Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wasichana Hawanipendi?

Kwa Nini Wasichana Hawanipendi?

Vijana Huuliza

Kwa Nini Wasichana Hawanipendi?

Anavutiwa sana na mimi. Nimemwambia mambo mengi sana kunihusu, kuhusu mali zangu, maeneo ambayo nimewahi kutembelea, watu ninaowajua. Lazima awe anataka sana tuwe marafiki wa karibu!

Natamani ardhi ifunguke inimeze! Yaani haelewi? Nitakatishaje mazungumzo haya bila kumuudhi?

UNA umri wa kutosha kuwa na rafiki wa karibu wa jinsia tofauti. Ungependa kumpata mtu anayevutia na aliye na imani kama zako za kidini. (1 Wakorintho 7:39) Hata hivyo, kila mara ulipojaribu kuanzisha uhusiano, ulihisi kana kwamba uligonga mwamba.

Ikiwa ungependa kumfahamu msichana vizuri zaidi, unapaswa kufikiria mambo gani? Na unapaswa kukumbuka kanuni gani za Biblia?

Unachopaswa Kufanya Kwanza

Kabla ya kuanzisha uhusiano na msichana yeyote, unapaswa kujifunza mbinu fulani ambazo zitakusaidia kufanya urafiki na mtu yeyote. Fikiria mambo yafuatayo.

Jifunze kuwa na adabu. Biblia inasema kwamba “mwenye upendo hakosi adabu.” (1 Wakorintho 13:5, Biblia Habari Njema) Ukiwa na adabu unaonyesha kwamba unawaheshimu wengine na unasitawisha utu mkomavu kama wa Kristo. Hata hivyo, adabu si kama suti unayovaa kuwapendeza wengine na unayovua unapofika nyumbani. Jiulize, ‘Je, mimi huwa na adabu ninaposhughulika na washiriki wa familia?’ Ikiwa hufanyi hivyo, basi unaposhirikiana na watu wengine itaonekana wazi kwamba unajisingizia tu. Kumbuka, msichana mwenye utambuzi atachunguza jinsi unavyowatendea watu wa familia yako ili akufahamu vizuri.—Waefeso 6:1, 2.

Kile ambacho wasichana husema: “Mimi huvutiwa sana na mvulana anayetenda kwa adabu katika mambo madogo kama vile, kunifungulia mlango, na anapofanya mambo makubwa kama vile, kuwa mwenye fadhili na ufikirio si kunielekea tu bali pia kuelekea watu wa familia yangu.”—Tina, 20. *

“Mimi huchukizwa na mtu ambaye tumetoka tu kufahamiana na mara moja anaanza kuniuliza maswali ya kibinafsi sana, kama vile ‘Una mpenzi?’ na ‘Una miradi gani?’ Hayo ni maswali yenye kuaibisha na hunifanya nijihisi vibaya!”—Kathy, 19.

Tunza usafi wako. Usafi huonyesha kwamba unawaheshimu wengine na pia unajiheshimu. (Mathayo 7:12) Ukijiheshimu, huenda wengine watakuheshimu. Kwa upande mwingine, ukipuuza usafi, utapoteza nafasi za kumvutia msichana.

Kile ambacho wasichana husema: “Mvulana mmoja aliyekuwa akipendezwa nami alikuwa ananuka mdomo sana. Singeweza kuvumilia jambo hilo.”—Kelly, 24.

Jifunze jinsi ya kuendeleza mazungumzo. Msingi wa uhusiano wa kudumu ni mawasiliano mazuri. Hilo linahusisha kuzungumzia mapendezi yako mwenyewe na pia kuzungumzia mapendezi ya rafiki yako.Wafilipi 2:3, 4.

Kile ambacho wasichana husema: “Mimi hufurahi sana mvulana anapoweza kuzungumza nami, anapokumbuka mambo niliyomwambia na kuuliza maswali yanayoendeleza mazungumzo.”—Christine, 20.

“Nafikiri wavulana huvutiwa na mambo wanayoona, lakini wasichana huvutiwa na mambo wanayosikia.”—Laura, 22.

“Zawadi ni nzuri. Lakini ikiwa mvulana anaweza kuendeleza mazungumzo, ikiwa anaweza kukufariji na kukutia moyo kwa maneno yake . . . Hilo linavutia wee!”—Amy, 21.

“Ninapendezwa na mtu mcheshi lakini ambaye pia anaweza kuzungumzia mambo mazito bila kuonekana anajifanya.”—Kelly, 24.

Ukifuata mapendekezo yaliyo hapo juu utakuwa na marafiki wazuri. Hata hivyo, unapohisi kwamba uko tayari kuanzisha uhusiano wa karibu na msichana fulani, unapaswa kufanya nini?

Hatua Inayofuata

Chukua hatua ya kwanza. Ukifikiri kwamba rafiki unayependezwa naye anaweza kuwa mwenzi mzuri wa ndoa, mwambie kwamba unapendezwa naye. Eleza hisia zako waziwazi na moja kwa moja. Ni kweli hilo linaweza kuogopesha sana. Unaogopa kukataliwa. Lakini unapochukua hatua ya kwanza unaonyesha kwamba umekomaa.

Kile ambacho wasichana husema: “Siwezi kusoma akili ya mtu. Kwa hiyo, ikiwa mtu anataka kunifahamu, anapaswa kuwa mnyoofu na kuniambia jambo hilo waziwazi.”—Nina, 23.

“Huenda likawa jambo lisilo la kawaida ikiwa mmekuwa marafiki kwa muda. Lakini ningemheshimu rafiki ambaye angeniambia anataka tuwe na uhusiano wa karibu zaidi.”—Helen, 25.

Heshimu uamuzi wa msichana. Lakini vipi ikiwa rafiki yako anasema kwamba hataki muwe na uhusiano wa karibu zaidi? Mheshimu kwa kuamini kwamba anajielewa na kwamba anapokataa anamaanisha hivyo. Utaonyesha kwamba hujakomaa ikiwa utaendelea kusisitiza. Kwa kweli, ukipuuza jibu la msichana huyo, na hata kukasirika kwa kuwa amekukataa, je, kweli unafikiria masilahi yake au yako mwenyewe?—1 Wakorintho 13:11.

Kile ambacho wasichana husema: “Mimi huudhika ninapomwambia mvulana simtaki na bado anaendelea kusisitiza.”—Colleen, 20.

“Nilimwambia mvulana mmoja kuwa sipendezwi naye lakini aliendelea kusisitiza eti nimpe namba yangu ya simu. Sikutaka kumuudhi. Bila shaka, haikuwa rahisi kwake kuniambia hisia zake. Lakini mwishowe nilihitaji kuwa thabiti.”—Sarah, 23.

Mambo Usiyopaswa Kufanya

Vijana fulani huhisi kwamba si vigumu kwao kuwafanya wasichana wawapende. Wanaweza hata kushindana ni nani anayeweza kuwavutia wasichana wengi zaidi. Hata hivyo, ni ukatili kushindana kwa njia hiyo na kutakuletea sifa mbaya. (Methali 20:11) Unaweza kuepuka jambo hilo ukifanya yafuatayo.

Usicheze-cheze kimapenzi. Mtu anayewachezea wengine kimapenzi hutumia usemi mtamu na ishara za mwili zinazoamsha hamu ya ngono. Hana nia ya kufuatia uhusiano wa kimapenzi unaoheshimika. Matendo na mtazamo kama huo hupuuza shauri la Biblia la kuwatendea “wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.” (1 Timotheo 5:2) Watu wanaowachezea wengine kimapenzi si marafiki wazuri na ni wenzi wa ndoa wasiofaa. Wasichana wenye utambuzi wanajua jambo hilo.

Kile ambacho wasichana husema: “Nafikiri ni jambo lisilopendeza hata kidogo mtu anapokuambia maneno matamu lakini unajua alimwambia rafiki yako maneno hayohayo mwezi uliopita.”—Helen, 25.

“Kijana mmoja mwenye kuvutia alianza kunichezea kimapenzi, akiniambia hasa kujihusu. Msichana mwingine alipokuja, alianza kufanya vivyo hivyo. Kisha msichana mwingine akaja na akaanza kutumia maneno yaleyale tena. Sikufurahi hata kidogo!”—Tina, 20.

Usichezee hisia za msichana. Usitazamie kwamba urafiki na mtu wa jinsia tofauti utakuwa sawa na urafiki na mtu wa jinsia yako. Kwa nini? Fikiria hili: Ukimwambia rafiki yako wa kiume kwamba anapendeza akiwa amevalia suti yake mpya au ikiwa wewe huzungumza naye kwa ukawaida na kumwambia mambo ya siri, haielekei kwamba atafikiri unapendezwa naye kimahaba. Lakini ukimwambia msichana kwamba anapendeza au ikiwa wewe huzungumza naye kwa ukawaida na kumwambia mambo ya siri, anaweza kufikiri kwamba unataka kuwa na uhusiano wa kimahaba naye.

Kile ambacho wasichana husema: “Sidhani wavulana wanaelewa kwamba hawawezi kuwatendea wasichana kama wanavyowatendea rafiki zao wa kiume.”—Sheryl, 26.

“Mvulana atachukua namba yangu ya simu, kisha anitumie ujumbe wa simu. Ana nia gani? Nyakati nyingine mnaweza kuwa na uhusiano kupitia kuandikiana ujumbe mfupi wa simu na huenda hilo likaamsha hisia za kimahaba, lakini huwezi kusema mengi kupitia ujumbe mfupi wa simu?”—Mallory, 19.

“Sidhani kama wavulana wanaelewa kwamba msichana anaweza kuvutiwa haraka kihisia, hasa ikiwa mvulana anajali na ana ulimi mtamu. Si eti msichana huyo anataka sana kuwa na uhusiano wa karibu. Nafikiri wasichana wengi hutaka kupendwa nao hutafuta mtu anayewafaa zaidi.”—Alison, 25.

Usijidanganye

Ni jambo lisilopatana na akili kufikiri kwamba wasichana wote watakupenda. Lakini huenda wasichana wengine wakakupenda ukikumbuka jambo hili: Jinsi unavyoonekana kwa nje si muhimu kuliko unavyoonekana ndani. Si ajabu kwamba Biblia inakazia uhitaji wa kusitawisha “utu mpya.”—Waefeso 4:24.

Kate mwenye umri wa miaka 21, anasema hivi: “Wavulana hufikiri kwamba ili wawavutie wasichana wanapaswa kuvalia kwa njia fulani au kuonekana kwa njia fulani. Ingawa kuna ukweli fulani katika jambo hilo, nafikiri wasichana wengi huvutiwa na sifa nzuri.” *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Majina yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unajiheshimu?

▪ Unaweza kumwonyesha msichana jinsi gani kwamba unaheshimu mawazo na hisia zake?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Adabu si kama suti unayovaa kuwapendeza wengine na unayovua unapofika nyumbani