Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Anakutazamia Ufanye Nini?

Mungu Anakutazamia Ufanye Nini?

Maoni ya Biblia

Mungu Anakutazamia Ufanye Nini?

KWA kuwa maisha yetu yana shughuli nyingi tunatazamiwa tutimize mengi. Nyakati nyingine ni vigumu kutimiza majukumu yetu yote. Lakini, tunapaswa kukumbuka kwamba uhai wenyewe ni zawadi ambayo tumepewa na Mungu. (Zaburi 36:9) Mungu anatazamia tutumie kwa kadiri gani wakati na nguvu zetu kumtumikia? Jibu la Biblia lenye usawaziko linatia moyo.

Yesu alijua vyema kuliko mtu mwingine yeyote kile ambacho Baba yake anawatazamia wanadamu wafanye. (Mathayo 11:27) Alipoulizwa ni amri gani iliyo kuu zaidi ya zote, Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Hilo linamaanisha nini? Je, tunadaiwa mengi sana?

Kumpenda Mungu kwa Nafsi Yote Kunahusisha Nini?

Upendo wetu kwa Mungu unaweza kuongezeka tukitafakari wema wake usio na kifani kutuelekea. Ikiwa tunampenda Mungu kwa nafsi yote, tutachochewa kumpa kilicho bora. Tutahisi kama alivyohisi mwandikaji wa Biblia ambaye aliuliza hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?” (Zaburi 116:12) Kumpenda Mungu kwa njia hiyo kunapaswa kuwa na uvutano gani kuhusu jinsi tunavyotumia wakati wetu?

Biblia haijatoa hesabu kamili ya saa ambazo mtu anapaswa kutenga kila juma kwa ajili ya ibada. Hata hivyo, inaonyesha mambo yanayopaswa kutangulizwa maishani na kwa nini yatangulizwe. Kwa mfano, Yesu alisema kwamba kupata ujuzi juu ya Mungu ni hatua muhimu inayoongoza kwenye “uzima wa milele.” (Yohana 17:3) Alisema kwamba wafuasi wake wanapaswa kuwasaidia wale wasiomjua Mungu wapate uzima wa milele kwa kuwafunza kumhusu Mungu. (Mathayo 28:19, 20) Biblia inatuagiza tukutanike pamoja na waamini wenzetu kwa ukawaida ili tuimarishane kiroho na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Wakati unahitajiwa ili kutimiza mambo yote hayo.

Je, Mungu hataki tujishughulishe na mambo mengine yoyote maishani ila tu ibada? Bila shaka la! Mambo mengine muhimu maishani lazima yashughulikiwe. Biblia inawaagiza vichwa vya familia watimize mahitaji ya familia zao inaposema hivi: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake . . . ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:8.

Mungu alimuumba mtu akiwa na uwezo wa kufurahia maisha. Hivyo, inafaa kutenga wakati wa kula chakula kitamu na kustarehe pamoja na familia na marafiki wetu. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.”—Mhubiri 3:12, 13.

Pia, Yehova Mungu anajua mipaka ya uwezo wa mwanadamu, “akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Biblia inaonyesha kwamba tuna uhitaji wa kupumzika vya kutosha. Baada ya pindi fulani yenye shughuli nyingi, Yesu aliwaambia wanafunzi wake waende ‘faraghani katika mahali pasipo na watu wapumzike kidogo.’—Marko 6:31.

Hivyo, maisha yanayompendeza Mungu yana usawaziko na yanaweza kutia ndani shughuli mbalimbali. Hata hivyo, shughuli zetu zote, iwe zinahusiana au hazihusiani moja kwa moja na ibada, zinapaswa kuonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa nafsi yetu yote. Biblia inashauri hivi: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

Kutanguliza Mambo Muhimu

Je, unaona kwamba kutanguliza ibada ya Mungu maishani mwako ni jambo lisilopatana na akili au lisilowezekana? Ni kweli kwamba ili tufanye kile ambacho Mungu anataka huenda tukahitaji kufanya marekebisho au hata kujidhabihu kuhusiana na jinsi tunavyotumia wakati wetu. Lakini kwa kweli Muumba wetu mwenye upendo hajatuagiza tufanye jambo lisilowezekana. Kwa hakika, anatusaidia sana kufanya mapenzi yake. Tunaweza kufanikiwa tukitegemea “nguvu ambazo Mungu hutoa.”—1 Petro 4:11.

Huenda ikawa vigumu kidogo kurekebisha ratiba yako ili ihusishe shughuli za kiroho. Zungumza mara nyingi na Yehova Mungu, yule “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Unaposali, unaweza kutaja mahangaiko yoyote unayokabili, ukijua kwamba ‘anakujali wewe.’ (1 Petro 5:7) Mfalme Daudi alisali hivi: “Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ni Mungu wangu.” (Zaburi 143:10) Hali kadhalika, unaweza kumwomba Mungu akusaidie kufanya marekebisho yanayohitajiwa maishani mwako.

Biblia inatoa mwaliko huu wenye kuchangamsha: ‘Mkaribie Mungu, naye atakukaribia wewe.’ (Yakobo 4:8) Unapoanza kufanya mambo yanayompendeza Mungu, kama vile kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, utamkaribia Mungu zaidi, naye atakuimarisha ili ufanye maendeleo zaidi.

Jelena, ambaye anajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, anasema hivi kuhusu jitihada zake za kutanguliza mambo muhimu, “Mambo hayajawa mswaki kwangu.” Lakini anaongeza hivi: “Mara tu nilipoanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo, nilipata nguvu za kutumia yale ambayo Biblia inasema. Utegemezo wa daima kutoka kwa wengine umenisaidia pia.” Faida za kumtumikia Mungu zinamchochea mtu pia. (Waefeso 6:10) Jelena anasema, “Nimeboresha uhusiano wangu na mume wangu na pia ninawatia nidhamu watoto wangu kwa njia bora zaidi.”

Licha ya matatizo ya maisha, roho takatifu ya Yehova yenye nguvu inaweza kukuimarisha na kukuchochea uchunguze mambo unayotanguliza maishani na ‘kununua wakati unaofaa’ ili kumtumikia Mungu. (Waefeso 3:16; 5:15-17) Yesu alisema: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.”—Luka 18:27.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Kwa nini utangulize mapenzi ya Mungu maishani mwako? —Zaburi 116:12; Marko 12:30.

▪ Mungu anatazamia ufanye mambo gani?—Mathayo 28:19, 20; Yohana 17:3; Waebrania 10:24, 25.

▪ Unaweza kufanikiwaje kutanguliza mambo muhimu maishani ili umpendeze Mungu?—Waefeso 5:15-17; Yakobo 4:8.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Usawaziko unahitajiwa ili kumpendeza Mungu