Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Sayansi Inapatana na Biblia?

Je, Sayansi Inapatana na Biblia?

Maoni ya Biblia

Je, Sayansi Inapatana na Biblia?

“Mimi hupata shangwe katika kazi yangu ya sayansi ninapovumbua kitu kipya na kujiambia, ‘Kumbe hivi ndivyo Mungu alivyofanya!’” —HENRY SCHAEFER, PROFESA WA KEMIA.

SAYANSI hutusaidia sana kuelewa ulimwengu wa asili kwa kufunua utaratibu, usahihi, na utata ambao watu wengi huona umetokana na Mungu mwenye akili na nguvu zisizo na kifani. Kwa maoni yao, sayansi haifunui tu mambo kuhusu ulimwengu wa asili bali pia inatufunulia akili ya Mungu.

Maoni hayo yanaungwa mkono na Biblia. Waroma 1:20 inasema hivi: “Sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” Vilevile Zaburi 19:1, 2 inasema: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake. Siku moja baada ya siku nyingine hufanya maneno yabubujike, na usiku mmoja baada ya usiku mwingine huonyesha ujuzi.” Hata hivyo, licha ya mambo yake mengi yenye kustaajabisha, ulimwengu wa asili unafunua tu baadhi ya sifa za Muumba wetu.

Sayansi Ina Mipaka

Sayansi haiwezi kutufundisha kweli nyingi kumhusu Mungu. Kwa mfano, mwanasayansi anaweza kufafanua kila molekuli iliyo ndani ya keki ya chokoleti, lakini je, ufafanuzi wake unaweza kuonyesha kwa nini keki hiyo iliokwa au ni ya nani? Ili kupata majibu ya maswali kama hayo ambayo watu wengi wataona ndiyo muhimu zaidi, mtu anapaswa kumwuliza yule aliyeoka keki hiyo.

Vivyo hivyo, sayansi “inatoa habari nyingi hakika,” akaandika Erwin Schrödinger, mwanafizikia kutoka Austria ambaye pia ni mshindi wa Tuzo la Nobeli, “lakini haifunui chochote . . . kabisa kuhusu mambo yaliyo muhimu kwetu.” Anasema mambo hayo yanatia ndani “Mungu na umilele.” Kwa mfano, ni Mungu peke yake anayeweza kujibu maswali yafuatayo: Kusudi la ulimwengu ni nini? Kwa nini sayari yetu ina viumbe wengi, kutia ndani viumbe wenye akili? Ikiwa kwa kweli Mungu ndiye mweza-yote, kwa nini anaruhusu uovu na kuteseka uendelee? Na je, kuna tumaini lolote kwa wafu?

Je, Mungu amejibu maswali hayo? Ndiyo, Biblia hujibu maswali hayo. (2 Timotheo 3:16) Huenda ukauliza, ‘Kuna uthibitisho gani kwamba kwa kweli Biblia ilitoka kwa Mungu?’ Kwa maoni ya wanasayansi, yale ambayo Biblia inasema kuhusu ulimwengu unaotuzunguka lazima yapatane na mambo hakika ya kisayansi, kwa hiyo, yale ambayo Biblia inasema hayapaswi kupingana na kile ambacho ameumba. Je, Biblia inapatana na sayansi? Chunguza mifano michache.

Biblia Ilitangulia Sayansi

Biblia ilipokuwa ikiandikwa, watu wengi waliamini kwamba miungu mbalimbali iliishi ulimwenguni na kwamba miungu hiyo ndiyo iliyodhibiti jua, mwezi, hali ya hewa, uzazi, na kadhalika, na vitu hivyo havikudhibitiwa na sheria za asili. Lakini manabii Waebrania wa kale wa Mungu hawakuamini hivyo. Bila shaka walijua kwamba Yehova Mungu angeweza kudhibiti moja kwa moja ulimwengu wa asili na alifanya hivyo pindi fulani hususa. (Yoshua 10:12-14; 2 Wafalme 20:9-11) Hata hivyo, John Lennox, profesa wa hesabu katika Chuo Kikuu cha Oxford, Uingereza, alisema kwamba manabii hao “hawakuhitaji kuacha kuamini kwamba [miungu ya kuwaziwa] ndiyo iliyodhibiti ulimwengu . . . , kwa kuwa hawakuwa wakiamini miungu hiyo. Hawakujihusisha katika imani hiyo ya kishirikina kwa sababu waliamini kwamba kuna Mungu Mmoja wa Kweli, Muumba wa mbingu na dunia.”

Imani hiyo iliwalinda namna gani na ushirikina? Kwanza, Mungu wa kweli aliwafunulia kwamba anaongoza ulimwengu kupitia sheria hususa. Kwa mfano, zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, Yehova Mungu alimwuliza hivi mtumishi wake Ayubu: “Je, umepata kujua sheria za mbingu?” (Ayubu 38:33) Katika karne ya saba K.W.K., nabii Yeremia aliandika kuhusu “sheria za mbingu na dunia.”—Yeremia 33:25.

Hivyo, wote walioishi nyakati za kale na ambao waliamini yale ambayo manabii wa Biblia waliandika wangejua kwamba ulimwengu hauongozwi na miungu ya kuwaziwa yenye hisia zinazobadilika-badilika, bali na sheria ambazo wanadamu wanaweza kuchunguza na kuelewa. Kwa sababu hiyo, watu waliomwogopa Mungu hawakuabudu vitu ambavyo Mungu ameumba kama vile jua, mwezi, nyota, wala hawakuwa na ushirikina wowote kuvielekea. (Kumbukumbu la Torati 4:15-19) Badala yake, waliona walipaswa kuchunguza uumbaji wa Mungu ili kuona hekima, nguvu, na sifa nyingine za Mungu.—Zaburi 8:3-9; Methali 3:19, 20.

Kwa kupatana na maoni ya wanasayansi wengi leo, Waebrania wa kale pia waliamini kwamba dunia ilikuwa na mwanzo. Mwanzo 1:1 inasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Pia, miaka 3,500 hivi iliyopita, Mungu alimfunulia mtumishi wake Ayubu kwamba dunia ‘imeitundikwa pasipo na kitu,’ au inaning’inia angani. (Ayubu 26:7) Na pia, zaidi ya miaka 2,500 iliyopita, nabii Isaya aliandika kwamba dunia ni mviringo au duara.—Isaya 40:22. *

Naam, Biblia inapatana na yale ambayo sayansi inasema kuhusu ulimwengu wa asili. Kwa kweli Biblia na sayansi hutusaidia kujifunza kumhusu Mungu kwani zinapatana. Kupuuza moja ni kama kufunga mlango ili tusipate ujuzi kumhusu Mungu.—Zaburi 119:105; Isaya 40:26.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kwa maelezo zaidi kuhusu kuwepo kwa Mungu na usahihi wa Biblia, tafadhali soma broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Uumbaji unaweza kutufundisha nini kumhusu Mungu?—Waroma 1:20.

● Ni mambo gani kumhusu Mungu ambayo hatuwezi kujifunza kupitia sayansi?—2 Timotheo 3:16.

● Kwa nini manabii wa kale wa Mungu wa kweli hawakuwa na ushirikina kuhusu uumbaji?—Yeremia 33:25.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Ulimwengu unaongozwa na sheria hususa—“sheria za mbingu na dunia.”—YEREMIA 33:25