Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Sababu ya Kuwaogopa Wafu?

Kuna Sababu ya Kuwaogopa Wafu?

Maoni ya Biblia

Kuna Sababu ya Kuwaogopa Wafu?

Watu wa kabila la Annang nchini Nigeria wanaamini kwamba wafu wasipozikwa kwa sifa na heshima inayofaa, nafsi zao zitawaletea washiriki wa familia shida na hata kifo. Pia, Wachina fulani wanaamini kwamba tamaduni za mazishi zisipofuatwa, nafsi za wafu zitavamia na hata kuwaua watu.

NI JAMBO la kawaida katika tamaduni nyingi ulimwenguni pote kuamini kwamba baada ya kufa kitu fulani hutoka mwilini, iwe ni nafsi, roho, au mzuka. Watu wengi pia wanaamini kwamba nafsi au roho inaweza kuathiri maisha ya washiriki wa familia au marafiki.

Lakini je, kuna kitu fulani chenye uhai ambacho huendelea kuishi mtu anapokufa? Na je, “kitu” hicho kinaweza kuwadhuru walio hai? Maoni ya Biblia ni nini?

Je, Wafu Wanajua Lolote?

Biblia inasema kwamba wafu “hawajui lolote kamwe.” Pia, inasema kwamba wafu ‘hawajiwezi katika kifo.’ (Mhubiri 9:5; Isaya 26:14) Kumhusu mtu wa kwanza, Adamu, Neno la Mungu linaeleza hivi: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.”Mwanzo 2:7.

Ona kwamba Adamu aliumbwa akiwa nafsi, yaani, mtu hai. Kulingana na Biblia, Adamu hakupewa nafsi ambayo ingeweza kuishi bila mwili. Kwa hiyo, Adamu alipofanya dhambi, alikufa. Akawa “nafsi . . . iliyokufa.” (Hesabu 6:6) “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa,” inasema Biblia. (Ezekieli 18:4) Sisi sote tulirithi dhambi, au kutokamilika, kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Kwa hiyo, tunapokufa, nafsi inakufa.—Waroma 5:12.

Biblia inapofafanua hali ya wafu, haitumii maneno yasiyoeleweka, bali inatumia maneno tunayoweza kuelewa, kama vile ‘kulala usingizi katika kifo.’ (Zaburi 13:3) Wakati mmoja Yesu alisema hivi kuhusu msichana mwenye umri wa miaka 12: “Hakufa bali analala usingizi.” Ndipo watu “wakaanza kumcheka kwa dharau, kwa sababu walijua alikuwa amekufa.” Lakini Biblia inasema kwamba Yesu alimwamsha kutoka katika usingizi wa kifo.—Luka 8:51-54.

Mambo yalikuwa hivyo pia Lazaro alipokufa. Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba alikuwa akienda kumtembelea Lazaro “ili kumwamsha kutoka usingizini.” Wanafunzi hawakuelewa Yesu alikuwa akimaanisha nini, kwa hiyo “Yesu akawaambia waziwazi: ‘Lazaro amekufa.’” Mtume Paulo pia alizungumza kuhusu wale “walalao usingizi katika kifo” na akasema kwamba wakati wa Mungu ukifika, watafufuliwa wawe hai.—Yohana 11:11-14; 1 Wathesalonike 4:13-15.

Ni muhimu kutambua kwamba hakuna mahali ambapo Biblia inafundisha kuwa nafsi huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kuwaogopa wafu. Basi ni nini kinachofanya watu wengi waamini kwamba kitu fulani ndani ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mtu kufa? Na kwa nini watu huogopa kwamba wafu wanaweza kuwadhuru watu walio hai?

Uwongo Unaoendelezwa

Dini za uwongo zimeendeleza wazo la kwamba wanadamu hawafi kabisa. Mapema katika historia ya wanadamu, fundisho la kutokufa kwa nafsi lilikubaliwa ulimwenguni pote. Kwa sababu hiyo, watawala fulani walipokufa—kama vile Mafarao wa Misri ya kale—watumwa wao waliuawa ili wakawahudumie watawala wao katika maisha yao ya baadaye.

Watu wengi wameteswa na kile walichofundishwa kuwa ni nafsi au roho za wafu. Wanasadiki kwamba wanateswa na nafsi ambazo hazijatulizwa za watu wa ukoo waliokufa na wafu wengine. Lakini, Maandiko yanaonyesha wazi kwamba hilo si kweli. Majeshi ya roho wasioonekana wanaoitwa mashetani wanasababisha mashambulizi hayo na wanafurahi kuwatesa na kuwaogopesha watu.—Luka 9:37-43; Waefeso 6:11, 12.

Maandiko yanasema kwamba Shetani ndiye “baba ya uwongo,” ambaye “huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” Yeye na mashetani wake ‘wanaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Yohana 8:44; 2 Wakorintho 11:14; Ufunuo 12:9) Kwa kweli, Shetani ndiye anayeendeleza uwongo kwamba nafsi haiwezi kufa na inaweza kuwadhuru walio hai.

Hata hivyo, watu wanaoiamini Biblia wanalindwa wasipotoshwe na uwongo kama huo. Wamekuja kujua ukweli wa kwamba Shetani anajaribu kuwadanganya watu waamini wafu wanaweza kuwasiliana na walio hai. Ukweli ni ule unatajwa katika Biblia: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Kwa kweli, Neno la Mungu lina kweli zinazowaweka watu huru kuhusu hali ya wafu!—Yohana 8:32.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, wafu wanajua jambo lolote?—Mhubiri 9:5; Isaya 26:14.

▪ Ni nini kinachofanya watu wengi waamini kwamba kitu fulani ndani ya mwanadamu huendelea kuishi baada ya mtu kufa?—Yohana 8:44.

▪ Tunaweza kupata wapi ukweli kuhusu hali ya wafu?—Yohana 8:32; 17:17.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Ni roho waovu ndio hufurahia kuwatesa wanadamu, wala si watu waliokufa