Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ona Jina la Mungu Nchini Denmark

Ona Jina la Mungu Nchini Denmark

Ona Jina la Mungu Nchini Denmark

KILA mwaka, maelfu ya watalii ambao hutembelea Copenhagen hushangaa kuona jina la Mungu, Yehova, au zile herufi nne za Kiebrania, יהוה, zinazowakilisha jina hilo zikiwa zimeandikwa kwenye makasri na majengo mengine katika mji huo mkuu. * Kwa mfano, katikati mwa jiji hilo kuna Kanisa la Dockyard (Holmens Kirke) ambalo lina lango lililoandikwa jina la Mungu kwa herufi kubwa za dhahabu. Pia, jina hilo limeandikwa ndani ya lango hilo kwenye bamba la ukumbusho la mwaka wa 1661.

Hatua chache kutoka Kanisa la Dockyard kuna jengo linaloitwa Mnara wa Mviringo (Rundetårn). Kwenye upande wa nje wa mnara huo, jina la Mungu huonekana likiwa limeandikwa kwa maandishi makubwa ya Kiebrania kama sehemu ya ishara ya Kilatini. Maandishi ya ishara hiyo yanapotafsiriwa yanasema hivi: “Yehova na aongoze mafundisho ya kweli na haki katika moyo wa Mfalme Christian wa Nne aliyetawazwa.” Watu nchini Denmark walipataje kulijua vizuri sana jina la Mungu?

Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti na Kutafsiriwa kwa Biblia

Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti yalichangia sana katika kuenezwa kwa jina la Mungu. Watu waliochochea marekebisho hayo huko Ulaya kama vile Martin Luther, John Calvin, na Huldrych Zwingli walijifunza Biblia na lugha zake za awali kwa bidii. Lugha hizo zilitia ndani Kiebrania, Kiaramu, na Kikoine, yaani Kigiriki cha kawaida. Kwa sababu hiyo, walilifahamu vizuri jina la kibinafsi la Mungu. Martin Luther alisema hivi katika mojawapo ya mahubiri yake, “Jina hili Yehova . . . ni la Mungu wa kweli peke yake.”

Hata hivyo, Luther alipotafsiri Biblia katika Kijerumani, alifuata desturi isiyo ya kimaandiko ya kubadili jina la Mungu kwa majina ya cheo kama vile “Bwana” au “Mungu.” Baadaye, Luther alimwomba mshiriki wake, Johannes Bugenhagen, atafsiri Biblia ya Luther katika Kijerumani cha Chini, yaani, lugha iliyozungumzwa upande wa kaskazini wa Ujerumani na kusini ya Denmark. Katika maneno ya utangulizi ya tafsiri ya 1541 (toleo la kwanza lilichapishwa mnamo 1533), Bugenhagen alitaja jina la Mungu mara kadhaa, na akasema hivi pia: “Yehova ni jina takatifu la Mungu.”

Mnamo 1604, mwanatheolojia mwenye umri mdogo anayeitwa Hans Paulsen Resen alizungumza na Mfalme Christian wa 4 kuhusu makosa fulani katika tafsiri ya Kidenmark ya Biblia ya Luther. Kwa hiyo, Resen aliomba ruhusu aweze kutafsiri upya akitumia maandishi ya awali ya Kiebrania na Kigiriki. Aliruhusiwa kufanya hivyo. Akiandika kuhusu Mwanzo 2:4, Resen aliandika kwamba “Yehova” ndiye “Mkuu Kuliko Wote, na Bwana peke yake.” *

Jina la Mungu lilipozidi kujulikana, lilianza kuonekana katika maeneo ya umma. Kwa mfano, mnamo 1624, baada ya Hans Paulsen Resen kuwekwa rasmi kuwa askofu, aliamuru bamba liwekwe ndani ya Kanisa la Bronshoj. Juu ya bamba hilo, aliandika kwa dhahabu jina la Mungu katika Kidenmark, Jehova. Pia, katika maandishi yake mengi akiwa askofu, Resen aliandika maneno haya chini ya sahihi yake “Yehova anatazama.”

Kuelekea mwisho wa karne ya 18, tafsiri ya Biblia ya Kijerumani ya Johann David Michaelis ilichapishwa katika Kidenmark. Biblia hiyo pia ina jina la Mungu katika sehemu nyingi. Vivyo hivyo, katika karne ya 19, watafsiri wa Biblia kama vile Christian Kalkar na wengine walitia ndani jina la Mungu katika sehemu nyingi ambapo jina hilo lilipatikana katika maandishi ya awali. Kisha mnamo 1985, Mashahidi wa Yehova walitoa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kidenmark. Watu wanaoipenda Biblia walifurahi sana kuona jina Yehova zaidi ya mara 7,000.

Yesu Kristo alisema hivi alipokuwa akisali kwa Mungu: “Nimelifunua jina lako.” (Yohana 17:6) Na katika sala ya kielelezo ambayo nyakati nyingine inaitwa Sala ya Baba Yetu, Yesu alisema: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kama historia ya kidini ya Denmark inavyoonyesha, watu wengi wamechukua maneno hayo kwa uzito.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Herufi hizo nne zinazoitwa Tetragramatoni, ni konsonanti, na zinazosomwa kutoka kulia kwenda kushoto. Kwa kawaida zinatafsiriwa YHWH au JHVH. Nyakati za kale msomaji angeingiza irabu zilizokosekana.

^ fu. 7 Jina la Mungu linapatikana kwa mara ya kwanza kabisa katika Mwanzo 2:4 kwenye maandishi ya awali ya Biblia Takatifu. Jina hilo ambalo linapatikana mara 7,000 hivi katika maandishi ya awali, linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa,” na hivyo kumtambulisha Yehova kuwa Yule ambaye kusudi lake hutimia sikuzote. Kile anachosema hutendeka.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

TYCHO BRAHE ALITUMIA JINA LA MUNGU

Mnamo 1597, Tycho Brahe, mtaalamu maarufu wa nyota wa Denmark, alihama nchi yake baada ya kutoelewana na familia ya kifalme ya Denmark na Mfalme Christian wa 4. Katika shairi la kuaga nchi ya Denmark, Brahe aliandika hivi kwa Kilatini: “Watu wa kigeni watanitendea kwa fadhili—hayo ndiyo mapenzi ya Yehova.”

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Lango la Kanisa la Dockyard

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Mnara wa Mviringo

[Picha katika ukurasa wa 25]

Hans Paulsen Resen

[Picha katika ukurasa wa 25]

Johannes Bugenhagen alitumia jina la Mungu katika maneno ya utangulizi ya tafsiri ya Biblia ya Luther ya Kijerumani cha Chini, ya mnamo 1541

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Hans Paulsen Resen and Tycho Brahe: Kobberstiksamlingen, Det Kongelige Bibliotek, København