Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?

Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?

Vijana Huuliza

Ninawezaje Kuwafahamu Wazazi Wangu Vizuri Zaidi?

Jessica na wazazi wake wanakula chakula pamoja na marafiki. Huku wakiendelea kula, mgeni mmoja anamwambia mamake Jessica, “Huwezi kuamini! Juzi nilimwona Richard, yule kijana aliyekuwa mpenzi wako ulipokuwa shule ya sekondari.”

Jessica anashtuka. Mama yake hajawahi kuzungumza kumhusu Richard!

“Eti nini! Yaani, Mama ulikuwa na mpenzi mwingine kabla ya kukutana na Baba? Sikujua hilo!”

JE, UMEWAHI kujua jambo fulani kuhusu wazazi wako ambalo lilikushangaza kama Jessica alivyoshangaa? Ikiwa ndivyo, huenda jambo hilo lilikufanya ujiulize ni jambo gani lingine ambalo hujui kuwahusu!

Kwa nini huenda kuna mambo fulani ambayo hujui kuwahusu wazazi wako? Kuna faida zipi za kuwafahamu wazazi wako vizuri zaidi? Na unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Mengi ya Kujifunza

Kwa nini huenda kuna mambo fulani ambayo hujui kuwahusu wazazi wako? Nyakati nyingine ni kwa sababu wazazi wako wanaishi mbali. “Wazazi wangu walitalikiana nilipokuwa na umri wa miaka minane,” anasema Jacob, * ambaye sasa ana umri wa miaka 22. “Kwa sababu hiyo, nilimwona baba yangu mara chache sana kwa mwaka. Kuna mambo mengi sana kumhusu ambayo ninatamani kuyajua.”

Hata kama umeishi na wazazi wako kwa miaka mingi, huenda hawajakuambia mambo yote kuhusu maisha yao. Kwa nini? Kama sisi sote, nyakati nyingine wazazi huaibikia makosa ambayo walifanya wakati uliopita. (Waroma 3:23) Pia, huenda wakaogopa kwamba wakikueleza makosa yao, hutawaheshimu, au yatakupa ujasiri wa kufanya makosa.

Hata hivyo, mara nyingi kuna mambo ambayo wazazi wako hawajakuambia kwa sababu nafasi ya kuyazungumzia haijawahi kujitokeza. Kijana anayeitwa Cameron anasema, “Ni jambo la ajabu kwamba unaweza kuishi na wazazi wako kwa miaka mingi na bado uwe na mengi ya kujifunza kuwahusu!” Kwa nini usichukue hatua ya kwanza kujifunza mengi zaidi kuwahusu wazazi wako? Fikiria faida nne ambazo unaweza kupata.

Faida ya 1: Huenda wazazi wako wakafurahi kwamba unataka kuwafahamu vizuri zaidi. Bila shaka watafurahi kujua kwamba unajali kuhusu maisha yao na huenda wakazungumza nawe kwa huruma zaidi!—Mathayo 7:12.

Faida ya 2: Utafahamu jinsi ambavyo wazazi wako huona mambo. Kwa mfano, je, wazazi wako walikuwa maskini zamani? Hilo litakusaidia kuelewa kwa nini wao ni wagumu sana kuhusu matumizi ya pesa, hata wakati unapoona hakuna haja ya kuzibana.

Kufahamu mambo kama hayo kuhusu wazazi wako kunaweza kukunufaisha sana. Kijana anayeitwa Cody anasema hivi, “Kwa sababu ya kujua jinsi wazazi wangu wanavyofikiri, ninaweza kufikiria jinsi maneno yangu yatakavyowaathiri kabla ya mimi kuzungumza.”—Methali 15:23.

Faida ya 3: Huenda ukajihisi huru kuzungumza kuhusu maisha yako. “Sikujihisi huru kuzungumza na Baba kumhusu kijana niliyempenda,” anasema Bridgette mwenye umri wa miaka 18. “Lakini nilipozungumza na Baba, aliniambia kuhusu msichana wa kwanza ambaye yeye alimpenda na jinsi jambo hilo lilivyomwathiri. Hata aliniambia kuhusu siku ambayo uhusiano wake na huyo msichana ulivunjika na jinsi alivyohisi vibaya. Hilo lilinifanya nijihisi huru hata zaidi kumwambia mengi kuhusu hali yangu.”

Faida ya 4: Huenda ukajifunza jambo fulani. Unaposikia kuhusu mambo ambayo wazazi wako walipitia unaweza kujifunza jinsi ya kushughulika na matatizo yako. “Ninataka kujifunza jinsi ambavyo wazazi wangu wanatunza familia kubwa yenye watu wenye mahitaji mbalimbali ya kimwili, kihisia, na kiroho,” anasema Joshua mwenye umri wa miaka 16. “Lazima kuwe na mambo muhimu ya kujifunza.” Biblia inauliza hivi: “Je, hekima haimo katikati ya wazee na uelewaji katika wingi wa siku?”—Ayubu 12:12.

Chukua Hatua ya Kwanza

Ikiwa ungependa kuwafahamu wazazi wako vizuri zaidi, unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Hapa kuna mapendekezo fulani.

Chagua wakati unaofaa. Si lazima mpange wakati hususa wa kuzungumza. Badala yake, jaribu kutafuta pindi zisizo rasmi. Unaweza kufanya hivyo unapocheza, kufanya kazi, kutembea, au kusafiri pamoja na wazazi wako. “Tumezungumza sana na wazazi wangu tulipokuwa tukisafiri kwenda mbali,” anasema Cody, aliyetajwa mapema. “Ni kweli kwamba ni rahisi zaidi kusikiliza muziki kwa kutumia vifaa vinavyotiwa masikioni au kulala tu, lakini nimeona kwamba ninapata faida kubwa zaidi kwa kuanzisha mazungumzo.”

Uliza maswali. Tuseme kweli: Hata katika wakati unaofaa, huenda mama yako asianze tu kukuambia kuhusu mpenzi wake wa kwanza, na baba yako hataanza kukuambia tu kuhusu wakati alipoharibu baiskeli ya baba yake. Lakini huenda wazazi wako wakakuambia mambo hayo ukiwauliza!—Ili upate maswali unayoweza kuwauliza wazazi wako, ona  sanduku kwenye ukurasa wa 12.

Uwe tayari kunyumbulika. Mara nyingi jibu la swali moja linaweza kutokeza hadithi nyingine. Huenda ukahisi kwamba unataka kurudisha mazungumzo mahali yalipoanzia, lakini jaribu kujizuia! Kumbuka kwamba lengo lako si kupata habari tu. Badala yake unataka kusitawisha uhusiano wa karibu zaidi na wazazi wako, na moja kati ya njia bora zaidi za kufanya hivyo ni kuzungumzia mambo ambayo yanawapendeza wao.Wafilipi 2:4.

Uwe na utambuzi. “Fikra za mtu zimefichika kama kilindi cha maji; lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.” (Methali 20:5, Biblia Habari Njema) Unahitaji kuwa na busara, au utambuzi, unapotaka wazazi wako wazungumzie habari ambazo huenda hawataki kuzizungumzia. Kwa mfano, huenda ukataka kujua makosa ambayo baba yako alifanya alipokuwa na umri wako na jinsi ambavyo angeshughulikia mambo kwa njia tofauti ikiwa angeweza. Lakini kabla ya kuanza kuzungumzia mambo hayo, huenda ukasema hivi, “Je, ni sawa nikikuuliza kuhusu . . . ”

Tumia busara. Wazazi wako wanapokuambia kuhusu maisha yao, ‘uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Hata wakuambie nini, usiwakejeli au kuwatukana wazazi wako. Kuna mambo fulani unayoweza kusema na yamzuie baba au mama yako kukuambia mambo mengine, kama vile kusema, “Eti! Siamini kwamba ulifanya hivyo!” au “Kumbe hiyo ndiyo sababu ninyi huwa wakali kwangu!” Pia hawatakueleza mambo mengine ikiwa utaeneza mambo waliyokuwambia.

Hujachelewa!

Madokezo yaliyotajwa yanaweza kukusaidia kuwaelewa wazazi wako vizuri zaidi ikiwa bado unaishi nyumbani. Lakini vipi ikiwa tayari umehama? Kanuni hizohizo zinaweza kukusaidia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na mzazi wako. Jacob, aliyetajwa awali, alifanya hivyo. Ingawa sasa anaishi peke yake, anasema hivi, “Siku hizi nimeanza kumfahamu baba yangu vizuri zaidi, na ninafurahia sana jambo hilo.”

Kwa hiyo, iwe unaishi nyumbani au unaishi peke yako, bado hujachelewa kuwafahamu wazazi wako. Mbona usitumie madokezo katika makala hii?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Ni mambo gani yaliyotajwa katika makala hii ambayo ungependa kuwauliza wazazi wako?

▪ Kujifunza kuhusu wazazi wako kunaweza kukusaidiaje ujielewe vizuri zaidi?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Waulize wazazi wako maswali kama haya:

 NDOA: Wewe na Mama (au Baba) mlikutanaje? Ni nini kilichokuvutia kwake? Mliishi wapi baada ya kuoana?

MAISHA YA UTOTONI: Ulizaliwa wapi? Mlikuwa mnapatana na ndugu na dada zako? Je, wazazi wako walikuwa wakali au walikuendekeza?

ELIMU: Ulipata maksi nyingi zaidi katika somo gani? Ulianguka somo gani? Je, kuna mwalimu uliyempenda zaidi? Kwa nini ulimpenda?

KAZI YA KUAJIRIWA: Ulifanya kazi gani mara ya kwanza? Je, ulifurahia kazi hiyo? Ikiwa ungepewa nafasi ya kuchagua kazi yoyote, ungefanya kazi gani?

MAPENDEZI: Ikiwa ungeweza kutembelea sehemu yoyote ulimwenguni, ungeenda wapi? Ni jambo gani ambalo ungependa kufanya ili kujifurahisha?

HISTORIA YA KIROHO: Je, ulilelewa na wazazi Wakristo? Ikiwa sivyo, nini kilichokuchochea ujifunze Biblia? Ulipata magumu gani ulipokuwa ukijaribu kuishi kupatana na viwango vya Biblia?

VIWANGO: Unafikiri ni mambo gani ambayo yanamfanya mtu awe rafiki mzuri? awe na furaha maishani? awe na ndoa yenye mafanikio? Ni mashauri gani bora zaidi ambayo umewahi kupewa?

Jaribu kufanya hivi: Chagua maswali machache yaliyotajwa hapa juu na ujaribu kuwazia wazazi wako wangeyajibuje. Kisha, waulize maswali hayo na ulinganishe majibu yao na majibu uliyofikiri wangekupa.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

TAARIFA KWA WAZAZI

Unakula chakula pamoja na mume wako, binti yako, na wageni fulani. Wakati wa mazungumzo, rafiki yako anamtaja mtu fulani wa jinsia tofauti ambaye alikuwa rafiki yako wa karibu kisha mkaachana kabla ya kukutana na mume wako. Hujawahi kumwambia binti yako jambo hilo. Sasa anataka kujua mengi zaidi. Utafanya nini?

Kwa kawaida, ni vizuri kujibu maswali ya mtoto wako. Kwani wakati anapouliza maswali na kusikiliza majibu yako, mnawasiliana —jambo ambalo wazazi wengi wanatamani kufanya.

Ni mambo gani unayopaswa kumwambia mwana au binti yako kuhusu maisha yako ya zamani? Kwa kawaida, haingefaa umwambie habari zenye kuaibisha. Hata hivyo, inapofaa, kuwaambia kuhusu makosa uliyofanya na shida uliyopitia kunaweza kuwasaidia watoto wako. Jinsi gani?

Fikiria mfano wa mtume Paulo. Pindi moja, alisema hivi kujihusu: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami. . . . Maskini mimi!” (Waroma 7:21-24) Yehova Mungu alitumia roho yake kuongoza maneno hayo yaandikwe na kuhifadhiwa katika Biblia kwa faida yetu. (2 Timotheo 3:16) Nasi kwa kweli tunafaidika, kwa sababu sisi sote tumewahi kuhisi kama Paulo alivyohisi.

Vivyo hivyo, kusikia kuhusu maamuzi mazuri na mabaya uliyofanya kunaweza kuwasaidia watoto wako wakuelewe vizuri. Bila shaka, ulilelewa wakati tofauti na watoto wako. Hata hivyo, ingawa nyakati zimebadilika, tabia za wanadamu hazijabadilika; ndivyo ilivyo na kanuni za Kimaandiko. (Zaburi 119:144) Kuzungumzia shida ambazo umepitia na jinsi ulivyozishinda kunaweza kuwasaidia vijana wako wanapotatua matatizo yao wenyewe. Kijana mmoja anayeitwa Cameron anasema hivi: “Unapogundua kwamba wazazi wako wamepitia shida kama zako, unawaona kuwa watu wasio wakamilifu kama wewe.” Anaongezea hivi: “Unapokabili tatizo wakati mwingine, unajiuliza ikiwa wazazi wako wamewahi kupitia hali kama hiyo pia.”

Tahadhari: Si lazima kila mara unapowasimulia watoto wako jambo lolote uwape shauri. Ni kweli kwamba huenda ukawa na wasiwasi kwamba kijana wako atakata kauli isivyofaa au hata akahisi kwamba ana haki ya kufanya makosa kama yale uliyofanya. Lakini badala ya kumwambia kile ambacho unataka ajifunze kutokana na mazungumzo yenu (“Hiyo ndiyo sababu wewe hupaswi . . . ”), sema kifupi jinsi wewe unavyohisi. (“Ninapotazama nyuma, najuta kwa nini nilifanya hivi au vile kwa sababu . . . ”) Hivyo, kijana au binti yako anaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na maisha yako. —Waefeso 6:4.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

“Siku moja, nilimwambia mama yangu kwamba mimi hujihisi huru nikiwa na wanafunzi wenzangu kuliko nikiwa na Wakristo wenzangu. Siku iliyofuata, nilikuta barua ya Mama juu ya meza. Katika barua hiyo, alinieleza kwamba kuna wakati alihisi kwamba hana marafiki Wakristo. Alinikumbusha kuhusu baadhi ya watu wanaotajwa katika Biblia waliomtumikia Mungu hata ingawa hakukuwa na watu wa kuwatia moyo. Pia, alinipongeza kwa jitihada zangu za kutafuta marafiki wanaofaa. Nilishangaa kujua kwamba si mimi peke yangu niliyekabili tatizo hilo. Mama yangu pia alipitia hali hiyo, na nilifurahi sana kujua kuhusu hilo hivi kwamba nikalia. Nilitiwa moyo sana na maneno ya mama yangu na nikaimarishwa kufanya yaliyo sawa.” —Junko, 17, Japani.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Waombe wazazi wako wakuonyeshe picha au vitu vingine vyao vya zamani. Mara nyingi mambo hayo huanzisha mazungumzo yenye kusisimua