Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ulimwengu Ungekuwa Bora Bila Dini?

Je, Ulimwengu Ungekuwa Bora Bila Dini?

Je, Ulimwengu Ungekuwa Bora Bila Dini?

KIKUNDI kipya cha watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu kinatarajia ulimwengu usio na dini—ulimwengu usio na walipuaji mabomu waliojitolea kufa, vita vya kidini, wainjilisti wa televisheni wanaowalaghai kondoo zao. Je, matarajio hayo yanakuvutia?

Kabla ya kujibu swali hilo, jiulize, ‘Je, kuna uthibitisho wowote kwamba ulimwengu utakuwa bora bila dini?’ Hebu fikiria hili: Wakambodia milioni 1.5 hivi walikufa wakati wanamgambo wa Khmer Rouge walipokuwa wakijaribu kuanzisha serikali ya Kikomunisti isiyoamini kwamba kuna Mungu. Na katika Muungano wa Sovieti uliotangaza waziwazi kwamba hauamini kuna Mungu, utawala wa Joseph Stalin ulisababisha vifo vya makumi ya mamilioni ya watu. Ni kweli kwamba uovu huo haukusababishwa moja kwa moja na watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu. Lakini unaonyesha kwamba utawala wa watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu hauleti amani na umoja.

Watu wengi wanakubali kwamba dini imesababisha matatizo mengi. Lakini je, Mungu ndiye wa kulaumiwa? La! Hatuwezi kumlaumu Mungu sawa tu na vile hatuwezi kumlaumu mtengenezaji wa magari ikiwa dereva wa gari angesababisha aksidenti kwa sababu ya kutumia simu ya mkononi. Kuna mambo mengi yanayofanya wanadamu wateseke, na kisababishi kikuu hakina uhusiano wowote na dini. Biblia inasema kwamba kisababishi hicho ni hali ya kutokamilika tuliyorithi. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Mwelekeo huo wa dhambi hufanya watu wawe na ubinafsi, kiburi, kutaka kujitegemea, na wajeuri. (Mwanzo 8:21) Pia unafanya watu wapuuze makosa na watake kufuata mafundisho ambayo yanapuuza makosa yao. (Waroma 1:24-27) Yesu Kristo alisema hivi: “Mawazo mabaya hutoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uwongo, makufuru.”—Mathayo 15:19.

Tofauti Kati ya Ibada ya Kweli na Ibada ya Uwongo

Kufikia hapa, lazima tofauti ionekane kati ya ibada ya kweli—yaani, ibada ambayo Mungu anakubali—na ibada ya uwongo. Ibada ya kweli huwasaidia watu wapinge mwelekeo wao wa dhambi. Inawatia moyo wawe na upendo wa kujidhabihu, amani, fadhili, wema, upole, kujizuia, wawe washikamanifu kwa wenzi wao wa ndoa, na kuwaheshimu wengine. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa upande mwingine, ibada ya uwongo hufuata mwelekeo unaopendwa na watu wengi—ili ‘kufurahisha masikio ya watu,’ kama Biblia inavyosema—kwa kuruhusu matendo mabaya ambayo Yesu aliyashutumu.—2 Timotheo 4:3.

Je, inawezekana kwamba imani ya kwamba hakuna Mungu imechangia hali ya kutatanisha kuhusu maadili? Profesa wa sheria, Phillip Johnson, anasema kwamba ikiwa ‘hakuna Mungu,’ basi hatuwajibiki kwa mamlaka yake, wala “hatulazimiki kufuata viwango vyovyote.” Kwa kuwa hakuna sheria hususa kuhusu maadili, basi kila mtu hujiamulia ikiwa atafuata au hatafuata viwango vyovyote. Si ajabu kwamba maoni hayo yamefanya watu fulani wavutiwe na fundisho la kwamba hakuna Mungu.—Zaburi 14:1.

Hata hivyo, Mungu hatavumilia milele uwongo unaoenezwa na watu wanaosema kwamba Yeye hayuko au uwongo unaoenezwa na watu wa dini. * Anaahidi hivi: “Wanyoofu [kiadili na kiroho] ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” (Methali 2:21, 22) Hilo litatokeza amani na furaha ulimwengu pote, jambo ambalo hakuna mwanadamu yeyote, falsafa ya kibinadamu, au shirika lolote la kibinadamu linaweza kutimiza.—Isaya 11:9.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Maelezo ya Biblia kuhusu kwa nini Mungu ameruhusu kwa muda uovu na kuteseka yanaweza kupatikana katika sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

MAONI YA MUNGU KUHUSU UKATILI WA KIDINI

Nchi waliyopewa Waisraeli wa kale ilikaliwa na Wakanaani waliofanya matendo machafu kingono kama vile kufanya ngono na watu wa familia, ulawiti, ngono na wanyama, na pia walitoa watoto wao kuwa dhabihu. (Mambo ya Walawi 18:2-27) Kitabu Archaeology and the Old Testament kinasema kwamba maeneo yaliyochimbuliwa yalikuwa na “marundo ya majivu na makaburi yenye mifupa ya vitoto vichanga yaliyozunguka madhabahu ya kipagani, na hilo lilionyesha jinsi ambavyo zoea la [kutoa watoto kuwa dhabihu] lilikuwa limeenea.” Kitabu kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema kwamba Wakanaani waliabudu miungu yao kwa kujihusisha katika uasherati na pia kwa kuwatoa wazaliwa wao wa kwanza kuwa dhabihu kwa miungu hiyohiyo. Kitabu hicho kinaongezea kusema: “Waakiolojia wanaochimbua magofu ya majiji ya Kanaani hushangaa ni kwa nini Mungu hakuwaharibu mapema zaidi ya alivyofanya.”

Kuharibiwa kwa Wakanaani kunatukumbusha kwamba Mungu hatavumilia milele uovu unaofanywa katika jina lake. Andiko la Matendo 17:31 linasema: “[Mungu] ameweka siku ambayo katika hiyo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watu wote, wawe wa kidini au wasio wa kidini wamefanya matendo ya ukatili

Kanisa liliunga mkono Hitler

Mafuvu ya watu waliouawa na Khmer Rouge, Kambodia

[Hisani]

AP Photo