Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Miradi Inayopatana na Akili?

Je, Una Miradi Inayopatana na Akili?

Je, Una Miradi Inayopatana na Akili?

● Unataka kufanya nini maishani? Je, unatazamia mambo yanayopatana na akili, au unaota kuhusu mambo ambayo huwezi kutimiza? Mtu fulani aliyechunguza utu wa wanadamu alitoa ushauri huu wenye hekima: “Hayo nayo ni bure kabisa; ni sawa na kufukuza upepo. Afadhali kuridhika na ulicho nacho kuliko kuhangaika kwa kutamani kitu kingine.”—Mhubiri 6:9, Biblia Habari Njema.

Maneno “ulicho nacho” yanarejelea hali zetu na mambo halisi ya sasa. Kwa kweli, hakuna ubaya kujaribu kuboresha maisha yetu. Hata hivyo, jambo kuu ambalo Biblia inataja ni kwamba si jambo la hekima kufuatia miradi isiyopatana na akili. Huenda miradi hiyo ikawa umashuhuri, utajiri, mwenzi bora kabisa wa ndoa, au afya kamilifu.

Isitoshe, huenda wale ambao hufikia miradi mingine, kama vile utajiri, wakatamani kupata zaidi. Biblia inasema hivi waziwazi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato. Hilo pia ni ubatili.” (Mhubiri 5:10) Kwa sababu hiyo, watu wenye hekima kiroho hujaribu kuridhika na kile ‘walicho nacho.’ Naam, wanatambua ukweli wa maneno haya: “Hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje.”—1 Timotheo 6:7.

Wanadamu wameumbwa kwa njia ya kwamba wale wanaotosheleza mahitaji yao ya kiroho ndio wanaopata furaha nyingi zaidi. (Mathayo 5:3) Tunaweza kufanya hivyo kwa njia gani? Yesu Kristo alisema hivi: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Maneno hayo yenye thamani yanapatikana katika Biblia, na mtu yeyote anaweza kufaidika nayo.

Maneno kama hayo yanapatikana katika Zaburi 37:4. Inasema hivi: “Upate furaha tele katika Yehova, naye atakupa maombi ya moyo wako.” Akiwa Mungu Mweza-Yote, Yehova atawapa waabudu wake waaminifu vitu ambavyo hakuna mwanadamu anaweza kuwapa: afya kamilifu, vitu vya kimwili, na uzima wa milele katika Paradiso duniani. (Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4) Inapatana na akili kuamini maneno hayo.