Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuishi Miaka Mingi—Je, Siri Inapatikana Okinawa?

Kuishi Miaka Mingi—Je, Siri Inapatikana Okinawa?

Kuishi Miaka Mingi—Je, Siri Inapatikana Okinawa?

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI JAPANI

▪ Mnamo 2006, visiwa vya Okinawa, Japani, ambavyo vina wakaaji milioni 1.3 vilikadiriwa kuwa na watu 740 hivi walio na zaidi miaka 100, na asilimia 90 kati yao walikuwa wanawake. Hilo linaonyesha kwamba kwa kila watu 100,000, watu 50 hivi wana umri wa zaidi ya miaka 100, kulingana na Uchunguzi wa Okinawa wa Watu Walio na Umri wa Zaidi ya Miaka 100 ulioongozwa na Dakt. Makoto Suzuki. Katika nchi nyingi zilizoendelea, kwa kila watu 100,000, watu kati ya 10 na 20 wana umri wa zaidi ya miaka 100.

Uchunguzi huo unaoendelea unaosemekana kuwa “uchunguzi wa muda mrefu zaidi wa watu walio na umri wa zaidi ya miaka 100 ulimwenguni,” ulionyesha kwamba “idadi kubwa sana ya watu walio na umri wa zaidi ya miaka 100 walikuwa na afya nzuri sana.” Ili wajue kwa nini watu hao huishi muda mrefu hivyo, Suzuki na kikundi chake walichunguza maisha na chembe za urithi za watu zaidi ya 900 walio na zaidi ya umri wa miaka 100 pamoja na wakaaji wengine wa Okinawa walio na umri wa miaka 70 au zaidi. Wachunguzi hao waligundua kwamba watu hao wazee walikuwa wembamba lakini wenye nguvu na afya, mishipa yao haikuwa na mafuta mengi, na hawakupatwa sana na kansa na magonjwa ya moyo. Na wale waliokaribia umri wa miaka 100, ni wachache tu waliokuwa na matatizo ya kusahau mambo wakilinganishwa na wengine katika nchi nyingine zilizoendelea. Siri ni nini?

Jambo moja linalochangia ni chembe za urithi. Lakini kulikuwa na sababu nyingine, kama vile kutumia kileo kwa kiasi, kupata lishe bora, na kuepuka kuvuta sigara. Chakula cha Okinawa hakina kalori nyingi, kina nyuzinyuzi za asili na mafuta mazuri (ya samaki), nao wenyeji hula mboga na matunda mengi. Na watu hao wanakula hadi wanapohisi wako karibu kushiba. “Unapaswa kuacha kula unapohisi tu umeshiba,” anasema Dakt. Bradley Willcox, mchunguzi katika uchunguzi huo. “Dakika 20 hivi hupita kabla ya tumbo kuambia ubongo kwamba limejaa.”

Wakaaji wa Okinawa hufanya mazoezi kwa kulima, kutembea kila siku, kucheza dansi za kitamaduni, au shughuli nyingine. Mtazamo wao ulipochunguzwa walionekana kwamba wana mtazamo mzuri na wako tayari kubadilika kulingana na hali. Walikabiliana vizuri na mfadhaiko na hasa wanawake “walikuwa na uhusiano mzuri na watu wengine.”

“Hakuna dawa ya kimuujiza” ya kuwasaidia watu kuishi muda mrefu, anasema Willcox. Kama uchunguzi huo ulivyoonyesha siri ni chembe za urithi, kula vizuri, kufanya mazoezi, kuwa na mazoea mazuri, “na kukabiliana vizuri na mfadhaiko.”