Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Roho Waovu Ni Nani?

Roho Waovu Ni Nani?

Maoni ya Biblia

Roho Waovu Ni Nani?

MIZUKA, mizimu, mazimwi, majini, pepo, ni baadhi ya viumbe wa roho ambao watu katika dini mbalimbali huamini na kuona kuwa ni wema au wabaya. Watu wengine husema kwamba kuamini roho hizo ni ushirikina tu au ni mambo ya kuwazia tu. Biblia inasema nini?

Biblia inafundisha kwamba Muumba ni Roho na kwamba viumbe wake wa kwanza walikuwa roho. (Yohana 4:24; Waebrania 1:13, 14) Isitoshe, Biblia pia inataja kwamba kuna roho waovu. (1 Wakorintho 10:20, 21; Yakobo 2:19) Lakini haifundishi kwamba Mungu ndiye aliyewaumba roho waovu. Basi wao ni nani, na walitokea jinsi gani?

“Malaika Waliofanya Dhambi”

Mungu alipowaumba viumbe wa roho, aliwaumba wakiwa na uhuru wa kuchagua ikiwa watatenda mema au mabaya. Kwa kusikitisha, baada ya wanadamu kuumbwa, idadi isiyojulikana ya malaika waliamua kutenda mabaya kwa kumwasi Mungu.

Roho wa kwanza kuasi na mwenye sifa mbaya zaidi akawa Shetani. “Hakusimama imara katika kweli,” akasema Yesu Kristo. (Yohana 8:44) Ni nini kilichomchochea Shetani kumwasi Mungu? Alianza kutamani ibada ambayo ilikuwa hasa ya Muumba, kisha akatenda kupatana na tamaa hiyo kwa kujifanya kuwa mungu. Kwa kufanya hivyo, akajifanya mwenyewe kuwa “Shetani,” neno linalomaanisha “mpinzani.” Karne nyingi baadaye, kabla ya Furiko la siku ya Noa, malaika wengine walijiunga na Shetani, wakaacha cheo chao mbinguni ili wawe wanadamu na kuishi duniani. (Mwanzo 6:1-4; Yakobo 1:13-15) Gharika ilipokuja, ‘malaika hao waliofanya dhambi’ walirudi katika makao ya roho. (2 Petro 2:4; Mwanzo 7:17-24) Kwa hiyo, baadaye wakawa roho waovu.—Kumbukumbu la Torati 32:17; Marko 1:34.

Sasa malaika hao waasi walijikuta katika hali tofauti kabisa na ile waliyokuwa wamefurahia kabla ya kuasi. Yuda 6 inasema: “Malaika ambao hawakubaki mahali pao pa kwanza bali wakayaacha makao yao wenyewe yanayofaa [Mungu] amewaweka akiba wakiwa na vifungo vya milele chini ya giza zito kwa ajili ya hukumu ya ile siku kuu.” Naam, Mungu hakuwaruhusu roho hao waovu wafurahie mapendeleo waliyokuwa nayo mbinguni lakini walitupwa katika “mashimo yenye giza zito,” wakiwa wametengwa na nuru yote ya kiroho.

‘Anaipotosha Dunia Nzima Inayokaliwa’

Ingawa ni wazi kwamba roho waovu wamezuiwa wasijigeuze kuwa wanadamu tena, bado wana nguvu na uvutano mwingi juu ya akili na maisha ya watu. Kwa kweli, Shetani, na roho wake waovu, ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9; 16:14) Kwa njia gani? Hasa kupitia “mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:1) Mafundisho hayo ya uwongo, ambayo mengi ni ya kidini, yamepofusha akili za mamilioni ya watu wasitambue ukweli kumhusu Mungu. (2 Wakorintho 4:4) Fikiria mifano kadhaa.

Fundisho kwamba wafu bado wako hai. Kwa kutumia mizuka, sauti, na mbinu fulani za ujanja, roho waovu huwadanganya watu waamini kwamba walio hai wanaweza kuwasiliana na waliokufa. Isitoshe, ujanja huo huwafanya watu waamini uwongo wa kwamba nafsi huendelea kuishi mwili unapokufa. Lakini Biblia inasema hivi waziwazi: “Wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5, 6) Kwa kuwa ‘wameingia mahali penye kimya,’ hawawezi hata kumsifu Mungu.—Zaburi 115:17. *

Ukosefu wa viwango vya maadili. “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” inasema 1 Yohana 5:19. Shetani na roho wake waovu hutumia nguvu zao vibaya kwa kutumia vyombo vya habari na njia nyingine kueneza wazo bovu kwamba wanadamu wanapaswa kutenda kulingana na tamaa zao za kimwili. (Waefeso 2:1-3) Kwa hiyo, ukosefu wa maadili wa kila aina, kutia ndani ngono zilizopotoka, umeenea sana leo. Tabia kama hizo huonwa kuwa za kawaida, huku viwango vya Biblia vikionwa kuwa vya zamani au vya kishamba.

Kuendeleza zoea la kuwasiliana na pepo. Mtume Paulo alikutana na kijakazi aliyekuwa na “roho mwovu wa uaguzi,” na kwa hiyo “alikuwa akiwapatia mabwana zake faida nyingi kwa kufanya ufundi wa kubashiri.” (Matendo 16:16) Kwa kuwa Paulo alitambua chanzo cha nguvu zake zisizo za kawaida, alikataa kumsikiliza kijakazi huyo. Isitoshe, hakutaka kumkasirisha Mungu, ambaye huchukizwa na aina zote za kuwasiliana na pepo—kutia ndani unajimu na kuomba msaada kutoka kwa makao ya roho.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Jilinde Dhidi ya Roho Waovu

Unaweza kujilinda jinsi gani dhidi ya roho waovu? Biblia inajibu hivi: “Jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Tunatii agizo hilo tunapoishi kupatana na mafundisho yaliyo katika Biblia, kitabu pekee kitakatifu ambacho kinamfichua Shetani, roho waovu, na “hila” zao. (Waefeso 6:11; 2 Wakorintho 2:11) Pia, Biblia inatuambia kwamba roho waovu pamoja na wote wanaompinga Mungu, hawatakuwapo milele. (Waroma 16:20) “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake,” inasema Methali 2:21.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kuhusu hali hasa ya wafu na tumaini la Biblia la ufufuo, tafadhali ona sura ya 6 na ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Je, Mungu ndiye aliyewaumba roho waovu?—2 Petro 2:4.

● Je, unaweza kuzungumza na wafu?—Mhubiri 9:5, 6.

● Unaweza kujilinda jinsi gani dhidi ya roho waovu?—Yakobo 4:7.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Roho waovu hujaribu kuwavuta watu katika njia nyingi