Karibu!

Kuzorota kwa hali za ulimwengu kunaonyesha kwamba mwisho wake uko karibu. “Wakati waovu wanapochipuka kama majani na wote wanaotenda mambo yenye kuumiza wanapochanuka, ni ili wao wapate kuangamizwa milele,” inasema Zaburi 92:7. Unaweza kuepukaje kukosa kibali cha Mungu na kuwa miongoni mwa wale atakaowakomboa? Yesu Kristo alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Je, ungependa kupata ujuzi huo wenye thamani? Ikiwa ndivyo, mbona usiwaombe Mashahidi wa Yehova wakusaidie kama walivyofanya Heide, Dorothy, na Firuddin, waliotajwa hapo awali? Watafurahi kujibu maswali yako bila malipo wala masharti yoyote.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

KUVUMILIA HALI INAYOONEKANA KUWA ISIYO YA HAKI

Emily, anayeishi Marekani aligunduliwa kuwa ana lukemia alipokuwa na umri wa miaka saba. Tofauti na marafiki wake ambao huugua tu homa au mafua, Emily amelazimika kuvumilia matibabu ya muda mrefu ambayo yanatia ndani tiba ya kemikali. Anasema: “Lukemia ni ugonjwa wenye kuogopesha sana!”

Ingawa anakabiliana na hali hiyo ngumu maishani, Emily hajakata tamaa. Badala yake, anangojea wakati ambapo, chini ya Ufalme wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) “Andiko ninalopenda zaidi,” anasema Emily, “ni Marko 12:30: ‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.’ Ninaposali kwa Yehova, yeye hunipa nguvu. Ninamshukuru Yehova kwa kunipa familia, kutaniko, na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya utakaokuwa Paradiso. Tumaini hilo limenisaidia sana.”

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Chini ya Ufalme wa Mungu, wanadamu wote watafurahia chakula kingi, na pia haki ya kweli na maisha bila ubaguzi